Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Alifarijiwa na Mungu Wake

Alifarijiwa na Mungu Wake

Igeni Imani Yao

Alifarijiwa na Mungu Wake

ELIYA alikimbia huku mvua ikimnyeshea nalo giza likizidi kutanda angani. Bado alihitaji kukimbia mwendo mrefu ili afike Yezreeli, naye hakuwa kijana. Hata hivyo, alikimbia bila kuchoka, kwa kuwa “mkono wa Yehova” ulikuwa juu yake. Kwa kweli, hakuwa amewahi kuwa na nguvu kama hizo. Nguvu hizo zilimwezesha kuwapita farasi waliokuwa wakivuta gari la Mfalme Ahabu!—1 Wafalme 18:46.

Sasa, Eliya alikuwa amekimbia mbali sana mbele ya Mfalme Ahabu, na bado alihitaji kukimbia mwendo mrefu ili afike. Wazia mvua ikimpiga usoni huku akikimbia na kutafakari matukio mengi ya siku hiyo ya pekee maishani mwake. Bila shaka, huo ulikuwa ushindi mkubwa kwa Mungu wa Eliya, Yehova, na kwa ibada ya kweli. Sasa Eliya hangeweza kuuona Mlima Karmeli, kwa kuwa alikuwa mbali, nayo mawingu ya dhoruba yalifanya anga liwe jeusi. Kwenye mlima huo, Yehova alikuwa amemtumia Eliya kuiangamiza kwa pigo lenye nguvu la kimuujiza ibada ya Baali. Mamia ya manabii wa Baali walifunuliwa kuwa wadanganyifu waovu na wakauawa. Kisha, Eliya akasali kwa Yehova ili ukame ambao uliwaumiza watu kwa miaka mitatu na nusu uishe. Baada ya sala hiyo, mvua ilinyesha! *1 Wafalme 18:18-45.

Alipokuwa akikimbia zile kilomita 30 kwenda Yezreeli, huenda Eliya aliwazia kwamba kwa kuwa manabii wa Baali walikuwa wameuawa, basi, kungekuwa na mabadiliko makubwa. Bila shaka, ingekuwa lazima Ahabu abadilike! Baada ya yale aliyoona, kwa kweli Ahabu hangekuwa na la kufanya ila kuacha ibada ya Baali, kumdhibiti Yezebeli, malkia wake, na kuacha kuwatesa watumishi wa Yehova.

Ni jambo la kawaida kuwa na matumaini mambo yanapoonekana kutuendea vizuri. Tunaweza kuanza kuwazia kwamba hali yetu itakuwa bora na hata kufikiri kuwa matatizo yetu makubwa yameisha. Halingekuwa jambo la kushangaza ikiwa Eliya angekuwa akifikiria hivyo, kwa sababu “alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu.” (Yakobo 5:17) Hata hivyo, matatizo ya Eliya hayakuwa yameisha. Kwa kweli, baada ya saa chache tu Eliya angekuwa na woga mwingi na kushuka moyo sana hivi kwamba angetamani kufa. Ni nini kilichotokea? Na Yehova alimsaidia jinsi gani nabii wake aimarishe imani na ujasiri wake? Acheni tuone.

Mambo Yabadilika Ghafla

Ahabu alipofika kwenye makao yake ya kifalme huko Yezreeli, je, alionyesha dalili yeyote kwamba alikuwa amebadilika na kuwa mtu wa kiroho zaidi? Tunasoma hivi: “Ahabu akamwambia Yezebeli mambo yote ambayo Eliya alikuwa amefanya na mambo yote kuhusu namna alivyowaua manabii wote kwa upanga.” (1 Wafalme 19:1) Ona kwamba Ahabu aliposimulia matukio ya siku hiyo, hakumtaja Yehova, Mungu wa Eliya. Kwa sababu Ahabu alikuwa mtu wa kimwili, alikuwa na maoni ya kibinadamu tu kuhusu matukio ya kimuujiza ya siku hiyo, yaani, yale “ambayo Eliya alikuwa amefanya.” Kwa kweli, hakuwa amejifunza kumheshimu Yehova Mungu. Naye Yezebeli aliyependa sana kulipiza kisasi, alifanya nini?

