Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kuna Habari Njema Ambayo Watu Wote Wanahitaji

Kuna Habari Njema Ambayo Watu Wote Wanahitaji

Kuna Habari Njema Ambayo Watu Wote Wanahitaji

“Habari njema . . . kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu.”—ROM. 1:16.

1, 2. Kwa nini unahubiri “habari njema ya ufalme,” na unakazia mambo gani kuhusu habari hiyo?

 ‘NINAFURAHI kuwahubiria watu habari njema kila siku.’ Inaelekea kwamba umewahi kusema au kufikiria maneno hayo. Ukiwa Shahidi wa Yehova ambaye amejitoa, unajua jinsi lilivyo jambo la maana kuhubiri “hii habari njema ya ufalme.” Labda unaweza kusema kutoka akilini unabii wa Yesu kuhusu kufanya kazi hiyo.—Mt. 24:14.

2 Unapohubiri “habari njema ya ufalme,” unaendelea kufanya kazi ambayo Yesu alianzisha. (Soma Luka 4:43.) Bila shaka, jambo moja ambalo unakazia ni kwamba hivi karibuni Mungu ataingilia kati ya mambo ya wanadamu. Kupitia ile “dhiki kuu,” atamaliza dini ya uwongo na kuondoa uovu wote duniani. (Mt. 24:21) Huenda pia unakazia kwamba Ufalme wa Mungu utarudisha tena Paradiso duniani ili amani na furaha isitawi. Kwa kweli, “habari njema ya ufalme” ni sehemu ya “habari njema [iliyotangazwa] kimbele kwa Abrahamu, yaani: ‘Kupitia kwako mataifa yote yatabarikiwa.’”—Gal. 3:8.

3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba mtume Paulo alikazia habari njema katika kitabu cha Waroma?

3 Je, inawezekana kwamba huenda hatukazii sana jambo fulani la maana kuhusu habari njema ambalo watu wanahitaji? Katika barua yake kwa Waroma, mtume Paulo alitumia neno “ufalme” mara moja tu, lakini alitumia maneno “habari njema” mara 12. (Soma Waroma 14:17.) Ni jambo gani kuhusu habari njema ambalo Paulo alitaja mara nyingi katika kitabu hicho? Kwa nini jambo hilo kuhusu habari njema ni la maana sana? Na kwa nini tunapaswa kukumbuka jambo hilo tunapowahubiria watu “habari njema ya Mungu” katika eneo letu?—Marko 1:14; Rom. 15:16; 1 The. 2:2.

Jambo Ambalo Watu Walioishi Huko Roma Walihitaji

4. Paulo alihubiri kuhusu nini alipokuwa amefungwa kwa mara ya kwanza huko Roma?

4 Tunajifunza mengi tunapochunguza mambo ambayo Paulo alizungumzia alipofungwa kwa mara ya kwanza huko Roma. Tunasoma kwamba alipotembelewa na kikundi cha Wayahudi, ‘alitoa ushahidi kamili kuhusiana na (1) ufalme wa Mungu na kutumia ushawishi kwao kuhusu (2) Yesu.’ Matokeo yalikuwa nini? “Wengine wakaanza kuamini mambo yaliyosemwa; wengine hawakuamini.” Baada ya hapo, Paulo alikuwa ‘akiwakaribisha kwa fadhili wale wote walioingia ndani kwake, akiwahubiria (1) ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu (2) Bwana Yesu Kristo.’ (Mdo. 28:17, 23-31) Ni wazi kwamba Paulo alikazia Ufalme wa Mungu. Lakini ni jambo gani lingine ambalo alikazia? Jambo fulani la msingi kuhusiana na Ufalme, yaani, daraka la Yesu katika kusudi la Mungu.

5. Ni uhitaji gani hasa ambao Paulo alizungumzia katika kitabu cha Waroma?

5 Watu wote wanahitaji kumjua Yesu na kumwamini. Katika kitabu cha Waroma, Paulo alizungumzia uhitaji huo. Kabla ya hapo, aliandika kuhusu “Mungu, ambaye ninamtolea utumishi mtakatifu kwa roho yangu kuhusiana na ile habari njema juu ya Mwana wake.” Aliongezea hivi: “Siionei aibu habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani.” Baadaye alizungumza kuhusu wakati “Mungu anapohukumu kupitia Kristo Yesu mambo ya siri ya wanadamu, kulingana na habari njema ninayoitangaza.” Na akasimulia hivi: “Kutoka Yerusalemu na kuzunguka mpaka Ilirikamu nimehubiri kikamili habari njema juu ya Kristo.” * (Rom. 1:9, 16; 2:16; 15:19) Unafikiri ni kwa nini Paulo alikazia habari kuhusu Yesu Kristo alipowaandikia Waroma?

