Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kwa Nini Ni Muhimu Sana ‘Kuendelea Kukesha’?

Kwa Nini Ni Muhimu Sana ‘Kuendelea Kukesha’?

Kwa Nini Ni Muhimu Sana ‘Kuendelea Kukesha’?

“NI NINI itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:3) Alipokuwa akijibu swali au ulizo hilo, Yesu aliwapa wanafunzi wake ishara iliyo wazi, yenye habari kamili na ya pekee ambayo ingeweza kutambuliwa kwa urahisi kama ilivyorekodiwa katika Mathayo sura ya 24, Marko sura ya 13, na Luka sura ya 21. Kisha akaongezea hivi: “Endeleeni kukesha.”—Mt. 24:42.

Kama ishara hiyo ingeonekana waziwazi, kwa nini Yesu aliongezea himizo hilo la ziada? Fikiria mambo haya mawili yanayoweza kutokea. Kwanza, vikengeusha-fikira vinaweza kuwafanya wengine waipuuze hiyo ishara na hivyo kudhoofika kiroho na kutoendelea kukesha. Pili, Mkristo anaweza kutambua sehemu mbalimbali za hiyo ishara lakini kwa sababu ya hali zinazomzunguka anaweza kuhisi kwamba haimhusu moja kwa moja. Hivyo, anaweza kufikiri kwamba “dhiki kuu,” yaani, ule upeo wa unabii wa Yesu, bado iko mbali na kwamba hana haja ya ‘kuendelea kukesha.’—Mt. 24:21.

“Hawakujali”

Yesu aliwakumbusha wafuasi wake kuhusu watu walioishi katika siku za Noa. Ni lazima watu hao waliona kazi ya kuhubiri ambayo Noa aliifanya, ujenzi wa safina kubwa, na jeuri iliyokuwa ikiendelea. Hata hivyo, watu wengi “hawakujali.” (Mt. 24:37-39) Mtazamo kama huo wa kupuuza maonyo umeenea sana leo. Kwa mfano, ishara za barabarani zinaonyesha waziwazi mwendo au kasi ambayo madereva wanapaswa kuendesha magari yao, hata hivyo, madereva wengi wanapuuza ishara hizo. Mara nyingi wenye mamlaka wanalazimika kuweka matuta katika barabara za miji ili kuwalazimisha madereva wapunguze mwendo. Vivyo hivyo, Mkristo anaweza kujua ishara ya siku za mwisho lakini bado akajihusisha na shughuli ambazo zinaweza kumkengeusha. Arielle, kijana anayeishi huko Afrika ya Magharibi, alikabili hali kama hiyo.

Arielle alipenda sana kutazama mpira wa mikono wa wanawake kwenye televisheni. Shule yake ilipoanzisha timu, alitumaini kushiriki katika mchezo huo na hivyo akakosa kuona hatari za kiroho ambazo angekabili. Akajiandikisha ili awe golikipa. Ni nini kilichofuata? Anaeleza hivi: “Wengine kati ya wachezaji wenzangu walikuwa na marafiki wa kiume ambao walitumia dawa za kulevya na kuvuta sigara. Walinicheka kwa sababu nilikuwa tofauti nao, lakini nilifikiri kwamba ningeweza kukabiliana na hali hiyo. Bila kutazamia, mchezo huo ukaanza kuharibu hali yangu ya kiroho. Nilipenda sana mpira wa mikono kwa akili na moyo wangu wote. Mara nyingi katika mikutano ya Kikristo, akili yangu ilitangatanga na kufikiria mambo yaliyokuwa uwanjani badala ya mambo yaliyokuwa yakiendelea katika Jumba la Ufalme. Utu wangu wa Kikristo pia ukabadilika. Badala ya kupenda tu mchezo huo, nikasitawisha tamaa kubwa ya kushinda. Nilifanya sana mazoezi ili nitosheleze tamaa yangu ya kushindana. Nikazidi kuwa na mkazo. Hata nilipoteza marafiki kwa sababu ya mchezo huo.

“Hali hiyo ilifikia kilele wakati timu tuliyokuwa tukishindana nayo ilipopewa penalti katika mchezo fulani. Nilikuwa tayari kulinda lango ili tusifungwe. Bila kujua, nilikuwa nimesali kwa Yehova anisaidie nizuie mpira huo! Tukio hilo lilifanya nitambue jinsi hali yangu ya kiroho ilivyokuwa mbaya. Nilipata tena nguvu za kiroho jinsi gani?

“Nilikuwa nimetazama DVD yetu Young People Ask—What Will I Do With My Life? (Les jeunes s’interrogent—Que vais-je faire de ma vie?) * Nikaamua kuitazama tena na wakati huu kwa makini hata zaidi. Kwa kweli, hali yangu ilikuwa kama ya André, kijana aliye katika drama hiyo. Nilikazia fikira hasa jambo fulani ambalo mzee fulani alimpendekezea André afanye—kusoma na kutafakari andiko la Wafilipi 3:8. Jambo hilo lilinisaidia na nikaacha mchezo huo.

“Maisha yangu yalibadilika kabisa! Roho ya mashindano na mkazo niliokuwa nao vikatoweka. Nilikuwa na furaha zaidi na nikawa karibu zaidi na marafiki wangu Wakristo. Nikaanza kuthamini zaidi mambo ya kiroho. Nilianza tena kukaza uangalifu kwenye mikutano na kuifurahia. Pia, huduma yangu ilizidi kuwa bora. Sasa ninatumikia kwa ukawaida nikiwa painia msaidizi.”

