Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha Yenye Maana Sasa na Milele

Maisha Yenye Maana Sasa na Milele

Maisha Yenye Maana Sasa na Milele

MAISHA yako yanaweza kuwa na maana hata sasa. Jinsi gani? Kwa kufuata kanuni zenye hekima zinazopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Acheni tuchunguze baadhi ya kanuni hizo.

KANUNI YA BIBLIA: “Hakuna jambo bora,” akaandika Mfalme Sulemani, kuliko kwamba mwanadamu “ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.”MHUBIRI 2:24.

Tuliumbwa tukiwa na tamaa ya kuridhika na kazi inayofaa. Hata unapokabili hali ngumu, unaweza kuridhika kwa kiasi fulani sasa kwa kufanya kazi kwa bidii na kwa unyofu.

KANUNI YA BIBLIA: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”MATENDO 20:35.

Watu wengi wametambua kwamba kuwasaidia wengine, yaani, kutumia wakati na nguvu zao ili kuwasaidia walio katika hali ngumu, ni jambo linalothawabisha na kuongeza maana katika maisha yao. Mfalme Sulemani aliandika: “Usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.”—Methali 3:27.

Fikiria kisa cha Ralph. Baada ya kustaafu, alijiunga na mke wake katika utumishi wa Kikristo wa wakati wote. Wanajitolea kutumia saa kadhaa kila mwezi katika utumishi huo, ili kuwafundisha wengine Biblia. Ralph anasema, “Tunapofika nyumbani jioni, huwa tumechoka kwa sababu ya kutumia nguvu zetu zote katika kumtumikia Baba yetu wa mbinguni, bali si kwa sababu tu ya uzee. Inafurahisha kuchoka kwa ajili ya kazi njema!” Yeye na mke wake wana furaha kwa sababu wanatumia wakati wao mwingi kuwasaidia wengine.

KANUNI YA BIBLIA: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”METHALI 17:17.

Inaweza kuwa rahisi kukabiliana na matatizo unapokuwa na marafiki. Mwanafalsafa Mwingereza Francis Bacon aliandika kwamba kwa wale wasiokuwa na marafiki wa kweli, “dunia ni kama nyika.” Kuwa na marafiki wa kweli na kuwa rafiki mzuri, ni mambo yanayoweza kukusaidia ukabiliane na hali ngumu na kufanya maisha yawe yenye kupendeza na kuridhisha.

KANUNI YA BIBLIA: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”MATHAYO 5:3.

Hivyo, Yesu alitaja jambo muhimu unalopaswa kufanya ili kufurahia kutimizwa kwa ahadi za Mungu. Jambo hilo ni kutambua na kutosheleza ‘uhitaji wako wa kiroho.’ Tofauti na wanyama, sisi tuna tamaa ya kiasili ya kujua maana na kusudi la uhai. Ni Yehova Mungu pekee anayeweza kututimizia uhitaji huo, na anafanya hivyo kupitia Neno lake, Biblia. Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, Biblia inafunua kusudi la Mungu kuelekea dunia. Inatueleza kwa nini tupo hapa, kwa nini watu wanateseka sana, na mambo ambayo Mungu anatazamia tufanye. Kuelewa kweli hizo za Kimaandiko ni muhimu ikiwa tunataka kuishi maisha yenye maana na yenye kuridhisha. Wale wanaotenga wakati wa kusoma Biblia na kufuata yale wanayojifunza, wanakuwa na furaha. Kwa nini? Kwa sababu kwa kufanya hivyo, wanajenga uhusiano mzuri na Muumba wetu, “Mungu mwenye furaha,” Yehova.—1 Timotheo 1:11.

KANUNI YA BIBLIA: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako . . . kabla siku zenye msiba hazijaja na miaka iwe imekaribia utakaposema: ‘Sioni maana ya maisha.’”MHUBIRI 12:1, THE NEW ENGLISH BIBLE.

Shauri la Mfalme Sulemani kwa vijana, ambao wakati wa ujana wao huenda wakakosa kutambua kwamba hatimaye maisha yanaweza kuwa yenye misiba, linatuhusu sote. Acha lengo lako maishani liwe kumtumikia Muumba wako. Hilo litafanya maisha yako yawe na kusudi halisi. Kataa kabisa mtazamo huu: “Tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Ikiwa utamtanguliza Mungu kwanza mambo ‘yatakuendea vyema,’ linasema andiko la Mhubiri 8:12.

Msichana anayeitwa Wendi alithibitisha jambo hilo kuwa kweli. Alipokuwa kijana, yeye na dada yake walijifunza Kihispania ili waweze kuhamia Jamhuri ya Dominika, ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa habari njema za Biblia. “Tulijidhabihu sana ili kutumika katika eneo lenye uhitaji wa wahubiri, lakini tulifurahia sana. Hakuna jambo lingine bora kuliko hilo ambalo ningefanya katika hiyo miezi sita! Baraka tulizopata zilikuwa nyingi zaidi kuliko mambo tuliyodhabihu.”

Ushikamanifu kwa Mungu Hufanya Maisha Yawe na Maana

Kusitawisha uhusiano mzuri na Yehova kunaweza kufanya maisha yako yawe na maana zaidi kwa njia ya pekee sana. Jinsi gani? Shetani hakuwadanganya Adamu na Hawa waasi utawala wa Mungu tu, bali pia alidai kuwa hakuna mwanadamu anayeweza kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu anapojaribiwa. (Ayubu 1:9-11; 2:4) Unaweza kusaidia kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo! Jinsi gani? Kwa kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu, kwa kutii kanuni zake, na kwa kuonyesha kwamba unatambua kuwa Yehova ana haki kamili ya kutuamulia lililo jema na lililo baya.—Ufunuo 4:11.

Nyakati nyingine huenda tukalazimika kuvumilia hali ngumu ikiwa tunataka kufuata njia inayofaa maishani. Je, hali hizo zitafanya maisha yetu yakose maana? Hebu wazia kwamba adui mkatili anasema mambo ya uwongo kumhusu rafiki yetu au mtu wetu wa ukoo. Ikiwa kukabiliana na adui huyo ili kututetea jina la rafiki huyo kutatuingiza katika matatizo, je, jambo hilo lingefanya maisha yetu yakose maana? Bila shaka, hapana! Tungekuwa tayari kukabiliana na hali hiyo ili kutetea jina zuri la rafiki yetu. Kuwa mshikamanifu kwa Mungu kunaweza kumaanisha hivyo pia. Kwa kweli, tunapoendelea kuwa washikamanifu chini ya hali hizi ngumu tunaufurahisha moyo wa Mungu.—Methali 27:11.

Maisha Yenye Maana Milele

Fanya yote unayoweza ili kujifunza kumhusu Mungu na kusudi lake. Yesu Kristo mwenyewe alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Mungu atakapotimiza kusudi lake la awali kuelekea dunia, wanadamu waaminifu watafurahia yale ambayo Yehova alikusudia wafurahie tangu mwanzo, yaani, “uzima wa milele” katika dunia paradiso. Kisha, maisha yatakuwa yenye maana na yenye kuridhisha kwelikweli.—Zaburi 145:16.

Unaweza kupata wapi ujuzi ambao Yesu alizungumzia? Katika Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. Ikiwa ungependa kupata msaada wa kujifunza Biblia, usisite kuwaandikia wachapishaji wa gazeti hili. Watafurahi kufanya mpango ili mtu akutembelee na kukusaidia kujifunza yale ambayo Biblia inafundisha hasa.