Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Utatii Maonyo Yaliyo Wazi Kutoka Kwa Yehova?

Je, Utatii Maonyo Yaliyo Wazi Kutoka Kwa Yehova?

Je, Utatii Maonyo Yaliyo Wazi Kutoka Kwa Yehova?

“Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”—ISA. 30:21.

1, 2. Shetani ameazimia kufanya nini, na Neno la Mungu linatusaidia jinsi gani?

 ISHARA ya barabarani ambayo inaelekeza upande usiofaa inapotosha na pia inaweza kusababisha hatari. Wazia kwamba rafiki anakuonya kuwa mtu fulani mwovu amebadili kimakusudi ishara ya barabarani kwa sababu anataka kuwaumiza wasafiri ambao hawajui njia. Bila shaka, utatii onyo la rafiki yako.

2 Kwa kweli, Shetani ni adui mwovu ambaye ameazimia kutudanganya. (Ufu. 12:9) Shetani ndiye anayesababisha hatari zote ambazo tumezungumzia katika habari iliyotangulia na hatari hizo zinakusudiwa kutufanya tuache barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele. (Mt. 7:13, 14) Tunashukuru kwamba Mungu wetu mwenye upendo anatuonya ili tusifuate ‘ishara za barabarani’ zenye kupotosha ambazo Shetani anatumia ili kutudanganya. Acheni sasa tuzungumzie hatari nyingine tatu ambazo Shetani anatumia ili kutudanganya. Tunapochunguza jinsi Neno la Mungu linavyotusaidia kuepuka kudanganywa, tunaweza kuwazia Yehova akitembea nyuma yetu na kutuelekeza upande unaofaa, akisema hivi: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.” (Isa. 30:21) Kutafakari kuhusu maonyo yaliyo wazi ya Yehova kutatusaidia kuazimia zaidi kuyatii.

Usiwafuate “Walimu wa Uwongo”

3, 4. (a) Kwa nini walimu wa uwongo ni kama visima ambavyo vimekauka? (b) Walimu wengi wa uwongo wanatoka wapi, na wanataka nini?

3 Wazia kwamba unasafiri katika jangwa. Kwa mbali, unaona kisima, na unaenda kwenye kisima hicho kwa sababu unafikiri kwamba utapata maji ya kumaliza kiu chako. Lakini unapofika kwenye kisima hicho, unaona kwamba kimekauka. Unavunjika moyo kama nini! Walimu wa uwongo ni kama visima ambavyo vimekauka. Mtu yeyote ambaye anaenda kutafuta maji ya kweli kutoka kwao atavunjika moyo kabisa. Kupitia mtume Paulo na Petro, Yehova anatuonya kuhusu walimu wa uwongo. (Soma Matendo 20:29, 30; 2 Petro 2:1-3.) Walimu hao wa uwongo ni nani? Maneno ya mitume hao wawili yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanatusaidia kutambua walimu wa uwongo wanatoka wapi na jinsi wanavyowadanganya watu.

4 Paulo aliwaambia hivi wazee wa kutaniko la Efeso: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka.” Naye Petro alisema hivi katika barua ambayo aliwaandikia Wakristo wenzake: ‘Kutakuwa na walimu wa uwongo katikati yenu.’ Kwa hiyo, walimu wa uwongo wanatoka wapi? Wanaweza kutoka ndani ya kutaniko. Walimu hao wa uwongo ni waasi-imani. * Wanataka nini? Hawatosheki tu kuacha tengenezo ambalo huenda mwanzoni walilipenda. Paulo alieleza kwamba kusudi lao ni “kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” Wanafunzi ambao Paulo anazungumzia ni wanafunzi wa Yesu Kristo. Badala ya kwenda kutafuta wanafunzi wao wenyewe, waasi-imani wanajaribu kuchukua au kuiba wanafunzi wa Kristo. Yesu alisema kwamba walimu wa uwongo ni kama “mbwa-mwitu wenye kunyafua” ambao wanatafuta kuwameza washiriki wa kutaniko wanaowafuata na hivyo kuharibu imani yao na kuwafanya waache kweli.—Mt. 7:15; 2 Tim. 2:18.

