Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Iliandikwa Wakati Gani?

Biblia Iliandikwa Wakati Gani?

Biblia Iliandikwa Wakati Gani?

Biblia ni kitabu cha kipekee. Zaidi ya watu bilioni tatu wanaiona Biblia kuwa maandishi matakatifu. Biblia ndicho kitabu ambacho kimeuzwa kwa wingi zaidi duniani. Inakadiriwa kwamba nakala 6,000,000,000 hivi za Biblia zimechapishwa (ikiwa nzima au kwa sehemu) katika lugha zaidi ya 2,400.

INGAWA Biblia ni kitabu kinachosomwa na watu wengi zaidi kuliko kitabu kingine chochote, watu wana maoni mbalimbali kuhusu wakati ilipoandikwa, hasa Maandiko ya Kiebrania, ambayo mara nyingi yanaitwa Agano la Kale. Huenda umewahi kusoma baadhi ya maoni hayo kwenye vitabu au magazeti, au umewahi kuwatazama wasomi fulani wakifafanua maoni yao kwenye vipindi vya televisheni. Zifuatazo ni baadhi ya taarifa zinazoonyesha maoni mbalimbali kuhusu Biblia katika siku zetu.

“Vitabu vingi vya Biblia viliandikwa kati ya karne ya nane hadi ya sita K.W.K., au, kati ya siku za nabii Isaya na Yeremia.”

“Kwa miaka 200 iliyopita wasomi wa Biblia wamekuwa na maoni ya kwamba Maandiko ya Kiebrania yaliandikwa na kusahihishwa hasa katika enzi za Waajemi na Wagiriki (kati ya karne ya tano na ya pili K.W.K.).”

“Maandishi yote ya Kiebrania kama yalivyo leo yalikuwepo kuanzia wakati wa utawala wa Wagiriki (kati ya karne ya pili hadi ya kwanza [K.W.K.]).”

Mkristo anayeamini kuwa “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu” anapaswa kuyaona jinsi gani maoni hayo yenye kupingana? (2 Timotheo 3:16) Ili kupata jibu, acheni tuchunguze sehemu zote mbili za jambo hilo.

Wakati wa Kuandikwa kwa Biblia

Maandiko ya Kiebrania yana marejeo mengi yanayoonyesha mfuatano wa matukio. Marejeo hayo yanaonyesha kuwa vitabu vya kwanza-kwanza viliandikwa wakati wa Musa na Yoshua, miaka 3,500 hivi iliyopita. * Samweli, Daudi, Sulemani, na wengine waliongezea maandishi mengine katika karne ya 11 K.W.K. Kisha, maandishi ya kihistoria, kishairi, na kinabii yakaandikwa katika ya karne ya tisa na ya tano K.W.K.

Nakala au sehemu za vitabu hivyo vya Biblia, isipokuwa kitabu cha Esta, ni kati ya Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi. Uchunguzi wa kutambua muda ambao hati hizo zimekuwepo kwa kutumia mbinu ya kupima kiasi cha kaboni katika hati za kale na pia mbinu ya paliografia (uchunguzi wa maandishi ya zamani), umethibitisha kwamba baadhi ya hati za zamani zaidi ni za mwaka wa 200 hivi K.W.K.

Maoni ya Wachambuzi

Sababu kuu inayofanya watu watilie shaka wakati wa kuandikwa kwa Biblia ni dai la Biblia yenyewe kuwa imeongozwa na Mungu. Katika kitabu chake The Old Testament Documents, Profesa Walter C. Kaiser, Jr., anaandika hivi kuhusu jambo hilo: “Maandishi hayo [Biblia] hayaaminiki kwa sababu yanadai kuwa yameongozwa na Mungu, na pia kwa sababu yanaeleza kuhusu miujiza na kumhusu Mungu.” Wasomi wasioamini kuwa Biblia iliongozwa na Mungu wanasema kwamba inapaswa kuchunguzwa na kukosolewa kama kitabu kingine chochote.

