Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Har–Magedoni Ni Nini?

Har–Magedoni Ni Nini?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Har–Magedoni Ni Nini?

▪ Watu wengi wanaposikia neno “Har–Magedoni,” jambo linalokuja akilini ni maangamizi makubwa yatakayotokana na vita vya kinyuklia, misiba mikubwa ya asili, au hata msiba wa kimazingira utakaosababishwa na kuongezeka kwa joto duniani. Lakini, kulingana na Biblia, neno Har–Magedoni halirejelei yoyote kati ya mambo hayo. Hivyo basi, neno Har–Magedoni linamaanisha nini kulingana na Biblia?

Neno “Har–Magedoni” linapatikana katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Linarejelea vita vya kipekee, “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” ambapo “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wanakusanywa kupigana pigano la mwisho pamoja na Mungu. Kuna maandiko mengine mengi yanayotaja vita hivyo.—Ufunuo 16:14-16; Ezekieli 38:22, 23; Yoeli 3:12-14; Luka 21:34, 35; 2 Petro 3:11, 12.

Vita hivyo vinahusisha nini? Kwa maneno ya mfano, kitabu cha Ufunuo kinatuambia: “Wafalme wa dunia na majeshi yao wamekusanyika pamoja ili kupigana vita na yule anayeketi juu ya farasi na jeshi lake.” Huyo “anayeketi juu ya farasi” ni Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliyewekwa rasmi na Mungu kuongoza maelfu ya malaika katika kuwashinda maadui wa Mungu. (Ufunuo 19:11-16, 19-21) Andiko la Yeremia 25:33 linaonyesha idadi kubwa ya watu wasiomwogopa Mungu ambao watauawa: “Wale waliouawa na Yehova siku hiyo hakika watakuwa kutoka mwisho mmoja wa dunia mpaka mwisho wa pili wa dunia.”

Kwa nini vita vya Har–Magedoni ni muhimu? Mataifa yanakataa kutambua enzi kuu ya Mungu na badala yake wanatangaza enzi yao. (Zaburi 24:1) Ukaidi wao unaelezwa kwenye Zaburi 2:2: “Wafalme wa dunia wanachukua msimamo wao nao maofisa wakuu wamejikusanya pamoja kama mtu mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake.”

Wafalme hao waasi ni kama watu wanaovamia shamba la mtu bila kibali chake, na ambao kando na kudai shamba hilo ni lao, wanalitumia vibaya na kuliharibu. Leo mataifa yanaiharibu dunia na kuchafua mazingira yake. Neno la Mungu lilitabiri hali hiyo mbaya kwa kusema: “Mataifa wakawa na ghadhabu, nayo ghadhabu [ya Mungu] mwenyewe ikaja.” Hivyo, Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.” (Ufunuo 11:18) Mungu ameamua kutumia vita vya Har–Magedoni kuamua ni nani aliye na haki ya kuwatawala wanadamu wote.—Zaburi 83:18.

Vita vya Har–Magedoni vitapiganwa wakati gani? Mwana wa Mungu alisema hivi waziwazi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:36) Hata hivyo, alipozungumza kuhusu Har–Magedoni, Mfalme-Shujaa, Yesu Kristo, aliongeza onyo hili: “Tazama! Ninakuja kama mwizi. Mwenye furaha ni yule anayekaa macho.” (Ufunuo 16:15) Hivyo, vita hivyo vya ulimwenguni pote vinahusianishwa na kuwapo kwa Kristo, ambako unabii wa Biblia unaonyesha kuwa kumeanza tayari.

Watakaoangamizwa katika vita vya Har–Magedoni ni wale tu ambao wameazimia kutenda uovu, lakini kuna “umati mkubwa” ambao utaokoka. (Ufunuo 7:9-14) Wataona utimizo wa maneno haya: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.

[Blabu katika ukurasa wa 10]

“Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani”