Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Anayepaswa Kuwafundisha Watoto Kumhusu Mungu?

Ni Nani Anayepaswa Kuwafundisha Watoto Kumhusu Mungu?

Ni Nani Anayepaswa Kuwafundisha Watoto Kumhusu Mungu?

“Mwanafunzi hampiti mwalimu wake, lakini kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.”—LUKA 6:40.

BAADHI ya wazazi huhisi kwamba hawana uwezo wa kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu. Huenda wakafikiri kwamba hawawezi kuwa walimu wazuri kwa sababu hawana elimu wala ujuzi wa kutosha kuhusu dini. Kwa hiyo, huenda wakamwachia mtu wa ukoo au kiongozi wa dini daraka hilo muhimu.

Ni nani basi , anayefaa zaidi kuwafundisha watoto kweli za kidini na maadili mazuri? Ona yale Biblia inayosema kuhusu jambo hilo, na uyalinganishe na yale ambayo watafiti wamegundua.

Baba Ana Daraka Gani?

Biblia inafundisha nini? “Akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana.”—Waefeso 6:4, “Union Version.”

Watafiti wamegundua nini? Akina baba wananufaika jinsi gani wanapositawisha imani yenye nguvu? Makala Fathers’ Religious Involvement and Early Childhood Behavior, iliyochapishwa mwaka wa 2009, ilisema: “Kushirikiana na kikundi fulani cha kidini kunaweza kuwasaidia wanaume kuwa baba wazuri. Dini inaandaa utegemezo na mwelekezo na pia mafundisho na miongozo katika maisha.”

Biblia inaonyesha kwamba baba ana daraka kubwa katika kulea na kufundisha watoto. (Methali 4:1; Wakolosai 3:21; Waebrania 12:9) Lakini shauri hilo linafaa leo? Katika mwaka wa 2009, Chuo Kikuu cha Florida kilichapisha makala iliyozungumzia uvutano ambao akina baba wanakuwa nao juu ya watoto wao. Watafiti hao walitambua kwamba kuna uwezekano mkubwa kwa watoto ambao baba zao walijihusisha sana katika malezi yao kuwa wenye huruma na wenye kujiheshimu. Pia, walitambua kwamba wasichana walikuwa na afya nzuri zaidi ya kiakili, huku wavulana wakiwa wenye adabu zaidi. Bila shaka, shauri la Biblia bado linafaa.

Daraka la Mama Ni Muhimu Kadiri Gani?

Biblia inafundisha nini? “Usiiache sheria ya mama yako.”—Methali 1:8.

Yale ambayo watafiti wamegundua: Katika mwaka wa 2006 kitabu Handbook of Child Psychology kilisema: “Kwa kawaida wakati ambao akina mama wanatumia pamoja na kila mtoto ni kati ya asilimia 65 na 80 zaidi ya ule unaotumiwa na akina baba. Na hali iko hivyo katika nchi nyingi.” Kwa kuwa mama anatumia wakati mwingi hivyo pamoja na mtoto wake, basi maneno, matendo, na mtazamo wake unakuwa na uvutano mkubwa katika ukuzi wa mtoto.

Wazazi wanaposhirikiana kuwafundisha watoto wao ukweli kumhusu Mungu, wanawapa angalau zawadi mbili zenye thamani. Kwanza, watoto wanapata nafasi ya kufanya urafiki pamoja na Baba yao wa mbinguni, urafiki ambao unaweza kuwanufaisha katika maisha yao yote. Pili, kutokana na mfano huo wa wazazi wao, watoto wanajifunza jinsi mume na mke wanavyopaswa kushirikiana ili kufikia malengo muhimu. (Wakolosai 3:18-20) Ingawa huenda wengine wakawasaidia wazazi, wazazi hao ndio wenye daraka la kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu na jinsi anavyotaka familia iwe.

Hivyo basi, wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao jinsi gani? Ni njia gani za kufundisha ambazo inaelekea zitafaa zaidi?