Alikasirika sana! Akiwa amejawa na hasira, Yezebeli alituma ujumbe huu kwa Eliya: “Miungu na ifanye hivyo, nayo izidishe jambo hilo, ikiwa wakati kama huu hapo kesho sitaifanya nafsi yako iwe kama nafsi ya kila mmoja wao!” (1 Wafalme 19:2) Huo ulikuwa ujumbe mkali wa kutishia uhai. Kwa kweli, ni kana kwamba Yezebeli alikuwa anaapa kwamba yeye mwenyewe anapaswa kufa ikiwa hatakuwa amemuua Eliya kufikia siku iliyofuata, ili kulipiza kisasi kwa ajili ya manabii wa Baali. Wazia Eliya akiamshwa kutoka usingizini, katika chumba cha kulala cha hali ya chini huko Yezreeli usiku huo wenye dhoruba kali, na kupewa ujumbe wenye kuogopesha kutoka kwa malkia. Ujumbe huo ulimwathiri jinsi gani?

Alemewa na Woga na Kuvunjika Moyo

Ikiwa Eliya alifikiri kwamba vita dhidi ya ibada ya Baali vilikuwa vimeisha, alitambua mara moja kwamba mambo hayakuwa hivyo. Yezebeli hakuwa ametishwa na mambo yaliyokuwa yametokea. Waaminifu wengi waliokuwa wakishirikiana na Eliya tayari walikuwa wameuawa kwa agizo la Yezebeli, na sasa, ilionekana kwamba ilikuwa zamu yake. Biblia inasema: ‘Eliya aliogopa.’ Je, Eliya alipiga picha akilini jinsi ambavyo Yezebeli angemuua kikatili? Ikiwa aliendelea kufikiria mambo hayo, si ajabu alikosa ujasiri kabisa. Vyovyote vile, Eliya “[alianza] kwenda kwa ajili ya nafsi yake”—akakimbia ili kuokoa maisha yake.—1 Wafalme 18:4; 19:3.

Eliya hakuwa mtu pekee wa imani aliyelemewa na woga. Miaka mingi baadaye, mtume Petro alipatwa na tatizo kama hilo. Kwa mfano, Yesu alipomwezesha kutembea juu ya maji, mtume huyo alianza ‘kuitazama ile dhoruba ya upepo.’ Hivyo, Petro akapoteza ujasiri na akaanza kuzama. (Mathayo 14:30) Kwa hiyo, mfano wa Petro na Eliya unatusaidia kuelewa jambo fulani muhimu. Ikiwa tunataka kudumisha ujasiri wetu, hatupaswi kuendelea kufikiria mambo hatari yanayotuogopesha. Tunahitaji kukaza uangalifu wetu katika Chanzo cha tumaini na nguvu zetu.

“Inatosha!”

Kwa sababu ya woga, Eliya alikimbilia Beer-sheba, eneo la kusini-magharibi lililokuwa umbali wa kilomita 150. Mji huo ulikuwa karibu na mpaka wa kusini wa Yuda. Alimwacha mtumishi wake huko na kuingia nyikani peke yake. Simulizi hilo linasema kwamba alienda “safari ya siku moja.” Hivyo, tunaweza kuwazia Eliya akianza safari hiyo asubuhi, akiwa hana chakula wala mahitaji mengine muhimu. Akiwa ameshuka moyo na kujawa na woga, Eliya aliendelea kutembea katika eneo hilo kavu na lenye mawemawe huku akichomwa na jua kali. Kufikia jioni wakati jua hilo kali lilipotua, Eliya alikuwa ameishiwa na nguvu. Akiwa amechoka, alikaa chini ya mti wa mretemu, mahali pekee ambapo mtu angeweza kujihifadhi katika eneo hilo kame.—1 Wafalme 19:4.

Eliya alisali akiwa amekata tamaa kabisa. Aliomba afe. Alisema: “Mimi si bora kuliko mababu zangu.” Eliya alijua kwamba mababu zake walikuwa tu mavumbi na mifupa katika makaburi yao, wakiwa hawawezi kumfanyia mtu jambo lolote zuri. (Mhubiri 9:10) Eliya alihisi hana thamani yoyote kama tu hao mababu zake. Haishangazi kwamba alilia hivi: “Inatosha!” Aliona hakuna haja ya kuendelea kuishi.

Je, ni jambo linaloshangaza kwamba mtu wa Mungu avunjike moyo kiasi hicho? Si lazima iwe hivyo. Biblia inataja wanaume na wanawake fulani ambao walihuzunika sana hivi kwamba walitamani kufa. Baadhi yao ni Rebeka, Yakobo, Musa, na Ayubu.—Mwanzo 25:22; 37:35; Hesabu 11:13-15; Ayubu 14:13.

