Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehova Ni Fungu Langu

Yehova Ni Fungu Langu

Yehova Ni Fungu Langu

“Mimi ni fungu lako na urithi wako katikati ya wana wa Israeli.”​—HES. 18:20.

1, 2. (a) Walawi walikuwa katika hali gani kuhusiana na urithi wa nchi? (b) Yehova aliwapa Walawi ahadi gani?

 BAADA ya Waisraeli kuchukua sehemu kubwa ya Nchi ya Ahadi, Yoshua alianza kazi ya kugawa nchi hiyo kwa kura. Alifanya kazi hiyo akishirikiana na Kuhani Mkuu Eleazari pamoja na wakuu wa makabila. (Hes. 34:13-29) Walawi hawakupaswa kupewa urithi wa nchi kama ule ambao yale makabila mengine yalipewa. (Yos. 14:1-5) Kwa nini kabila la Lawi halikuwa na eneo, au fungu, katika ile Nchi ya Ahadi? Je, walisahauliwa?

2 Jibu linapatikana katika maneno ambayo Yehova aliwaambia Walawi. Ili kukazia kwamba hakuwa amewaacha, Yehova aliwaambia hivi: “Mimi ni fungu lako na urithi wako katikati ya wana wa Israeli.” (Hes. 18:20) Aliwapa ahadi yenye kutia moyo sana: “Mimi ni fungu lako”! Ungehisi namna gani ikiwa Yehova angekwambia hivyo? Huenda mwanzoni ungejiuliza hivi: ‘Ninastahili kweli kuhakikishiwa hivyo na Mweza-Yote?’ Pia, huenda ukajiuliza hivi: ‘Je, Yehova anaweza kweli kuwa fungu la Mkristo yeyote asiye mkamilifu leo?’ Maswali au maulizo hayo yanakuhusu wewe na wapendwa wako. Basi, acheni tuone maana ya maneno hayo ya Mungu. Kufanya hivyo kutatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyoweza kuwa fungu la Wakristo leo. Anaweza hasa kuwa fungu lako, iwe una tumaini la kuishi mbinguni au tumaini la kuishi katika paradiso duniani.

Yehova Aliwatunza Walawi

3. Ni nini kilichomfanya Mungu awachukue Walawi kwa ajili ya utumishi wake?

3 Kabla Yehova hajawapa Waisraeli Sheria, vichwa vya familia walitumikia wakiwa makuhani katika familia zao. Mungu alipowapa Sheria, alichagua watu fulani kutoka katika kabila la Lawi ili watumike daima wakiwa makuhani na wasaidizi. Alifanya hivyo jinsi gani? Mungu alipowaangamiza wazaliwa wa kwanza huko Misri, aliwatakasa wazaliwa wa kwanza wa Israeli, na kuwaweka kando ili wawe wake, wawe mali yake. Kisha Mungu akafanya badiliko hili kubwa: “Nawachukua Walawi . . . mahali pa wazaliwa wote wa kwanza katikati ya wana wa Israeli.” Kwa kuwa hesabu ya watu ilionyesha kwamba wazaliwa wa kwanza wa Israeli walikuwa wengi kuliko Walawi, bei ya fidia au ukombozi ililipwa ili kujazia tofauti hiyo. (Hes. 3:11-13, 41, 46, 47) Hivyo, Walawi wangeweza kutimiza daraka lao la kumtumikia Mungu wa Israeli.

4, 5. (a) Mungu alimaanisha nini aliposema kwamba alikuwa fungu la Walawi? (b) Mungu aliwatunza Walawi jinsi gani?

