Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kwa Nini Dorkasi Alipendwa?

Kwa Nini Dorkasi Alipendwa?

Wafundishe Watoto Wako

Kwa Nini Dorkasi Alipendwa?

SOTE tunataka watu watupende. Je, wewe unahisi hivyo? * Biblia inasimulia kumhusu Dorkasi, mwanamke aliyependwa sana na watu wengi.

Dorkasi aliishi Yopa, jiji lililokuwa kando ya Bahari ya Mediterania. Yerusalemu lilikuwa umbali wa kilomita zipatazo 56 kutoka Yopa. Dorkasi alikuwa mmoja wa wanafunzi wa mapema wa Yesu.

Unafikiri ni kwa nini Dorkasi alipendwa sana?— Biblia inasema kwamba alifanya mambo mema na kutoa zawadi nzuri. Alishona mavazi mazuri kwa ajili ya wajane, yaani, wanawake waliokuwa wamefiwa na waume zao. Pia, aliwaeleza watu wengi kumhusu Mungu wa kweli, Yehova, kama vile Yesu alivyofanya.

Je, unajua Dorkasi anapatwa na jambo gani baya?— Anakuwa mgonjwa sana na anakufa. Rafiki zake wote wanajawa na huzuni. Hivyo wanawatuma watu fulani kwa mtume Petro anayeishi kilomita 16 kutoka Yopa. Watu hao wanamwomba Petro aende Yopa haraka. Petro anapofika, anapanda juu ghorofani mahali Dorkasi alipo. Wanawake wote wanalia na kumwonyesha Petro mavazi waliyoshonewa na Dorkasi.

Kisha Petro anawasihi wote watoke nje ya chumba hicho. Petro na mitume wengine wamewahi kufanya miujiza mingine hapo awali, lakini hakuna hata mmoja wao amewahi kufufua mtu. Unafikiri Petro atafanya nini?

Petro anapiga magoti kando ya mwili wa Dorkasi na kusali kwa Yehova. Kisha anamwambia Dorkasi ainuke. Naye anainuka! Petro anamnyooshea mkono na kumsaidia kuinuka. Kisha anawaita wale wajane na watu wengine na kuwaonyesha Dorkasi. Je, unaweza kuwazia jinsi wote wanavyofurahi?

Hebu sasa tufikirie unachoweza kujifunza kutokana na hadithi hii ya kufufuliwa kwa Dorkasi. Jambo moja tunalojifunza ni kwamba ukiwasaidia watu wengine, wengi wao watakupenda. Lakini jambo muhimu hata zaidi ni kwamba utapendwa na kukumbukwa na Mungu. Hatasahau mambo mazuri unayowatendea wengine. Na atakupa zawadi ya uzima wa milele na furaha katika ulimwengu wake mpya wenye uadilifu.

Soma Katika Biblia Yako

Matendo 9:36-43

Ufunuo 21:3-5

[Maelezo ya Chini]

^ Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.