Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

4 Mungu Hatendi kwa Haki—Je, Ni Kweli?

4 Mungu Hatendi kwa Haki—Je, Ni Kweli?

4 Mungu Hatendi kwa Haki​—Je, Ni Kweli?

Jambo ambalo huenda umesikia: “Mungu ndiye anayeutawala ulimwengu huu, na kila kitu kinatendeka kwa mapenzi yake. Kwa hiyo, kwa kuwa ulimwengu umejaa ukosefu wa haki, ukandamizaji, na ubaguzi yeye ndiye anayepaswa kulaumiwa.”

Biblia inafundisha nini?: Mungu hasababishi ukosefu wa haki ulimwenguni. Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Mungu ni mkarimu kwa wote, hata kwa wale wanaoonekana kama hawastahili. Kwa mfano, “yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:45) Anawatendea kwa haki watu wa jamii na tamaduni zote, kama andiko la Matendo 10:34, 35 linavyoonyesha: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”

Hivyo basi, chanzo cha ukosefu wa haki ni nini? Watu wengi huchagua kutenda isivyo haki, wakikataa kumwiga Mungu ambaye anafuata haki. (Kumbukumbu la Torati 32:5) Pia, Biblia inaonyesha kwamba Mungu amemruhusu adui yake Ibilisi autawale ulimwengu. * (1 Yohana 5:19) Hata hivyo, hivi karibuni Mungu ataukomesha utawala wa Ibilisi ambao haufuati haki. Tayari ameandaa njia yake ya ‘kuzivunja kazi za Ibilisi.’—1 Yohana 3:8.

Jinsi kujua ukweli kunavyokusaidia: Unaweza kushangazwa na ripoti nyingi zinazotolewa kuhusu ufisadi, ukandamizaji, na ukosefu wa haki. Kujua chanzo cha matatizo hayo kutakusaidia uelewe kwa nini hali ni mbaya sana na kwa nini jitihada za mwanadamu za kuwa na ulimwengu bora hushindwa nyakati zote. (Zaburi 146:3) Badala ya kutumia wakati na nguvu kufanya mabadiliko ambayo ni ya muda tu, unaweza kuwa na tumaini hakika kuhusu wakati ujao linalotegemea imani yako katika ahadi za Mungu.—Ufunuo 21:3, 4.

Kuelewa chanzo halisi cha ukosefu wa haki kutatusaidia hasa tunapopatwa na matatizo. Tunapotendewa isivyo haki, huenda tukasema kama mtumishi wa Mungu Habakuki: “Sheria hufa ganzi, na haki haitendeki kamwe.” (Habakuki 1:4) Mungu hakumkemea Habakuki kwa kusema hivyo. Badala yake, alimhakikishia Habakuki kwamba ameweka wakati wa kurekebisha mambo na akamsaidia kupata furaha wakati huo wa taabu. (Habakuki 2:2-4; 3:17, 18) Vivyo hivyo, kuamini ahadi ya Mungu kwamba ataondoa ukosefu wa haki kunaweza kukusaidia kupata utulivu na amani ya akili katika ulimwengu huu usiofuata haki.

[Maelezo ya Chini]

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Je, kweli Mungu ndiye anayesababisha mateso na ukosefu wa haki?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

© Sven Torfinn/Panos Pictures