4 Mgawo huo ulimaanisha nini kwa Walawi? Yehova alisema kwamba angekuwa fungu lao kumaanisha kwamba badala ya kupewa urithi wa nchi, walikabidhiwa pendeleo lenye thamani sana la utumishi. Wangepata urithi wa kuwa “ukuhani wa Yehova.” (Yos. 18:7) Mistari mingine inayozunguka andiko la Hesabu 18:20 inaonyesha kwamba jambo hilo halikufanya wawe maskini kimwili. (Soma Hesabu 18:19, 21, 24.) Walawi walipaswa kupewa “kila sehemu ya kumi katika Israeli iwe urithi wao kwa sababu ya utumishi wao.” Wangepokea asilimia 10 ya mazao yote ya Waisraeli na ya wanyama walioongezeka. Kisha Walawi walipaswa kutoa sehemu ya 10 ya vitu walivyopokea kuwa mchango, “ule ulio bora zaidi,” ili kutegemeza ukuhani. * (Hes. 18:25-29) Makuhani walipewa pia “michango yote mitakatifu” ambayo wana wa Israeli walimletea Mungu mahali pake pa Ibada. Hivyo, washiriki wa ukuhani walikuwa na sababu nzuri za kuamini kwamba Yehova angewatunza.

5 Inaonekana kwamba Sheria ya Musa iliwaagiza Waisraeli watoe sehemu nyingine ya kumi. Familia za Waisraeli zilitumia sehemu hiyo kununua vyakula na vinywaji na pia kujifurahisha wakati wa makusanyiko matakatifu kila mwaka. (Kum. 14:22-27) Hata hivyo, mwishoni mwa kila mwaka wa tatu na wa sita wa mzunguko wa sabato wa miaka saba, sehemu hiyo ya kumi iliwekwa kwenye malango ili kuwasaidia maskini na pia Walawi. Kwa nini Walawi walipewa pia msaada huo? Kwa sababu ‘hawakuwa na fungu wala urithi’ katika Israeli.—Kum. 14:28, 29.

6. Kwa kuwa kabila la Lawi halikuwa na fungu la nchi katika Israeli, Walawi wangeishi wapi?

6 Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Walawi hawakugawiwa nchi yoyote, wangeishi wapi?’ Mungu aliwapa mahali pa kuishi. Aliwapa majiji 48 pamoja na viwanja vya malisho vilivyozunguka majiji hayo. Majiji hayo yalitia ndani majiji sita ya makimbilio. (Hes. 35:6-8) Hivyo, Walawi walikuwa na mahali pa kuishi wakati ambapo hawakuwa wakitumika katika patakatifu pa Mungu. Yehova aliwatunza kabisa wale ambao walijitoa wenyewe katika utumishi wake. Ni wazi kwamba Walawi walionyesha kuwa Yehova ni fungu lao kwa kutegemea uwezo na utayari wake wa kuwatunza.

7. Walawi walihitaji kuwa na nini ili Yehova awe fungu lao?

7 Sheria haikutaja adhabu yoyote ambayo Mwisraeli angepata ikiwa angekosa kutoa sehemu ya kumi. Watu walipopuuza kutoa sehemu ya kumi, makuhani na Walawi waliumia. Ndivyo ilivyokuwa katika siku za Nehemia. Matokeo yalikuwa kwamba Walawi walilazimika kufanya kazi katika mashamba yao, na kupuuza huduma yao. (Soma Nehemia 13:10.) Ni wazi kwamba Walawi walipata tu mahitaji yao wakati taifa hilo lilipotii Sheria ya Yehova. Zaidi ya hayo, makuhani na Walawi wenyewe walihitaji kuwa na imani katika Yehova na njia yake ya kuwaandalia mahitaji yao.

