Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Jibu la Swali Hilo Ni Muhimu?

Je, Jibu la Swali Hilo Ni Muhimu?

Je, Jibu la Swali Hilo Ni Muhimu?

“Nilikuwa na umri wa miaka kumi nilipoanza kutembea na wavulana. Mwanzoni, tungeshikana mikono na kupigana busu. Lakini muda si muda, tukaanza kushikana sehemu za siri na kuchezeana kingono. Nilipofika umri wa miaka 15, nilipata kazi ya kuajiriwa na wanaume niliofanya kazi nao walianza kunifuata wakitaka kufanya ngono nami. Bila woga, nilitaka kufanya mambo yote ambayo wafanyakazi wenzangu walikuwa wakifanya. Nilitaka wanikubali, jambo ambalo liliniongoza nifanye ngono zaidi na zaidi.”—SARAH, * AUSTRALIA.

JE, UNAWEZA kuamini kwamba Sarah alilelewa katika familia iliyomwogopa Mungu? Wazazi wake walijitahidi kumlea na kumfundisha kuishi kulingana na viwango vya Biblia kuhusu maadili. Lakini Sarah akachagua kuishi kwa njia tofauti.

Watu wengi wanaweza kukubaliana na uamuzi wa Sarah. Wanaamini kwamba mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono yamepitwa na wakati kabisa. Wengine wanaona kwamba ni sawa kwa mtu kufuata dini na wakati huohuo kujihusisha na mwenendo mchafu kingono.

Je, ni muhimu kujua na kuishi kulingana na mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu ngono? Biblia ‘imeongozwa na roho ya Mungu nayo ni yenye faida kwa kufundisha.’ (2 Timotheo 3:16) Ikiwa unaamini kwamba Mungu aliwaumba wanadamu na kwamba Biblia ni Neno lake lililoongozwa na roho yake, basi ni muhimu kujua mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono.

Jambo la kusikitisha ni kwamba watu wengi wametatanishwa na mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu ngono. Viongozi wa kidini ambao wanadai kwamba wanaiheshimu Biblia, wanafundisha mambo yanayotofautiana kuhusu ngono. Kwa kweli mafundisho hayo tofauti yamesababisha migawanyiko katika makanisa makubwa-makubwa.

Badala ya kutegemea mambo ambayo wengine wanasema, kwa nini usitenge muda kidogo na uchunguze jambo hilo wewe mwenyewe? Makala inayofuata inazungumzia maswali kumi yanayoulizwa kwa ukawaida juu ya mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono. Katika makala hiyo utapata majibu yaliyo wazi yanayotegemea mambo ambayo Biblia inafundisha hasa. Makala ya mwisho katika mfululizo huu itazungumzia kwa nini maamuzi tunayofanya ni muhimu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Jina limebadilishwa.