Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Makala hii ina maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Ufalme wa Mungu ni nini?

Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni, nao utaondoa serikali nyingine zote. Chini ya Ufalme huo, mapenzi ya Mungu yatafanywa mbinguni na duniani. Kwa hiyo, Ufalme wa Mungu ndio utakaotimiza uhitaji wetu wa kuwa na serikali nzuri.—Soma Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

Lazima ufalme uwe na mfalme. Yehova alimweka Mwana wake, Yesu, awe Mfalme wa Ufalme Wake.—Soma Luka 1:30-33.

2. Kwa nini Yesu ndiye Mtawala anayefaa?

Mwana wa Mungu ndiye Mfalme anayefaa kwa sababu ni mwenye fadhili, anafuatia haki, na ana uwezo wa kuwasaidia watu. (Mathayo 11:28-30) Baada ya kufufuliwa, Yesu alipaa mbinguni na kuketi kwenye mkono wa kuume wa Yehova akingoja kupewa ufalme. (Waebrania 10:12, 13) Mwishowe, Mungu alimpa mamlaka ya kuanza kutawala kutoka mbinguni.—Soma Danieli 7:13, 14.

3. Ni nani wengine watakaotawala pamoja na Yesu?

Kikundi cha watu wanaoitwa “watakatifu” wanachaguliwa na Mungu watatawala pamoja na Yesu mbinguni. (Danieli 7:27) Wanafunzi wa Yesu ndio waliokuwa watu wa kwanza kuchaguliwa kuwa watakatifu. Yehova ameendelea kuchagua wanaume na wanawake waaminifu kuwa watakatifu hadi sasa. Kama Yesu, watakatifu hao wanafufuliwa katika mwili wa roho.—Soma Yohana 14:1-3; 1 Wakorintho 15:42-45.

Ni watu wangapi wanaoenda mbinguni? Yesu aliwaita “kundi dogo.” (Luka 12:32) Mwishowe, hesabu yao itakuwa 144,000, nao watatawala pamoja na Yesu juu ya dunia.—Soma Ufunuo 5:9, 10; 14:1.

4. Ufalme wa Mungu ulianza kutawala wakati gani?

Yesu aliwekwa kuwa Mfalme mwaka wa 1914. * Muda mfupi baadaye, alimtupa Shetani na mashetani wake duniani. (Ufunuo 12:7-10, 12) Tangu wakati huo, matatizo ya wanadamu yameongezeka sana. Vita, matetemeko ya ardhi, njaa, magonjwa yenye kuenea, na uasi-sheria ni sehemu ya ishara kwamba ulimwengu huu unakaribia mwisho wake. (2 Timotheo 3:1-5) Wote wanaotaka kufaidika na Ufalme wa Mungu wanapaswa kujifunza jinsi wanavyoweza kuwa wafuasi wa Mfalme, Yesu.—Soma Luka 21:7, 10, 11, 31, 34, 35.

5. Ufalme wa Mungu unatimiza nini?

Kupitia kazi inayofanywa duniani kote ya kuhubiri, tayari Ufalme wa Mungu unawasaidia mamilioni ya watu kutoka mataifa yote kujifunza njia za Mungu. (Mathayo 24:14) Wakati Ufalme huo utakapoharibu ulimwengu huu mwovu, utaulinda “umati mkubwa” wa raia washikamanifu wa Yesu.—Soma Ufunuo 7:9, 10, 13-17.

Katika kipindi cha miaka 1,000, Ufalme huo utaigeuza dunia hatua kwa hatua kuwa paradiso. Mwishowe, Yesu atamrudishia Baba yake Ufalme. (1 Wakorintho 15:24-26) Je, unajua mtu yeyote ambaye ungependa kumweleza kuhusu Ufalme wa Mungu?—Soma Zaburi 37:10, 11, 29.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 8 na 9 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ Kwa habari zaidi kuhusu jinsi unabii wa Biblia unavyothibitisha kwamba Yesu alianza kutawala 1914, ona ukurasa wa 215-218 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.