Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ni Nani Aliyetunga Sheria Zinazoongoza Ulimwengu Wetu?

Ni Nani Aliyetunga Sheria Zinazoongoza Ulimwengu Wetu?

Ni Nani Aliyetunga Sheria Zinazoongoza Ulimwengu Wetu?

“JE! UNAZIJUA amri zilizoamuriwa mbingu?” (Ayubu 38:33, Union Version) Mungu alimuuliza Ayubu swali hilo ili amsaidie mtumishi huyo aliyefadhaika kuelewa kwamba ujuzi wa mwanadamu ni mdogo sana ukilinganishwa na hekima ya Muumba isiyo na kifani. Una maoni gani kuhusu ulinganisho huo?

Wanadamu wamejifunza mambo mengi sana kuhusu sheria zinazoongoza mbingu zenye nyota, lakini wanasayansi wengi watakubali mara moja kwamba bado kuna mambo mengi zaidi ya kujifunza. Uvumbuzi mpya umewafanya wanasayansi wafikirie tena na tena nadharia zao kuhusu mwendo wa nyota na sayari. Je, uvumbuzi huo mpya umefanya swali ambalo Mungu alimuuliza Ayubu lisiwe na maana yoyote? Au unathibitisha kwamba Yehova ndiye Chanzo cha sheria zinazoongoza mbingu?

Biblia ina habari zenye kuvutia zinazotusaidia kujibu maswali hayo. Ni kweli kwamba Biblia haidai kuwa kitabu cha kisayansi. Hata hivyo, inapozungumza kuhusu mbingu zenye nyota, inataja mambo fulani sahihi kabisa kisayansi, ambayo mwanadamu alivumbua maelfu ya miaka baadaye.

Mambo Ambayo Wengine Walisema Kuhusu Ulimwengu

Ili kuelewa yale ambayo Biblia inasema kuhusu ulimwengu, acheni turudi nyuma hadi karne ya nne K.W.K., karne moja hivi baada ya kuandikwa kwa Agano la Kale—sehemu ya Biblia iliyoandikwa kwa Kiebrania. Wakati huo, Aristoto, mwanafalsafa Mgiriki alikuwa akiwafundisha wasomi mashuhuri wa siku zake kuhusu mbingu zenye nyota. Leo, bado anaonwa kuwa mmoja kati ya wanasayansi wenye uvutano mkubwa zaidi duniani. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 25.) Kitabu kimoja cha marejeo (Encyclopædia Britannica) kinasema, “Aristoto ndiye mwanasayansi wa kwanza wa kweli katika historia. . . . Kila mwanasayansi anapaswa kuthamini mambo ambayo Aristoto alitimiza.”

Aristoto alichora kwa makini mchoro ulioonyesha jinsi ulimwengu wetu ulivyo. Kwenye mchoro huo, alionyesha kuwa dunia ndiyo kitovu cha ulimwengu na imezungukwa na miviringo ya fuwele zaidi ya 50 yenye umbo la pete, moja ndani ya nyingine. Nyota zilikuwa zimeshikizwa kwenye mviringo ulio mbali zaidi na dunia, nazo sayari kwenye miviringo iliyo karibu na dunia. Alisema kwamba vitu vingine vyote isipokuwa dunia, ni vya milele na havibadiliki. Huenda mambo hayo yakasikika kuwa ya ajabu leo, lakini yaliathiri maoni ya wanasayansi kwa miaka 2,000 hivi.

Hata hivyo, mafundisho ya Aristoto yana tofauti gani na ya Biblia? Ni mafundisho gani ambayo yamethibitika kuwa ya kweli? Acheni tuchunguze maswali matatu kuhusu sheria zinazoongoza ulimwengu wetu. Majibu ya maswali hayo yatatusaidia kuwa na imani katika Mtungaji wa Biblia, ambaye ndiye aliyetunga “sheria za mbingu.”—Ayubu 38:33.

1. Je, Ulimwengu Unabadilika?

Aristoto alisema kwamba miviringo iliyozunguka dunia haingeweza kubadilika. Kama vile tu miviringo mingine, ukubwa wa mviringo ulioshikilia nyota mahali pake haungeweza kuongozeka wala kupungua.

