Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Huduma mbalimbali katika hekalu la Yehova huko Yerusalemu zililipiwaje?

Huduma mbalimbali katika hekalu zililipiwa kupitia kodi, hasa kupitia takwa la kutoa zaka, au sehemu ya kumi. Pia, kulikuwa na kodi za aina nyingine. Kwa mfano, wakati wa ujenzi wa maskani, au hema la kukutania, Yehova alimwagiza Musa akusanye nusu shekeli ya fedha, kama “mchango kwa Yehova,” kutoka kwa kila Mwisraeli aliyeandikishwa.—Kutoka 30:12-16.

Inaelekea kwamba baada ya muda ilikuwa desturi kwa kila Myahudi kutoa mchango wa kiasi hicho kama kodi ya hekalu kila mwaka. Hiyo ndiyo kodi ambayo Yesu alimwagiza Petro alipe kwa kutumia sarafu aliyotoa kwenye mdomo wa samaki.—Mathayo 17:24-27.

Miaka kadhaa iliyopita, sarafu mbili za fedha zinazofanana na zile zilizotumiwa kulipia kodi ya hekalu zilipatikana jijini Yerusalemu. Sarafu moja ambayo ilitengenezwa huko Tiro mwaka wa 22 W.K., ilipatikana katika mtaro wa kupitishia maji uliochimbwa katika karne ya kwanza. Upande mmoja wa sarafu hiyo una picha ya Melkart, au Baali, mungu mkuu wa Tiro, na upande wa pili una picha ya tai ambaye ametua kwenye sehemu ya mbele ya meli. Sarafu ya pili, ambayo ilipatikana katika mabomoko yaliyotolewa kwenye eneo la hekalu la mlimani, ilikuwa ikitumiwa katika mwaka wa kwanza wa maasi ya Wayahudi dhidi ya Waroma yaliyotukia kati ya mwaka wa 66-67 W.K. Sarafu hiyo imechorwa ua lenye umbo la kikombe na makomamanga matatu yanayochipuka. Pia ina maneno “Nusu Shekeli” na “Yerusalemu Takatifu.” Kuhusiana na sarafu hiyo, Profesa Gabriel Barkay anasema kwamba ina “ishara zinazoonyesha kuwa iliharibiwa na moto, na inaelekea sana kwamba moto huo ni ule ulioharibu Hekalu la Pili mwaka wa 70 WK.”

Majengo ya Nebukadneza, Mfalme wa Babiloni, yalikuwa ya kifahari na yenye kuvutia kadiri gani?

Katika kitabu cha Biblia cha Danieli tunapata maneno haya ya Nebukadneza: “Je, hili si Babiloni Mkubwa, ambalo mimi mwenyewe nimelijenga kwa ajili ya nyumba ya kifalme kwa nguvu za uwezo wangu na kwa ajili ya heshima ya utukufu wa enzi yangu?” (Danieli 4:30) Je, kweli jiji hilo la zamani lilikuwa la kifahari?

Wanahistoria wanasema kwamba Nebukadneza alijenga mahekalu, majumba ya kifalme, kuta za jiji, na bustani nzuri ajabu zenye kuning’inia. Hekalu kuu lililokuwa katikati ya Babiloni lilikuwa na mnara, au ziggurat, ambao huenda ulikuwa na urefu wa zaidi ya mita 70. Hata hivyo, kitabu Babylon—City of Wonders kinasema: “Miradi ya ujenzi [ya Nebukadneza] iliyo maarufu zaidi ni Njia ya Maandamano na Lango la Ishtari.” Kandokando ya Njia ya Maandamano, ambayo ilipita katikati ya Lango la Ishtari, kulikuwa na sanamu za simba waliochongwa kana kwamba wanatembea. Kitabu hicho kinasema hivi kuhusu lango hilo la kifahari zaidi la Babiloni: “Mtu aliyetembelea jiji hilo la kale hangeweza kamwe kusahau lango hilo kwa sababu lilijengwa kwa matofali ya rangi ya bluu yenye kung’aa na kurembeshwa kwa michongo ya mamia ya mafahali na majoka yaliyoonekana kana kwamba yanatembea.”

Mwanzoni mwa karne ya 20, waakiolojia walichimbua maelfu ya vipande vya ile Njia ya Maandamano na vya Lango la Ishtari, kisha wakaunganisha vingi kati ya vipande hivyo katika Jumba la Makumbusho la Pergamon, huko Berlin, Ujerumani.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ukubwa halisi

[Hisani]

Top: Clara Emit, Courtesy of Israel Antiquities Authority; bottom: Zev Radovan

[Picha katika ukurasa wa 12]

Lango la Ishtari lililojengwa upya