Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

KWA nini mwanamke mwenye umri wa miaka 60 hivi aliacha kuabudu sanamu? Ni nini kilichomchochea kuhani wa dini ya Shinto aache kazi yake hekaluni na kuwa mhudumu Mkristo? Ni nini kilichomwezesha mwanamke ambaye wazazi wake waliamua kisheria alelewe na wazazi wengine mara tu baada ya kuzaliwa, aweze kukabiliana na hali ya kuhisi kwamba amekataliwa? Hebu ona mambo ambayo watu hao wanasema.

“Situmikii Sanamu Tena.”​—ABA DANSOU

MWAKA WA KUZALIWA: 1938

NCHI: BENIN

HISTORIA: MWABUDU SANAMU

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika kijiji kinachoitwa So-Tchahoué, kilicho katika eneo lenye majimaji karibu na ziwa. Wanakijiji huvua samaki na kufuga ng’ombe, mbuzi, kondoo, nguruwe, na ndege. Eneo hilo halina barabara, hivyo watu wanasafiri kwa mashua na mitumbwi. Kwa kawaida, wao hujenga nyumba kwa mbao na nyasi, ingawa wengine hujenga kwa matofali. Watu wengi katika eneo hilo ni maskini. Hata hivyo, hakuna uhalifu mwingi kama ilivyo mijini.

Nilipokuwa mdogo, mimi na dada yangu tulipelekwa na baba yetu katika makao ya waabudu wa sanamu zinazoaminika kuwa na nguvu za pepo, ambako tulifundishwa mapokeo ya ibada hiyo ya sanamu. Nilipokuwa mtu mzima nilimchagua Dudua (Oduduwa), mungu wa Wayoruba, kuwa mungu wangu. Nilimjengea madhabahu na kutoa kwa ukawaida dhabihu za viazi vikuu, mafuta ya mawese, konokono, kuku, njiwa, na aina nyingine za wanyama. Dhabihu hizo zilikuwa za bei ya juu na mara nyingi nilitumia karibu mapato yangu yote.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipoanza kujifunza Biblia, nilijua kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli. Nilijifunza pia kwamba hapendezwi na ibada ya sanamu. (Kutoka 20:4, 5; 1 Wakorintho 10:14) Nilielewa ninachopaswa kufanya. Hivyo, nilitupa sanamu zangu zote na kuondoa nyumbani kwangu kila kitu kilichohusiana na ibada ya sanamu. Niliacha kutafuta habari kupitia uaguzi na sikushiriki tena katika matambiko na desturi za mazishi.

Haikuwa rahisi kwangu—mwanamke mwenye umri wa miaka 60 hivi—kufanya mabadiliko hayo. Rafiki, watu wa familia, na jirani zangu walinipinga na kunicheka. Lakini nilisali kwa Yehova ili nipate nguvu za kufanya yaliyo sawa. Nilifarijiwa sana na andiko la Methali 18:10, linalosema hivi: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.”

Jambo lingine lililonisaidia sana ni kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Katika mikutano hiyo nilijionea upendo wa Kikristo, na nilivutiwa sana kwa sababu watu hao wanajitahidi kuishi kulingana na viwango vya juu vya Biblia vya maadili. Mambo niliyoona yalinisadikisha kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaofuata dini ya kweli.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kufuata kanuni za Biblia kumenisaidia kuboresha uhusiano wangu pamoja na watoto wangu. Pia, ninahisi kuwa mzigo mkubwa umeondolewa mabegani mwangu. Nilikuwa nikipoteza mapato yangu kwa ajili ya sanamu zisizo na uhai ambazo hazikuninufaisha kwa vyovyote. Sasa ninamwabudu Yehova, ambaye hutoa suluhisho la kudumu kwa matatizo yetu yote. (Ufunuo 21:3, 4) Ninafurahi sana kwamba situmikii sanamu tena, badala yake, ninamtumikia Yehova! Yeye ananipa ulinzi na usalama wa kweli.

