Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamfanya Yehova Awe Fungu Lako?

Je, Unamfanya Yehova Awe Fungu Lako?

Je, Unamfanya Yehova Awe Fungu Lako?

“Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—MT. 6:33.

1, 2. (a) “Israeli wa Mungu” wanaotajwa katika Wagalatia 6:16 wanafananisha nani? (b) Katika andiko la Mathayo 19:28, ni nani wanaofananishwa na “yale makabila kumi na mawili ya Israeli”?

UNAPOSOMA jina Israeli katika Biblia, unafikiria nini? Je, unamfikiria Yakobo mwana wa Isaka, ambaye jina lake lilibadilishwa na kuwa Israeli? Au unawafikiria wazao wake, taifa la kale la Israeli? Namna gani kuhusu Israeli wa kiroho? Jina Israeli linapotumiwa kwa njia ya mfano, kwa kawaida linahusu “Israeli wa Mungu,” wale 144,000, ambao wametiwa mafuta kwa roho takatifu ili kuwa wafalme na makuhani mbinguni. (Gal. 6:16; Ufu. 7:4; 21:12) Lakini fikiria jinsi makabila 12 ya Israeli yanavyozungumziwa kwa njia ya pekee katika andiko la Mathayo 19:28.

2 Yesu alisema hivi: “Katika uumbaji-mpya Mwana wa binadamu atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi ambao mmenifuata mtaketi pia juu ya viti vya ufalme kumi na viwili, mkiyahukumu yale makabila kumi na mawili ya Israeli.” Katika mstari huo, “yale makabila kumi na mawili ya Israeli” ni wale ambao watahukumiwa na wanafunzi watiwa-mafuta wa Yesu na ambao wanatumaini kupata uzima wa milele katika Paradiso duniani. Watafaidika kutokana na utumishi wa kikuhani wa wale 144,000.

3, 4. Watiwa-mafuta waaminifu wameweka mfano gani mzuri?

3 Kama makuhani na Walawi wa zamani, watiwa-mafuta leo wanaona utumishi wao kuwa pendeleo. (Hes. 18:20) Watiwa-mafuta hawatazamii kupewa eneo au mahali fulani duniani kuwa urithi wao. Badala yake, wanatazamia kuwa wafalme na makuhani mbinguni pamoja na Yesu Kristo. Wataendelea kumtumikia Yehova katika mgawo huo, kama inavyoonyeshwa na mambo tunayosoma katika andiko la Ufunuo 4:10, 11 kuhusu watiwa-mafuta wakiwa katika cheo chao mbinguni.—Eze. 44:28.

4 Wakiwa duniani, watiwa-mafuta wanaishi kwa njia ambayo inaonyesha kwamba Yehova ni fungu lao. Pendeleo lao la kumtumikia Mungu ni la maana sana kwao. Wanaonyesha imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo na wanaendelea kumfuata, na hivyo ‘kufanya mwito na kuchaguliwa kwao kuwe hakika.’ (2 Pet. 1:10) Kila mmoja wao ana hali na uwezo tofauti. Hata hivyo, hawatumii udhaifu wowote walio nao kuwa kisingizio cha kufanya machache tu katika utumishi wa Mungu. Badala yake, wanatanguliza kabisa utumishi wa Mungu, na kufanya yote wanayoweza. Nao wanawawekea mfano mzuri wale ambao wanatumaini kuishi katika paradiso duniani.

5. Wakristo wote wanaweza kumfanya Yehova kuwa fungu lao jinsi gani, na kwa nini huenda isiwe rahisi kufanya hivyo?

5 Iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au la kuishi duniani, ni lazima ‘tujikane wenyewe na kuuchukua mti wetu wa mateso na kumfuata Kristo sikuzote.’ (Mt. 16:24) Mamilioni ya watu ambao wanatazamia kuishi katika Paradiso duniani wanamwabudu Mungu na kumfuata Kristo kwa njia hiyo. Hawatosheki kufanya mambo machache tu ikiwa wanaona kwamba wanaweza kutimiza mengi zaidi. Wengi wamechochewa kurahisisha maisha yao na wamekuwa mapainia. Wengine wao wanafanya upainia miezi fulani kila mwaka. Na kuna wengine, ingawa hawawezi kufanya upainia, wanajikaza kabisa katika huduma. Watu hao ni kama Maria aliyejitoa, ambaye alimmiminia Yesu mafuta yenye marashi. Yesu alisema hivi: “Amenifanyia tendo zuri. . . . Alifanya jambo ambalo aliweza.” (Marko 14:6-8) Huenda isiwe rahisi kwetu kufanya yote tunayoweza, kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu ambao unatawaliwa na Shetani. Hata hivyo, tunajikaza wenyewe kabisa na kumtegemea Yehova. Fikiria jinsi tunavyofanya hivyo katika sehemu nne hasa.

Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu

6. (a) Watu kwa ujumla wanaonyesha jinsi gani kwamba fungu lao liko katika maisha haya tu? (b) Kwa nini ni jambo bora zaidi kuwa na mtazamo kama wa Daudi?

6 Yesu aliwafundisha wafuasi wake watafute kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu. Watu wa ulimwengu wana mwelekeo wa kutafuta kwanza faida zao binafsi kama “watu wa mfumo huu wa mambo, ambao fungu lao liko katika maisha haya.” (Soma Zaburi 17:1, 13-15.) Watu wengi wanampuuza Muumba wao na kujitoa wenyewe kutafuta maisha ya raha, kuwa na familia, na kuacha urithi. Fungu lao liko katika maisha haya tu. Lakini Daudi alitaka kujifanyia jina zuri mbele za Yehova, kama vile baadaye mwana wake alivyopendekeza watu wote wafanye. (Mhu. 7:1) Kama tu Asafu, Daudi aliona kwamba kuwa Rafiki ya Yehova lilikuwa jambo bora zaidi kuliko kutanguliza faida zake mwenyewe maishani. Alipata shangwe katika kutembea pamoja na Mungu. Leo, Wakristo wengi wametanguliza utendaji wa kiroho badala ya kazi yao ya kimwili.

7. Ndugu mmoja alipata baraka gani kwa kutanguliza Ufalme?

7 Mfikirie Jean-Claude, anayeishi katika Jamhuri ya Afrika ya Kati. Ni mzee wa kutaniko aliye na mke na watoto watatu. Katika nchi hiyo, ni vigumu kupata kazi, na watu wengi wanafanya jambo lolote lile ili wasipoteze kazi yao. Siku moja, msimamizi wa kazi alimwambia Jean-Claude aanze kufanya kazi usiku, kuanzia saa kumi na mbili na nusu jioni, siku saba kwa juma. Jean-Claude alimweleza kwamba zaidi ya kuitunza familia yake kimwili, alihitaji pia kutunza hali yao ya kiroho. Pia, alisema kwamba alikuwa na daraka la kulisaidia kutaniko. Msimamizi huyo alimwambia nini? “Ikiwa umefanikiwa kupata kazi, ni lazima usahau mambo mengine yote, kutia ndani mke wako, watoto wako, na matatizo yako. Ni lazima ujitoe kabisa katika kazi yako—usijitoe kwa kitu kingine chochote ila kazi yako. Chagua jambo moja: dini yako au kazi yako.” Wewe ungefanya nini? Jean-Claude alitambua kwamba ikiwa angepoteza kazi yake, Mungu angemtunza. Bado angekuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Mungu, na Yehova angemsaidia kutosheleza mahitaji ya kimwili ya familia yake. Kwa hiyo, alihudhuria mkutano uliofuata wa katikati ya juma. Kisha, akajitayarisha kwenda kazini, lakini hakuwa na hakika kwamba angeendelea kufanya kazi hiyo. Kwa ghafula, alipigiwa simu. Yule msimamizi alikuwa amefutwa kazi, lakini ndugu yetu akaendelea na kazi yake.

8, 9. Tunaweza kuwaiga makuhani na Walawi jinsi gani katika kumfanya Yehova awe fungu letu?

8 Watu fulani ambao wamekuwa katika hatari ya kupoteza kazi yao wamejiuliza hivi: ‘Nitatimiza jinsi gani daraka langu la kuiandalia familia yangu mahitaji?’ (1 Tim. 5:8) Iwe umewahi kujikuta katika hali kama hiyo au hapana, inaelekea kutokana na mambo uliyojionea una hakika kwamba wale ambao wanamfanya Mungu kuwa fungu lao na kuthamini sana pendeleo la kumtumikia hawawezi kamwe kukata tamaa. Yesu alipowaambia wanafunzi wake waendelee kutafuta kwanza ufalme, aliwahakikishia hivi: “Nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote,” kama vile chakula, kinywaji, au mavazi.—Mt. 6:33.

9 Fikiria Walawi, ambao hawakupata urithi wa nchi. Kwa kuwa walihangaikia hasa ibada safi, ili kupata mahitaji yao walihitaji kumtegemea Yehova, ambaye aliwaambia hivi: “Mimi ni fungu lako.” (Hes. 18:20) Ingawa hatutumikii katika hekalu halisi kama makuhani na Walawi walivyofanya, tunaweza kuiga roho yao, tukiwa na uhakika kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu. Kadiri tunavyozidi kuingia katika siku za mwisho, ndivyo linavyokuwa jambo la maana zaidi kutegemea nguvu za Mungu za kutuandalia mahitaji yetu.—Ufu. 13:17.

Kuutafuta Kwanza Uadilifu wa Mungu

10, 11. Watu fulani wamemtegemea Yehova jinsi gani inapohusu kazi ya kimwili? Toa mfano.