Je, Biblia inakubaliana na wazo hilo? Hapana. Biblia haitoi kauli ya moja kwa moja kuhusu wazo hilo. Hata hivyo, ona ufafanuzi wake wenye kuvutia: “Kuna Yeye anayekaa juu ya mviringo wa dunia, ambayo wakaaji wake ni kama panzi, Yeye anayetandaza mbingu kama shashi bora, anayezitandaza kama hema la kukaliwa ndani.”—Isaya 40:22. *

Ni jambo gani linalokubalika leo kati ya mambo hayo mawili—mchoro wa Aristoto au ufafanuzi wa Biblia? Wanakosmolojia wa kisasa (watafiti kuhusu chanzo cha ulimwengu) wana maoni gani kuhusu ulimwengu? Katika karne ya 20, wataalamu wa nyota walishangaa walipovumbua kwamba ulimwengu unapanuka. Hata makundi ya nyota yanaonekana kuwa yanasonga kwa kasi sana mbali na mengine. Ni wanasayansi wachache ambao wangefikiri kwamba ulimwengu unapanuka. Leo, wanakosmolojia wanaamini kwamba mwanzoni nyota na sayari zilikuwa karibu-karibu sana, lakini zimekuwa zikisonga kuelekea sehemu tofauti-tofauti. Kwa kweli, kulingana na sayansi, mchoro wa Aristoto umepitwa na wakati.

Namna gani ufafanuzi wa Biblia? Si vigumu kuwazia nabii Isaya akitazama juu angani na kuona kwamba mbingu zenye nyota zinafanana na hema maridadi lilitotandazwa juu. * Huenda pia aliona kwamba kikundi cha nyota cha Kilimia kinafanana na “shashi bora.”

Zaidi ya hayo, maneno ya Isaya yanatuchochea tupige picha akilini. Tunaweza kuwazia jinsi hema lilivyokuwa nyakati za Biblia; labda tunawazia tu kitambaa kigumu kinachoonekana kuwa kidogo kikikunjuliwa na kutandazwa juu ya nguzo ili kutengeneza makao. Vivyo hivyo, tunaweza kuwazia mfanyabiashara akiinua shashi bora na kuitandaza ili mnunuzi aweze kuichunguza. Katika mifano yote miwili, kitu kinachoonekana kuwa kidogo kinakuwa kikubwa kinapotandazwa.

Kwa kweli, hatusemi kwamba mfano huo wa Biblia kuhusu hema na shashi bora unakusudiwa kufafanua jinsi ulimwengu unavyopanuka. Hata hivyo, je, si jambo linalovutia kwamba Biblia inafafanua ulimwengu katika njia inayopatana vizuri na sayansi ya kisasa? Isaya aliishi zaidi ya miaka mia tatu kabla ya Aristoto, na zaidi ya miaka 2,000 kabla sayansi haijathibitisha mambo hayo. Lakini, ufafanuzi ulioandikwa na nabii huyo Mwebrania ambaye hakuwa mtaalamu wa mambo ya sayari na nyota, hauhitaji kurekebishwa kama ule mchoro wa Aristoto.

2. Ni Nini Kinachoshikilia Nyota na Sayari Mahali Pake?

Kulingana na Aristoto, ulimwengu ulikuwa umejaa kabisa. Alifikiri kwamba dunia na anga-hewa yake zimefanyizwa kwa vitu vinne—dunia, maji, hewa, na moto. Nje ya eneo la dunia kulikuwa na miviringo ya fuwele yenye umbo la pete, iliyofanyizwa kwa kitu chenye kudumu milele alichokiita ether. Nyota na sayari zilikuwa zimeshikizwa kwenye miviringo hiyo. Kwa miaka mingi, wanasayansi walikubaliana na maoni ya Aristoto kwa sababu yalipatana na dhana hii ya msingi: Lazima kitu kiwekwe juu ya kingine au kishikiliwe, la sivyo kitaanguka.

Namna gani Biblia? Ina maneno ya mwanamume mwaminifu Ayubu, aliyesema hivi kumhusu Yehova: ‘Anaitundika dunia pasipo na kitu.’ (Ayubu 26:7) Bila shaka, Aristoto angeliona wazo kama hilo kuwa la kipuuzi.