“Nimekuwa Nikimtafuta Mungu Tangu Utotoni.”—SHINJI SATO

MWAKA WA KUZALIWA: 1951

NCHI: JAPANI

HISTORIA: KUHANI WA DINI YA SHINTO

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mji fulani wa mashambani katika Wilaya ya Fukuoka. Wazazi wangu walikuwa watu wa kidini sana, na tangu utotoni walinifundisha kuiheshimu miungu ya Shinto. Nikiwa mvulana mdogo, mara nyingi nilitafakari kuhusu wokovu wangu na nilikuwa na tamaa kubwa ya kuwasaidia watu wenye shida. Ninakumbuka wakati fulani nilipokuwa katika shule ya msingi, mwalimu alituuliza tungependa kufanya kazi gani tutakapokuwa watu wazima. Wanafunzi wenzangu walitaja mambo makubwa, kama vile kuwa wanasayansi. Lakini mimi nikasema kwamba ningependa kuwa mtumishi wa Mungu. Wote walinicheka.

Baada ya kumaliza shule ya sekondari, nilijiunga na shule ya walimu wa dini. Katika shule hiyo, nilikutana na kuhani wa dini ya Shinto ambaye alitumia muda wake wa ziada kusoma kitabu fulani chenye jalada jeusi. Siku moja aliniuliza, “Sato, unajua hiki ni kitabu gani?” Nilikuwa nimeona jalada la kitabu hicho hivyo nikamjibu, “Biblia.” Naye akaniambia, “Yeyote anayetaka kuwa kuhani wa dini ya Shinto, anapaswa kusoma kitabu hiki.”

Niliondoka mara moja na kwenda kununua Biblia. Niliiweka mahali pa pekee kwenye rafu ya vitabu na kuitunza sana. Hata hivyo, sikupata nafasi ya kuisoma, kwa sababu tulikuwa na mambo mengi sana ya kufanya shuleni. Nilipomaliza shule, nilianza kufanya kazi katika hekalu nikiwa kuhani wa dini ya Shinto. Ndoto yangu ya tangu utotoni ilikuwa imetimia.

Hata hivyo, mambo hayakwenda kama nilivyotarajia kabla ya kuwa kuhani wa dini ya Shinto. Makuhani wengi hawakuwajali wala kuwapenda watu wengine. Pia, wengi wao hawakuwa na imani. Hata mmoja wa wasimamizi wangu aliniambia hivi: “Ikiwa unataka kufanikiwa hapa, unapaswa tu kuzungumzia mambo ya falsafa. Ni marufuku kuzungumza kuhusu imani.”

Maneno hayo yalinivunja moyo kuhusiana na dini ya Shinto. Hata ingawa niliendelea kufanya kazi katika hekalu hilo, nilianza kuchunguza dini nyingine. Lakini hakuna yoyote iliyoonekana kuwa nzuri. Kadiri nilivyoendelea kuchunguza dini, ndivyo nilivyozidi kuvunjika moyo. Niliona kwamba dini zote hazina ukweli.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mnamo 1988, nilikutana na Mbudha ambaye alinitia moyo nisome Biblia. Nilimkumbuka yule kuhani wa dini ya Shinto, ambaye miaka mingi awali alinitia moyo nifanye jambo hilohilo. Niliamua kutumia shauri hilo. Nilipoanza kusoma Biblia, ilinivutia sana. Nyakati nyingine ningeisoma usiku kucha.

Yale niliyosoma yalinichochea nitamani kusali kwa Mungu wa Biblia. Nilianza na sala ya kielelezo inayopatikana katika Mathayo 6:9-13. Niliirudia-rudia kila baada ya saa mbili hata nilipokuwa nikiendesha ibada katika hekalu la Shinto.

Nilikuwa na maswali mengi kuhusu yale niliyokuwa nikisoma. Kufikia wakati huo, nilikuwa nimeoa, na nilijua kuwa Mashahidi wa Yehova wanawafundisha watu Biblia kwa sababu walikuwa wamewahi kumtembelea mke wangu. Nilimtafuta Shahidi mmoja na kumuuliza maswali mengi. Nilivutiwa sana alipotumia Biblia kujibu maswali hayo yote. Alifanya mpango ili mwanamume mmoja Shahidi ajifunze Biblia pamoja nami.

Muda mfupi baadaye, nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Wakati huo, sikutambua kwamba miongoni mwao kulikuwa na watu niliowatendea kwa ukali zamani. Hata hivyo, walinisalimia kwa uchangamfu na kunifanya nihisi nimekaribishwa.

Katika mikutano hiyo, nilijifunza kwamba Mungu anatarajia waume wawapende na kuwaheshimu watu wao wa familia. Kufikia wakati huo, nilikuwa nimejishughulisha sana na kazi yangu ya ukuhani hivi kwamba nilimpuuza mke wangu na watoto wetu wawili. Nilianza kutambua kwamba nilikuwa nikiwasikiliza kwa makini watu waliokuja kuabudu kwenye hekalu, lakini sikuwa nimewahi kumsikiliza mke wangu hata siku moja.

