Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tafrija Unayochagua Inakujenga?

Je, Tafrija Unayochagua Inakujenga?

Je, Tafrija Unayochagua Inakujenga?

“Endeleeni kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.”—EFE. 5:10.

1, 2. (a) Neno la Mungu linaonyesha jinsi gani kwamba Yehova anataka tufurahie maisha? (b) Kuona wakati wa kujifurahisha kuwa “zawadi ya Mungu” kutatuchochea kufanya nini?

KATIKA Biblia nzima, tunapata maneno yanayoonyesha kwamba Yehova hataki tuishi tu bali pia anataka tufurahie maisha. Kwa mfano, andiko la Zaburi 104:14, 15 linasema kwamba Yehova anafanya ‘chakula kitokezwe duniani, na divai ambayo hufanya moyo wa mwanadamu anayeweza kufa ushangilie, na kuufanya uso ung’ae kwa mafuta, na mkate unaotegemeza moyo wa mwanadamu anayeweza kufa.’ Kwa kweli, Yehova anafanya mimea ikue na kutokeza nafaka, mafuta, na divai ili kutegemeza uhai wetu. Lakini pia divai inafanya ‘moyo ushangilie.’ Hata ingawa divai si ya lazima ili kuendeleza uhai, inaweza kutuletea shangwe zaidi. (Mhu. 9:7; 10:19) Ndiyo, Yehova anataka tushangilie, anataka mioyo yetu ijae “uchangamfu.”—Mdo. 14:16, 17.

2 Kwa hiyo, hakuna sababu ya kujihisi kuwa na hatia tunapopanga mara kwa mara kuwa na wakati wa ‘kuwaangalia kwa makini ndege wa mbinguni,’ na “mayungiyungi ya shamba” au kufurahia utendaji mbalimbali ambao unatuburudisha na kufanya maisha yetu yawe yenye kufurahisha. (Mt. 6:26, 28; Zab. 8:3, 4) Kuwa na afya nzuri na furaha maishani ni “zawadi ya Mungu.” (Mhu. 3:12, 13) Kuona kwamba wakati wa kujifurahisha ni sehemu ya zawadi hiyo kutatuchochea kutumia wakati huo kwa njia ambayo inampendeza Mpaji wa zawadi hiyo. *

Tafrija Mbalimbali na Mipaka

3. Kwa nini ni jambo linalopatana na akili kuwaruhusu watu wajichagulie aina ya tafrija wanayopenda?

3 Watu wenye maoni yenye usawaziko kuhusu tafrija wanashiriki katika utendaji mbalimbali lakini bado wanatambua kwamba wanahitaji kuwa na mipaka. Kwa nini? Ili kujibu swali hilo, acheni tulinganishe tafrija na chakula. Vyakula vinavyopendwa vinatofautiana katika sehemu mbalimbali za ulimwengu. Kwa kweli, vyakula vinavyopendwa sana na watu wa eneo fulani huenda visipendwe na watu wa eneo lingine. Vivyo hivyo, tafrija inayopendwa na Wakristo katika sehemu fulani ya ulimwengu huenda isiwavutie Wakristo katika sehemu nyingine. Ndivyo ilivyo pia kati ya Wakristo wanaoishi katika sehemu moja, Mkristo fulani anaweza kuona kwamba kusoma kitabu kizuri akiwa ameketi kwa starehe kuwa jambo la kuburudisha, lakini huenda Mkristo mwingine akaliona jambo hilo kuwa lenye kuchosha. Huenda mwingine akafurahia sana kuendesha baiskeli huku akifurahia mazingira, lakini huenda mwingine akaona jambo hilo kuwa lenye kuchosha. Hata hivyo, tunakubali kwamba inapohusu mambo kama vile chakula na tafrija, kila mtu ana uhuru wa kuchagua mambo tofauti anayopenda.—Rom. 14:2-4.

4. Kwa nini tunahitaji kuweka mipaka kuhusu aina ya tafrija tunayochagua? Toa mfano.

4 Hata hivyo, tunatambua pia kwamba ingawa kila mtu ana uhuru wa kujichagulia aina ya tafrija anayopenda hiyo si sababu ya kupita mipaka. Kwa mfano, fikiria tena kuhusu chakula. Hata ikiwa huenda tunapenda kula vyakula mbalimbali, hatuwezi kula kimakusudi chakula kilichooza. Si jambo linalopatana na akili kula chakula kilichooza na kufanya hivyo kunaweza kuhatarisha afya yetu. Vivyo hivyo, ingawa tunaweza kupata vitumbuizo vizuri vya kila aina, hatupaswi kutafuta vitumbuizo na tafrija ambazo zinahatarisha uhai, zenye jeuri, au zinazoonyesha maadili yaliyooza. Kushiriki katika utendaji wa aina hiyo hakupatani na kanuni za Biblia na kunahatarisha afya yetu ya kimwili au ya kiroho. Ili kuhakikisha kwamba hatupiti mipaka inayofaa, ni vizuri tuamue mapema ikiwa tafrija fulani tunayopenda inajenga au haijengi. (Efe. 5:10) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

