Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tunaishi Karibu na Mlima wa Moto

Tunaishi Karibu na Mlima wa Moto

Barua Kutoka Kongo (Kinshasa)

Tunaishi Karibu na Mlima wa Moto

JUA linapochomoza katika jiji la Goma, anga huonekana kuwa na mchanganyiko wa rangi ya waridi na ya machungwa. Kila siku, tunatazama mlima wenye kupendeza wa Nyiragongo, mojawapo ya milima ya volkano inayolipuka sana duniani. Wingu la moshi mwingi hupaa angani kutoka katika shimo lililo katikati ya kilele cha mlima huo. Usiku, wingu hilo hung’aa na kutoa mwangaza mwekundu kwa sababu ya rangi ya lava iliyo ndani ya shimo hilo.

Wenyeji wa eneo hilo wanauita Mulima ya Moto, yaani, Mlima wa Moto. Mlipuko mkubwa wa mwisho wa Mlima Nyiragongo ulitokea mwaka wa 2002. Majirani wetu wengi hapa Goma walipoteza kila kitu. Katika maeneo fulani ambayo mimi na mume wangu tunahubiri, tunatembea juu lava iliyokauka, jambo linalofanya nihisi kana kwamba tunatembea juu ya mwezi. Watu wanaoishi katika eneo hilo ni tofauti kabisa na lava hiyo iliyokauka. Ni wachangamfu, wenye moyo mzuri, na wanasikiliza habari njema tunayowatangazia. Hilo linafanya utumishi wetu katika eneo hilo la Mlima wa Moto uwe wenye kufurahisha.

Jumamosi asubuhi, nimeamka nikiwa na matazamio makubwa. Mimi na mume wangu, wamishonari wenzetu, pamoja na rafiki zetu waliotutembelea, tutaenda kuhubiri siku nzima katika kambi moja ya wakimbizi iliyo Mugunga, eneo lililo nje ya jiji, upande wa magharibi. Wengi wa wakimbizi hao wametoroka miji ya kwao kwa sababu ya vita.

Tunajaza gari letu trakti, magazeti, na vitabu vya Biblia katika lugha ya Kifaransa, Kiswahili, na Kinyarwanda. Kisha tunaanza safari. Tunaposafiri kwenye barabara ya Route Sake yenye mashimo-mashimo, tunaona kwamba tayari shughuli za jiji zimeanza. Vijana wameanza kusukuma chukudu (mikokoteni iliyotengenezwa kwa mbao) ambazo zimejaa bidhaa. Wanawake waliojifunga kanga zenye rangi zinazong’aa, wanatembea kandokando ya barabara wakiwa wamebeba mizigo mikubwa kichwani. Nayo magari ya abiria yameanza kubeba watu ili kuwapeleka kazini au sokoni. Eneo hilo lina nyumba zilizotapakaa ambazo zimejengwa kwa mbao. Nyumba hizo zenye rangi ya kahawia-nyeusi zimepambwa kwa rangi ya bluu.

Tunafika kwenye Jumba la Ufalme la Ndosho na kukutana na Mashahidi wenzetu ambao watajiunga nasi kuhubiri katika ile kambi. Ninaguswa moyo sana ninapowaona vijana, wajane, mayatima, na wale wenye udhaifu wa kimwili wakiwa tayari kujiunga nasi. Wengi wao wamepitia hali ngumu lakini maisha yao yamekuwa bora kwa sababu wameamua kufuata kanuni za Biblia. Tumaini la Biblia linawachochea sana, na wana hamu ya kuwaeleza wengine kulihusu. Baada ya mkutano mfupi ambapo tunapewa madokezo kuhusu mistari fulani ya Biblia ambayo itawatia moyo watu tutakaozungumza nao, sote watu 130 tunaingia ndani ya mabasi matano madogo na gari moja lenye kuendeshwa kwa magurudumu yote manne.

Baada ya kusafiri kwa muda wa dakika 30 hivi, tunafika kwenye kambi hiyo. Kuna mamia ya mahema madogo meupe katika eneo hilo lenye lava iliyokauka. Katikati ya kambi hiyo kuna vyoo vya watu wote vilivyopangwa vizuri pamoja na sehemu za kufulia nguo. Kuna watu kila mahali ambao wanafua nguo, kupika, kutoa maganda ya maharagwe, na kufagia sehemu ya mbele ya mahema yao.

Tunakutana na mwanamume anayeitwa Papa Jacques, anayesimamia sehemu fulani ya kambi hiyo. Anahangaika kuhusu kuwalea watoto wake katika nyakati hizi ngumu. Anafurahi sana tunapomwachia kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na anasema atakisoma, kisha akusanye vikundi vya watu na kuwaeleza mambo atakayojifunza.

Muda mfupi baadaye tunakutana na mwanamke anayeitwa Mama Beatrice. Anatuuliza kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka. Anafikiri kwamba lazima iwe Mungu anamwadhibu. Mume wake aliuawa vitani, binti yake ambaye hana mume anapambana kumlea mtoto wake kambini, naye mwana wake alitekwa nyara miezi kadhaa iliyopita na hajui yuko wapi.

Mambo hayo yenye kusikitisha ambayo Mama Beatrice anatueleza yananikumbusha jinsi Ayubu alivyohisi baada ya kupata habari mbaya. Tunamwonyesha sababu zinazofanya tuteseke na kumhakikishia kwamba kuteseka si adhabu kutoka kwa Mungu. (Ayubu 34:10-12; Yakobo 1:14, 15) Pia, tunamweleza kuhusu mabadiliko ambayo Mungu ataleta duniani hivi karibuni kupitia Ufalme wake. Tunapomweleza hayo, Mama Beatrice anaanza kutabasamu na kusema kwamba ameazimia kuendelea kujifunza Biblia na kusali kwa Mungu ili amsaidie.

Leo, kila mmoja wetu amefurahia utumishi na tunahisi kwamba Yehova ametusaidia sana kuwapa tumaini na kuwatia moyo watu tuliokutana nao. Tunapoondoka katika kambi hiyo, watu wengi wanatokea wakiwa wameshika trakti, magazeti, na vitabu tulivyowaachia huku wakitupungia mkono kutuaga.

Tunaposafiri kurudi nyumbani ninapata wakati wa kutafakari. Ninashukuru sana kwa sababu ya siku hiyo ya pekee. Ninakumbuka jinsi Papa Jacques alivyoonyesha uthamini, jinsi Mama Beatrice alivyoanza kutabasamu, na jinsi mama mmoja mzee alivyonisalimu kwa shauku ingawa hatungeweza kuwasiliana kwa njia nyingine yoyote isipokuwa kwa kutabasamu. Ninafikiria pia vijana waliouliza maswali yaliyoonyesha kwamba wamekomaa kiakili ingawa wana umri mdogo. Ninapendezwa sana na watu hao ambao niliona wakitabasamu na kucheka ingawa wanakabili hali ngumu.

Katika eneo hilo tunakutana na watu wengine wengi ambao wanajitahidi kwa moyo mweupe kuwasaidia watu wanaoteseka. Leo, tumepata pendeleo kubwa la kutumia Biblia kuwaonyesha watu suluhisho la kudumu kwa matatizo yao. Ninafurahi sana kuwa mmoja wa watu wanaotoa msaada mkubwa zaidi wa kiroho kuwahi kutolewa duniani.