Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Kimbieni Ili Kwamba Mpate Tuzo’

‘Kimbieni Ili Kwamba Mpate Tuzo’

‘Kimbieni Ili Kwamba Mpate Tuzo’

“Kimbieni kwa namna ya kwamba mweze kupata tuzo.”—1 KOR. 9:24.

1, 2. (a) Paulo alitumia mfano gani ili kuwatia moyo Wakristo Waebrania? (b) Watumishi wa Mungu wanatiwa moyo wafanye nini?

KATIKA barua yake kwa Waebrania, mtume Paulo alitumia mfano mzuri sana wa shindano la mbio ili kuwatia moyo Wakristo wenzake. Aliwakumbusha kwamba hawakuwa wakikimbia peke yao katika shindano la mbio ya uzima. Walikuwa wamezungukwa na ‘wingu kubwa la mashahidi,’ ambao walifanikiwa kumaliza shindano hilo. Kukumbuka matendo ya imani na bidii ya wakimbiaji hao wa nyakati za kale kungewachochea Wakristo Waebrania wasonge mbele na wasiache kukimbia katika shindano lao la mbio.

2 Katika habari iliyotangulia, tulizungumzia maisha ya watu fulani kati ya ‘wingu hilo la mashahidi.’ Wote walionyesha kwamba imani isiyoyumba-yumba iliwawezesha kubaki washikamanifu kwa Mungu, kana kwamba walikuwa wakisonga mbele katika shindano la mbio mpaka mwisho. Tunaweza kujifunza somo fulani kutokana na jinsi walivyofanikiwa. Kama tulivyozungumzia katika habari hiyo, Paulo aliwatia moyo hivi watumishi wenzake, kutia ndani sisi: “Acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.”—Ebr. 12:1.

3. Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na shauri la Paulo kuhusu wakimbiaji katika michezo ya Wagiriki?

3 Kuhusu shindano la mbio za miguu, ambalo ni kati ya mashindano yaliyopendwa sana zamani, kitabu kimoja (Backgrounds of Early Christianity) kinatuambia kwamba “Wagiriki walifanya mazoezi na walishindana wakiwa uchi.” * Wakimbiaji walikimbia wakiwa uchi kwa sababu hawakutaka kitu chochote chenye uzito kiwazuie kushinda tuzo au zawadi. Ingawa leo tunaweza kuona kukimbia uchi kuwa ukosefu wa kiasi na heshima, Wagiriki hao walikimbia hivyo wakiwa na kusudi moja tu la kushinda zawadi. Wazo la Paulo lilikuwa kwamba ili kushinda zawadi katika shindano la mbio ya uzima, ni jambo la maana kwa wakimbiaji kuondoa katika maisha yao kitu chochote ambacho kinaweza kuwazuia kupata zawadi ya uzima wa milele. Hilo lilikuwa shauri zuri kwa Wakristo Waebrania, na ni shauri zuri kwetu leo pia. Ni uzito au mizigo gani ambayo inaweza kutuzuia kupata zawadi katika shindano la mbio ya uzima?

“Tuondoe Kila Uzito”

4. Watu katika siku za Noa walijishughulisha sana na mambo gani?

4 Paulo alitushauri “tuondoe kila uzito.” Hilo linatia ndani kila kitu ambacho kinaweza kutuzuia kukazia fikira kikamili shindano la mbio na kutuzuia tusijitahidi kabisa kumaliza shindano hilo. Ni vitu gani vinavyoweza kutuongezea uzito? Yesu anatusaidia kuelewa jambo hilo. Alizungumza kuhusu wakati wa Noa, ambaye alikuwa mmoja wa watu wenye imani waliotajwa na Paulo. Yesu alieleza hivi: “Sawa na vile ilivyotukia katika siku za Noa, ndivyo itakavyokuwa pia katika siku za Mwana wa binadamu.” (Luka 17:26) Yesu hakuwa akizungumza hasa kuhusu uharibifu mkubwa sana ambao utakuja; alikuwa akizungumza kuhusu namna watu walivyokuwa wakiishi. (Soma Mathayo 24:37-39.) Watu wengi katika siku za Noa hawakupendezwa na mambo ya Mungu, wala hawakujaribu kumpendeza. Ni nini kilichowakengeusha fikira? Si mambo yasiyo ya kawaida. Yalikuwa mambo ya kawaida ya maisha kama vile kula, kunywa, na kuoa. Kama Yesu alivyosema, tatizo lao hasa lilikuwa kwamba “hawakujali.”

5. Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanikiwa kumaliza shindano la mbio?

5 Kama Noa na familia yake, tuna mambo mengi ya kufanya kila siku. Tunahitaji kufanya kazi ili kujitunza wenyewe na familia yetu. Hilo linaweza kuchukua sehemu kubwa ya wakati, nguvu, na mali zetu. Ni rahisi kuhangaikia sana mahitaji ya maisha hasa tunapokuwa na matatizo ya kiuchumi. Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, pia tuna madaraka mengine ya kiroho ambayo ni ya maana. Tunahubiri, tunatayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na tunafanya funzo la kibinafsi na ibada ya familia ili tuendelee kuwa na nguvu kiroho. Ingawa Noa alikuwa na mambo mengi ya kufanya katika utumishi wa Mungu, “alifanya vivyo hivyo.” (Mwa. 6:22) Bila shaka, ikiwa tunataka kumaliza kukimbia shindano la mbio ya Kikristo ni jambo la maana kupunguza uzito tunaobeba na pia kuepuka kujitwika mzigo wowote usio wa lazima.

6, 7. Tunapaswa kukumbuka mashauri gani ya Yesu?

6 Paulo alimaanisha nini aliposema tuondoe “kila uzito”? Bila shaka, hatuwezi kujiondolea kabisa kila daraka tulilo nalo. Kuhusiana na hilo, kumbuka maneno haya ya Yesu: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.” (Mt. 6:31, 32) Maneno ya Yesu yanamaanisha kwamba hata vitu vinavyoitwa eti vya kawaida kama vile chakula na nguo vinaweza kuwa mzigo au vitu vya kukwaza tukivitanguliza maishani.

7 Fikiria maneno haya ya Yesu: “Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.” Maneno hayo yanamaanisha kwamba Baba yetu wa mbinguni, Yehova, atatimiza sehemu yake ili kutosheleza mahitaji yetu. Kwa hakika, kuwa na “vitu hivi vyote” hakumaanishi kupata kila kitu tunachopenda au tunachotaka. Hata hivyo, tunaambiwa tusihangaikie “vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa.” Kwa nini? Baadaye, Yesu aliwashauri wasikilizaji wake hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.

8. Kwa nini huu hasa ndio wakati wa ‘kuondoa kila uzito’?

8 Mstari wa kumalizia mbio uko tu mbele yetu. Ni jambo lenye kuhuzunisha kama nini ikiwa tutajiruhusu tulemewe na mizigo mizito isiyo ya lazima ambayo inaweza kutuzuia tukiwa karibu sana kumaliza mbio! Hivyo, shauri hili la mtume Paulo ni lenye hekima kwelikweli: “Ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu.” (1 Tim. 6:6) Tukichukua kwa uzito maneno ya Paulo, tutakuwa na nafasi nzuri zaidi ya kupata ile zawadi.

“Dhambi Ambayo Hututatanisha kwa Urahisi”

9, 10. (a) Maneno “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi” yanamaanisha nini? (b) Tunaweza kutegwa au kutatanishwa jinsi gani?

9 Zaidi ya kuondoa “kila uzito,” Paulo alisema tuondoe pia “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” Hiyo inaweza kuwa nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kutatanisha kwa urahisi’ linapatikana mara moja tu ndani ya Biblia, katika mstari huo. Msomi mmoja anayeitwa Albert Barnes alisema hivi: “Kama vile mkimbiaji wa wakati huo alivyokuwa mwangalifu ili asivae nguo ambayo ingemfunga miguu na kumzuia asikimbie, ndivyo Mkristo anavyopaswa hasa kuondoa kitu chochote kama hicho kinachoweza kumzuia asikimbie.” Mkristo anaweza kutatanishwa jinsi gani hivi kwamba imani yake idhoofike?

10 Mkristo hapotezi imani yake kwa ghafula tu. Hilo linaweza kutokea hatua kwa hatua, na hata bila kujua. Mwanzoni mwa barua yake, Paulo alionya kuhusu hatari ya ‘kupeperushwa’ na kusitawisha “moyo mwovu unaokosa imani.” (Ebr. 2:1; 3:12) Nguo ya mkimbiaji ikimtega miguu, bila shaka ataanguka. Hatari ya kutegwa ni kubwa hasa ikiwa mkimbiaji anapuuza hatari ya kuvaa nguo fulani wakati anapokimbia. Ni nini kinachoweza kumfanya apuuze hatari hiyo? Labda ni kutojali au kujiamini kupita kiasi au vikengeusha-fikira fulani. Tunaweza kujifunza somo gani kutokana na shauri la Paulo?