5. Tunaweza kujua jinsi gani ikiwa tafrija inatimiza viwango vya Mungu?

5 Ili tafrija itujenge na kuwa yenye kupendeza machoni pa Yehova, inahitaji kutimiza viwango fulani vya wazi vilivyoandikwa katika Neno la Mungu. (Zab. 86:11) Ili kujua ikiwa tafrija unayopenda inatimiza viwango hivyo, unaweza kuchunguza mambo matatu ambayo huenda ukafikiria. Mambo hayo yanatia ndani maswali haya matatu, ni tafrija gani, wakati gani, na nitashiriki pamoja na nani? Acheni tuzungumzie kila swali.

Ni Tafrija Gani?

6. Tunahitaji kukataa kabisa vitumbuizo vya aina gani, na kwa nini?

6 Kabla ya kushiriki katika tafrija fulani, swali la kwanza ambalo unapaswa kujiuliza ni hili, ni tafrija gani?—yaani, ‘Ninavutiwa na tafrija ya aina gani?’ Unapotafuta jibu, kuna faida ya kukumbuka kwamba kuna aina mbili tu za tafrija. Aina ya kwanza ya tafrija inatia ndani mambo ambayo hatuwezi kamwe kufanya na aina ya pili inatia ndani mambo ambayo tunaweza kuamua kufanya. Tafrija ya kwanza ni ya aina gani? Katika ulimwengu huu mwovu, tafrija au vitumbuizo vingi vinatia ndani matendo ambayo yanapingana waziwazi na kanuni za Biblia au kuvunja sheria za Mungu. (1 Yoh. 5:19) Wakristo wa kweli wanakataa kabisa tafrija au vitumbuizo vyote vya aina hiyo. Vitumbuizo hivyo vinatia ndani matendo ya ukatili, ibada ya roho waovu, ngono za watu wa jinsia moja, ponografia (picha au habari za ngono), jeuri, au vitumbuizo ambavyo vinatukuza mazoea mengine machafu ya kingono yaliyopotoka. (1 Kor. 6:9, 10; soma Ufunuo 21:8.) Tunapokataa kabisa vitumbuizo vya aina hiyo, popote pale tulipo, tunamwonyesha Yehova kwamba ‘tunachukia maovu.’—Rom. 12:9; 1 Yoh. 1:5, 6.

7, 8. Tunaweza kujua jinsi gani ikiwa tafrija fulani ni nzuri au si nzuri? Toa mfano.

7 Aina ya pili ya tafrija inatia ndani vitumbuizo ambavyo havina mazoea yanayokatazwa moja kwa moja katika Neno la Mungu. Katika hali kama hizo, kabla ya kuchagua tafrija za aina hiyo, tunapaswa kulinganisha kwa uangalifu tafrija hizo na yale ambayo Yehova anaona kuwa yanafaa, kulingana na kanuni za Biblia. (Met. 4:10, 11) Kisha tunahitaji kufanya uamuzi wa kibinafsi ambao utatuacha tukiwa na dhamiri njema. (Gal. 6:5; 1 Tim. 1:19) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Fikiria jambo hili: Kabla ya kula chakula ambacho hatujawahi kula, kwanza tunauliza kimechanganywa na vitu gani. Vivyo hivyo, kabla ya kushiriki katika tafrija yoyote, tunahitaji kuchunguza inatia ndani mambo gani.—Efe. 5:17.

8 Kwa mfano, labda unapenda michezo, na hilo linaeleweka. Michezo inaweza kufurahisha na kusisimua. Hata hivyo, namna gani ikiwa unavutiwa na michezo fulani kwa sababu kuna ushindani mkali, watu wanahatarisha kabisa uhai wao, wanaumia kwa urahisi, wanasherehekea kwa fujo, inachochea roho ya utaifa, au inatia ndani mambo mengine kama hayo? Baada ya kuchunguza mambo yaliyo katika michezo hiyo, inaelekea kwamba utaona kuwa ni vigumu kupatanisha njia yako ya kufikiri na njia ya Yehova ya kufikiri na pia na ujumbe wa amani na upendo ambao tunawahubiria wengine. (Isa. 61:1; Gal. 5:19-21) Kwa upande mwingine, ikiwa tafrija fulani inatia ndani mambo yanayofaa machoni pa Yehova, basi tafrija kama hiyo inaweza kukunufaisha na kukuburudisha.—Gal. 5:22, 23; soma Wafilipi 4:8.

Niwe na Tafrija Wakati Gani?

