Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Faraja kwa Waliovunjika Moyo

Faraja kwa Waliovunjika Moyo

Mkaribie Mungu

Faraja kwa Waliovunjika Moyo

‘YEHOVA hawezi kunipenda.’ Hivyo ndivyo alivyosema mwanamke fulani Mkristo ambaye amepambana na hali ya kushuka moyo kwa muda mrefu sana. Aliamini kwamba lazima Yehova awe mbali sana naye. Je, kweli Yehova yuko mbali na waabudu wake ambao huenda wakawa wameshuka moyo? Jibu lenye kufariji linapatikana katika maneno ambayo mtunga-zaburi Daudi aliongozwa na roho ya Mungu kuandika katika Zaburi 34:18.

Daudi alijua jinsi mwabudu mwaminifu wa Yehova anavyoweza kuathiriwa na mfadhaiko mkubwa. Akiwa kijana, Daudi aliishi kama mkimbizi, akifukuzwa wakati wote na Sauli, mfalme mwenye wivu aliyeazimia kumuua. Daudi alikimbilia sehemu ambayo huenda alifikiri Sauli hangemtafuta. Alikimbilia Gathi, jiji la maadui wa Israeli, lililokuwa katika eneo la Wafilisti. Lakini baada ya kutambuliwa, Daudi aliokoka kifo kwa kujifanya mwenda wazimu. Daudi alimtukuza Mungu kwa kuwa alimwokoa, na kwa sababu hiyo, akaandika Zaburi ya 34.

Je, Daudi aliamini kwamba Mungu yuko mbali na wale ambao kwa sababu ya kuvunjika moyo wanakata tamaa au kuhisi kuwa hawafai mbele Zake? Daudi anaandika: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” (Mstari wa 18) Hebu tuone jinsi maneno hayo yanavyotufariji na kutupa tumaini.

“Yehova yuko karibu.” Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba maneno hayo ni “njia nyingine ya kueleza kwamba Bwana yuko macho na anawalinda watu wake, wakati wote akiwa tayari kuwasaidia na kuwaokoa.” Inatia moyo kujua kwamba Yehova yuko macho kuelekea watu wake. Anaona matatizo yanayowapata katika ‘nyakati hizi za hatari,’ na anajua hisia zao za ndani kabisa.—2 Timotheo 3:1; Matendo 17:27.

“Wale waliovunjika moyo.” Katika tamaduni fulani, “kuvunjika moyo” kunahusianishwa na kupenda mtu asiyekupenda. Lakini maneno ya mtunga-zaburi yanarejelea “ile hali ya kawaida ya kuwa na majonzi na huzuni,” anasema msomi mmoja. Ndiyo, hata waabudu waaminifu wa Mungu wanaweza kupatwa na hali ngumu sana zinazoweza kuwavunja moyo.

“Wale waliopondwa roho.” Watu waliovunjika moyo wanaweza kujihisi kuwa hawafai kabisa na hivyo kukosa tumaini kwa muda. Kitabu fulani kwa ajili ya watafsiri wa Biblia kinasema kwamba maneno hayo yanaweza kumaanisha “wale wasiokuwa na matazamio yoyote mazuri.”

Yehova anawasaidia jinsi gani wale “waliovunjika moyo” na “waliopondwa roho”? Je, anakuwa mbali nao, akiwaona kuwa watu wasiostahili upendo wala uangalifu wake? Bila shaka, hapana! Kama baba mwenye upendo anayemshika na kumfariji mtoto aliyevunjika moyo, Yehova yuko karibu na waabudu wake wanaolilia msaada wake. Anatamani kuwafariji na kutuliza mioyo yao iliyovunjika na roho zao zilizopondeka. Anaweza kuwapa hekima na nguvu za kukabiliana na majaribu yoyote ambayo huenda yakawapata.—2 Wakorintho 4:7; Yakobo 1:5.

Tunakutia moyo ujitahidi kujua jinsi unavyoweza kumkaribia Yehova. Mungu huyu mwenye huruma anaahidi hivi: “Mimi ninakaa . . . pamoja na mtu aliyepondwa na mwenye roho ya unyenyekevu, ili kuipa uhai roho ya watu wa hali ya chini na kuupa uhai moyo wa wale wanaopondwa.”—Isaya 57:15.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Juni (Mwezi wa 6):

Zaburi 26-59