Katika karne ya 17 W.K., miaka 3,000 hivi baada ya siku za Ayubu, wanasayansi wengi walikuwa na maoni kwamba ulimwengu haukuwa umejaa miviringo, bali umajimaji fulani. Hata hivyo, mwishoni mwa karne hiyo, mwanafizikia Sir Isaac Newton alidokeza wazo tofauti kabisa. Alisema nguvu za uvutano zilifanya nyota na sayari zivutane. Hivyo, Newton alikuwa amekaribia sana kutambua kwamba dunia, nyota, na sayari nyingine zilining’inia tu angani, “pasipo na kitu.”

Maoni ya Newton kuhusu nguvu za uvutano yalipingwa sana. Bado ilikuwa vigumu kwa wanasayansi wengi kuamini kwamba nyota na sayari nyingine hazikushikiliwa na kitu. Ingewezekana jinsi gani dunia yetu kubwa au sayari nyingine zining’inie pasipo na kitu? Wengine waliona jambo hilo kuwa linawezekana tu kwa nguvu zisizo za kibinadamu. Tangu siku za Aristoto, wanasayansi wengi waliamini kwamba anga lazima liwe limejaa kitu fulani.

Ayubu hakujua chochote kuhusu nguvu zisizoonekana ambazo zinaifanya dunia ibaki mahali pake na isiyumbeyumbe inapolizunguka jua. Hivyo basi, ni nini kilichomwongoza kusema kwamba dunia yetu inaning’inia “pasipo na kitu”?

Isitoshe, wazo la kwamba hakuna kitu kinachoishikilia dunia mahali pake linatokeza swali lingine: Ni nini kinachoongoza dunia, nyota, na sayari nyingine katika mizunguko yake? Ona maneno yenye kuvutia ambayo Mungu alimwambia Ayubu: “Je, unaweza kufunga vifungo vya kundi-nyota la Kima, au, je, unaweza kufungua kamba za kundi-nyota la Kesili?” (Ayubu 38:31) Katika maisha yake marefu, Ayubu aliona makundi hayo ya nyota yakitokea na kutoweka, usiku baada ya usiku. * Lakini kwa nini yalionekana vilevile, mwaka baada ya mwaka, miaka baada ya miaka? Ni vifungo gani vilivyofunga nyota hizo na sayari nyingine mahali pake? Bila shaka, Ayubu alistaajabu sana alipowazia mambo hayo.

Kama nyota zingekuwa zimeshikizwa kwenye miviringo fulani, vifungo ambavyo Ayubu alitaja havingehitajika. Miaka 2,000 hivi ilipita kabla ya wanasayansi kupata ujuzi zaidi kuhusu “vifungo” au “kamba” hizo zisizoonekana ambazo zinashikilia nyota na sayari mahali pake, wakati zinaposonga angani. Isaac Newton na baadaye Albert Einstein walipata umaarufu kwa uvumbuzi wao kuhusu jambo hilo. Kwa kweli, Ayubu hakujua lolote kuhusu nguvu ambazo Mungu anatumia kushikilia makundi ya nyota na sayari mahali pake. Hata hivyo, baada ya maelfu ya miaka, maneno ya kitabu cha Ayubu yaliyoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu yamethibitika kuwa ya kweli tofauti na maoni ya msomi Aristoto. Hakuna mwingine anayeweza kuwa na hekima kama hiyo isipokuwa tu Mtungaji wa sheria zinazoongoza mbingu.

3. Je, Ulimwengu Unadumu Milele au Unaweza Kuharibika?

Aristoto aliamini kwamba kuna tofauti kubwa kati ya mbingu zenye nyota na dunia. Alisema kwamba dunia inaweza kubadilika, kuharibika, na kuchakaa, lakini mbingu zenye nyota haziwezi kubadilika, zinadumu milele. Aliamini kuwa miviringo aliyotaja na nyota ambazo zimeshikizwa kwenye miviringo hiyo haziwezi kubadilika, kuchakaa, wala kutoweka.

Je, Biblia inafundisha hivyo? Andiko la Zaburi 102:25-27 linasema: “Wewe uliiweka misingi ya dunia zamani za kale, nazo mbingu ni kazi ya mikono yako. Hizo zitaangamia, lakini wewe mwenyewe utaendelea kusimama; nazo zote zitachakaa kama vazi. Utazibadili kama mavazi, nazo zitamaliza zamu yake. Lakini wewe ni yuleyule, nayo miaka yako mwenyewe haitamalizika.”

