Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sitawisheni Mtazamo Mzuri wa Kiroho Mkiwa Mume na Mke

Sitawisheni Mtazamo Mzuri wa Kiroho Mkiwa Mume na Mke

Siri ya Furaha ya Familia

Sitawisheni Mtazamo Mzuri wa Kiroho Mkiwa Mume na Mke

Frederick *: “Mara tu baada ya kufunga ndoa, nilisisitiza kwamba mimi na mke wangu tunapaswa kujifunza Biblia pamoja. Nilijitahidi kuhakikisha kwamba anakuwa makini wakati wa kujifunza. Lakini Leanne hakutulia kamwe. Na nilipouliza maswali, alijibu tu kwa kusema ndiyo au la. Hakutoa majibu yenye habari kamili kwa njia ambayo nilitazamia ajibu.”

Leanne: “Nilikuwa na umri wa miaka 18 nilipoolewa na Frederick. Tulijifunza Biblia pamoja kwa ukawaida, lakini Frederick alitumia kila pindi ya kujifunza kama nafasi ya kutaja makosa yangu yote na mambo ambayo nilihitaji kuboresha nikiwa mke. Niliumia sana na kuvunjika moyo!”

UNAFIKIRI Frederick na Leanne walikuwa na tatizo gani katika uhusiano wao? Walikuwa na nia nzuri. Wote wawili walimpenda Mungu. Na wote waliona uhitaji wa kujifunza Biblia pamoja. Lakini ilionekana kwamba jambo hilo ambalo lingewaunganisha liliharibu uhusiano wao. Ingawa walikuwa wakijifunza pamoja, hawakuwa wakisitawisha mtazamo mzuri wa kiroho wakiwa mume na mke.

Mtazamo mzuri wa kiroho ni nini? Kwa nini mume na mke wanapaswa kujitahidi kuusitawisha? Huenda wakakabili matatizo gani, na wanaweza kuyashindaje?

Mtazamo Mzuri wa Kiroho Ni Nini?

Maneno “hali ya kiroho” yanatumiwa katika Biblia kumaanisha mtazamo au maoni fulani kuelekea maisha. (Yuda 18, 19) Kwa mfano, Paulo mwandikaji wa Biblia anaeleza tofauti kati ya mtazamo wa mtu wa kiroho na mtu wa kimwili. Paulo anasema kwamba watu wenye mtazamo wa kimwili wanajifikiria sana kuliko jinsi wanavyowafikiria wengine. Wanafanya mambo ambayo wao wenyewe wanaona yanafaa, badala ya kujaribu kuishi kulingana na viwango vya Mungu.—1 Wakorintho 2:14; Wagalatia 5:19, 20.

Tofauti na watu hao, watu wenye mtazamo mzuri wa kiroho wanathamini viwango vya Mungu. Wanamwona Yehova Mungu kuwa Rafiki yao na wanajitahidi kuiga sifa zake. (Waefeso 5:1) Hivyo, wanashughulika na wengine kwa upendo, fadhili, na upole. (Kutoka 34:6) Na wanamtii Mungu hata inapokuwa vigumu kwao kufanya hivyo. (Zaburi 15:1, 4) Darren anayeishi huko Kanada, na ambaye amekuwa katika kifungo cha ndoa kwa miaka 35 anasema hivi: “Kulingana na maoni yangu, mtu aliye na mtazamo mzuri wa kiroho anafikiria sikuzote jinsi maneno na matendo yake yatakavyoathiri urafiki wake na Mungu.” Mke wake Jane, anaongezea: “Ninafikiri kwamba mwanamke wa kiroho ni yule anayejitahidi kila siku kusitawisha tunda la roho katika maisha yake.”—Wagalatia 5:22, 23.

Bila shaka, si lazima mtu awe amefunga ndoa ili asitawishe mtazamo huo wa kiroho. Hata Biblia inafundisha kwamba kila mtu ana daraka la kujifunza kumhusu Mungu na kumwiga.—Matendo 17:26, 27.

Kwa Nini Msitawishe Mtazamo Mzuri wa Kiroho Mkiwa Mume na Mke?