Nilipoendelea kujifunza, nilielewa mambo mengi kumhusu Yehova ambayo yalinivuta kwake. Nilivutiwa hasa na andiko la Waroma 10:13, linalosema: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” Nilikuwa nikimtafuta Mungu tangu utotoni, lakini sasa hatimaye nilikuwa nimempata!

Nilianza kuhisi kuwa sikustahili tena kuwa hekaluni. Mwanzoni, nilikuwa na wasiwasi kuhusu jinsi ambavyo wengine wangeniona ikiwa ningeacha dini ya Shinto. Lakini nilikuwa nimeazimia kuiacha ikiwa ningemjua Mungu wa kweli. Hivyo, mnamo 1989, niliamua kutii dhamiri yangu. Niliacha kuhudumu hekaluni na kujikabidhi mikononi mwa Yehova.

Haikuwa rahisi kuacha kazi yangu hekaluni. Wasimamizi wangu walinikemea na kujaribu kunilazimisha niendelee na kazi hiyo. Ilikuwa vigumu hata zaidi kuwaambia wazazi wangu kuhusu jambo hilo. Nilipokuwa njiani kwenda nyumbani kwa wazazi, nilikuwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba niliumwa na kifua na miguu yangu ikakosa nguvu! Nilisimama mara nyingi njiani, nikisali kwa Yehova anipe nguvu.

Nilipofika kwa wazazi wangu, sikuweza kuwaambia mara moja kilichonipeleka kwa kuwa niliogopa sana. Saa kadhaa zilipita. Mwishowe, baada ya kusali sana, nilimweleza baba yangu kila kitu. Nilimweleza kwamba nimempata Mungu wa kweli na kwamba nilikuwa nimeamua kuacha dini ya Shinto ili niweze kumtumikia. Baba yangu alishtuka na kuhuzunika. Watu wengine wa ukoo walikuja na kujaribu kunishawishi nibadili maoni yangu. Sikutaka kuiumiza familia yangu, lakini wakati huohuo, nilijua kwamba kumtumikia Yehova ndilo jambo linalofaa. Baada ya muda, familia yangu ilianza kuniheshimu kwa uamuzi niliofanya.

Ingawa nilikuwa nimeondoka hekaluni kihalisi, bado nilikuwa nikiwaza sana kuhusu kazi yangu huko. Maisha ya ukuhani yalikuwa yametia mizizi sana ndani yangu. Nilijitahidi sana kuyasahau, lakini ilikuwa kana kwamba kila kitu kilichokuwa nyumbani mwetu kilinikumbusha maisha hayo ya zamani.

Kuna mambo mawili yaliyonisaidia kukabiliana na hali hiyo. Kwanza, niliipekua nyumba yangu kwa makini ili kuondoa chochote kilichohusiana na dini yangu ya zamani. Halafu nikateketeza kila kitu—vitabu, picha, na hata vitu vya ukumbusho vyenye thamani. Pili, nilitumia wakati mwingi iwezekanavyo pamoja na Mashahidi. Urafiki na utegemezo wao ulinisaidia sana. Kisha, hatua kwa hatua, nikasahau maisha yangu ya zamani.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilikuwa nikimpuuza mke wangu na watoto wetu, jambo lililowafanya wajihisi wapweke sana. Lakini nilipoanza kutumia wakati pamoja nao, kama vile Biblia inavyowafundisha waume kufanya, uhusiano wetu ukawa mzuri. Baada ya muda, mke wangu alijiunga nami katika kumtumikia Yehova. Sasa mimi na mke wangu, mwana wetu, binti yetu, na mume wake, tumeungana pamoja katika ibada ya kweli.

Ninapotafakari kuhusu ndoto yangu ya tangu utotoni ya kumtumikia Mungu na kuwasaidia wengine, ninatambua kwamba nimepata yote niliyokuwa nikitafuta—na hata zaidi. Sina maneno ya kueleza shukrani zangu kwa Yehova.