5. Walimu wa uwongo wanatumia njia gani mbalimbali?

5 Walimu wa uwongo wanawadanganya watu jinsi gani? Njia wanazotumia zinaonyesha kwamba ni wajanja sana. Waasi-imani ‘wanaingiza kimya-kimya’ mawazo yenye kupotosha ndani ya kutaniko. Kama watu wanaofanya biashara ya magendo, wanaingiza kisiri-siri maoni ya uasi-imani kwa njia ya ujanja. Na kama vile mhalifu mjanja anavyojaribu kufanya vyeti vya uwongo vionekane kuwa ni vya kweli, ndivyo waasi-imani wanavyotumia “maneno yasiyo ya kweli,” au mawazo ya uwongo, kujaribu kufanya maoni yao ya uwongo yaonekane kuwa ya kweli. Wanaeneza ‘mafundisho ya udanganyifu,’ ‘wakiyapotosha Maandiko’ ili yalingane na mawazo yao wenyewe. (2 Pet. 2:1, 3, 13; 3:16) Ni wazi kwamba waasi-imani hawatujali hata kidogo. Tukiwafuata, tutaacha tu barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele.

6. Biblia inatupatia onyo gani lililo wazi kuhusu walimu wa uwongo?

6 Tunaweza kujilinda wenyewe jinsi gani kutokana na walimu wa uwongo? Biblia inatupatia mashauri yaliyo wazi kuhusu jinsi ya kushughulika nao. (Soma Waroma 16:17; 2 Yohana 9-11.) Neno la Mungu linasema hivi: “Mjiepushe nao.” Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kukaa mbali nao! Shauri hilo ambalo liliongozwa na roho ya Mungu liko wazi kabisa. Tuseme kwamba daktari anakuambia uepuke kumkaribia mtu ambaye ana ugonjwa hatari wenye kuambukiza. Utaelewa kile ambacho daktari huyo anamaanisha, na utatii kabisa onyo lake. Kwa kweli, waasi-imani ni ‘wagonjwa kiakili,’ na wanajaribu kuwaambukiza wengine mafundisho yao ya uwongo. (1 Tim. 6:3, 4) Yehova, ambaye ndiye Daktari Mkuu, anatuambia tuwaepuke kabisa waasi-imani. Tunajua hilo linamaanisha nini, lakini je, tumeazimia kutii onyo lake katika kila njia?

7, 8. (a) Ni lazima tufanye nini ili tuwaepuke walimu wa uwongo? (b) Kwa nini umeazimia kuwaepuka kabisa walimu wa uwongo?

7 Ni lazima tufanye nini ili tuwaepuke walimu wa uwongo? Hatuwasalimu au kuwakaribisha katika nyumba zetu. Pia, tunakataa kusoma vitabu vyao, kutazama vipindi vyao kwenye televisheni, kuchunguza vituo vyao katika Intaneti, au kutoa maoni yetu kuhusu habari ambazo wanaandika katika Intaneti. Kwa nini tumeazimia kabisa kuwaepuka? Kwa sababu tunampenda “Mungu wa ukweli.” Kwa hiyo, hatutaki kusikiliza mafundisho yaliyopotoshwa ambayo yanapingana na Neno lake la kweli. (Zab. 31:5; Yoh. 17:17) Pia, tunapenda tengenezo la Yehova, ambalo ametumia kutufundisha kweli zenye kusisimua, kama vile jina la Yehova na maana yake, kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia, hali ya wafu, na tumaini la ufufuo. Je, unakumbuka jinsi ulivyofurahi sana ulipojifunza kwa mara ya kwanza kweli hizo na kweli nyingine zenye thamani? Basi, kwa nini ukubali kudanganywa na mtu yeyote ambaye anadharau tengenezo ambalo lilikufundisha kweli hizo?—Yoh. 6:66-69.