Ona kwamba mtunga-zaburi huyo aliyeandika maneno hayo yapata miaka 200 kabla ya siku za Aristoto, hasemi kuna tofauti kati ya dunia na mbingu zenye nyota, kana kwamba dunia inaweza kuharibika na nyota kudumu milele. Badala yake, anaonyesha kwamba mbingu na dunia ni tofauti kabisa na Yehova Mungu. Hivyo, Yehova ambaye ni Roho mwenye nguvu ndiye aliyeelekeza mbingu na dunia ziumbwe. * Zaburi hii inaonyesha kwamba nyota zinaweza kuharibika sawa na vitu vingine duniani. Lakini wanasayansi wa kisasa wamevumbua nini?

Wanajiolojia (wataalamu wa miamba ya dunia) wanaunga mkono maoni ya Biblia na ya Aristoto kwamba dunia inaweza kuharibika. Bila shaka, mawe ya dunia yetu yanaendelea kumomonyoka na mengine kutokea kupitia milipuko ya volkano na mabadiliko mengine yanayotokea katika miamba iliyo chini ya ardhi.

Namna gani nyota? Je, zinaweza kuharibika, kama Biblia inavyodokeza, au zinadumu milele, kama Aristoto alivyofundisha? Katika karne ya 16 W.K., wataalamu wa nyota barani Ulaya walianza kutilia shaka maoni ya Aristoto kwamba nyota zinadumu milele wakati ambapo, kwa mara ya kwanza, waliona nyota ikilipuka. Tangu wakati huo wanasayansi wametambua kwamba nyota zinaweza kulipuka kwa nguvu na kutoweka au kuteketea polepole, au hata kuzimika. Lakini, wataalamu wa nyota wameona nyota mpya zikitokea kwenye mawingu ya gesi ambayo yanafanywa kuwa mazito na vumbi linalotokana na nyota zilizolipuka. Hivyo, mfano wa mwandikaji wa Biblia kuhusu vazi linalochakaa na kubadilishwa unafaa kabisa. * Ni jambo la ajabu kama nini kwamba mtunga-zaburi huyo wa kale aliandika maneno yanayopatana vizuri na uvumbuzi wa siku hizi!

Hata hivyo, huenda ukauliza: ‘Je, Biblia inafundisha kwamba wakati fulani dunia au mbingu zenye nyota zitafikia kikomo au zihitaji kubadilishwa?’ Hapana, Biblia inaahidi kwamba zitadumu milele. (Zaburi 104:5; 119:90) Lakini hilo halimaanishi kwamba vitu hivyo ni vya milele; badala yake, Mungu aliyeviumba ameahidi kuvidumisha. (Zaburi 148:4-6) Hasemi jinsi atakavyofanya hivyo, lakini ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba Muumba wa ulimwengu ana uwezo wa kuudumisha, sawa na vile mjenzi stadi anavyoweza kuitunza vizuri nyumba aliyojenga kwa ajili yake mwenyewe na familia yake.

Ni Nani Anayestahili Utukufu na Heshima?

Kutafakari kuhusu sheria chache za mbingu kunatusaidia kuelewa jibu la swali hilo. Je, hatustaajabu tunapotafakari kumhusu yule aliyeziweka nyota zisizo na hesabu angani, anayezishikilia mahali pake kwa kutumia nguvu za uvutano, na anayezidumisha katika mzunguko wake usio na kikomo?

Yamkini andiko la Isaya 40:26 linatoa sababu nzuri zinazofanya tustaajabu: “Inueni macho yenu juu, mwone. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina.” Nyota zinalinganishwa na jeshi linaloweza kuwa na wanajeshi wengi sana. Bila kamanda wa kutoa maagizo, jeshi hilo linaweza kuwa tu kama umati wenye vurugu. Bila sheria kutoka kwa Yehova, sayari, nyota, na makundi ya nyota hayangeweza kufuata njia zake kwa utaratibu; mambo yangevurugika. Lakini, wazia jeshi lenye mabilioni ya wanajeshi ambalo lina Kamanda anayetoa maagizo kuhusu mahali wanapopaswa kwenda na anayejua jina la kila mmoja wao, mahali alipo, na hali zake kwa undani!