Leo, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” hivyo, si jambo linaloshangaza kwamba watu wengi, hata watumishi waaminifu wa Mungu, wanavunjika moyo nyakati nyingine. (2 Timotheo 3:1) Ikiwa unakabili hali ngumu kama hiyo, iga mfano wa Eliya: Mweleze Mungu yote yaliyo moyoni mwako. Yehova ni “Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3) Je, alimfariji Eliya?

Yehova Amtegemeza Nabii Wake

Unafikiri Yehova alihisi jinsi gani alipotazama chini kutoka mbinguni na kumwona nabii wake mpendwa amelala chini ya ule mti nyikani akiomba afe? Hatuna haja ya kukisia. Baada ya Eliya kulala usingizi, Yehova alituma malaika wake. Malaika huyo alimwamsha Eliya kwa kumgusa kwa wororo na kumwambia: “Amka, ule.” Eliya alifanya hivyo, kwa kuwa malaika alikuwa amemwandalia chakula chepesi, yaani, mkate wa moto na maji. Je, Eliya alimshukuru malaika huyo? Simulizi hilo linasema tu kwamba nabii huyo alikula na kunywa na kisha akaendelea kulala. Je, Eliya alikuwa amevunjika moyo sana hivi kwamba hangeweza kuzungumza? Vyovyote vile, malaika huyo alimwamsha tena, labda wakati wa mapambazuko. Na kwa mara nyingine tena alimhimiza Eliya, “Amka, ule,” kisha akasema maneno haya yenye kushangaza, “kwa maana safari ni ndefu mno kwako.”—1 Wafalme 19:5-7.

Kwa sababu ya uwezo aliopewa na Mungu, malaika huyo alijua Eliya alikuwa akielekea wapi. Pia, alijua kuwa safari hiyo itakuwa ndefu sana na Eliya hataweza kuimaliza kwa nguvu zake mwenyewe. Inatia moyo kama nini kumtumikia Mungu ambaye anajua vizuri malengo na udhaifu wetu kuliko sisi wenyewe! (Zaburi 103:13, 14) Chakula hicho kilimsaidia Eliya jinsi gani?

Tunasoma hivi: “Akaamka, akala na kunywa, naye akazidi kwenda katika nguvu za chakula kile kwa siku 40, mchana na usiku, mpaka Horebu, mlima wa Mungu wa kweli.” (1 Wafalme 19:8) Kama Musa aliyeishi karne sita kabla ya Eliya na pia Yesu aliyeishi karne kumi hivi baada yake, Eliya alifunga kwa siku 40, mchana na usiku. (Kutoka 34:28; Luka 4:1, 2) Mlo huo mmoja haukumaliza shida zake zote, lakini ulimwimarisha kwa njia ya kimuujiza. Wazia mtu huyo mwenye umri mkubwa aking’ang’ana kutembea katika nyika isiyo na barabara wala njia, siku baada ya siku, juma baada ya juma, kwa karibu mwezi mmoja na nusu!

Leo pia, Yehova anawategemeza watumishi wake, si kwa kuwalisha vyakula vya kimwili kimuujiza, bali kwa njia muhimu hata zaidi. Anawaandalia watumishi wake chakula cha kiroho. (Mathayo 4:4) Kujifunza kumhusu Mungu kupitia Neno lake na machapisho ambayo yanategemea Biblia, kunatutegemeza kiroho. Huenda chakula hicho cha kiroho kisituondolee matatizo yetu yote, lakini kinaweza kutusaidia tuvumilie jambo ambalo huenda tusingeweza kuvumilia. Chakula hicho pia kinatusaidia kupata “uzima wa milele.”—Yohana 17:3.

Eliya alitembea karibu kilomita 320 mpaka Mlima Horebu, ambako miaka mingi iliyopita Yehova Mungu alimtokea Musa kupitia malaika katika mti wa miiba uliokuwa ukiwaka moto na baadaye Yehova akafanya agano la Sheria na Waisraeli. Eliya alikaa katika pango.