Basi, kwa nini mume na mke wanapaswa kujitahidi kusitawisha mtazamo mzuri wa kiroho wakiwa pamoja? Fikiria mfano huu: Wakulima wawili wanamiliki shamba fulani pamoja na wanataka kupanda mboga. Mmoja anaamua kupanda mbegu wakati fulani wa mwaka huku mwenzake akifikiri kwamba mbegu zinapaswa kupandwa baadaye. Mmoja anaamua kutumia aina fulani ya mbolea, lakini mwenzake anapinga kabisa jambo hilo na kusema kwamba mimea hiyo haihitaji mbolea. Mmoja wao anataka kufanya kazi kila siku katika lile shamba, huku mwenzake akifurahia kukaa kitako tu bila kufanya kazi yoyote. Katika hali kama hiyo, huenda shamba likatoa mazao fulani, lakini halitatoa mazao kwa kiwango ambacho lingetoa kama wakulima wote wawili wangekubaliana kuhusu kazi inayohitaji kufanywa, kisha washirikiane kuifanya.

Mume na mke ni kama wakulima hao. Ikiwa mmoja wao tu ndiye anayesitawisha mtazamo mzuri wa kiroho, huenda uhusiano wao ukawa bora. (1 Petro 3:1, 2) Hata hivyo, matokeo yangekuwa bora hata zaidi kama wote wawili wangekubaliana kuishi kulingana na viwango vya Mungu na kujitahidi kutegemezana wanapomtumikia! Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja.” Kwa nini? “Kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.”—Mhubiri 4:9, 10.

Inaelekea kwamba unatamani kusitawisha mtazamo mzuri wa kiroho pamoja na mwenzi wako wa ndoa. Lakini kama vile kazi ya kilimo ilivyo, mtu hawezi kupata matokeo mazuri kwa kutamani tu. Fikirieni matatizo mawili mnayoweza kukabili na jinsi mnavyoweza kuyatatua.

TATIZO LA 1: Hatuna wakati wa kujifunza. “Mume wangu hunichukua kutoka kazini saa moja jioni,” anasema Sue, ambaye aliolewa hivi karibuni. “Tunapofika nyumbani tunalazimika kufanya kazi zote za nyumbani. Ni pambano kati ya akili na mwili; akili zetu zinatuambia kwamba tunahitaji kutumia wakati ili kujifunza kumhusu Mungu tukiwa pamoja, lakini miili yetu inatamani kupumzika.”

Suluhisho: Muwe tayari kubadili ratiba yenu na mshirikiane. Sue anasema: “Mimi na mume wangu tuliamua kuamka mapema ili tusome na kuzungumzia sehemu fulani ya Biblia pamoja kabla ya kwenda kazini. Ananisaidia pia kufanya kazi fulani za nyumbani ili nipate wakati wa kuwa pamoja naye.” Wamefaidika jinsi gani kwa kujitahidi kwa njia hiyo? Ed, mume wa Sue, anasema: “Nimeona kwamba mimi na Sue tunapozungumzia mambo ya kiroho kwa ukawaida, tunatatua vizuri zaidi matatizo tunayokabili na kushughulikia vyema zaidi mahangaiko yetu.”

Zaidi ya kuzungumza pamoja, ni muhimu pia kutumia dakika chache kila siku kusali pamoja. Hilo linaweza kuwasaidiaje? Ryan ambaye amekuwa katika kifungo cha ndoa kwa miaka 16 anasema hivi: “Wakati fulani uliopita, mimi na mke wangu tulikuwa na wakati mgumu sana katika ndoa yetu. Lakini tulitenga wakati wa kusali pamoja kila usiku, na kumweleza Mungu mahangaiko yetu. Ninahisi kwamba kusali pamoja kulitusaidia kutatua matatizo yetu na kupata tena shangwe katika ndoa yetu.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Tengeni angalau dakika chache kila jioni ili kuzungumzia mambo yoyote mazuri mliyofurahia mkiwa mume na mke, mambo ambayo mnaweza kumshukuru Mungu kuyahusu. Zungumzieni pia matatizo mnayokabili, matatizo ambayo hasa mnahitaji msaada wa Mungu ili kuyatatua. Tahadhari: Usitumie pindi hiyo kama nafasi ya kutaja makosa ya mwenzi wako. Badala yake, mnaposali taja tu matatizo ambayo mnapaswa kuyashughulikia pamoja. Kisha, siku inayofuata mjitahidi kutenda kulingana na mambo mliyotaja katika sala yenu.