8 Hata walimu wa uwongo waseme nini, hatutawafuata! Kwa nini twende kwenye visima hivyo ambavyo vimekauka ili kudanganywa tu na kukatishwa tamaa? Badala yake, acheni tuazimie kubaki washikamanifu kwa Yehova na kwa tengenezo lake ambalo kwa muda mrefu limekuwa likitupatia maji safi yenye kuburudisha ya kweli kutoka katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake ambayo yanamaliza kiu chetu.—Isa. 55:1-3; Mt. 24:45-47.

Usifuate “Hadithi za Uwongo”

9, 10. Paulo alimpa Timotheo onyo gani kuhusu “hadithi za uwongo,” na huenda Paulo alikuwa akifikiria nini? (Ona pia maelezo ya chini.)

9 Nyakati fulani, si rahisi kutambua kwamba ishara ya barabarani imebadilishwa na inaelekeza upande usiofaa. Nyakati nyingine, inaweza kuwa vigumu kutambua uwongo. Ndivyo ilivyo na uwongo wa Shetani; tusipokuwa waangalifu, anaweza kutudanganya kwa urahisi na mambo fulani ya uwongo. Mtume Paulo anatuonya kuhusu moja ya njia au mbinu za werevu za Shetani, “hadithi za uwongo.” (Soma 1 Timotheo 1:3, 4.) Ili tusipotoshwe kutoka kwenye barabara inayoongoza kwenye uzima, tunahitaji kujua hadithi za uwongo ni nini, na jinsi tunavyoweza kuepuka kuzisikiliza.

10 Onyo la Paulo kuhusu hadithi za uwongo liko katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, mwangalizi Mkristo ambaye alipewa daraka la kulinda usafi wa kutaniko na kuwasaidia waamini wenzake kubaki waaminifu. (1 Tim. 1:18, 19) Paulo anatumia neno la Kigiriki ambalo linamaanisha hadithi ya kutungwa, au uwongo. Kitabu kimoja (The International Standard Bible Encyclopaedia) kinasema kwamba neno hilo linahusu “hadithi (ya kidini) ambayo haina uhusiano wowote na mambo halisi.” Labda Paulo alikuwa akifikiria kuhusu uwongo wa kidini ambao ulienezwa na hadithi za zamani zenye kusisimua ambazo watu walitunga au kuwazia tu. * Hadithi kama hizo ‘zinatokeza tu maswali ya utafiti,’ yaani, zinatokeza maswali au maulizo ambayo yanawafanya watu wafanye utafiti usio na maana yoyote. Hadithi za uwongo zinatumiwa na Shetani, yule mwongo mkubwa, ambaye anatumia uwongo wa kidini na hadithi ambazo hazimpendezi Mungu ili kuwapotosha watu wasiojua. Shauri la Paulo liko wazi: Usisikilize hadithi za uwongo!

11. Shetani ametumia jinsi gani dini ya uwongo kwa werevu ili kuwadanganya watu, na tunapaswa kutii onyo gani ili tusidanganywe?

11 Ni hadithi gani za uwongo ambazo zinaweza kutudanganya tusipokuwa waangalifu? Tunaweza kusema kwamba “hadithi za uwongo” ni fundisho lolote la kidini au hadithi ya kutungwa ya kidini ambayo inaweza kugeuza masikio yetu “kutoka kwenye kweli.” (2 Tim. 4:3, 4) Shetani, ambaye anajifanya kuwa “malaika wa nuru,” amekuwa akitumia kwa werevu dini ya uwongo ili kuwadanganya watu. (2 Kor. 11:14) Dini zinazodai kuwa za Kikristo zinasema kwamba zinamfuata Kristo, lakini zinafundisha mafundisho ya uwongo ambayo yanategemea hadithi za uwongo, kama vile Utatu, moto wa mateso, na kutokufa kwa nafsi. Dini hizo pia zinaendeleza sikukuu kama vile Krismasi na Ista, ambazo zinaonekana kuwa desturi nzuri lakini kwa kweli zinatokana na upagani na hadithi za kutungwa. Hatutadanganywa na hadithi za uwongo ikiwa tutatii onyo la Mungu la kujitenga na ‘kuacha kugusa kitu kilicho najisi.’—2 Kor. 6:14-17.