Ikiwa vikengeusha-fikira vinakufanya uipuuze ile ishara ambayo Yesu alitupatia, chukua hatua zinazohitajiwa kama alivyofanya Arielle. Unaweza kujaribu kufanya mambo yafuatayo. Chunguza Fahirisi, ambayo inalinganishwa na ramani inayoelekeza kwenye hazina zilizofichwa. Fahirisi ina habari ambazo zitakusaidia kupata mashauri mazuri na masimulizi yanayoonyesha jinsi wengine walivyopambana na majaribu. Faidika kwa ukamili na mikutano ya Kikristo kwa kutayarisha vizuri na kuandika mambo makuu. Wengine wameona kwamba kukaa mbele katika Jumba la Ufalme kunasaidia sana. Wasikilizaji wanapoombwa watoe maelezo, jitahidi kutoa maelezo yako mapema. Zaidi ya hayo, endelea kuwa macho kiroho kwa kulinganisha matukio ya hivi karibuni na sehemu mbalimbali za ile ishara na hali nyingine za “siku za mwisho.”—2 Tim. 3:1-5; 2 Pet. 3:3, 4; Ufu. 6:1-8.

“Iweni Tayari”

Ishara ya siku za mwisho inahusu mataifa yote, yaani, “dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:7, 14) Mamilioni ya watu wanaishi katika maeneo yanayokumbwa na magonjwa ya kuambukiza, upungufu wa chakula, matetemeko ya nchi, na matukio mengine yaliyotabiriwa. Lakini, watu wengine wengi wanaishi katika maeneo yenye utulivu na usalama wa kadiri fulani. Ikiwa wewe binafsi hujashuhudia sehemu fulani za ile ishara, je, unapaswa kufikiri kwamba bado dhiki kuu iko mbali sana? Hilo halingekuwa jambo la hekima.

Kwa mfano, fikiria kile ambacho Yesu alitabiri kuhusu “tauni na upungufu wa chakula.” (Luka 21:11) Kwanza, Yesu hakusema kwamba matukio hayo yangetokea katika maeneo yote kwa wakati mmoja au kwa kiwango kilekile. Badala yake, alisema kuwa matukio hayo yangetokea “katika mahali pamoja baada ya pengine.” Hivyo, hatuwezi kutazamia matukio yaleyale yatokee kila mahali kwa wakati uleule. Pili, mara tu baada ya kutaja upungufu wa chakula, Yesu alionyesha kwamba wafuasi wake wangepaswa kuwa macho ili wasile kupita kiasi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi.” (Luka 21:34) Hivyo, Wakristo wote hawapaswi kutazamia kuona kila sehemu ya ile ishara. Badala yake, Yesu alisema: “Wakati mnapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.” (Luka 21:31) Vifaa vya kisasa vya mawasiliano vinatuwezesha kuona sehemu zote za ile ishara, hata iwe tunakabili hali gani katika eneo letu.

Kumbuka pia kwamba tayari Yehova ameweka ‘siku na saa’ ambayo dhiki kuu itaanza. (Mt. 24:36) Jinsi matukio hayo yanavyoendelea kutukia duniani hakutabadili tarehe hiyo.

Yesu aliwahimiza Wakristo kila mahali hivi: “Iweni tayari.” (Mt. 24:44) Tunapaswa kuwa tayari sikuzote. Bila shaka, hatuwezi kujihusisha na utendaji wa kiroho nyakati zote. Zaidi ya hayo, hakuna yeyote kati yetu anayejua atakuwa akifanya nini dhiki kuu itakapoanza. Huenda wengine watakuwa wakifanya kazi shambani au kufanya kazi za nyumbani. (Mt. 24:40, 41) Basi, tunapaswa kufanya nini ili tuwe tayari?

Emmanuel, Victorine, na mabinti wao sita wanaishi katika eneo fulani la Afrika ambako hawakabiliani moja kwa moja na matukio yote ya ile ishara. Hivyo, waliamua kuwa na mazungumzo ya kiroho kila siku ili yawasaidie kuwa tayari. Emmanuel anasema hivi: “Haikuwa rahisi kupata wakati unaofaa wa sisi sote kukutana. Mwishowe tuliamua kufanya mazungumzo hayo kuanzia saa 12 hadi saa 12:30 asubuhi. Baada ya kuchunguza andiko la siku, tunatayarisha mafungu machache kwenye moja ya vitabu ambavyo tunajifunza katika kutaniko juma hilo.” Je, programu hiyo imewasaidia kuendelea kukesha? Bila shaka! Emmanuel ni mratibu wa baraza la wazee kutanikoni. Mara nyingi Victorine anatumikia akiwa painia msaidizi na amewasaidia wengi kukubali kweli. Mabinti wao wote wanaendelea vizuri kiroho.

Yesu anatuhimiza hivi: “Endeleeni kutazama, endeleeni kukesha.” (Marko 13:33) Usiruhusu vikengeusha-fikira vikufanye ukose kuwa macho kiroho. Badala yake, fuata shauri zuri linalopatikana katika vitabu na mikutano yetu ya kutaniko, kama alivyofanya Arielle. Kama familia ya Emmanuel inavyofanya, jitahidi kufanya jambo fulani kila siku ili kuwa tayari na hivyo ‘kuendelea kukesha.’

[Maelezo ya Chini]

^ Ni drama ya kisasa kuhusu kijana Mkristo anayejitahidi kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Mazungumzo ya kiroho kila siku yanamsaidia Emmanuel na familia yake ‘kuendelea kuwa tayari’