Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Maisha Yana Maana Yoyote?

Je, Maisha Yana Maana Yoyote?

Je, Maisha Yana Maana Yoyote?

“JE, MAISHA yana maana yoyote?” Watu wengi wameuliza swali hilo. Jambo la kusikitisha ni kwamba hata wawe na maoni gani kuhusu maisha, wengi wao hawawezi kuepuka kile mtaalamu wa mfumo wa neva kutoka Australia, Viktor E. Frankl, anaeleza kuwa “hali ya kuhisi kwamba maisha hayana maana na ni ubatili.”

Kwa nini watu wengi wanahisi hivyo? Sababu moja ni kwamba mamilioni ya watu kotekote ulimwenguni wanaishi katika hali mbaya sana na zenye kusikitisha. Kila siku wanakabili umaskini, magonjwa, jeuri isiyo na sababu, na ukandamizaji. Kwa kweli, wanahisi kwamba maisha yao ‘yamejaa msukosuko,’ kama Ayubu wa kale alivyosema kuhusu mateso ya wanadamu. (Ayubu 14:1) Hangaiko lao kuu katika maisha ni kupata mahitaji yao ya siku baada ya siku.

Wakati huohuo, mamilioni ya wengine wanafurahia utajiri na usalama wa kadiri fulani. Inaonekana kwamba wana kila kitu kinachohitajika ili kuwa na furaha maishani. Lakini sivyo ilivyo kwa wengi. Kwa nini? Kwa sababu mara kwa mara, “taabu na mambo yenye kuumiza”—matatizo ya kifedha yasiyotazamiwa au misiba yenye kuumiza kama vile kifo cha mtoto—hukatiza matumaini na ndoto zao.—Zaburi 90:10.

Kuna jambo lingine linalofanya watu wahisi kwamba maisha “hayana maana na ni ubatili.” Ni jambo gani hilo? Ufupi wa maisha. Kwa wengi, ni jambo lisilopatana na akili kwamba wanadamu wanaishi maisha mafupi sana ingawa wana uwezo wa kutimiza mambo mengi makubwa. Hawawezi kuelewa ukweli ambao sote tunakabili: Hata kama tutaepuka misiba mikubwa inayowapata wanadamu, mwishowe tutakufa tu.—Mhubiri 3:19, 20.

Je, Maisha Yatakosa Maana Sikuzote?

Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alieleza waziwazi jambo hilo. Alitazama jinsi watu katika siku zake walivyofanya kazi kwa bidii wakitumia vipawa na uwezo wao katika kupanda mashamba yao, kupalilia, kujenga, na kutunza familia zao, kama vile tu tunavyofanya leo. Hivyo, akauliza, ‘Watu wanapata faida gani?’ Alifikia mkataa wa kwamba kila kitu ambacho watu wanafanya ni “ubatili na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 2:17.

Lakini, je, Mfalme Sulemani aliamini kwamba kila kitu ambacho wanadamu wanafanya kingekuwa “ubatili na kufuatilia upepo” sikuzote? Hapana. Alikuwa tu akieleza mambo halisi yanayotokea maishani katika ulimwengu huu. Hata hivyo, Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linatuhakikishia kwamba maisha hayataendelea kuwa jinsi yalivyo sasa!

Unaweza kupata uhakika huo jinsi gani? Tafadhali soma makala mbili zinazofuata. Zinaweza kukusaidia kuelewa kwa nini maisha yaonekana kuwa yasiyo na maana, jinsi hali hiyo itakavyorekebishwa, na unayoweza kufanya ili maisha yako yawe na maana hata sasa.