10 Yesu aliwatia moyo pia wanafunzi wake ‘waendelee kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu.’ (Mt. 6:33) Hilo linamaanisha kutanguliza kiwango cha Yehova cha mambo yanayofaa na yasiyofaa badala ya desturi za wanadamu. (Soma Isaya 55:8, 9.) Huenda unakumbuka kwamba zamani, watu fulani walipanda au kuuza tumbaku, waliwafundisha wengine kupigana vitani, au walitengeneza na kuuza silaha za vita. Baada ya kupata ujuzi wa ile kweli, wengi wao waliamua kubadili kazi yao na hivyo kustahili kubatizwa.—Isa. 2:4; 2 Kor. 7:1; Gal. 5:14.

11 Mfano mmoja ni Andrew. Wakati yeye na mke wake walipojifunza kumhusu Yehova, waliazimia kumtumikia. Andrew aliipenda sana kazi yake lakini akaiacha. Kwa nini? Kwa sababu alikuwa akifanya kazi katika shirika ambalo liliunga mkono vita na alikuwa ameazimia kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu. Andrew alipoacha kazi hiyo, alikuwa na watoto wawili, na alikuwa na pesa za kutumia kwa miezi michache tu na hakuwa na mshahara wowote. Kwa maoni ya wanadamu, huenda ilionekana kwamba hakuwa na ‘urithi’ wowote. Alitafuta kazi huku akimtegemea Mungu. Yeye na familia yake wanapofikiria wakati huo wanaweza kusema kwa hakika kwamba mkono wa Yehova si mfupi. (Isa. 59:1) Kwa kurahisisha maisha yao, Andrew na mke wake hata wamepata pendeleo la kufanya utumishi wa wakati wote. Andrew anasema hivi: “Nyakati fulani tumehangaika sana kwa sababu ya pesa, nyumba, afya, na kuzeeka. Lakini sikuzote Yehova ametutegemeza. . . . Tunaweza kusema bila shaka yoyote kwamba, kumtumikia Yehova ndilo jambo bora na lenye kuthawabisha zaidi katika maisha ya wanadamu.” *Mhu. 12:13.

12. Ni sifa gani inayohitajiwa ili kutanguliza viwango vya Mungu? Toa mifano ya kwenu.

12 Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mkiwa na imani inayotoshana na mbegu ya haradali, mtauambia mlima huu, ‘Ondoka hapa uende pale,’ nao utaondoka, na hakuna jambo litakalowashinda.” (Mt. 17:20) Je, utatanguliza viwango vya Mungu hata ikiwa utapata matatizo kwa kufanya hivyo? Ikiwa huna uhakika kwamba unaweza kufanya hivyo, zungumza na washiriki wengine wa kutaniko. Bila shaka, utaburudishwa kiroho ukiwasikia wakisimulia mambo waliyojionea maishani.

Kuthamini Maandalizi ya Kiroho Kutoka kwa Yehova

13. Tunapojikaza kabisa katika utumishi wa Yehova, tunaweza kutazamia nini kuhusu maandalizi ya kiroho?

13 Ikiwa unathamini sana pendeleo lako la kumtumikia Yehova, unaweza kuwa na hakika kwamba atatosheleza mahitaji yako ya kimwili na ya kiroho, kama vile tu alivyowatunza Walawi. Mfikirie Daudi. Ingawa alikuwa ndani ya pango, alikuwa na hakika kwamba Mungu angemwandalia mahitaji yake. Sisi pia tunaweza kumtegemea Yehova hata inapoonekana kwamba hakuna njia ya kutokea. Kumbuka kwamba wakati Asafu ‘alipoingia katika patakatifu pakuu pa Mungu,’ ndipo alipoelewa vizuri jambo ambalo lilikuwa likimhangaisha. (Zab. 73:17) Sisi pia, tunahitaji kutafuta msaada kutoka kwa Mungu ambaye ni Chanzo cha utegemezo wetu wa kiroho. Hivyo, tunaonyesha kwamba tunathamini pendeleo letu la kumtumikia Mungu katika hali yoyote ile tunayokabili. Kwa njia hiyo tunamfanya Yehova awe fungu letu.

14, 15. Tunapaswa kutenda jinsi gani nuru inapoongezeka kuhusu maandiko fulani, na kwa nini?

14 Unatenda jinsi gani wakati Yehova, ambaye ni Chanzo cha elimu ya kiroho, anapofunua nuru zaidi kuhusu “mambo mazito ya Mungu” yaliyo katika Biblia? (1 Kor. 2:10-13) Mtume Petro alituwekea mfano bora kabisa wakati Yesu alipowaambia hivi wasikilizaji Wake: “Ninyi msipoula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu wenyewe.” Wanafunzi wengi walielewa maneno hayo kihalisi na kusema hivi: “Maneno hayo yanashtua; ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?” Kisha “wakaenda zao kwenye mambo yaliyo nyuma.” Lakini Petro akasema: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—Yoh. 6:53, 60, 66, 68.