Kwa muda fulani, fundisho la mageuzi la Darwin lilitumiwa kueleza kwamba dini za wanadamu ziligeuka hatua kwa hatua. Watu walianza kwa kuabudu vitu vya asili, kisha wakaanza kuabudu miungu mingi na mwishowe ibada ya mungu mmoja ikatokea. Kwa kuwa vitabu vya Biblia vya kwanza-kwanza vinaeleza kuhusu ibada ya Mungu mmoja, watu fulani wanasema kwamba ni lazima viwe viliandikwa miaka mingi baadaye, kuliko inavyodaiwa.

Biblia imechambuliwa katika njia mbalimbali kufikia sasa. Kwa mfano, kamusi fulani ya hivi karibuni ya Agano la Kale ina makala zinazochambua maneno yaliyotumika katika Biblia, usahihi wa masimulizi yake kihistoria, na jinsi masimulizi yake yanavyopatana na mapokeo.

Ingawa wasomi wengi wana maoni yanayopingana kuhusu wakati ambapo vitabu vya Biblia viliandikwa, wengi wanaunga mkono maoni ya Profesa R. E. Friedman. Anasema hivi: “Kwa mamia ya miaka, waandishi wa kale waliandika mashairi, sheria, na makala nyinginezo. Kisha, waandishi wakatumia maandishi hayo kama vyanzo vya habari walizotumia kuandika Biblia.”

Kitabu Faith, Tradition, and History kinazungumzia maoni hayo na mengineyo ambayo yanaichambua Biblia. Hata hivyo, kitabu hicho kinasema hivi kwa ufupi: “Ingawa wasomi wanakubaliana kwamba Maandiko hayaaminiki, nao wanaamini kwa dhati maoni yao wenyewe, wao wenyewe wanachambuana sana.”

Hoja Zinazothibitisha Wakati Ambapo Biblia Iliandikwa

Vitabu vya kwanza-kwanza vya Biblia viliandikwa kwenye vifaa vinavyoweza kuharibika. Kwa hiyo, ni jambo lisilopatana na akili kutazamia kwamba maandishi hayo ya kwanza au nakala za mapema za wakati wa Musa, Yoshua, Samweli, au Daudi zinaweza kupatikana. Hata hivyo, inawezekana kuchunguza uthibitisho wa kihistoria usio wa moja kwa moja, unaodokeza kwamba kukubali wakati ambao Biblia yenyewe inataja iliandikwa ni jambo linalopatana na akili, kama ambavyo wasomi na wataalamu fulani wa vitu vya kale wanaoheshimika wamefanya. Uthibitisho huo unatuonyesha nini? Fikiria mifano kadhaa.

Je, maandishi yaliyoandikwa kwa mkono yalikuwepo miaka 3,500 iliyopita katika Mashariki ya Kati, wakati ambao, kulingana na Biblia, Musa na Yoshua waliishi? Maandishi ya kihistoria, kidini, kisheria, na maandishi mengine yaliandikwa katika Mesopotamia na Misri ya kale. Namna gani maandishi ya Musa na ya Waisraeli wengine? Kamusi, Dictionary of the Old Testament: Pentateuch, inajibu: “Hakuna sababu ya kutilia shaka kwamba maandishi yaliyoandikwa kwa mkono yalikuwepo nchini Kanaani mwishoni mwa Enzi ya Shaba [kati ya mwaka wa 1550 na 1200 K.W.K. hivi].” Inaendelea kusema: “Kupatana na desturi za uandishi za zamani, hakuna sababu ya kuwa na shaka kwamba maandishi yanayodaiwa kuwa ya Musa na maandishi mengine ya Kiebrania, yaliandikwa wakati ambao Biblia inasema yaliandikwa.” —Kutoka 17:14; 24:4; 34:27, 28; Hesabu 33:2; Kumbukumbu la Torati 31:24.