Watu Mmoja-Mmoja Ambao Yehova Alikuwa Fungu Lao

8. Eleza tatizo ambalo Asafu alikuwa nalo.

8 Kwa ujumla, Yehova angekuwa fungu la kabila lote la Walawi. Hata hivyo, ni vizuri kuona kwamba Walawi wakiwa mtu mmoja-mmoja walitumia maneno “Yehova ni fungu langu” ili kuonyesha kwamba walijitoa kwa Mungu na kumtegemea yeye. (Omb. 3:24) Mlawi mmoja aliyesema hivyo alikuwa mwimbaji na mtungaji wa nyimbo. Tutamwita Asafu, ingawa huenda alikuwa mshiriki wa familia ya Asafu, yule Mlawi ambaye aliongoza waimbaji katika siku za Mfalme Daudi. (1 Nya. 6:31-43) Katika Zaburi ya 73 tunasoma kwamba Asafu (au mmoja wa wazao wake) alishangaa. Aliwaonea wivu watu waovu ambao walikuwa na maisha mazuri na akafikia hatua ya kusema hivi: “Hakika nimeusafisha moyo wangu bure na kuiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia.” Inaonekana kwamba alikosa kuthamini pendeleo lake la utumishi; hakuthamini kwamba Yehova alikuwa fungu lake. Aliteseka kiroho ‘mpaka alipoingia katika patakatifu pakuu pa Mungu.’—Zab. 73:2, 3, 12, 13, 17.

9, 10. Kwa nini Asafu alisema kwamba Mungu ni ‘fungu lake mpaka wakati usio na kipimo’?

9 Akiwa katika patakatifu, Asafu alianza kuona mambo kama Mungu alivyoyaona. Labda umewahi kuwa na maoni kama ya Asafu. Labda wakati fulani ulikosa kuthamini kwa kadiri fulani mapendeleo yako ya kiroho na kuanza kukazia fikira vitu vya kimwili ambavyo hukuwa navyo. Lakini ulipojifunza Neno la Mungu na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ulianza kuona mambo kama Yehova anavyoyaona. Asafu alitambua jambo ambalo mwishowe lingewapata waovu. Alifikiria kuhusu hali yake na kutambua kwamba Yehova angeushika mkono wake wa kuume na kumwongoza. Hivyo, Asafu alimwambia Yehova hivi: “Isipokuwa wewe sina mapendezi mengine duniani.” (Zab. 73:23, 25) Kisha akasema kwamba Mungu ni fungu lake. (Soma Zaburi 73:26.) Hata kama ‘mwili na moyo wa mtunga-zaburi huyo ungeshindwa,’ Mungu angekuwa ‘fungu lake mpaka wakati usio na kipimo.’ Mtunga-zaburi huyo alikuwa na hakika kwamba Yehova angemkumbuka akiwa rafiki. Utumishi wake mwaminifu haungesahauliwa. (Mhu. 7:1) Bila shaka, Asafu alitiwa moyo sana na jambo hilo. Aliimba hivi: “Mimi, kumkaribia Mungu ni kwema kwangu. Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”—Zab. 73:28.

10 Asafu aliona kwamba Yehova kuwa fungu lake ni jambo la maana zaidi kuliko vitu vya kimwili ambavyo alipewa akiwa Mlawi. Alikazia hasa pendeleo lake la utumishi na uhusiano wake pamoja na Yehova, na urafiki ambao alikuwa amesitawisha pamoja na Aliye Juu Zaidi. (Yak. 2:21-23) Ili kulinda uhusiano huo, mtunga-zaburi huyo alihitaji kuendelea kuwa na imani katika Yehova na kumtegemea. Asafu alipaswa kuwa na uhakika kwamba mwishowe angepata thawabu maishani ikiwa angeishi kulingana na viwango vya Mungu. Unaweza kuwa na uhakika kama huo katika Mweza-Yote.