15 Petro hakuelewa kabisa Yesu alimaanisha nini aliposema kuhusu kula mwili Wake na kunywa damu Yake. Lakini mtume huyo alimtegemea Mungu ili amwelimishe kiroho. Nuru ya kiroho kuhusu jambo fulani inapozidi kuongezeka, je, unajitahidi kuelewa sababu za Kimaandiko za marekebisho hayo? (Met. 4:18) Waberoya wa karne ya kwanza walilipokea neno “kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku.” (Mdo. 17:11) Ukiwaiga utathamini hata zaidi pendeleo lako la kumtumikia Yehova, na kumfanya kuwa fungu lako.

Kuoa au Kuolewa Katika Bwana Tu

16. Mungu anaweza kuwa fungu letu jinsi gani inapohusu amri iliyo katika 1 Wakorintho 7:39?

16 Pia, Wakristo wanahitaji kukumbuka makusudi ya Mungu kuhusu kufuata mwongozo wa Biblia wa kuoa au kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Wengi wameamua kubaki waseja badala ya kupuuza shauri hilo kutoka kwa Mungu. Mungu anawatunza vizuri wale wanaofanya hivyo. Daudi alifanya nini alipohisi upweke na kuona ni kana kwamba hakuwa na mtu wa kumsaidia? Alisema hivi: “Mbele [za Mungu] niliendelea kumwaga hangaiko langu; mbele zake niliendelea kutangaza juu ya taabu yangu mwenyewe, roho yangu ilipozimia ndani yangu.” (Zab. 142:1-3) Huenda nabii Yeremia ambaye alimtumikia Mungu kwa uaminifu kwa makumi ya miaka akiwa mseja alihisi hivyo pia. Unaweza kuchunguza mfano alioweka ambao umezungumziwa katika sura ya 8 ya kitabu Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia.

17. Dada mmoja mseja anapambana jinsi gani na upweke wa mara kwa mara?

17 Dada mmoja huko Marekani anasema hivi: “Sijawahi kamwe kuazimia kubaki mseja. Nitaolewa ikiwa nitampata mtu anayefaa. Mama yangu ambaye si mwamini alijaribu kunisadikisha niolewe na mtu yeyote yule ambaye ningempata. Nilimuuliza ikiwa angekubali kulaumiwa ikiwa ndoa yangu ingeharibika. Baada ya muda, aliona kwamba nilikuwa na kazi nzuri, nilikuwa nikijitunza mwenyewe, na nilikuwa na furaha. Akaacha kunisukuma niolewe.” Nyakati nyingine dada huyo anahisi upweke. Anasema hivi: “Wakati huo, ninajitahidi kumtegemea Yehova. Haniachi kamwe.” Ni nini ambacho kimemsaidia kumtegemea Yehova? “Sala inanisaidia kutambua kwamba Mungu ni halisi na kwamba siko peke yangu. Ikiwa Aliye Juu Zaidi katika ulimwengu mzima anasikiliza, je, ninaweza kweli kukosa shangwe na kuhisi siheshimiwi?” Akiwa na uhakika kabisa kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea,” dada huyo anasema hivi: “Ninajitahidi kujitoa kuwasaidia wengine, bila kutazamia kulipwa. Ninapojiuliza, ‘Ninaweza kumsaidia namna gani mtu huyu?’ Ninapata shangwe moyoni.” (Mdo. 20:35) Ndiyo, Yehova ni fungu lake, naye anafurahia pendeleo la kumtumikia.

18. Yehova anaweza kukufanya jinsi gani uwe fungu lake?

18 Hata ukipatwa na hali gani, unaweza kumfanya Mungu kuwa fungu lako. Ukifanya hivyo, utahesabiwa kati ya watu wake wenye furaha. (2 Kor. 6:16, 17) Kisha, unaweza kuwa fungu la Yehova, kama ilivyokuwa kwa watu wengine zamani. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:9, 10.) Kama taifa la Israeli lilivyokuwa fungu la Mungu kati ya mataifa, anaweza kukuchagua uwe mali au fungu lake na kukutunza kwa upendo.—Zab. 17:8.

[Maelezo ya Chini]

Ungesema Nini?

Unaweza kumfanya Yehova kuwa fungu lako jinsi gani

• kwa kuutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na uadilifu wake?

• kwa kuthamini chakula cha kiroho?

• kwa kutii amri ya Mungu kuhusu kuoa au kuolewa katika Bwana tu?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Yehova anakuwa fungu letu tunapohangaikia hasa utumishi wake

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mfano wa Yeremia unatia moyo