Je, waandishi wa Biblia walitumia maandishi ya kale kama marejeo? Ndiyo, wengine wamerejelea ‘vitabu,’ ambavyo huenda vilikuwa hati za serikali, rekodi za ukoo, na hati za kihistoria, na hati nyinginezo za kabila au familia.—Hesabu 21:14; Yoshua 10:13; 2 Samweli 1:18; 1 Wafalme 11:41; 2 Mambo ya Nyakati 32:32.

Kwa nini hakuna hati nyingine zozote za Biblia ambazo ni za kale zaidi kuliko Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi ambazo zimewahi kupatikana? Gazeti Biblical Archaeology Review, linaeleza hivi: “Hati za mafunjo na ngozi hazingeweza kudumu katika maeneo mengi ya Palestina, isipokuwa katika maeneo kame kama vile eneo lililo karibu na Bahari ya Chumvi. Mafunjo na ngozi huoza yakiwa katika udongo wenye unyevunyevu. Kutopatikana kwa hati hizo hakumaanishi kwamba hazikuwepo.” Ukweli ni kwamba mamia ya mihuri ya udongo ambayo ilitumiwa kupiga hati hizo mihuri imepatikana. Hati za mafunjo na ngozi ziliharibika kutokana na moto au udongo wenye unyevunyevu, lakini mihuri ya udongo ipo hadi leo. Mihuri hiyo ilikuwepo kuanzia karne ya tisa hadi ya tano hivi K.W.K.

Hati za Biblia zilihifadhiwa jinsi gani? Kitabu The Bible as It Was, kinaeleza hivi: “Lazima hadithi, zaburi, unabii, na sheria ambazo tunasoma leo kama sehemu ya Biblia ziwe zilinakiliwa tena na tena mara nyingi hata katika kipindi ambacho Biblia yenyewe iliandikwa. . . . Ikiwa maandishi hayo yalinakiliwa mara kadhaa katika kipindi ambacho Biblia yenyewe iliandikwa, jambo hilo linamaanisha kwamba yalikuwa yakitumiwa na yalikuwa muhimu katika maisha ya kila siku. . . . Hakuna mtu ambaye angepoteza wakati wake akinakili maandishi ambayo si muhimu.”—Kumbukumbu la Torati 17:18; Methali 25:1.

Kuhusu vitabu vya kwanza-kwanza vya Biblia, hilo lilimaanisha kwamba vitabu hivyo vilinakiliwa tena na tena katika kipindi cha miaka 1,500 hivi hadi karne ya kwanza W.K. Kazi hiyo ya kunakili kwa usahihi ilitia ndani “kubadili sarufi na maneno yaliyopitwa na wakati, kazi iliyofanywa kotekote katika Mashariki ya Karibu ya kale,” kinasema kitabu On the Reliability of the Old Testament. * Jambo hilo linafanya tusiamini uchambuzi unaotegemea mbinu na mtindo wa uandishi wa vitabu hivyo.

Biblia Iliandikwa Wakati Gani?

Je, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba kutopatikana kwa maandishi ya kale kama ya Musa, Yoshua, Samweli, na wengineo, kunaonyesha kwamba vitabu vya Biblia havikuandikwa miaka ya mapema kama inavyodaiwa? Wasomi wengi wanakubali kwamba kwa kuwa hati za kale hazipatikani, huo si uthibitisho wa kwamba hazikuwepo. Kwa kweli, ni hati ngapi zilizotengenezwa kwa vifaa vinavyoweza kuharibika ambazo zingeweza kuhifadhiwa? Kwa mfano, mtaalamu K. A. Kitchen, anayefanya uchunguzi kuhusu Misri ya kale, alisema kwamba karibu hati zote za mafunjo za Misri zilizoandikwa kabla ya utawala wa Wagiriki na Waroma zimeharibika.