11. Ni swali gani ambalo Yeremia aliuliza, na lilijibiwa jinsi gani?

11 Nabii Yeremia ni Mlawi mwingine aliyemwona Yehova kuwa fungu lake. Acheni tuone alichomaanisha alipotumia maneno hayo. Yeremia aliishi huko Anathothi, jiji la Walawi ambalo lilikuwa karibu na Yerusalemu. (Yer. 1:1) Pindi moja, Yeremia alishangaa na kuuliza: Kwa nini waovu walikuwa wakifanikiwa huku waadilifu wakiteseka? (Yer. 12:1) Baada ya kuona mambo yaliyokuwa yakitokea Yerusalemu na Yuda, alihisi kwamba alipaswa ‘kulalamika’ kuhusu mambo aliyoona. Yeremia alijua kwamba Yehova ni mwadilifu. Swali la nabii Yeremia lilijibiwa kwa hakika kupitia mambo ambayo Yehova alimwongoza nabii huyo kutabiri baadaye kwa uwezo wa roho takatifu na jinsi Yehova alivyoyatimiza. Kulingana na unabii mbalimbali kutoka kwa Mungu, wale ambao walitii mwongozo wa Yehova ‘walipata nafsi yao kama nyara,’ lakini watu waovu waliokuwa matajiri walipuuza onyo na kuangamia.—Yer. 21:9.

12, 13. (a) Ni nini kilichomchochea Yeremia atangaze hivi: “Yehova ni fungu langu,” na alikuwa na mtazamo gani? (b) Kwa nini makabila yote ya Israeli yalihitaji kusitawisha mtazamo wa kungojea?

12 Baadaye Yeremia alipoangalia nchi yake iliyobaki ukiwa, alihisi kana kwamba alikuwa akitembea katika giza. Ilikuwa ni kana kwamba Yehova alimfanya ‘aketi mahali penye giza kama watu waliokufa zamani.’ (Omb. 1:1, 16; 3:6) Yeremia alikuwa ameliambia taifa hilo lenye kuasi limrudie Baba yao wa mbinguni, lakini ubaya ulikuwa mwingi hivi kwamba Mungu alilazimika kuruhusu Yerusalemu na Yuda kuangamizwa. Yeremia aliumia alipoona hivyo, hata ingawa kosa halikuwa lake. Alipokuwa akiteseka, nabii huyo alikumbuka rehema za Mungu. Alisema hivi: “Hatujaisha.” Kwa kweli, rehema za Yehova ni mpya kila asubuhi! Ndipo Yeremia alipotangaza hivi: “Yehova ni fungu langu.” Aliendelea kuwa na pendeleo la kumtumikia Yehova akiwa nabii.—Soma Maombolezo 3:22-24.

13 Kwa miaka 70, Waisraeli hawangekuwa na nchi yao. Ingeachwa ukiwa. (Yer. 25:11) Lakini maneno “Yehova ni fungu langu” yaliyosemwa na Yeremia yalionyesha alikuwa na uhakika kwamba Mungu angewarehemu, na hilo lilimpa sababu ya kuwa na “mtazamo wa kungojea.” Makabila yote ya Israeli yalikuwa yamepoteza urithi wao, hivyo yalihitaji kusitawisha mtazamo kama wa nabii huyo. Yehova peke yake ndiye aliyekuwa tumaini lao. Baada ya miaka 70, watu wa Mungu walirudishwa katika nchi yao na wakapata pendeleo la kumtumikia huko.—2 Nya. 36:20-23.

Wengine Wangeweza Kumfanya Yehova Kuwa Fungu Lao

14, 15. Zaidi ya Walawi, ni nani ambaye alimfanya Yehova kuwa fungu lake, na kwa nini?

14 Asafu na Yeremia walikuwa wa kabila la Lawi, lakini je, ni Walawi peke yao ambao wangekuwa na pendeleo la kumtumikia Yehova? Hapana! Kijana Daudi, ambaye baadaye angekuwa mfalme wa Israeli, alimwita Mungu “fungu langu katika nchi ya walio hai.” (Soma Zaburi 142:1, 5.) Daudi alipotunga zaburi hiyo, hakuwa katika nyumba ya mfalme au hata katika nyumba yoyote. Alikuwa ndani ya pango, akijificha maadui wake. Katika pindi mbili hivi, Daudi alikimbilia katika mapango—pango moja lilikuwa karibu na Adulamu na lingine lilikuwa katika jangwa la En-gedi. Huenda alitunga Zaburi ya 142 akiwa ndani ya moja la mapango hayo.

