Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kimalagasi Kilisikika Kama Muziki Mtamu

Kimalagasi Kilisikika Kama Muziki Mtamu

Barua Kutoka Madagaska

Kimalagasi Kilisikika Kama Muziki Mtamu

MIMI na mume wangu tulikuwa tumepata mgawo mpya wa umishonari wa kwenda kisiwani Madagaska. Tuliwaaga rafiki zetu na watu wa familia yetu huku tukijizuia tusitokwe na machozi. Tulikuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia kufaulu katika mgawo wetu.

Hata hivyo, hatutasahau mkutano wa kwanza wa Kikristo tuliohudhuria kisiwani Madagaska. Ndugu aliyeongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi alionekana kana kwamba anaongoza kikundi cha wanamuziki. Kwa kuwa hatukuelewa Kimalagasi, watu walipozungumza maneno yao yalikuwa kama muziki mtamu. Ingetuchukua muda mrefu kuelewa vizuri yale waliyokuwa wakisema.

Mara ya kwanza nilipoelewa swali fulani la ziada lililoulizwa, nilijipata nimelijibu kwa sauti kubwa kimakosa. Wale waliokuwa wameketi karibu nami walisikia, na nilihitaji kujizuia nisicheke. Ingawa niliona aibu, nilifurahi kwa sababu angalau nilikuwa nimeelewa kilichokuwa kimesemwa.

Badala ya kuwawekea wengine mfano katika utumishi, nilihisi kwamba mimi ndiye niliyekuwa nikisaidiwa. Ndugu na dada walinionyesha kwa upendo jinsi ya kuwahubiria watu kwa njia inayoeleweka, wakinieleza mambo ya kusema na maandiko ya kusoma.

Nakumbuka siku moja nilipokuwa nikihubiri, mtoto mmoja alianza kuniita, “Vazaha! Vazaha!” Hili ni neno la Kimalagasi linalotumiwa sana kumaanisha “mgeni.” Tulianza kutembea haraka-haraka tukitumaini kwamba hakuna watoto zaidi ambao wangejiunga naye kuendelea kuniita hivyo. Kisha mvulana fulani akamkemea mtoto huyo. Alimwambia, “Huyu si mgeni, anaweza kuongea lugha yetu!” Dada niliyekuwa naye alinifasiria yale ambayo walisema kwa sababu waliongea haraka sana hivi kwamba singeweza kuwaelewa. Lakini, nilifurahi kwamba nilikuwa nimefanya maendeleo fulani. Mwishowe, nilianza kuhisi kama Madagaska ni nyumbani.

Mara kadhaa nilipojihisi mpweke, nilitiwa moyo wakati watoto waliponionyesha kwamba wananipenda kwa kunishika mkono na kutabasamu hata ingawa hatungeweza kuwasiliana vizuri. Watoto kutanikoni ni baraka kubwa kutoka kwa Yehova. Dada mmoja mdogo anayeitwa Hasina, amekuwa mfasiri wangu. Wakati hakuna mtu anayenielewa, yeye anaelewa ninachosema. Mara kwa mara yeye hunisaidia wakati ninapojaribu kuwasiliana na rafiki zangu kutanikoni, kwa kuwasaidia kuelewa yale ninayosema.

Mimi na mume wangu tulikuwa katika kutaniko fulani ambalo lilikuwa karibu kugawanywa na kuwa makutaniko mawili. Hilo lilimaanisha kwamba wanafunzi fulani wa Biblia walihitaji kupewa ndugu wengine kwa sababu wanafunzi hao waliishi katika eneo la kutaniko jipya. Dada mmoja aliniomba nijifunze Biblia na mwanafunzi wake. Niliogopa na kumwambia kwamba sikuwa tayari, lakini akanisihi nijifunze na mwanafunzi huyo. Alinihakikishia kwamba kwa msaada wa Yehova nitafanikiwa. Alinitazama kwa huruma na fadhili, na kwa kutumia maneno rahisi awezavyo, akanieleza kwamba hivi karibuni nitakuwa na uwezo wa kufundisha wengine jinsi ambavyo ningependa. Maneno hayo yalinitia moyo sana.

Tangu wakati huo mwanafunzi huyo ameendelea vizuri. Siku moja nilipokuwa nje, nilisikia akiniita. Yeye na mume wake walikuwa wakienda kuhalalisha ndoa yao. Mume wake ameanza kujifunza Biblia, na wamejiwekea miradi fulani ambayo wanajaribu kuitimiza, kutia ndani mradi wa kubatizwa. Jambo hilo lilinifurahisha, ingawa ninajua kwamba Yehova ndiye anayewavuta watu kwake.

Tumejifunza mambo mengi katika mgawo wetu mpya. Ingawa tunawakosa rafiki zetu tuliowaacha nyumbani, tunahisi kana kwamba hatukuwaacha kabisa. Mara nyingi sisi huwaeleza akina ndugu na dada wa Madagaska kuwahusu, nao rafiki zetu wa nyumbani hutuuliza kuhusu jinsi ndugu hawa wanavyoendelea. Tunatazamia kwa hamu wakati ambapo rafiki zetu wote, wa hapa Madagaska na hata wale wa nyumbani, watakutana.

Watu wanapoongea, bado mimi ninasikia kama wanaimba. Lakini sasa ninaelewa yale wanayosema. Ninangoja kwa hamu wakati nitakapokuwa na uwezo wa kuongea vizuri kama wengine, badala ya kutaja maneno haraka-haraka bila mpangilio. Yesu alisema: “Msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.” (Mathayo 6:34) Kwa hiyo, tutaendelea kujifunza neno moja baada ya lingine. Na kwa sasa, nitaendelea kutega sikio langu, kutayarisha akili yangu, na moyo wangu ili niweze kufanya kazi bega kwa bega na ndugu na dada zangu wenye upendo na uvumilivu hapa Madagaska.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikihubiri na Hasina