Huenda watu wanaoheshimu Biblia wakajiuliza, ‘Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu Maandiko ya Kiebrania?’ Wakati huo, hakukuwa na ubishi wowote kuhusu wakati ambapo Biblia iliandikwa. Yesu, kama tu Wayahudi wengine, aliamini habari kuhusu mfuatano wa matukio katika Biblia. Je, alikubali kwamba vitabu vya kwanza-kwanza vya Biblia viliandikwa na wale wanaotajwa kuwa waliviandika?

Yesu alirejelea maandishi ya Musa. Kwa mfano, alitaja “kitabu cha Musa.” (Marko 12:26; Yohana 5:46) Alirejelea masimulizi ya kitabu cha Mwanzo (Mathayo 19:4, 5; 24:37-39); Kutoka (Luka 20:37); Mambo ya Walawi (Mathayo 8:4); Hesabu (Mathayo 12:5); na Kumbukumbu la Torati (Mathayo 18:16). Alisema hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa katika sheria ya Musa na katika Manabii na Zaburi juu yangu lazima yatimizwe.” (Luka 24:44) Ikiwa alikubali kwamba Musa na waandishi wengine ndio walioandika vitabu vya kwanza-kwanza vya Biblia, basi, ni wazi kuwa alikubali kwamba habari kuhusu mfuatano wa matukio ya Maandiko ya Kiebrania ni sahihi.

Basi, Biblia iliandikwa wakati gani? Je, habari zilizo katika Biblia kuhusu wakati ambapo Biblia iliandikwa zinategemeka? Tumechunguza maoni ya wasomi wengi wanaochambua Biblia na vilevile habari zilizo katika Biblia yenyewe, uthibitisho wa kihistoria usio wa moja kwa moja, na maoni ya Yesu. Kwa kutegemea hayo, je, jibu lako litaonyesha kuwa unakubaliana na maneno ya Yesu aliposali kwa Baba yake, Yehova Mungu: “Neno lako ni kweli”?—Yohana 17:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ukitaka kujifunza mengi zaidi kuhusu mfuatano wa matukio ya Biblia, ona kitabu Insight on the Scriptures, Buku la 1 ukurasa wa 447-467 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 1 ukurasa wa 451-470, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 23 Ona makala yenye kichwa “Waandishi wa Zamani na Neno la Mungu” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2007 (15/3/2007), ukurasa wa 18-20.

[Chati/​Picha katika ukurasa wa 20-23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

(Mfuatano wa matukio unaoonyesha miaka ambayo uandikaji wa vitabu vya Biblia ulikamilika)

2000 K.W.K.

1800

[Picha]

Waandishi Wamisri walikuwa wameandika maandishi fulani hata kabla ya wakati wa Musa

[Hisani]

© DeA Picture Library/Art Resource, NY

1600

[Picha]

Musa alimaliza kuandika kitabu cha Mwanzo kufikia mwaka wa 1513 K.W.K., kwenye vifaa vinavyoweza kuharibika

Mwanzo 1513 K.W.K.

Yoshua

1400

1200

Samweli

1000 K.W.K.

[Picha]

Mamia ya mihuri ya udongo inapatikana hata leo

Kuanzia mwaka wa 900 hadi 500 K.W.K.

Yona

800

Isaya

600

Yeremia

Danieli

[Picha]

Hati ya kukunjwa iliyotengenezwa kwa mafunjo na iliyofungwa kwa uzi na kuwekwa mhuri wa udongo

Kuanzia mwaka wa 449 K.W.K.

[Hisani]

Brooklyn Museum, Bequest of Theodora Wilbour from the collection of her father, Charles Edwin Wilbour

400

200

[Picha]

Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vilifunikwa kwa kitani na kuhifadhiwa ndani ya mitungi. Hayo ndiyo maandishi ya Biblia ya kale zaidi yanayopatikana leo

Viliandikwa katika mwaka wa 200 hivi K.W.K.

[Hisani]

Shrine of the Book, Photo © The Israel Museum, Jerusalem