Jinsi Yehova Alivyomfariji na Kumtia Nguvu Nabii Wake

Huko Horebu, “neno” la Yehova—yaelekea lilimjia kupitia malaika—lilimuuliza swali hili rahisi: “Una kazi gani hapa, Eliya?” Inaelekea swali hilo liliulizwa kwa njia ya upole, kwa kuwa Eliya alitumia nafasi hiyo kueleza yote yaliyokuwa moyoni mwake. Naye akajieleza kwelikweli! Alisema: “Nimekuwa na wivu kwelikweli kwa ajili ya Yehova Mungu wa majeshi; kwa maana wana wa Israeli wameliacha agano lako, wamezibomoa madhabahu zako, nao wamewaua manabii wako kwa upanga, hivi kwamba ni mimi peke yangu nimebaki; nao wanaanza kuitafuta nafsi yangu ili kuiondoa.” (1 Wafalme 19:9, 10) Maneno ya Eliya yanaonyesha angalau sababu tatu za kuvunjika moyo.

Kwanza, Eliya alihisi kwamba kazi yake imekuwa ya bure. Ingawa kwa miaka mingi alikuwa na “wivu kwelikweli” katika utumishi wake kwa Yehova, akitanguliza jina takatifu la Mungu na ibada yake, aliona kama hali zilizidi kuwa mbaya tu. Bado watu walikuwa hawana imani na wakaidi, nayo ibada ya uwongo ilizidi kuenea. Pili, Eliya alihisi upweke. “Mimi peke yangu nimebaki,” akasema, kana kwamba yeye peke yake ndiye aliyekuwa mtumishi wa Yehova aliyebaki katika nchi ya Israeli. Tatu, Eliya aliogopa. Tayari manabii wenzake wengi walikuwa wameuawa, na alikuwa na hakika kwamba sasa ilikuwa zamu yake. Huenda haikuwa rahisi kwa Eliya kukiri kwamba mambo hayo yalimhangaisha, lakini hakuruhusu kiburi au aibu imzuie. Alimweleza Mungu yote yaliyokuwa moyoni mwake kupitia sala, na hivyo kuwawekea watu wote waaminifu mfano mzuri.—Zaburi 62:8.

Yehova alishughulikia jinsi gani woga na mahangaiko ya Eliya? Malaika alimwambia Eliya asimame kwenye mlango wa pango. Alitii, bila kujua yale ambayo yangetokea. Ghafla, upepo wenye nguvu ukavuma! Ni lazima upepo huo ulikuwa na kelele kubwa, kwa sababu ulivuma kwa nguvu sana hivi kwamba ulipasua milima na miamba. Hebu wazia Eliya akijaribu kukinga macho yake huku aking’ang’ana kushikilia vazi lake gumu lenye manyoya wakati upepo huo ulipokuwa ukivuma. Pia, alihitaji kuangalia asianguke, kwa kuwa ardhi ilianza kutikisika na kusukasuka kwani eneo hilo lilikumbwa na tetemeko! Kabla hajaelewa vizuri kilichokuwa kikiendelea, moto mkubwa ulipita, ukimlazimisha arudi ndani ya pango ili asiunguzwe na joto kali.—1 Wafalme 19:11, 12.

Katika kila moja ya matukio hayo, simulizi hilo linatuambia kwamba Yehova hakupatikana katika maonyesho hayo yenye kustaajabisha ya nguvu za asili. Eliya alijua kwamba Yehova si kama mungu wa kuwaziwa, kama vile Baali, ambaye alitukuzwa na waabudu wake waliodanganywa kuwa yeye ni “Mwendeshaji wa Mawingu,” au mleta mvua. Yehova ndiye Chanzo halisi cha nguvu zote zisizo na kifani zinazopatikana katika vitu vya asili, lakini pia ni mkuu sana kuliko kitu chochote alichoumba. Hata mbingu haziwezi kumtosha! (1 Wafalme 8:27) Hayo yote yalimsaidia Eliya jinsi gani? Kumbuka kwamba alikuwa na woga. Akiwa na Mungu kama Yehova, mwenye nguvu nyingi sana, Eliya hakupaswa kuwaogopa Ahabu na Yezebeli!—Zaburi 118:6.

Baada ya moto kupita, kimya kilitokea na Eliya akasikia “sauti tulivu, ya chini.” Ilimkaribisha ajieleze tena, naye akafanya hivyo, akieleza mahangaiko yake yote kwa mara ya pili. * Labda hilo lilimtuliza. Bila shaka, Eliya alitulizwa hata zaidi na maneno ambayo ile “sauti tulivu, ya chini” ilifuatia kusema. Yehova alimhakikishia Eliya kwamba alikuwa mwenye thamani sana. Jinsi gani? Mungu alimfunulia mengi kuhusu makusudi yake ya wakati ujao kuhusiana na vita vyake dhidi ya ibada ya Baali nchini Israeli. Kwa wazi, kazi ya Eliya haikuwa ya bure, kwa kuwa makusudi ya Mungu yalikuwa yakitimia bila kuzuiwa. Zaidi ya hayo, Eliya alikuwa na sehemu katika utimizo wa makusudi hayo, kwa kuwa Yehova alimtuma tena, akimpa maagizo hususa.—1 Wafalme 19:12-17.

