Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Lazima Ulipe Kodi?

Je, Ni Lazima Ulipe Kodi?

Je, Ni Lazima Ulipe Kodi?

NI WATU wachache wanaofurahia kulipa kodi. Wengi wanahisi kwamba kodi wanazolipa zinatumiwa vibaya kwa sababu ya uzembe, udanganyifu, au kuibwa moja kwa moja. Hata hivyo, wengine wanakataa kulipa kodi kwa sababu pesa za kodi zinatumiwa kwa njia isiyofaa. Wakazi wa mji mmoja wa Mashariki ya Kati walisema hivi kuhusu uamuzi wao wa kutolipa kodi: “Hatutalipia risasi ambazo zinatumiwa kuwaua watoto wetu.”

Hayo si maoni mapya wala si ya watu wachache tu. Aliyekuwa kiongozi Mhindu, Mohandas K. Gandhi, alieleza kwa nini dhamiri yake haingemruhusu alipe kodi: “Mtu yeyote anayetegemeza Serikali iliyo na jeshi—iwe ni moja kwa moja au si moja kwa moja—anatenda dhambi. Kila mwanamume awe mzee au kijana anashiriki dhambi hiyo kwa kutegemeza Serikali kupitia kulipa kodi.”

Pia, mwanafalsafa wa karne ya 19, Henry David Thoreau alikataa kulipa kodi kwa sababu pesa hizo zilitumiwa kutegemeza vita. Aliuliza: “Je, raia anapaswa kumruhusu mtunga-sheria amfanyie maamuzi ambayo anapaswa kujifanyia akiongozwa na dhamiri yake? Basi, kwa nini kila mtu ana dhamiri?”

Jambo hilo linawahusu Wakristo, kwa kuwa Biblia inafundisha waziwazi kwamba wanapaswa kuwa na dhamiri safi katika mambo yote. (2 Timotheo 1:3) Kwa upande mwingine, Biblia inataja kwamba serikali zina mamlaka ya kukusanya kodi. Inasema: “Kila nafsi na ijitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa [serikali za wanadamu], kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizopo zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri. Kwa hiyo kuna sababu ya lazima kwenu muwe mkijitiisha, si kwa sababu ya ghadhabu hiyo tu, bali pia kwa sababu ya dhamiri yenu. Kwa maana hiyo ndiyo sababu mnalipa kodi pia; kwa maana wao ni watumishi wa Mungu kwa watu wote wakitumikia daima kwa kusudi hili. Wapeni wote haki zao, yeye anayetaka kodi, kodi.”—Waroma 13:1, 5-7.

Kwa sababu hiyo, Wakristo wa karne ya kwanza walijulikana sana kwa kulipa kodi bila kulazimishwa hata ingawa kiasi fulani kinatumika kutegemeza jeshi. Leo Mashahidi wa Yehova wanafanya vivyo hivyo. * Kwa nini Wakristo walipe kodi huku wakijua kwamba kiasi fulani cha kodi hiyo kinatumiwa kufanya mambo yasiyopatana na imani yao? Je, Mkristo anapaswa kupuuza dhamiri yake anapoombwa alipe kodi?

Kodi na Dhamiri

Kwa kweli, katika karne ya kwanza kiasi fulani cha kodi ambayo Wakristo waliagizwa walipe kilitumiwa kutegemeza jeshi. Hilo ndilo jambo linalohusu dhamiri ambalo baadaye lilifanya Gandhi na Thoreau wakatae kulipa kodi.

Ona kwamba Wakristo walitii amri iliyo katika Waroma sura ya 13 si kwa sababu tu walitaka kuepuka kuadhibiwa lakini pia “kwa sababu ya dhamiri” zao. (Waroma 13:5) Kwa kweli, dhamiri ya Mkristo inamsukuma alipe kodi, hata kama kodi hiyo itatumiwa kutegemeza mambo ambayo hakubaliani nayo. Ili kuelewa jambo hilo ambalo huenda lisieleweke kwa urahisi, tunapaswa kutambua jambo muhimu kuhusu dhamiri zetu, ile sauti ya ndani ambayo hutueleza ikiwa mambo tunayotenda yanafaa au hayafai.

Kila mtu ana sauti ya ndani, kama Thoreau alivyotaja, lakini si lazima iwe yenye kutegemeka. Ili tumpendeze Mungu, ni lazima dhamiri yetu ituongoze kupatana na viwango vyake vya maadili. Mara kwa mara, tunapaswa kurekebisha mawazo au maoni yetu ili yapatane na ya Mungu, kwa sababu mawazo yake ni makuu kuliko yetu. (Zaburi 19:7) Kwa hiyo, tunapaswa kujitahidi kuelewa maoni ya Mungu kuhusu serikali za wanadamu. Ana maoni gani?

Tunaona kwamba mtume Paulo aliziita serikali za wanadamu “watumishi wa Mungu kwa watu wote.” (Waroma 13:6) Hilo linamaanisha nini? Kwa ujumla linamaanisha kwamba wanadumisha utaratibu na kutekeleza majukumu mengi muhimu kwa ajili ya jamii. Mara nyingi, hata serikali ambazo ni fisadi zaidi zinatoa huduma kama vile kutuma barua, elimu, kuzima moto, na kuhakikisha kwamba watu wanatii sheria. Ingawa Mungu anajua kabisa kasoro za serikali hizo za wanadamu, ameziruhusu ziwepo kwa muda na ametupatia jukumu la kulipa kodi ili tuonyeshe kwamba tunaheshimu mpango wake, yaani, kuruhusu serikali hizo ziwatawale wanadamu.