6, 7. Tunaweza kusema nini kuhusu kuanzishwa kwa kutaniko la Roma na kuhusu watu waliokuwa katika kutaniko hilo?

6 Hatujui jinsi kutaniko la Roma lilivyoanzishwa. Je, Wayahudi au watu waliogeuzwa imani ambao walikuwapo wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. walirudi Roma wakiwa Wakristo? (Mdo. 2:10) Au je, wafanyabiashara na wasafiri waliokuwa Wakristo ndio walioeneza kweli huko Roma? Kwa vyovyote vile, Paulo alipoandika kitabu hicho, karibu mwaka wa 56 W.K., tayari kutaniko hilo lilikuwa limeanzishwa muda mrefu kabla ya mwaka huo. (Rom. 1:8) Kutaniko hilo lilikuwa na watu wa aina gani?

7 Wengine wao walikuwa na asili ya Kiyahudi. Paulo anawasalimu Androniko na Yunia akiwaita “jamaa zangu,” inaelekea anamaanisha watu wa ukoo ambao walikuwa Wayahudi wenzake. Akila aliyekuwa akitengeneza mahema huko Roma pamoja na mke wake Prisila, alikuwa pia Myahudi. (Rom. 4:1; 9:3, 4; 16:3, 7; Mdo. 18:2) Lakini inaelekea kwamba ndugu na dada wengi ambao Paulo aliwatumia salamu walikuwa Watu wa Mataifa. Huenda wengine wao walikuwa watu “wa nyumbani mwa Kaisari,” labda ikimaanisha watumwa na maofisa wa cheo cha chini wa Kaisari.—Flp. 4:22; Rom. 1:6; 11:13.

8. Watu waliokuwa huko Roma walikuwa katika hali gani ngumu?

8 Kila Mkristo huko Roma alikuwa katika hali ngumu na kila mmoja wetu pia yuko katika hali hiyo. Paulo alieleza hivi hali hiyo: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rom. 3:23) Ni wazi kwamba watu wote ambao Paulo aliwaandikia walihitaji kutambua kwamba walikuwa watenda-dhambi na walipaswa kuwa na imani katika njia ya Mungu ya kutimiza uhitaji huo.

Kutambua Tatizo la Dhambi

9. Paulo alikazia matokeo gani ambayo yanaweza kuletwa na habari njema?

9 Mapema katika barua kwa Waroma, Paulo alitaja kuhusu matokeo mazuri ajabu ambayo yangetokana na habari njema ambayo alitaja mara nyingi: “Siionei aibu habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani, kwa Myahudi kwanza na pia kwa Mgiriki.” Ndiyo, watu wangeweza kuokolewa. Hata hivyo, imani ilihitajiwa, kulingana na kweli muhimu inayotegemea Habakuki 2:4: “Mwadilifu—ataishi kwa njia ya imani.” (Rom. 1:16, 17; Gal. 3:11; Ebr. 10:38) Lakini hiyo habari njema, ambayo inaweza kufanya mtu aokolewe, inahusiana jinsi gani na ukweli wa kwamba “wote wamefanya dhambi”?

10, 11. Kwa nini jambo linalotajwa katika Waroma 3:23 si jipya kwa watu fulani lakini ni jipya kwa wengine?

10 Kabla mtu hajasitawisha imani inayoweza kuokoa uhai wake, ni lazima akubali kwamba yeye ni mtenda-dhambi. Hilo si wazo jipya kwa wale ambao tangu utotoni wamemwamini Mungu na kujua Biblia kwa kiasi fulani. (Soma Mhubiri 7:20.) Iwe wanakubali au wana mashaka, hata hivyo, wanajua kwa kadiri fulani Paulo alimaanisha nini aliposema: “Wote wamefanya dhambi.” (Rom. 3:23) Lakini, tunapoendelea kutimiza huduma yetu, tunaweza kukutana na watu ambao hawaelewi maneno hayo.

11 Katika nchi fulani, tangu utotoni mtu wa kawaida hafundishwi kwamba alizaliwa akiwa mwenye dhambi, na kwamba alirithi dhambi. Ni kweli kwamba huenda akatambua kuwa anakosea, ana tabia zisizopendeza, na huenda amefanya mambo fulani mabaya. Na anaona kwamba watu wengine wako katika hali kama yake. Hata hivyo, kwa sababu ya malezi yake, haelewi kwa kweli ni kwa nini yeye na wengine wako hivyo. Hata katika lugha fulani, ukisema kwamba mtu ni mtenda-dhambi, huenda wengine wakafikiri unasema kwamba mtu huyo ni mhalifu au amevunja sheria fulani. Bila shaka, huenda isiwe rahisi kwa mtu anayelelewa katika mazingira kama hayo kufikiri kwamba yeye ni mtenda-dhambi kwa njia ambayo Paulo alimaanisha.

