Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wafu Wana Tumaini Lolote?

Je, Wafu Wana Tumaini Lolote?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Je, Wafu Wana Tumaini Lolote?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Wafu wana tumaini gani?

Yesu alipofika Bethania karibu na Yerusalemu, rafiki yake Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne. Yesu alienda mahali Lazaro alipozikwa akiandamana na Martha na Maria, dada zake. Punde si punde, umati ukakusanyika. Je, unaweza kuwazia shangwe ambayo Martha na Maria walipata wakati Yesu alipomfufua Lazaro?—Soma Yohana 11:20-24, 38-44.

Martha aliamini kwamba wafu wangefufuliwa. Kwa muda mrefu, watumishi waaminifu wa Yehova wamejua kwamba wakati ujao, Mungu atawafufua wafu ili waishi duniani tena.—Soma Ayubu 14:14, 15.

2. Wafu wako katika hali gani?

Ingawa nguvu fulani ya uhai, au “roho,” inawasaidia wanadamu na wanyama kuendelea kuwa hai, hiyo haimaanishi kwamba mwanadamu ana roho au nafsi isiyoweza kufa ambayo inaendelea kuishi baada ya mwili kufa. (Mhubiri 3:19; Mwanzo 7:21, 22) Sisi ni viumbe tulioumbwa kutokana na mavumbi. (Mwanzo 2:7; 3:19) Ubongo wetu unapokufa, mawazo yetu yanapotea. Hivyo, Lazaro alipofufuliwa hakusema chochote kuhusu hali yake alipokuwa mfu, kwa kuwa wafu hawajui lolote.—Soma Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5, 10.

Ni wazi kwamba wafu hawawezi kuteseka. Kwa hiyo, fundisho la kwamba Mungu anawatesa watu baada ya kufa ni la uwongo. Fundisho hilo linamharibia Mungu sifa. Wazo la kuwatesa watu katika moto linamchukiza sana.—Soma Yeremia 32:35.

3. Je, tunaweza kuzungumza na wafu?

Wafu hawawezi kuzungumza. (Zaburi 115:17) Lakini malaika waovu wanapozungumza na watu, wanaweza kudai kwa uwongo kuwa roho ya mtu aliyekufa. (2 Petro 2:4) Yehova ametukataza tusijaribu kuzungumza na wafu.—Soma Kumbukumbu la Torati 18:10, 11.

4. Ni nani watakaofufuliwa?

Katika ulimwengu mpya unaokuja, mamilioni ya watu walio makaburini watafufuliwa. Hata wafu fulani waliofanya mambo mabaya kwa sababu hawakumjua Yehova, watafufuliwa.—Soma Luka 23:43; Matendo 24:15.

Watakaofufuliwa wataweza kujifunza ukweli kumhusu Mungu na kuonyesha imani yao katika Yesu kwa kumtii. (Ufunuo 20:11-13) Wale watakaofufuliwa na kufanya mema wataweza kufurahia uzima wa milele duniani. Hata hivyo, baadhi ya wale watakaofufuliwa wataendelea kufanya mabaya. Hivyo, ufufuo wao utakuwa “ufufuo wa hukumu.”—Soma Yohana 5:28, 29.

5. Ufufuo unatufunulia nini kumhusu Yehova?

Ufufuo unawezekana kwa sababu Mungu alimtuma Mwana wake ili afe kwa ajili yetu. Kwa hiyo, ufufuo ni wonyesho wa upendo na fadhili zisizostahiliwa za Yehova.—Soma Yohana 3:16; Waroma 6:23.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 6 na 7 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Adamu aliumbwa kutokana na mavumbi