Hata hivyo, namna gani kuhusu upweke ambao Eliya alihisi? Yehova alifanya mambo mawili kuhusu hilo. Kwanza, Yehova alimwambia Eliya amtie mafuta Elisha awe nabii ambaye mwishowe angechukua mahali pake. Mwanamume huyo kijana angekuwa mwandamani na msaidizi wa Eliya kwa miaka kadhaa. Msaada huo ulimfariji sana! Pili, Yehova alifunua habari hii yenye kuchangamsha: “Nimewaacha watu elfu saba wabaki katika Israeli, magoti yote ambayo hayakumwinamia Baali, na kila kinywa ambacho hakikumbusu.” (1 Wafalme 19:18) Eliya hakuwa peke yake. Ni lazima Eliya alifurahi sana kusikia kuhusu maelfu ya watu waaminifu ambao walikataa kumwabudu Baali. Walitaka Eliya aendelee na utumishi wake wa uaminifu na kuwa kielelezo cha ushikamanifu usioyumba-yumba kwa Yehova wakati huo mgumu. Haikosi Eliya aliguswa moyo sana kusikia maneno hayo kutoka kwa malaika wa Yehova, ile “sauti tulivu, ya chini.” Ilikuwa ni kana kwamba Mungu mwenyewe amezungumza naye.

Kama Eliya, huenda tumepigwa na bumbuazi kwa sababu ya nguvu za asili zinazoonekana katika uumbaji. Uumbaji unafunua wazi nguvu za Muumba. (Waroma 1:20) Bado Yehova anapenda kutumia nguvu zake zisizo na kifani ili kuwasaidia watumishi wake waaminifu. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Hata hivyo, Mungu anasema nasi kwa ukamili zaidi kupitia Neno lake, Biblia. (Isaya 30:21) Kwa namna fulani, Biblia ni kama ile “sauti tulivu, ya chini,” ambayo Yehova anatumia leo kutuongoza, kuturekebisha, kututia moyo, na kutuhakikishia upendo wake.

Je, Eliya alikubali faraja ambayo Yehova alitoa kwenye Mlima Horebu? Bila shaka! Muda si muda, alianza kutenda tena, akiwa nabii mwaminifu na jasiri na kusimama imara dhidi ya uovu wa ibada ya uwongo. Ikiwa tutatafakari kwa uzito maneno haya, “faraja kutokana na Maandiko,” ambayo yameongozwa na roho ya Mungu, tutaweza kuiga imani ya Eliya.—Waroma 15:4.

[Maelezo ya Chini]

^ Ona makala “Igeni Imani Yao” “Alitetea Ibada Safi” na pia makala “Alikaa Macho, na Alingoja” chini ya mfululizo wenye kichwa “Igeni Imani Yao” kwenye Mnara wa Mlinzi wa Januari 1 na Aprili 1, 2008.

^ “Sauti tulivu, ya chini” inaweza kuwa ya yule malaika aliyetumiwa kupeleka “neno la Yehova” anayetajwa katika 1 Wafalme 19:9. Mstari wa 15 unamtaja “Yehova” ambaye anawakilishwa na, malaika huyo. Huenda tukakumbuka mjumbe kutoka kwa Yehova ambaye alitumiwa kuwaongoza Waisraeli nyikani na ambaye Mungu alisema hivi kumhusu: “Jina langu limo ndani yake.” (Kutoka 23:21) Bila shaka, hatuwezi kusema kwa hakika kabisa kuhusu hilo, hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba kabla ya kuwa binadamu, Yesu alitumika akiwa “Neno,” Msemaji maalumu wa Yehova kwa watumishi wake.—Yohana 1:1.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Yehova alimbariki sana Eliya, nyakati nzuri na mbaya

[Picha katika ukurasa wa 20]

Akiwa amesononeka sana, Eliya alimweleza Yehova yote yaliyokuwa moyoni mwake

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yehova alitumia nguvu zake zisizo na kifani kumfariji na kumtia moyo Eliya