12. Kwa nini watu wengi hawaamini kwamba wanadamu wote ni watenda-dhambi?

12 Hata katika nchi zinazodai kuwa za Kikristo, watu wengi hawaamini kwamba wao ni watenda-dhambi. Kwa nini? Hata kama wanaenda kanisani mara kwa mara, wanaona simulizi la Biblia kuhusu Adamu na Hawa kuwa hadithi tu. Wengine wanalelewa katika mazingira ambayo watu hawaamini kwamba kuna Mungu. Hivyo, wana shaka kuhusu kuwapo kwa Mungu na hawaelewi kwamba Mtu Mkuu Kuliko Wote aliwawekea wanadamu viwango vya maadili na kwamba kutofuata viwango hivyo ni dhambi. Kwa njia fulani, wao ni kama watu walioishi katika karne ya kwanza ambao Paulo alisema kwamba ‘hawakuwa na tumaini’ na ‘walikuwa bila Mungu katika ulimwengu.’—Efe. 2:12.

13, 14. (a) Ni sababu gani moja inayofanya wale wasioamini kwamba kuna Mungu na pia dhambi wasiweze kujitetea? (b) Kutoamini kwamba kuna Mungu na pia dhambi kumewaongoza watu wengi kufanya nini?

13 Katika barua kwa Waroma, Paulo alitoa sababu mbili zinazoonyesha kwa nini malezi kama hayo hayawezi kuwa kisingizio leo na hata wakati wa zamani. Sababu ya kwanza ni kuwa uumbaji wenyewe unatoa ushahidi wa kwamba kuna Muumba. (Soma Waroma 1:19, 20.) Hilo linapatana na maneno ambayo Paulo alisema alipowaandikia Waebrania akiwa huko Roma: “Kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Ebr. 3:4) Hata hivyo, sababu aliyotoa inaonyesha kwamba kuna Muumba aliyeujenga, au kuutokeza, ulimwengu wote mzima.

14 Kwa hiyo, Paulo alikuwa na sababu nzuri ya kuwaandikia Waroma kwamba mtu yeyote ‘hakuwa na sababu ya kujitetea,’ kutia ndani Waisraeli wa kale ambao waliabudu sanamu zisizo na uhai. Inaweza kusemwa hivyo pia kuhusu wale ambao walijiingiza katika mwenendo mpotovu kingono kinyume cha matumizi ya asili ya mwili wa mwanamume na mwanamke. (Rom. 1:22-27) Akirejelea sababu kama hizo, kwa kufaa Paulo alikata kauli kwamba “Wayahudi na vilevile Wagiriki wote wako chini ya dhambi.”—Rom. 3:9.

‘Mtoa Ushahidi’

15. Ni nani ambao wana dhamiri, na hilo lina matokeo gani?

15 Kitabu cha Waroma kinataja sababu nyingine ambayo inapaswa kuwafanya watu watambue kwamba wao ni watenda-dhambi na wanahitaji msaada ili watoke katika hali hiyo ngumu. Kuhusu sheria ambazo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale, Paulo aliandika hivi: “Wale wote waliofanya dhambi chini ya sheria watahukumiwa kwa sheria.” (Rom. 2:12) Akiendelea kutoa sababu zake, anasema kwamba mara nyingi vikundi vya jamii au watu wa mataifa ambao hawajui sheria za Mungu ‘wanafanya kwa asili mambo ya sheria.’ Kwa nini watu kama hao kwa kawaida wanapinga ngono kati ya watu wa ukoo, kuua, na kuiba? Paulo alitaja sababu: Wana dhamiri.—Soma Waroma 2:14, 15.

16. Kwa nini kuwa na dhamiri hakumaanishi kwamba mtu ataepuka dhambi?

16 Hata hivyo, inaelekea umeona kwamba kuwa na dhamiri inayofanya kazi kama mtoa ushahidi ndani yetu hakumaanishi kwamba mtu atafuata mwongozo wa dhamiri hiyo. Mfano wa Waisraeli wa kale unaonyesha jambo hilo. Ingawa Waisraeli walikuwa na dhamiri waliyopewa na Mungu na sheria zilizo wazi kutoka kwa Mungu ambazo zilikataza kuiba na kufanya uzinzi, mara nyingi walipuuza dhamiri zao na wakavunja Sheria ya Yehova. (Rom. 2:21-23) Walikuwa na hatia mara mbili na hivyo bila shaka wakawa watenda-dhambi, na kushindwa kufuata viwango vya Mungu na mapenzi yake. Hilo liliharibu kabisa uhusiano wao na Muumba wao.—Law. 19:11; 20:10; Rom. 3:20.