9. Jibu letu kwa swali, ‘Niwe na tafrija wakati gani?’ linafunua nini?

9 Swali la pili ambalo unapaswa kujiuliza ni, Wakati gani?—yaani, ‘Niwe na tafrija wakati gani? Nitatumia muda mwingi kadiri gani katika tafrija?’ Jinsi tunavyojibu swali, tafrija gani? inafunua mengi kuhusu mielekeo yetu, yaani, mambo tunayoona kuwa yanakubalika na yale tunayoona hayakubaliki. Hata hivyo, jibu letu kwa swali wakati gani? linaonyesha mambo tunayotanguliza, yaani, mambo tunayoona kuwa ya maana na yale ambayo hatuyaoni kuwa ya maana. Basi ni nini kinachoweza kutusaidia kujua ni kwa kadiri gani tafrija fulani ni ya maana katika maisha yetu?

10, 11. Maneno ya Yesu katika Mathayo 6:33 yanatusaidia jinsi gani kuamua muda tunaopaswa kutumia katika tafrija?

10 Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Kwa hiyo, jambo la kwanza katika maisha yetu ni kumpenda Yehova. Tunaonyesha kwamba tunafanya hivyo kwa kufuata shauri hili la Yesu: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mt. 6:33) Maneno hayo yanaweza kutusaidia jinsi gani kujua ni muda mwingi kadiri gani tunaotumia katika tafrija na ni ya maana kadiri gani?

11 Ona kwamba Yesu alituambia ‘tuendelee kuutafuta kwanza ufalme.’ Hakutuambia ‘tuendelee kuutafuta ufalme tu.’ Bila shaka, Yesu alijua kwamba tungehitaji kutafuta vitu vingine vingi katika maisha zaidi ya kuutafuta Ufalme. Tunahitaji makao, chakula, mavazi, elimu ya kadiri, kazi ya kimwili, tafrija, na kadhalika. Hata hivyo, kati ya mambo yote ambayo tunatafuta, mambo ambayo tunapaswa kutafuta kwanza ni mambo ya Ufalme tu. (1 Kor. 7:29-31) Ukweli huo wa msingi unapaswa kutuchochea kufuatia mambo mengine ya ziada, kama vile tafrija, kwa njia itakayotuwezesha kutimiza kazi yetu kuu, yaani, kazi ya Ufalme. Tukifanya hivyo, tafrija ya kiasi inaweza kutujenga.

12. Kanuni iliyo katika andiko la Luka 14:28 inaweza kutumiwa jinsi gani kuhusiana na tafrija?

12 Hivyo basi, inapohusu kutumia wakati katika tafrija, ni vizuri tuhesabu gharama mapema. (Luka 14:28) Tunahitaji kujua tafrija fulani itagharimu, yaani, itahitaji muda mwingi kadiri gani. Kisha tunahitaji kujua muda ambao tunapaswa kutumia katika tafrija hiyo. Ikiwa kufuatia aina fulani ya tafrija kutafanya tupuuze mambo ya maana kama vile funzo la kibinafsi la Biblia, ibada ya familia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, au kushiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme, basi tafrija hiyo haifai. (Marko 8:36) Lakini ikiwa tafrija tunayofurahia mara kwa mara inatusaidia kupata nguvu za kuendelea kufanya kazi ya Ufalme, basi tunaweza kusema kwamba tafrija hiyo haitupotezei wakati.

Ninashirikiana na Nani?

13. Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uangalifu kuhusu wale tunaoshirikiana nao katika tafrija?

13 Swali la tatu ambalo tunapaswa kujiuliza ni hili, Ninashirikiana na nani?—yaani, ‘Ninataka kushirikiana na watu wa aina gani katika tafrija zangu?’ Ni jambo la maana kufikiria swali hilo inapohusu tafrija. Kwa nini? Kwa sababu ubora wa tafrija tunayochagua unategemea sana ubora wa marafiki tunaochagua. Kama vile tu ambavyo tunafurahia zaidi chakula tunapokula pamoja na marafiki wazuri, vivyo hivyo, kwa kawaida tunafurahia tafrija tunapokuwa na marafiki wazuri. Kwa hiyo, ni jambo linaloeleweka kuona kwamba wengi wetu, hasa vijana, wanafurahia tafrija pamoja na wengine. Hata hivyo, ili kuhakikisha kwamba tafrija itatujenga, ni jambo la hekima kuamua mapema aina ya watu ambao tutachagua wawe marafiki wetu na wale ambao tunapaswa kuepuka.—2 Nya. 19:2; soma Methali 13:20; Yak. 4:4.

14, 15. (a) Yesu aliweka mfano gani katika kuchagua marafiki wanaofaa? (b) Tunapaswa kujiuliza maswali gani kuhusu marafiki wetu?