11. Ni nini kinachoweza kufanya tupoteze imani?

11 Tunapaswa kukumbuka kwamba mambo ambayo huenda tunafanya kwa siku nyingi ndiyo yanayosababisha tupoteze imani. Msomi mwingine anasema kwamba “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi” ni ile “dhambi iliyo na uvutano mkubwa zaidi juu yetu kwa sababu ya hali zetu, udhaifu wetu, na watu tunaoshirikiana nao.” Wazo ni kwamba mazingira yetu, udhaifu wetu wenyewe, na watu tunaoshirikiana nao ni mambo ambayo yanaweza kuwa na uvutano mkubwa juu yetu. Mambo hayo yanaweza kudhoofisha imani yetu au hata kufanya tuipoteze.—Mt. 13:3-9.

12. Ni vikumbusho gani ambavyo tunapaswa kuchukua kwa uzito ili tusipoteze imani?

12 Kwa miaka mingi, mtumwa mwaminifu na mwenye busara amekuwa akitukumbusha kuwa waangalifu kuhusu mambo tunayotazama na kusikiliza, yaani, mambo ambayo mioyo na akili zetu zinakazia. Tumeonywa kuhusu hatari ya kujitatanisha kwa kutafuta sana pesa na mali. Tunaweza kukengeushwa na vitumbuizo vinavyovutia sana au vitu vingi vipya vinavyotengenezwa siku baada ya siku. Ni hatari sana kuona kwamba mashauri kama hayo yanatunyima uhuru na yanawahusu tu wengine, na kwamba sisi tumekingwa kutokana na hatari hizo. Ulimwengu wa Shetani unatutatanisha kwa njia za ujanja na za udanganyifu. Kutojali, kujiamini kupita kiasi, na vikengeusha-fikira vimewaangusha wengine, na mambo hayo yanaweza kuharibu tumaini letu la kupata zawadi ya uzima.—1 Yoh. 2:15-17.

13. Tunaweza kujilinda jinsi gani na uvutano mbalimbali wenye kudhuru?

13 Kila siku, watu walio katika ulimwengu wa Shetani wanajaribu kutushawishi ili tuwe na miradi, mwenendo, na kufikiri kama wao. (Soma Waefeso 2:1, 2.) Lakini tunaweza kuamua jinsi tutakavyotenda tunaposhawishiwa na mawazo hayo. “Hewa” ambayo Paulo alitaja inasababisha kifo. Tunapaswa kuwa macho kila mara ili tusisongwe, au kukosa hewa safi, na hivyo kushindwa kumaliza shindano la mbio. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kukimbia katika shindano hilo la mbio? Kwa kweli Yesu ndiye mkimbiaji mkamilifu anayetuongoza katika shindano hilo. (Ebr. 12:2) Pia, tuna mfano wa Paulo ambaye alijiona kuwa kati ya wakimbiaji katika shindano la mbio ya Kikristo na akawahimiza waamini wenzake wamwige.—1 Kor. 11:1; Flp. 3:14.

Jinsi ‘Unavyoweza Kupata Tuzo’

14. Paulo alikuwa na maoni gani kuhusu jinsi alivyoshiriki katika shindano la mbio?

14 Paulo alikuwa na maoni gani kuhusu jinsi alivyoshiriki katika shindano la mbio? Katika maneno yake ya mwisho kwa wazee wa Efeso, alisema hivi: “Siifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye thamani sana kwangu, kama tu ningepata kumaliza mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu.” (Mdo. 20:24) Alikuwa tayari kudhabihu kila kitu, kutia ndani uhai wake, ili kumaliza shindano hilo la mbio. Bidii na kazi yote ambayo Paulo alifanya kuhusiana na habari njema ingekuwa ya bure ikiwa angeshindwa kumaliza shindano hilo. Hata hivyo, hakujiamini na kufikiri kwamba bila shaka angefanikiwa kushinda shindano hilo la mbio. (Soma Wafilipi 3:12, 13.) Alisema hivi mwishoni mwa maisha yake akiwa na uhakika wa kadiri fulani: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.”—2 Tim. 4:7.