17. Tunatiwa moyo jinsi gani na kitabu cha Waroma?

17 Huenda mambo ambayo tumechunguza katika kitabu cha Waroma yakafanya mtu afikiri kwamba wanadamu wana hali yenye kuhuzunisha sana mbele za Mweza-Yote, kutia ndani sisi. Hata hivyo, Paulo hakuachia hapo. Akitaja maneno ya Daudi katika Zaburi 32:1, 2, mtume huyo aliandika hivi: “Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa na ambao dhambi zao zimefunikwa; mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hatahesabu dhambi yake kamwe.” (Rom. 4:7, 8) Ndiyo, Mungu amepanga njia nzuri ya kisheria ya kusamehe dhambi.

Habari Njema Iliyokazia Yesu

18, 19. (a) Katika katibu cha Waroma, Paulo alikazia fikira jambo gani kuhusu habari njema? (b) Tunapaswa kutambua nini ili tupate baraka za Ufalme?

18 Kwa kufaa huenda ukasema hivi: “Kwa kweli hiyo ni habari njema!” Bila shaka hiyo ni habari njema, na hilo linaturudisha kwenye jambo fulani kuhusu habari njema ambalo Paulo alikazia katika kitabu cha Waroma. Kama ilivyotajwa, Paulo aliandika hivi: “Siionei aibu habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu.”—Rom. 1:15, 16.

19 Hiyo habari njema ilikazia daraka la Yesu katika kutimiza kusudi la Mungu. Paulo alitazamia ‘siku ambayo Mungu atahukumu kupitia Kristo Yesu mambo ya siri ya wanadamu, kulingana na habari njema.’ (Rom. 2:16) Aliposema hivyo, hakuwa akipunguza uzito wa “ufalme wa Kristo na wa Mungu” au mambo ambayo Mungu atafanya kupitia Ufalme. (Efe. 5:5) Lakini alionyesha kwamba ili tuishi na kufurahia baraka ambazo zitaletwa na Ufalme wa Mungu, ni lazima tutambue (1) hali yetu tukiwa watenda-dhambi machoni pa Mungu na (2) kwa nini tunahitaji kuwa na imani katika Yesu Kristo ili dhambi zetu zisamehewe. Mtu anapoelewa na kukubali mambo hayo kuhusu kusudi la Mungu na kuona hali ambazo atafurahia wakati ujao, anaweza kwa kufaa kusema hivi: “Kwa kweli, hiyo ni habari njema!”

20, 21. Katika huduma yetu, kwa nini tunapaswa kukumbuka habari njema inayokaziwa katika kitabu cha Waroma, na tunaweza kupata matokeo gani?

20 Bila shaka, tunapaswa kukumbuka jambo hilo kuhusu habari njema tunapoendelea na huduma yetu ya Kikristo. Akizungumza kuhusu Yesu, Paulo alinukuu maneno ya Isaya: “Yeyote anayemwamini hatakata tamaa.” (Rom. 10:11; Isa. 28:16) Huenda ujumbe wa msingi kumhusu Yesu usiwe mpya kwa wale ambao wanaelewa mambo ambayo Biblia inasema kuhusu dhambi. Hata hivyo, kwa wengine, ujumbe huo ni mpya kabisa, jambo ambalo halijulikani au ambalo kwa kawaida watu hawaliamini katika jamii zao. Watu kama hao wanapomwamini Mungu na kuamini Maandiko, tutahitaji kueleza daraka la Yesu. Habari inayofuata itazungumzia jinsi Waroma sura ya 5 inavyoeleza jambo hilo kuhusu habari njema. Huenda utaona kwamba funzo hilo litakusaidia katika huduma yako.

21 Ni jambo lenye kuthawabisha kama nini kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu kuelewa habari njema inayotajwa tena na tena katika kitabu cha Waroma, habari njema ambayo ‘kwa kweli, ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani.’ (Rom. 1:16) Mbali na kuthawabishwa kwa njia hiyo, tutaona wengine wakikubaliana na maneno ambayo Paulo alinukuu katika Waroma 10:15: “Jinsi ilivyo yenye kupendeza miguu ya wale wanaotangaza habari njema ya mambo mema!”—Isa. 52:7.

[Maelezo ya Chini]

^ Maneno kama hayo yanapatikana katika vitabu vingine vilivyoandikwa chini ya mwongozo wa roho ya Mungu.—Marko 1:1; Mdo. 5:42; 1 Kor. 9:12; Flp. 1:27.

Je, Unakumbuka?

• Kitabu cha Waroma kinakazia jambo gani kuhusu habari njema?

• Ni jambo gani la hakika ambalo tunahitaji kuwasaidia wengine kuelewa?

• “Habari njema juu ya Kristo” inaweza jinsi gani kumaanisha baraka kwetu na kwa wengine?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Habari njema inayokaziwa katika Waroma ilihusu daraka la maana la Yesu katika kusudi la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 9]

Sisi sote tulizaliwa na kasoro inayosababisha kifo, yaani, dhambi!