Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Kweli Mungu Anaona Jamii Moja Kuwa Bora Kuliko Nyingine?

Je, Kweli Mungu Anaona Jamii Moja Kuwa Bora Kuliko Nyingine?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Kweli Mungu Anaona Jamii Moja Kuwa Bora Kuliko Nyingine?

▪ Hapana. Biblia inasema hivi waziwazi: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

Maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo ni bora zaidi kuliko ya wanadamu wasio wakamilifu. Watu wengi wanaamini kwamba jamii moja (hasa yao) ni bora kuliko jamii nyingine. Ubaguzi kama huo unapatana na maoni ya Charles Darwin, aliyeandika: “Kuna uwezekano mkubwa kwamba wakati fulani ujao, . . . jamii za wanadamu zilizostaarabika zitaangamiza zile ambazo hazijastaarabika.” Kwa kusikitisha, jamii nyingi zimekandamizwa na watu wa jamii nyingine wanaojiona kuwa bora.

Je, maoni ya kwamba jamii fulani ni bora kuliko jamii nyingine yana msingi wowote? Kwa mfano, je, wanasayansi wamethibitisha kupitia uchunguzi wa chembe za urithi kwamba jamii fulani ni bora na nyingine ni duni? Bryan Sykes, mchunguzi wa chembe za urithi na profesa wa chuo kikuu cha Oxford, anasema: “Hakuna msingi wowote unaotegemea chembe za urithi wa kutenganisha watu kulingana na kabila au jamii zao. . . . Mara nyingi mimi huulizwa kama kuna DNA [chembe za urithi] za Wagiriki au Waitaliano, lakini hakuna kitu kama hicho. . . . Sote tuna uhusiano wa karibu.”

Habari hizo zinapatana na Maandiko. Biblia inafundisha kwamba Mungu aliumba mwanamume na mwanamke mmoja tu, na sote ni wazao wa watu hao wawili. (Mwanzo 3:20; Matendo 17:26) Kwa hiyo, machoni pa Mungu kuna jamii moja tu—jamii ya kibinadamu.

Kwa Yehova, rangi ya ngozi na sura ya mtu ni mambo yasiyo na maana hata kidogo. Yeye anathamini kitu fulani ambacho ni muhimu zaidi—moyo wetu wa mfano, au jinsi moyo wetu ulivyo. Anasema: “Watu wanahukumu wengine kulingana na sura yao, lakini mimi huwahukumu watu kulingana na yale yaliyo katika mioyo yao.” (1 Samweli 16:7, Contemporary English Version) Tunaweza kutiwa moyo sana kukumbuka jambo hilo. Jinsi gani?

Hata tuwe wa jamii gani, wengi wetu hatupendezwi na mambo fulani kuhusu sura yetu, lakini tuna uwezo mdogo sana wa kubadili mambo hayo. Hata hivyo, tunaweza kubadili mambo yaliyo muhimu zaidi—mawazo na maoni ya moyo wetu. (Wakolosai 3:9-11) Ikiwa tutajichunguza kwa unyofu, huenda tukatambua kwamba tuna mwelekeo wa kujiona kuwa bora, au hata wa hali ya chini, tunapojilinganisha na jamii nyingine. Kwa kuwa maoni hayo mawili hayapatani na maoni ya Mungu, tunapaswa kujitahidi sana kuyaondoa kabisa katika moyo wetu.—Zaburi 139:23, 24.

Tunapojitahidi kujiona na kuwaona wengine jinsi Yehova anavyotuona na anavyowaona, tuna hakika kwamba atatusaidia. Neno lake linatukumbusha: “Kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Hilo ni kweli hata iwe sisi ni wa jamii gani.