Hata hivyo, Mungu ameruhusu serikali za wanadamu ziwepo kwa muda mfupi. Mungu anakusudia kuondoa serikali hizo zote na kuleta Ufalme wake wa kimbingu na hivyo kuondolea mbali uharibifu wote ambao utawala wa kibinadamu umewaletea wanadamu kwa miaka mingi. (Danieli 2:44; Mathayo 6:10) Hata hivyo, kwa sasa Mungu anataka Wakristo watii serikali hizo kwa kulipa kodi au kwa njia nyinginezo.

Lakini, namna gani ikiwa bado una maoni kama ya Gandhi kwamba kulipa kodi zinazotegemeza vita ni dhambi? Sawa tu na vile tunavyoweza kuona eneo fulani vizuri kwa kupanda mahali palipoinuka, ndivyo pia tunavyoweza kupatanisha kwa urahisi zaidi maoni yetu na ya Mungu kwa kutafakari jinsi maoni yake yalivyo juu kuliko yetu. Kupitia nabii Isaya, Mungu alisema: “Kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”—Isaya 55:8, 9.

Je, Serikali Zina Mamlaka Kamili?

Biblia inapofundisha kuhusu kulipa kodi haimaanishi kwamba serikali za wanadamu zina mamlaka kamili juu ya wanadamu. Yesu alifundisha kwamba Mungu amezipa serikali hizo kiasi fulani tu cha mamlaka. Yesu alipoulizwa kama ilifaa machoni pa Mungu kulipa kodi kwa serikali ya Waroma iliyokuwa mamlakani wakati huo, alijibu kwa kutumia maneno haya yenye busara: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.”—Marko 12:13-17.

Serikali—zinazowakilishwa na “Kaisari”—zinatengeneza pesa na kusaidia kuamua thamani yake. Hivyo, kwa maoni ya Mungu wana haki ya kutaka pesa hizo zilipwe kama kodi. Hata hivyo, Yesu alionyesha kwamba hakuna serikali yoyote ya wanadamu inayoweza kudai “vitu vya Mungu,” yaani, uhai wetu na ibada yetu. Sheria za wanadamu zinapopingana na sheria za Mungu, ni ‘lazima Wakristo wamtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:29.

Leo, huenda Wakristo wasifurahie jinsi kodi wanazolipa zinavyotumiwa, lakini hawajaribu kuingilia serikali hizo kwa kutozitii au kutolipa kodi. Hilo lingeonyesha kwamba hawaamini Mungu ndiye anayeweza kutatua matatizo ya wanadamu. Badala yake, wanangoja kwa subira wakati ambapo Mungu ataingilia kati mambo ya wanadamu kupitia utawala wa Mwana wake, Yesu, aliyesema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.”—Yohana 18:36.

Faida za Kufuata Mafundisho ya Biblia

Unaweza kufaidika kwa njia mbalimbali unapotii mafundisho ya Biblia kuhusu kulipa kodi. Utaepuka adhabu ambayo watu wanaovunja sheria wanapata na pia hutakuwa na wasiwasi wa kukamatwa. (Waroma 13:3-5) Jambo la maana zaidi ni kwamba utakuwa na dhamiri safi mbele za Mungu na utamletea sifa kwa kuwa na zoea la kutii sheria. Hata ingawa huenda ukapata hasara kifedha kwa kulinganishwa na wale wanaokataa kulipa kodi au kutumia njia za udanganyifu, unaweza kutegemea ahadi ya Mungu ya kuwatunza watumishi wake washikamanifu. Mwandishi wa Biblia Daudi alisema hivi: “Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.”—Zaburi 37:25.

Mwishowe, kuelewa na kufuata agizo la Biblia kuhusu kulipa kodi ni jambo linaloweza kufanya uwe na amani ya akili. Hutakuwa na hatia mbele za Mungu kwa sababu ya mambo yote ambayo serikali inafanya kwa kutumia kodi unayolipa, kama vile tu huwezi kuwa na hatia kuhusiana na jinsi mwenye nyumba anavyotumia kodi unayomlipa. Kabla ya kujifunza Biblia, mwanamume anayeitwa Stelvio alijaribu kwa miaka mingi kuleta mabadiliko ya kisiasa huko kusini mwa Ulaya. Akieleza kwa nini aliacha jitihada zake za kuleta mabadiliko, alisema: “Nililazimika kukubali kwamba mwanadamu hawezi kuleta haki, amani, na undugu ulimwenguni. Kwa kweli, Ufalme wa Mungu tu ndio unaoweza kuleta mabadiliko na jamii bora.”

‘Ukimlipa Mungu vitu vya Mungu’ kwa ushikamanifu, wewe pia unaweza kuwa na uhakika kama vile tu Stelvio. Utakuwepo wakati Mungu atakapoleta utawala wenye uadilifu duniani kote, na kuondoa uharibifu na ukosefu wa haki ambao umeletwa na utawala wa wanadamu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyolipa kodi, ona gazeti Mnara wa Mlinzi, la Novemba 1, 2002 (1/11/2002), ukurasa wa 13, fungu la 15, na Mei 1, 1996, ukurasa wa 17, fungu la 7.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Tunapaswa kurekebisha maoni yetu ili yapatane na ya Mungu kwa sababu mawazo yake ni makuu kuliko yetu

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Kwa kuwa watiifu na kulipa kodi, Wakristo wanakuwa na dhamiri safi mbele za Mungu na wanaonyesha kwamba wana hakika Mungu atawatimizia mahitaji yao

[Picha katika ukurasa wa 22]

“Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu”

[Hisani ya Picha]

Copyright British Museum