12, 13. (a) Shetani ameeneza uwongo gani mbalimbali, na ukweli ni nini kuhusu kila moja ya uwongo huo? (b) Ni lazima tufanye nini ikiwa hatutaki kudanganywa na hadithi za uwongo za Shetani?

12 Shetani ameeneza uwongo mwingine mwingi ambao unaweza kutupotosha tusipokuwa waangalifu. Fikiria mifano mitatu. Uwongo wa kwanza ni huu: Unaweza kufanya jambo lolote unalotaka; amua mwenyewe mambo yanayofaa na yale yasiyofaa. Mara nyingi tunasikia hivyo katika televisheni, sinema, vitabu, magazeti, na katika Intaneti. Kwa kuwa tunasikia uwongo huo kila wakati, ni rahisi kwetu kuanza kufikiri kwa njia hiyo na kufuata mawazo ya ulimwengu yaliyopotoka kimaadili. Lakini ukweli ni kwamba tunahitaji sana mwongozo kutoka kwa Mungu kuhusu mambo yanayofaa na yale yasiyofaa. (Yer. 10:23) Uwongo wa pili ni huu: Mungu hatabadili kamwe jambo lolote duniani. Tukianza kufuata maoni hayo ya kuishi tu kwa ajili ya leo tunaweza kuwa “wasiotenda au wasiozaa matunda” katika utumishi wetu kwa Mungu. (2 Pet. 1:8) Ukweli ni kwamba siku ya Yehova inakaribia haraka, na ni lazima tuendelee kuitazamia. (Mt. 24:44) Uwongo wa tatu ni huu: Mungu hakujali wewe binafsi. Tukiamini uwongo huo wa Shetani tunaweza kukata tamaa, na kuhisi kwamba hatustahili kamwe kupendwa na Mungu. Ukweli ni kwamba Yehova anampenda na kumthamini kila mtu anayemwabudu.—Mt. 10:29-31.

13 Ni lazima sikuzote tujilinde kwa sababu mawazo na mitazamo ya ulimwengu wa Shetani inaweza kuonekana kwa nje kuwa inafaa. Hata hivyo, kumbuka kwamba Shetani ni hodari katika kudanganya. Tunaweza kuepuka kudanganywa na ‘hadithi za uwongo za Shetani zilizotungwa kwa ufundi [“hadithi zilizotungwa kwa werevu,” The New American Bible],’ kwa kutii tu mashauri na vikumbusho vya Neno la Mungu.—2 Pet. 1:16.

‘Usimfuate Shetani’

14. Paulo aliwapa wajane fulani vijana onyo gani, na kwa nini sisi sote tunahitaji kutii maneno yake?

14 Wazia kwamba kuna ishara ya barabarani inayosema, “Njia Hii Inaongoza kwa Shetani.” Ni nani kati yetu anayeweza kufuata ishara hiyo? Hata hivyo, Paulo anatuonya kuhusu njia mbalimbali ambazo Wakristo waliojiweka wakfu wanaweza ‘kugeuzwa kando na kumfuata Shetani.’ (Soma 1 Timotheo 5:11-15.) Paulo aliwaandikia maneno hayo ‘wajane fulani vijana,’ lakini kanuni ambazo anataja zinatuhusu sisi sote. Huenda Wakristo hao wanawake katika karne ya kwanza hawakufikiri kwamba walikuwa wakimfuata Shetani, lakini matendo yao yalionyesha kwamba kwa kweli walikuwa wakimfuata. Tunaweza jinsi gani kuepuka kumfuata Shetani bila kujua? Acheni tuchunguze onyo la Paulo kuhusu porojo zenye kuumiza.