Sheria za mbingu zinatusaidia kuelewa hekima isiyo na kifani ya Kamanda huyo. Ni nani mwingine ambaye angetunga sheria kama hizo na kuwaongoza watu kwa roho yake waziandike kwa usahihi karne nyingi na hata maelfu ya miaka kabla wanasayansi hawajazielewa? Bila shaka basi, tuna kila sababu ya kumpa Yehova “utukufu na heshima.”—Ufunuo 4:11.

[Maelezo ya Chini]

^ Ni jambo la ajabu kwamba Biblia inasema dunia ni mviringo, au duara, kama vile neno la Kiebrania linavyoweza kutafsiriwa pia. Aristoto na Wagiriki wengine wa kale walifikiri vivyo hivyo, lakini maoni hayo yalitokeza mjadala ulioendelea kwa zaidi ya miaka 2,000 baadaye.

^ Mfano huu unatumiwa mara nyingi katika Biblia.​—Ayubu 9:8; Zaburi 104:2; Isaya 42:5; 44:24; 51:13; Zekaria 12:1.

^ Huenda “kundi-nyota la Kima” linarejelea kundi la nyota linaloitwa Pleiades, nalo “kundi-nyota la Kesili,” linarejelea kundi la nyota linaloitwa Orion. Inachukua makumi ya maelfu ya miaka kwa nyota kama hizo kubadilika kabisa.

^ Kwa kuwa Yehova alimtumia Mwana wake mzaliwa-pekee kama “stadi wa kazi” ili kuumba vitu vyote, maneno ya andiko hili yanaweza pia kumrejelea Mwana.​—Methali 8:30, 31; Wakolosai 1:15-17; Waebrania 1:10.

^ Katika karne ya 19, mwanasayansi William Thomson, ambaye pia anaitwa Lord Kelvin, alivumbua sheria ya pili kuhusu uhusiano kati ya joto na aina nyingine za nishati, inayoeleza kwa nini baada ya muda, mfumo wa asili huanza kuharibika na kubadilika. Alielewa sheria hiyo baada ya kuchunguza kwa makini Zaburi 102: 25-27.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Mafundisho Yenye Uvutano Mkubwa

“Aristoto alikuwa mwanafalsafa na mwanasayansi maarufu sana katika ulimwengu wa kale,” kinasema kitabu The 100​—A Ranking of the Most Influential Persons in History. Unaweza kuona ni kwa nini inasemwa hivyo kumhusu mtu huyu asiye wa kawaida. Aristoto (384-322 K.W.K.) alikuwa mwanafunzi wa mwanafalsafa maarufu, Pilato. Baadaye Aristoto alimfundisha Aleksanda, mwana wa mfalme, ambaye alikuja kuwa Aleksanda Mkuu. Kulingana na orodha za kale, Aristoto aliandika vitabu 170 hivi, na 47 kati ya vitabu hivyo vinapatikana leo. Aliandika mambo mengi kuhusu nyota, biolojia, kemia, zuolojia, fizikia, jiolojia, na saikolojia. Aristoto aliandika habari nyingi sana na zenye kuvutia kuhusu viumbe hai fulani muda mrefu kabla ya mtu mwingine yeyote kufanya uvumbuzi kuhusu viumbe hivyo. “Mafundisho ya Aristoto yaliathiri sana maoni ya watu wa Magharibi,” kinasema kitabu The 100. Hata hivyo, kitabu hicho kinaongeza kusema: “Heshima ambayo watu walimpa Aristoto katika enzi za kati ilikuwa kubwa sana hivi kwamba walikuwa karibu kumwabudu.”

[Hisani]

Royal Astronomical Society / Photo Researchers, Inc.

From the book A General History for Colleges and High Schools, 1900

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Nguvu za uvutano zinashikilia nyota na sayari mahali pake

[Hisani]

NASA and The Hubble Heritage Team (AURA/​STScl)

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Kundi la nyota linaloitwa Pleiades

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nyota nyingi hulipuka

[Hisani]

ESA/​Hubble

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nyota hutokea katika wingu la gesi

[Hisani]

J. Hester and P. Scowen (AZ State Univ.), NASA

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 24]

© Peter Arnold, Inc./Alamy