Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Yehova Ni Mchungaji Wangu”

“Yehova Ni Mchungaji Wangu”

Mkaribie Mungu

“Yehova Ni Mchungaji Wangu”

HEBU tazama picha iliyo katika ukurasa huu. Je, unaweza kuwazia usalama ambao mwana-kondoo huyo anahisi akiwa kifuani mwa mchungaji wake? Katika Zaburi ya 23, Biblia inatumia mfano wa mchungaji na kondoo kuonyesha jinsi Yehova anavyowatunza waabudu wake kwa wororo. Anataka tuhisi usalama ambao unafurahiwa na wale ambao, kama mtunga-zaburi Daudi, wanaweza kusema hivi kwa uhakika: “Yehova ni Mchungaji wangu.” *​—Mstari wa 1.

Daudi aliye mwandishi wa zaburi hii alikuwa mchungaji alipokuwa kijana. Alijua mahitaji ya kondoo na majukumu ya mchungaji. Daudi ambaye katika maisha yake aliona jinsi Yehova anavyowatunza watumishi wake, aliandika ile inayoitwa “zaburi ya uhakikisho au tumaini.” Jina la Mungu, Yehova, linapatikana katika mstari wa kwanza na wa mwisho wa zaburi hiyo. (Mstari wa 16) Maneno yaliyo katika mstari wa 2-5 yanaeleza njia tatu ambazo Yehova huwajali watu wake kama tu vile mchungaji anavyowajali kondoo wake.—Zaburi 100:3.

Yehova anawaongoza kondoo wake. Ni rahisi kondoo kupotea wakiwa bila mchungaji. Vilevile, sisi tunahitaji msaada ili kupata mwongozo unaofaa maishani. (Yeremia 10:23) Daudi anaeleza kwamba Yehova anawaongoza watu wake katika “malisho yenye majani mengi” na “mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha.” Anawaongoza katika “mapito ya uadilifu.” (Mstari wa 23) Maelezo hayo kuhusu mchungaji yanatuhakikishia kwamba tunaweza kumtumani Mungu. Kwa kufuata mwongozo wa Mungu kupatana na Biblia, tunaweza kuishi maisha yenye kuridhisha, kuburudisha, na salama.

Yehova anawalinda kondoo wake. Kondoo wasipokuwa na mchungaji wao, wanakuwa na woga na ni rahisi kushambuliwa. Yehova anawaambia watu wake kwamba hawahitaji kuogopa, hata ‘wanapotembea katika bonde lenye kivuli kizito’—katika kipindi ambacho huenda kikaonekana kuwa kigumu maishani mwao. (Mstari wa 4) Yehova huwalinda wakati wote, akiwa tayari kuwasaidia. Anaweza kuwapa waabudu wake hekima na nguvu wanazohitaji ili kukabiliana na majaribu.—Wafilipi 4:13; Yakobo 1:2-5.

Yehova huwalisha kondoo wake. Kondoo humtegemea mchungaji wao awatafutie chakula. Sisi tuna uhitaji wa kiroho ambao tunaweza tu kuutosheleza kwa msaada wa Mungu. (Mathayo 5:3) Tunashukuru kwamba Yehova ni mwandalizi mkarimu, anayewaandalia watumishi wake meza iliyojaa chakula cha kiroho. (Mstari wa 5) Biblia na vitabu vinavyoweza kutusaidia kuilewa, kama gazeti unalosoma sasa, ni vyanzo vya chakula cha kiroho kinachotosheleza uhitaji wetu wa kujua umuhimu wa maisha na kusudi la Mungu kwa wanadamu.

Daudi alihisi akiwa salama, akijua kwamba kama angeendelea kuwa karibu na Mchungaji wake wa mbinguni, Yehova, angepata utunzaji wenye upendo “siku zote za maisha [yake].” (Mstari wa 6) Je, unatamani kupata usalama kama huo? Ikiwa ndivyo, jifunze jinsi unavyoweza kumkaribia Yehova. Hivyo, utahisi ukiwa salama mikononi mwa Mchungaji Mkuu, anayewaongoza, kuwalinda, na kuwalisha wale wanaoendela kuwa washikamanifu kwake.—Isaya 40:11.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Mei (Mwezi wa 5):

Ayubu 38-42Zaburi 1-25

[Maelezo ya Chini]

^ Wasomaji wengi wa Biblia wanafahamu maneno, “BWANA ndiye Mchungaji wangu.” Ili uweze kufahamu kwa nini baadhi ya tafsiri za Biblia zimeondoa jina la Mungu, Yehova, ona ukurasa wa 195-197 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.