15. Shetani anataka nini, na Paulo anafunua jinsi gani mbinu au njia za Shetani?

15 Shetani anataka kutunyamazisha ili tusizungumze kuhusu imani yetu. Anataka tuache kuhubiri habari njema. (Ufu. 12:17) Hivyo, anajaribu kutushawishi tufuatie mambo ambayo yanapoteza wakati au kusababisha migawanyiko kati yetu. Ona jinsi Paulo anavyofunua mbinu au njia za Shetani. Paulo alisema kwamba wale wajane wa siku zake ‘hawakuwa na kazi, na walizunguka-zunguka nyumba kwa nyumba.’ Wajane hao walitumia wakati wao mwingi kuwatembelea marafiki wao na kuzungumza kuhusu mambo ambayo hayakuwa na maana. Tunahitaji kuwa waangalifu ili tusifanye hivyo. Kwa mfano, tunaweza kutumia wakati wetu mwingi na wa watu wengine tukisoma na kutuma barua-pepe (e-mail) kuhusu mambo ambayo si ya maana na hata huenda si ya kweli. Paulo alisema pia kwamba wajane hao walikuwa “wenye kupiga porojo.” Porojo zenye kuumiza zinaweza kugeuka na kuwa uchongezi, yaani, kusema uwongo kuhusu watu wengine. Mara nyingi uwongo huo unasababisha ugomvi. (Met. 26:20) Iwe wanajua au hawajui, wale ambao wanaeneza uwongo wenye kuumiza kuhusu wengine wanamwiga Shetani Ibilisi. * Kisha, Paulo alisema kwamba wajane hao ‘walijiingiza katika mambo ya watu wengine.’ Hatuna haki ya kuwaambia wengine jinsi ya kufanya mambo yao ya kibinafsi. Tabia hiyo isiyofaa na inayosababisha matatizo inaweza kutukengeusha kuacha kazi ambayo tumepewa na Mungu ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Tukiacha kufanya kazi ya Yehova kwa bidii, basi tunaanza kumfuata Shetani. Ni lazima kila mmoja wetu achague upande ambao ataunga mkono.—Mt. 12:30.

16. Tunaweza kuepuka ‘kugeuzwa kando kumfuata Shetani’ tukitii shauri gani?

16 Kutii mashauri ya Biblia kunaweza kutusaidia kuepuka ‘kugeuzwa kando na kumfuata Shetani.’ Fikiria mashauri fulani yenye hekima ambayo Paulo alitoa. Alisema kwamba tunapaswa kuwa “na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58) Kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Ufalme kutatulinda tuepuke hatari za kufanya mambo ambayo si ya maana na ambayo yanatupotezea wakati. (Mt. 6:33) Paulo anatuambia pia tuzungumze mambo ‘mema kwa ajili ya kujenga.’ (Efe. 4:29) Azimia kutosikiliza na kutoeneza porojo zenye kuumiza. * Jifunze kuwaamini na kuwaheshimu ndugu na dada zako. Tukifanya hivyo, sikuzote tutasema maneno yenye kujenga badala ya kubomoa. ‘Uwe na shabaha ya kukazia akili mambo yako mwenyewe.’ (1 The. 4:11) Waonyeshe watu kwamba unawajali, lakini fanya hivyo kwa heshima. Kumbuka kwamba huenda kukawa na mambo ya kibinafsi ambayo hawataki kuzungumzia na ambayo hawataki wengine wajue. Pia, kumbuka kwamba hatupaswi kuwalazimisha wengine wafuate maoni yetu katika maamuzi yao ya kibinafsi.—Gal. 6:5.

17. (a) Kwa nini Yehova anatuonya kuhusu mambo ambayo hatupaswi kufuata? (b) Umeazimia kufanya nini kuhusu njia ambayo Yehova anataka tufuate?