15 Ikiwa ndivyo ilivyokuwa, basi Mfalme Sauli ndiye aliyekuwa akimuwinda Daudi, akitafuta kumuua. Daudi alikimbia na kuingia ndani ya pango ambalo halingeweza kufikiwa kwa urahisi. (1 Sam. 22:1, 4) Katika eneo hilo lililojificha, huenda Daudi alihisi kwamba hakuwa na rafiki kando yake ambaye angeweza kumtegemeza kwa kumlinda. (Zab. 142:4) Huo ndio wakati ambao Daudi alimwomba Mungu msaada.

16, 17. (a) Ni sababu gani zilizomfanya Daudi akate tamaa? (b) Daudi angeweza kumwomba nani msaada?

16 Kufikia wakati ambapo Daudi alitunga Zaburi ya 142, huenda alipata habari kuhusu jambo lililompata Kuhani Mkuu Ahimeleki, ambaye bila kujua alimsaidia Daudi alipokuwa akimkimbia Sauli. Mfalme Sauli mwenye wivu aliagiza Ahimeleki pamoja na watu wa nyumba yake wauawe. (1 Sam. 22:11, 18, 19) Daudi aliona kwamba ni yeye aliyesababisha vifo vyao. Alihisi ni kana kwamba alimuua kuhani ambaye alikuwa amemsaidia. Kama ungekuwa katika hali ya Daudi, je, ungejiona kuwa na hatia? Daudi alipata mkazo zaidi kwa sababu hakupumzika kwa kuwa Sauli aliendelea kumfuata.

17 Muda mfupi baadaye nabii Samweli alikufa, ambaye alikuwa amemtia Daudi mafuta ili awe mfalme. (1 Sam. 25:1) Huenda hilo lilimfanya Daudi akate tamaa zaidi. Hata hivyo, Daudi alijua kwamba Yehova ndiye angemsaidia. Daudi hakuwa na pendeleo la utumishi kama la Walawi, lakini alikuwa tayari ametiwa mafuta ili kutimiza utumishi wa aina nyingine, mwishowe angekuwa mfalme wa watu wa Mungu. (1 Sam. 16:1, 13) Kwa hiyo, Daudi alimimina moyo wake mbele za Yehova na kuendelea kufuata mwongozo wa Mungu. Wewe pia unaweza na unapaswa kumfanya Yehova kuwa fungu lako na kimbilio lako unapojikaza katika utumishi wake.

18. Watu ambao tumezungumzia katika habari hii walionyesha jinsi gani kwamba Yehova alikuwa fungu lao?

18 Watu ambao tumezungumzia walimfanya Yehova kuwa fungu lao katika maana ya kwamba walipokea mgawo wa kazi katika utumishi wake. Walimtegemea Mungu awatunze walipokuwa wakimtumikia. Walawi na pia Waisraeli wa makabila mengine, kama vile Daudi, wangeweza kumfanya Mungu kuwa fungu lao. Wewe pia unaweza jinsi gani kumfanya Yehova awe fungu lako? Tutazungumzia jambo hilo katika habari inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ukuhani ulivyotegemezwa, ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 684 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 655.

Ungesema Nini?

• Yehova alikuwa fungu la Walawi katika maana gani?

• Asafu, Yeremia, na Daudi walifanya nini, na hivyo kuonyesha kwamba Yehova alikuwa fungu lao?

• Unahitaji sifa gani ili Mungu awe fungu lako?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Walawi hawakupokea urithi wa nchi. Badala yake, Yehova alikuwa fungu lao, kwa sababu walikuwa na pendeleo kubwa la kumtumikia

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yehova alikuwa fungu la makuhani na Walawi jinsi gani?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ni nini kilichomsaidia Asafu kuendelea kumfanya Yehova kuwa fungu lake?