14 Tutafaidika sana tukiiga mfano wa Yesu katika kuchagua marafiki. Tangu wakati wa uumbaji na kuendelea, Yesu aliwapenda wanadamu. (Met. 8:31) Alipokuwa duniani, aliwatendea kwa fadhili na upendo watu wa kila aina. (Mt. 15:29-37) Hata hivyo, Yesu aliweka mpaka kati ya kuwa mwenye urafiki na kuwa rafiki wa karibu. Ingawa alikuwa mwenye urafiki kuelekea watu kwa ujumla, alikuwa rafiki wa karibu wa wale tu ambao walitimiza matakwa fulani. Akiongea na mitume wake waaminifu 11, Yesu alisema hivi: “Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya ninalowaamuru ninyi.” (Yoh. 15:14; ona pia Yohana 13:27, 30.) Watu pekee ambao Yesu alikubali wawe marafiki wake ni wale ambao walimfuata yeye na kumtumikia Yehova.

15 Kwa hiyo, unapoamua kumchagua au kutomchagua mtu fulani ili awe rafiki yako wa karibu, ni jambo la hekima kukumbuka maneno hayo ya Yesu. Jiulize maswali kama haya: ‘Je, mtu huyu anaonyesha kwa maneno na kwa matendo kwamba anatii amri za Yehova na Yesu? Je, ana viwango na maadili kama yangu yanayotegemea Biblia? Ikiwa nitashirikiana naye, je, atanitia moyo nitangulize Ufalme katika maisha yangu na kuwa mtumishi mshikamanifu wa Yehova?’ Ikiwa una hakika kwamba majibu ya maswali hayo ni ndiyo, basi umepata rafiki mzuri ambaye unaweza kufurahia naye tafrija.—Soma Zaburi 119:63; 2 Kor. 6:14; 2 Tim. 2:22.

Je, Tafrija Tunayopenda Inatimiza Matakwa Hayo?

16. Tunahitaji kuchunguza mambo gani kuhusu tafrija tunayochagua?

16 Tumezungumzia kwa ufupi mambo matatu kuhusu tafrija na vitumbuizo, yaani, ubora wake, muda tunaopaswa kutumia, na watu tunaopaswa kushirikiana nao. Ili tafrija yetu iwe yenye kujenga inapaswa kutimiza ipasavyo viwango vya Biblia katika kila moja ya mambo hayo. Kwa hiyo, kabla ya kushiriki katika tafrija fulani, tunahitaji kuchunguza ikiwa inatimiza viwango hivyo. Inapohusu ubora, tunapaswa kujua jambo hili: ‘Tafrija hiyo inatia ndani nini? Je, inafaa au ni chafu?’ (Met. 4:20-27) Kuhusu muda tunaotumia, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Nitatumia muda mwingi kadiri gani katika tafrija hiyo? Je, muda huo unafaa au unapita kiasi?’ (1 Tim. 4:8) Na kuhusu watu tunaoshirikiana nao, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Nitashirikiana na nani katika tafrija hiyo? Je, ni marafiki wazuri au wabaya?’—Mhu. 9:18; 1 Kor. 15:33.

17, 18. (a) Tunaweza kuchunguza wenyewe jinsi gani ili kujua ikiwa tafrija yetu inatimiza viwango vya Biblia? (b) Wewe binafsi umeazimia kufanya nini kuhusiana na tafrija unayochagua?

17 Ikiwa tafrija haitimizi viwango vya Biblia katika jambo lolote kati ya mambo hayo matatu, basi tafrija hiyo haifai. Kwa upande mwingine, tukihakikisha kwamba tafrija zetu zinafuata viwango vya Biblia katika mambo hayo yote matatu, basi tafrija zetu zitamletea Yehova heshima na kutujenga.—Zab. 119:33-35.

18 Hivyo basi, inapohusu tafrija, acheni tujitahidi kufanya jambo linalofaa kwa wakati unaofaa na pamoja na watu wanaofaa. Ndiyo, kila mmoja wetu na aazimie kutoka moyoni kufuata shauri hili la Biblia: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Kor. 10:31.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Katika habari hii, maneno “tafrija” na “vitumbuizo” yanatumiwa kumaanisha wakati tunaotenga ili kushiriki katika utendaji mbalimbali unaostarehesha ambao unatuletea furaha.

Je, Unaweza Kueleza?

Kuhusu tafrija au vitumbuizo, unaweza kutumia jinsi gani kanuni iliyo katika . . .

Wafilipi 4:8?

Mathayo 6:33?

Methali 13:20?

[Maswali ya Funzo]

[Mchoro katika ukurasa wa 9]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Tafrija Gani?

[Mchoro katika ukurasa wa 10]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Wakati Gani?

[Mchoro katika ukurasa wa 12]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Pamoja na Nani?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Tunaweza kufuata jinsi gani mfano wa Yesu tunapochagua marafiki wetu na tafrija au vitumbuizo vyetu ?