17 Tunamshukuru sana Yehova kwa sababu anatuambia waziwazi mambo ambayo hatupaswi kufuata! Hata hivyo, usisahau kamwe kwamba Yehova anatupatia maonyo ambayo tumezungumzia katika habari hii na ile iliyotangulia kwa sababu anatupenda sana. Anataka tuepuke maumivu na taabu ambayo inawapata wale ambao wanafuata ‘ishara za barabarani’ za Shetani ambazo zinapotosha. Huenda njia ambayo Yehova anataka tufuate ina nafasi ndogo, lakini inaongoza mahali bora kabisa, kwenye uzima wa milele. (Mt. 7:14) Ni lazima sikuzote tuazimie kutii shauri hili la Yehova: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”—Isa. 30:21.

[Maelezo ya Chini]

^ “Uasi-imani” ni hali ya kujitenga na ibada ya kweli, kuanguka, kuasi, na kuacha ibada hiyo.

^ Kwa mfano, kitabu cha Tobiti, au Tobia, ambacho kiliandikwa katika karne ya tatu hivi K.W.K. na ambacho kilikuwapo katika siku za Paulo, kimejaa ushirikina na hadithi za ajabu za uchawi ambazo zinaonyeshwa kana kwamba ni za kweli.—Ona Insight on the Scriptures, Buku la 1, ukurasa wa 122 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 1, ukurasa wa 135.

^ Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa kuwa “ibilisi” (di·aʹbo·los), linamaanisha “mchongezi.” Neno hilo linatumiwa kama jina lingine la cheo la Shetani, ambaye ni mchongezi mkuu kuliko wote.—Yoh. 8:44; Ufu. 12:9, 10.

Ungesema Nini?

Wewe binafsi unaweza kutumia jinsi gani maonyo yaliyo katika maandiko yafuatayo?

2 Petro 2:1-3

1 Timotheo 1:3, 4

1 Timotheo 5:11-15

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

 Kutawanya Manyoya Katika Upepo

Kuna hadithi moja ya zamani ya Wayahudi ambayo inaonyesha vizuri matokeo mabaya ya kueneza porojo zenye kuumiza.

Mtu fulani alieneza porojo au uwongo katika kijiji chao kuhusu mtu aliyekuwa na hekima zaidi katika kijiji hicho. Baadaye, yule mtu aliyeeneza porojo hiyo mbaya alitambua kosa lake akaenda kumwona yule mtu mwenye hekima ili kumwomba msamaha. Kwa hiyo, alimuuliza hivi yule mtu mwenye hekima: “Ninaweza kufanya nini ili nikuonyeshe kwamba ninasikitika kwa sababu ya mambo niliyosema kukuhusu?” Yule mtu mwenye hekima akamwambia hivi: “Kuna jambo moja ambalo unaweza kufanya. Chukua mto wa kulalia ambao umejaa manyoya. Upasue mto huo, na utawanye manyoya yake katika upepo.” Mtu huyo hakujua kwa nini aliambiwa afanye hivyo, lakini alifanya kama yule mtu mwenye hekima alivyomwambia. Baadaye, alirudi kwa yule mtu mwenye hekima na kumuuliza: “Je, umenisamehe sasa?” Yule mtu mwenye hekima akamwambia hivi: “Kwanza, nenda ukusanye manyoya hayo yote.” Mtu huyo akasema: “Lakini ni vigumu sana kufanya hivyo. Upepo umetawanya manyoya hayo kila mahali. Siwezi kuyapata.” Kisha, mtu huyo mwenye hekima akajibu hivi: “Kama vile manyoya yalivyotawanyika sehemu mbalimbali, ndivyo uwongo wako ulivyowafikia watu wengi. Na kama vile ambavyo huwezi kukusanya manyoya hayo, vivyo hivyo huwezi kuwafanya watu wasahau mambo uliyosema.”

Somo ni wazi. Hatuwezi kubadili mambo tunayosema baada ya kuyasema, na huenda tusiweze kubadili matokeo yake. Kwa hiyo, kabla ya kuanza kueneza porojo, ni jambo la hekima kukumbuka kwamba tuko karibu kutawanya manyoya katika upepo.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Watu fulani wanaweza jinsi gani kuwakaribisha waasi-imani katika nyumba zao?