Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

NI NINI kilichomchochea mwanamume fulani aliyekuwa mcheza-kamari na mwizi aache mazoea yake na kubadili maisha yake? Soma yale anayosema.

“Nilipenda Sana Mashindano ya Farasi.”—RICHARD STEWART

MWAKA WA KUZALIWA: 1965

NCHI: JAMAIKA

HISTORIA: MCHEZA-KAMARI NA MWIZI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika eneo fulani huko Kingston, jiji kuu la Jamaika. Eneo hilo lilikuwa na wakaaji wengi sana maskini. Watu wengi hawakuwa wameajiriwa na uhalifu ulikuwa umeenea sana. Magenge ya wahalifu yalifanya watu waishi kwa woga. Nilisikia milio ya risasi karibu kila siku.

Mama yangu aliyefanya kazi kwa bidii, alijitahidi awezavyo kutulea—mimi, ndugu yangu, na dada yangu mdogo. Alihakikisha kwamba tulipata elimu nzuri. Sikufurahia kwenda shuleni, lakini nilipenda sana mashindano ya farasi. Ningekosa kwenda shuleni na badala yake kwenda kwenye uwanja wa mashindano ya farasi. Hata niliendesha farasi.

Muda mfupi baadaye, nilianza kujihusisha sana na kucheza kamari kwenye uwanja wa mashindano ya farasi. Niliishi maisha mapotovu kimaadili na nilifanya ngono na wanawake wengi sana. Nilivuta bangi na kufanya uhalifu ili kugharimia maisha yangu mapotovu. Nilikuwa na bunduki nyingi, lakini ninashukuru kwamba hakuna mtu aliyeuawa katika mashambulizi mengi ya kijambazi niliyohusika.

Mwishowe, nilikamatwa na polisi na kufungwa gerezani kwa sababu ya uhalifu niliofanya. Baada ya kuachiliwa, nilirudia maisha yangu ya uhalifu. Sasa, nilikuwa mbaya kuliko hapo awali. Ingawa kwa nje nilionekana kuwa mtu mzuri, nilikuwa mshupavu, mwenye kukasirika kwa urahisi, na sikuwa na huruma. Sikujali mtu mwingine yeyote isipokuwa mimi binafsi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Katika kipindi hicho kigumu cha maisha, mama yangu alijifunza Biblia na kuwa Shahidi wa Yehova. Niliona jinsi alivyobadilika na kuwa mtu mzuri na hilo likanichochea kutaka kujua jambo lililofanya abadilike. Niliamua kuchunguza jambo hilo, hivyo nikaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.

Niligundua kwamba mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni tofauti na ya dini nyingine na nikatambua kuwa mafundisho yao yote yanategemea Biblia. Ni Mashahidi wa Yehova pekee wanaohubiri nyumba kwa nyumba, kama Wakristo wa karne ya kwanza walivyofanya. (Mathayo 28:19; Matendo 20:20) Nilikuwa na hakika kwamba nimepata dini ya kweli nilipoona upendo usio na unafiki ambao Mashahidi wa Yehova wanaonyeshana.—Yohana 13:35.

Mambo niliyojifunza kutoka katika Biblia yalinisaidia kuona uhitaji wa kufanya mabadiliko fulani makubwa maishani mwangu. Nilijifunza kuwa Yehova Mungu anachukia uasherati na kwamba ili nimpendeze, ningelazimika kuacha mazoea yote yaliyochafua mwili wangu. (2 Wakorintho 7:1; Waebrania 13:4) Niliguswa moyo sana nilipojifunza kuwa Yehova ana hisia na kwamba matendo yangu yangemhuzunisha au kumfurahisha. (Methali 27:11) Hivyo, niliazimia kuacha kuvuta bangi, nikasalimisha bunduki zangu, na kujaribu kuboresha tabia zangu. Kati ya mabadiliko magumu zaidi ambayo nilifanya yalikuwa kuacha maisha mapotovu kingono na kuacha kucheza kamari.

Mwanzoni, sikutaka marafiki zangu wajue kwamba nilikuwa nikijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, niliamua kufanya mabadiliko niliposoma maneno haya ya Yesu katika andiko la Mathayo 10:33: “Yeyote yule anayenikana mimi mbele ya watu, mimi pia nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.” Maneno hayo yalinisukuma niwaeleze rafiki zangu kwamba nilikuwa nikijifunza na Mashahidi. Walishtuka sana. Hawakuamini mtu kama mimi alitaka kuwa Mkristo. Lakini nikawaambia kwamba sikutaka kuhusishwa kamwe na maisha yangu ya zamani.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Mama yangu alifurahi sana alipoona nimeanza kuishi kulingana na kanuni za Biblia. Sasa hana wasiwasi kwamba huenda ninafanya mambo mabaya. Siku hizi tunazungumzia jambo ambalo linatuvuta pamoja—upendo wetu kwa Yehova. Nyakati nyingine ninafikiria jinsi maisha yangu yalivyokuwa na ni ajabu kuona mabadiliko ambayo Mungu amenisaidia kufanya. Sitamani tena maisha mapotovu kingono wala kupenda vitu vya kimwili.

Kama singekubali kujifunza Biblia, huenda leo ningekuwa nimekufa au nimefungwa gerezani. Hata hivyo, sasa nina familia nzuri na yenye furaha. Ninafurahia sana kumtumikia Yehova Mungu pamoja na mke wangu anayenitegemeza sana, na binti yetu mtiifu. Ninamshukuru Yehova sana kwa kunipa fursa ya kuwa sehemu ya undugu wa Kikristo wenye upendo. Ninashukuru pia kuwa mtu fulani alijitahidi kunifundisha kweli za Biblia. Ninathamini pendeleo nililo nalo la kuwasaidia wengine wajifunze mambo ambayo Biblia inafundisha. Ninafurahi hata zaidi kwa kuwa Yehova Mungu alinivuta kwake kwa sababu ya fadhili zake zenye upendo.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

‘Nilijifunza kuwa Yehova ana hisia na kwamba matendo yangu yangemhuzunisha au kumfurahisha’

[Picha katika ukurasa wa 11]

Niliona mabadiliko makubwa katika utu wa mama yangu

[Picha katika ukurasa wa 11]

Nikiwa na mke wangu na binti yetu