TATIZO LA 2: Uwezo wetu unatofautiana. “Sijawahi kamwe kufurahia kusoma,” anasema Tony. Natalie, mke wake, anasema: “Ninapenda kusoma na kuzungumzia mambo ambayo nimejifunza. Nyakati nyingine ninafikiri kwamba Tony anaogopeshwa na ujuzi wangu tunapozungumzia habari za Biblia.”

Suluhisho: Muunge mkono mwezi wako, usishindane naye wala kumhukumu. Mpongeze na kumtia moyo kuhusu sifa zake nzuri. “Nyakati nyingine ninahisi nimelemewa kidogo na shauku ya mke wangu anapozungumzia habari za Biblia,” anasema Tony, “na zamani nilisita kuzungumzia mambo ya kiroho pamoja naye. Hata hivyo, Natalie ananiunga mkono sana. Sasa tunazungumzia kwa ukawaida mambo ya kiroho, na nimetambua kwamba sihitaji kuogopa chochote. Ninafurahia kuzungumzia mambo ya kiroho pamoja naye. Hilo limetusaidia kuwa na utulivu zaidi na amani tukiwa mume na mke.”

Wenzi wengi wa ndoa wameona kwamba ndoa zao zinakuwa bora wanapotenga wakati fulani kila juma ili kusoma na kujifunza Biblia pamoja. Hata hivyo, kuna tahadhari: Mnapozungumzia shauri lolote lile taja jinsi wewe binafsi unavyoweza kulifuata, bali si mwenzi wako. (Wagalatia 6:4) Wakati wa kujifunza, msizungumzie mambo yanayoweza kusababisha ugomvi. Tengeni wakati tofauti wa kuzungumzia mambo hayo. Kwa nini?

Fikiria hili: Ikiwa ungekuwa unakula chakula pamoja na familia yako, je, ungetumia pindi hiyo kuosha na kufunga kidonda chenye usaha? Huwezi kufanya hivyo. Utafanya kila mtu akose hamu ya kula. Yesu alisema kujifunza kumhusu Mungu na kufanya mapenzi yake ni kama kula chakula. (Mathayo 4:4; Yohana 4:34) Ikiwa unazungumzia vidonda vya kihisia kila mara mnapojifunza Biblia, unaweza kumfanya mwenzi wako apoteze hamu ya chakula cha kiroho. Bila shaka, kuna uhitaji wa kuzungumzia matatizo. Lakini yazungumzieni wakati ambao mmetenga kufanya hivyo.—Methali 10:19; 15:23.

JARIBU KUFANYA HIVI: Andika sifa mbili au tatu za mwenzi wako ambazo unathamini zaidi. Wakati mtakapozungumzia mambo ya kiroho yanayohusiana na sifa hizo, mwambie mwenzi wako kwamba unathamini jinsi anavyoonyesha sifa hizo.

Mtavuna Mnachopanda

Mkipanda, au kusitawisha mtazamo mzuri wa kiroho mkiwa mume na mke, mwishowe mtavuna ndoa yenye amani na yenye kuridhisha zaidi. Kwa kweli, Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba “lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6:7.

Frederick na Leanne, waliotajwa mwanzoni mwa makala hii, walijifunza ukweli wa kanuni hiyo ya Biblia. Sasa wamekuwa katika kifungo cha ndoa kwa miaka 45 na wamefaidika kwa sababu wameendelea kujitahidi kuwa na mtazamo mzuri wa kiroho. “Nilikuwa nikimlaumu mke wangu kwa sababu alionekana kuwa hafurahii mazungumzo,” anasema Frederick. “Hata hivyo, baada ya muda nilitambua kwamba nilihitaji kujitahidi pia.” Leanne anasema: “Jambo ambalo hasa lilitusaidia katika pindi hizo ngumu ni kwamba sote tulimpenda Yehova Mungu. Kwa miaka mingi, tumekuwa tukijifunza na kusali pamoja kwa ukawaida. Ninapomwona Frederick akijitahidi kuonyesha sifa za Kikristo, inakuwa rahisi zaidi kwangu kumpenda.”

[Maelezo ya Chini]

^ Majina yamebadilishwa.

JIULIZE . . .

▪ Je, ninaweza kukumbuka mara ya mwisho tuliposali pamoja tukiwa mume na mke?

▪ Ninaweza kufanya nini ili nimchochee mwenzi wangu ajihisi huru zaidi kuzungumzia mambo ya kiroho pamoja nami?