Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Kweli Abrahamu Alikuwa na Ngamia?

Je, Kweli Abrahamu Alikuwa na Ngamia?

Je, Kweli Abrahamu Alikuwa na Ngamia?

BIBLIA inasema kwamba ngamia walikuwa kati ya wanyama wa kufugwa ambao Farao alimpa Abrahamu. (Mwa. 12:16) Mtumishi wa Abrahamu alipofunga safari ndefu kwenda Mesopotamia, ‘alichukua ngamia kumi kutoka kwa ngamia za bwana wake.’ Kwa hiyo, Biblia inasema waziwazi kwamba Abrahamu alikuwa na ngamia mwanzoni mwa mwaka wa 2000 K.W.K.—Mwa. 24:10.

Watu wengine hawakubali hivyo. Kitabu kimoja (New International Version Archaeological Study Bible) kinasema hivi: “Wasomi wamebishana kuhusu usahihi wa kihistoria wa habari hiyo kuhusu ngamia kwa sababu wengi wao wanaamini kwamba wanyama hao walianza tu kufugwa katika sehemu nyingi karibu mwaka wa 1200 K.K., miaka mingi baada ya siku za Abrahamu.” Kwa hiyo, inaweza kuonekana kwamba maandiko yoyote ya Biblia yaliyotaja ngamia si sahihi kwa sababu ngamia hawakutumiwa hivyo katika vipindi vinavyotajwa katika masimulizi hayo ya Biblia.

Hata hivyo, wasomi wengine wanadai kwamba ingawa ngamia walianza kufugwa kwa wingi karibu mwisho wa miaka elfu mbili ya kwanza K.W.K., hilo halimaanishi kwamba ngamia hawakutumiwa kabla ya hapo. Kitabu kimoja (Civilizations of the Ancient Near East) kinasema hivi: “Utafiti wa hivi karibuni unaonyesha kwamba ngamia walifugwa kusini-mashariki mwa Arabia kabla ya mwaka wa 3000 hivi [K.W.K.]. Mwanzoni, huenda ngamia hao walifugwa kwa sababu ya maziwa yao, manyoya, ngozi, na nyama, lakini labda muda si muda watu waligundua kwamba wangeweza kuwatumia ngamia kubeba mizigo.” Inaonekana kwamba vipande vya mifupa na mabaki mengine ya vitu vya kale yanaunga mkono wazo la kuwapo kwa ngamia kabla ya siku za Abrahamu.

Maandishi ya kale yanaunga pia mkono jambo hilo. Kitabu hichohicho kinasema hivi: “Huko Mesopotamia, maandishi ya kale yanataja kiumbe huyo [ngamia] na mihuri mingi ina picha yake, kuonyesha kwamba huenda mnyama huyo alifika Mesopotamia baada ya mwaka wa 1000 K.W.K.,” yaani, kufikia wakati wa Abrahamu.

Wasomi fulani wanaamini kwamba wafanyabiashara wa uvumba kutoka Arabia Kusini walitumia ngamia kusafirisha vitu vyao kaskazini kupitia jangwani, kuelekea katika maeneo kama vile Misri na Siria na hivyo wakaanzisha ufugaji wa ngamia katika maeneo hayo. Labda biashara hiyo ilikuwa imeenea sana mwanzoni mwa mwaka wa 2000 K.W.K. Kwa kweli, andiko la Mwanzo 37:25-28 linawataja wafanyabiashara Waishmaeli ambao walitumia ngamia kusafirisha uvumba mpaka Misri karibu miaka 100 baada ya siku za Abrahamu.

Labda ngamia hawakutumiwa sana zamani katika Mashariki ya Karibu baada ya mwaka wa 1000 K.W.K., lakini uthibitisho unaonyesha kwamba ngamia walijulikana kwa kadiri fulani katika eneo hilo. Hivyo, kitabu kimoja cha utafiti (The International Standard Bible Encyclopedia) kinakata kauli hivi: “Hakuna tena haja ya kuona kwamba masimulizi yanayotaja ngamia katika nyakati za wazee wa ukoo si sahihi, kwa kuwa kuna mambo mengi ya kale yanayoonyesha kwamba ngamia walifugwa kabla ya nyakati za wazee wa ukoo.”