15. Paulo aliwatia moyo jinsi gani wakimbiaji wenzake katika shindano la mbio?

15 Zaidi ya hayo, Paulo alikuwa na tamaa kubwa ya kuona Wakristo wenzake wakimaliza shindano la mbio bila kushindwa njiani. Kwa mfano, aliwatia moyo Wakristo huko Filipi wafanye kazi kwa bidii kwa ajili ya wokovu wao. Walihitaji kuendelea “kulishika sana neno la uzima.” Aliendelea kusema hivi: “Ili niwe na sababu ya kufurahi katika ile siku ya Kristo, kwamba sikukimbia bure wala kufanya kazi kwa bidii bure.” (Flp. 2:16) Vivyo hivyo, aliwatia moyo hivi Wakristo Wakorintho: “Kimbieni kwa namna ya kwamba mweze kupata tuzo.”—1 Kor. 9:24.

16. Kwa nini kusudi au zawadi inapaswa kuwa wazi katika akili zetu?

16 Katika shindano refu la mbio, kama vile mashindano ya masafa marefu, mstari wa kumalizia hauonekani mwanzoni. Hata hivyo, katika muda wote wa shindano hilo, mkimbiaji anakazia fikira mstari huo wa kumalizia. Anakazia fikira zaidi mstari wa kumalizia anapojua kwamba yuko karibu kutimiza kusudi lake. Tunapaswa kufanya vivyo hivyo katika shindano letu la mbio. Kusudi, au zawadi, inapaswa kuwa halisi kwetu. Hilo litatusaidia kupata zawadi hiyo.

17. Imani inahusika jinsi gani katika kuendelea kukazia fikira zawadi?

17 Paulo aliandika hivi: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Ebr. 11:1) Abrahamu na Sara walikuwa tayari kuacha maisha ya starehe na kuishi wakiwa “wageni na wakaaji wa muda katika nchi.” Ni nini kilichowasaidia kufanya hivyo? ‘Waliona kwa mbali utimizo wa ahadi za Mungu.’ Musa alikataa “kufurahia dhambi kwa muda” na pia “hazina za Misri.” Alipata jinsi gani imani na nguvu za kufanya hivyo? “Alikaza macho kwenye malipo ya thawabu.” (Ebr. 11:8-13, 24-26) Inaeleweka kwa nini Paulo alisema kwamba kila mmoja wa watu hao alitenda “kwa imani.” Imani iliwawezesha kuepuka kukazia fikira majaribu na matatizo yaliyowapata na ikawasaidia kuona mambo ambayo Mungu alikuwa akifanya na yale ambayo bado angefanya kwa faida yao.

18. Tunaweza kuchukua hatua gani ili kuepuka “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi”?

18 Tukitafakari juu ya wanaume na wanawake wenye imani wanaotajwa katika Waebrania sura ya 11 na kuiga mfano wao, tunaweza kusitawisha imani na kuepuka “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” (Ebr. 12:1) Pia, tunaweza ‘kufikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri’ kwa kukusanyika pamoja na watu ambao wanasitawisha imani kama hiyo.—Ebr. 10:24.

19. Una maoni gani kuhusu kuendelea kukazia fikira zawadi?

19 Tunakaribia mwisho wa shindano letu la mbio. Ni kana kwamba tunaona mstari wa kumalizia shindano hilo. Kupitia imani na kwa msaada wa Yehova, sisi pia tunaweza ‘kuondoa kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.’ Ndiyo, tunaweza kukimbia kwa namna ya kwamba tuweze kupata tuzo au zawadi, yaani, baraka ambazo Mungu na Baba yetu, Yehova, aliahidi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Michezo hiyo iliwachukiza Wayahudi wa nyakati za kale. Kitabu cha pili cha Makabayo ambacho hakikuongozwa na roho takatifu, kinasema kwamba Wayahudi wengi walikasirika wakati Kuhani Mkuu Yasoni aliyekuwa mwasi-imani alipopendekeza kujengwa kwa jumba la mazoezi huko Yerusalemu ili kuwafanya watu wafuate utamaduni wa Ugiriki.—2 Mak. 4:7-17.

Je, Unakumbuka?

• Inamaanisha nini kuondoa “kila uzito”?

• Ni nini kinachoweza kumfanya Mkristo apoteze imani?

• Kwa nini ni lazima tuendelee kukazia fikira zawadi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi” ni nini, na inaweza kututatanisha jinsi gani?