‘Nilihisi Kwamba Nilikuwa Nimekosa Kitu Fulani.’—LYNETTE HOUGHTING

MWAKA WA KUZALIWA: 1958

NCHI: AFRIKA KUSINI

HISTORIA: ALIHISI KWAMBA AMEKATALIWA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa huko Germiston, mji wenye machimbo ya madini ambao wakaaji wake si matajiri sana, na ambao hauna uhalifu mwingi. Wazazi wangu waliwapa wazazi wengine haki ya kisheria ya kunilea kwa kuwa walihisi kwamba hawangeweza kunilea. Wazazi hao wenye upendo ambao nilikuja kuwaona kama baba na mama, walinichukua nikiwa na umri wa siku 14 tu. Hata hivyo, nilipojua historia yangu, nilipambana na hali ya kuhisi kwamba nimekataliwa. Nilijihisi kama sikuwa mmoja wa familia iliyokuwa ikinilea, nao kwa kweli hawakunielewa.

Nilipokuwa na umri wa miaka 16 hivi, nilianza kwenda kwenye vilabu vya pombe, ambako mimi na rafiki zangu tungecheza na kusikiliza muziki uliopigwa na wanamuziki jukwaani. Nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilianza kuvuta sigara. Nilitaka kuwa mwembamba kama wanamitindo niliowaona kwenye matangazo ya sigara. Nilipofikia umri wa miaka 19, nilipata kazi jijini Johannesburg, ambako mara moja nilianza kushirikiana na rafiki wabaya. Punde si punde, nilianza kutumia lugha chafu, kuvuta sigara kupindukia, na miisho-juma, nilikuwa nikinywa pombe kupita kiasi.

Hata hivyo, sikuwa mzembe. Mara kwa mara, nilicheza mpira wa miguu wa wanawake na michezo mingine. Pia, nilifanya kazi kwa bidii na kujulikana sana kwa ujuzi wangu wa kompyuta. Kwa hiyo, nilipata pesa nyingi, na watu wengi waliona kuwa nimefanikiwa sana maishani. Hata hivyo, sikuwa na furaha hata kidogo—nilihisi nimepotea na kuvunjika moyo. Nilihisi moyoni kwamba nilikuwa nimekosa kitu fulani.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipoanza kujifunza Biblia, nilianza kuelewa kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo. Pia, nilijifunza kwamba ameonyesha upendo huo kwa kutupa Neno lake, Biblia. Ni kama ametuandikia barua ya kibinafsi ili kutuongoza. (Isaya 48:17, 18) Nilitambua kwamba ili niweze kunufaika na mwongozo wenye upendo wa Yehova, nilipaswa kufanya mabadiliko makubwa maishani mwangu.

Badiliko moja nililohitaji kufanya ni kuacha marafiki wabaya. Nilikumbuka maneno ya andiko la Methali 13:20, linalosema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” Kanuni hiyo ilinichochea kuwaacha rafiki zangu wa zamani na kutafuta rafiki wapya miongoni mwa Mashahidi wa Yehova.

Tatizo kubwa nililokabili ni kuacha kuvuta sigara, kwa sababu nilikuwa mvutaji sugu. Nilipokuwa ninaendelea kukabiliana na tatizo hilo, nilikumbwa na tatizo lingine. Kuacha kuvuta sigara kulifanya uzito wangu uongezeke kwa kilo 13.6! Hilo lilikuwa pigo kubwa kwangu, na ilinichukua miaka kumi hivi kupunguza uzito huo. Hata hivyo, nilijua kwamba kuacha kuvuta sigara ni uamuzi unaofaa. Niliendelea kusali kwa Yehova, naye akaniwezesha kushinda tatizo hilo.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Sasa ninafurahia afya nzuri. Pia, nimeridhika kwa kuwa sifuatilii tena furaha ya muda mfupi inayotokana na kazi ya kimwili, cheo, na mali. Badala yake, ninapata furaha ya kweli kwa kuwahubiria wengine kweli za Biblia. Kwa sababu hiyo, rafiki zangu watatu wa zamani sasa wanamtumikia Yehova pamoja nami na mume wangu. Kabla wazazi walionilea hawajafa, niliweza kuzungumza nao kuhusu ahadi ya Biblia ya ufufuo katika dunia paradiso.

Kumkaribia Yehova kumenisaidia kukabiliana na ile hali ya kuhisi kwamba nimekataliwa. Amenifanya nihisi kuwa ninapendwa kwa kuniwezesha kuwa sehemu ya familia ya ulimwenguni pote ya waabudu wake. Miongoni mwao, nimepata mama, baba, ndugu, na dada wengi.—Marko 10:29, 30.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nimejionea upendo wa Kikristo kati ya Mashahidi wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 13]

Zamani niliabudu katika hekalu hili la Shinto