Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini kulikuwa na watu waliobadili pesa katika hekalu la Yerusalemu?

Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alishughulikia ukosefu mkubwa wa haki uliokuwa ukiendelea ndani ya hekalu. Biblia inasema hivi: ‘Yesu aliwafukuza wale wote waliokuwa wakiuza na kununua katika hekalu, na kuzipindua meza za wale waliokuwa wakibadili pesa na viti vya wale waliokuwa wakiuza njiwa. Naye akawaambia: “Imeandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala,’ lakini ninyi mnaifanya kuwa pango la wanyang’anyi.”’—Mathayo 21:12, 13.

Wayahudi wa karne ya kwanza walioenda hekaluni huko Yerusalemu walitoka katika maeneo na majiji mbalimbali, na walibeba sarafu kutoka maeneo ya kwao. Hata hivyo, walipaswa kutumia pesa zilizokubalika ili kulipia kodi ya hekalu iliyotolewa kila mwaka. Walipaswa pia kununua wanyama kwa ajili ya kutoa dhabihu na vilevile kutoa michango mingine ya hiari. Hivyo, watu waliobadili pesa waliwatoza malipo fulani ili kuwabadilishia sarafu za maeneo walikotoka na kuwapa pesa zilizotumika hekaluni. Sherehe za Wayahudi zilipokaribia, watu hao waliobadili pesa waliweka meza zao ndani ya hekalu kwenye Ua wa Mataifa.

Kwa kuwa Yesu alisema watu waliokuwa wakibadili pesa walifanya hekalu kuwa “pango la wanyang’anyi,” inaonekana walitoza malipo ya juu kupita kiasi.

Kwa nini mizeituni ilithaminiwa sana nyakati za Biblia?

Mizeituni na mashamba ya mizabibu ilikuwa baadhi ya baraka ambazo Mungu aliwaahidi watu wake ikiwa wangekuwa waaminifu kwake. (Kumbukumbu la Torati 6:10, 11) Leo pia, mizeituni inathaminiwa sana katika maeneo ambapo inakua. Inaweza kuzaa matunda kwa mamia ya miaka hata bila kutunzwa sana. Mzeituni uliopandwa shambani unaweza kuhimili ukame wa mara kwa mara na kuzaa hata kama umepandwa katika eneo lenye mawemawe. Mzeituni unapokatwa, shina lake linatokeza miche ambayo inaweza kukua na kuwa miti mikubwa.

Katika nyakati za Biblia, maganda na majani ya mti huo yalithaminiwa sana kwa kuwa yalitumiwa kama dawa ya kupunguza homa. Umajimaji unaonata na wenye harufu nzuri ya vanila ambao unatoka kwenye matawi ya zamani ulitumiwa kutengeneza marashi. Hata hivyo, sababu kuu iliyofanya mti huo uwe wenye thamani ni kwamba ulitokeza chakula, yaani, matunda na hasa mafuta yake. Karibu nusu ya utomvu wa zeituni iliyoiva ni mafuta.

Mti uliozaa vizuri ungetokeza lita 57 za mafuta kwa mwaka. Pia, mafuta ya zeituni yalitumiwa kama mafuta ya taa kwa ajili ya sherehe na mambo ya kidini, kama mafuta ya nywele na ngozi, na kama dawa ya vidonda na ya kutuliza majeraha.—Kutoka 27:20; Mambo ya Walawi 2:1-7; 8:1-12; Ruthu 3:3; Luka 10:33, 34.