Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wazazi Wanapaswa Kuwafundisha Watoto Wao Kuhusu Ngono?

Je, Wazazi Wanapaswa Kuwafundisha Watoto Wao Kuhusu Ngono?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Wazazi Wanapaswa Kuwafundisha Watoto Wao Kuhusu Ngono?

▪ Wazazi wengi wanafanya yote wanayoweza ili kuwalinda watoto wao wasiambukizwe magonjwa hatari. Wazazi wanapaswa kujitahidi vivyo hivyo ili kuwalinda watoto wao wasiathiriwe na mitazamo mibaya kuhusu maadili. Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwafundisha habari zinazofaa kuhusu ngono. (Methali 5:3-23) Ni muhimu kwa wazazi kuwafundisha watoto wao na kuwapa mwongozo huo unaofaa kwa sababu mambo ya ngono yanaonyeshwa waziwazi kwenye televisheni, Intaneti, vitabu, na vichekesho.

Profesa wa elimu na mwandishi, Diane Levin anasema: “Leo, tatizo si kwamba watoto wetu wanajifunza kuhusu ngono. Tatizo ni yale wanayojifunza, umri wao wanapoanza kujifunza, na wale wanaowafundisha. Mambo ambayo watoto wanajifunza kutokana na matangazo ya biashara na desturi zinazopendwa na wengi, yana uvutano na madhara makubwa.”

Wazazi wanahitaji kuwalinda watoto wao kutokana na maoni yasiyofaa na yaliyopotoka kiadili ambayo yanaharibu jamii. (Methali 5:1; Waefeso 6:4) Watoto wanahitaji kujua jinsi miili yao inavyofanya kazi, jinsi wanavyoweza kujitunza kimwili, na jinsi ya kujilinda dhidi ya watu wenye maadili mapotovu. Kabla ya kubalehe—wakati ambapo mwili wa mtoto unaanza kuonyesha ishara za kukomaa kingono—binti anahitaji kuelezwa kuhusu mabadiliko yatakayotokea katika mwili wake na kuelewa ni kwa nini ataanza kupata hedhi na jinsi inavyotokea. Vivyo hivyo, mvulana anahitaji kujua mapema kuhusu kutokwa na shahawa usiku. Watoto wanapokuwa wadogo, wazazi wanaweza kuanza kuwafundisha majina sahihi ya sehemu za mwili. Wazazi wanaowapenda watoto wao huwafundisha mambo matatu muhimu kuhusu sehemu hizo: (1) Sehemu hizo ni za siri na ni za pekee. (2) Hazipaswi kuzungumziwa kwa njia isiyofaa. (3) Hazipaswi kuguswa wala kuonwa na watu wengine. Watoto wanapoendelea kukomaa, wazazi wanahitaji kutambua wakati wa kuwaeleza jinsi mwanamke anavyoshika mimba. *

Wazazi wanapaswa kuanza lini kuwafundisha watoto wao habari hizo? Mapema zaidi kuliko vile wengine wanavyofikiria. Huenda msichana akapata hedhi kwa mara ya kwanza akiwa na umri wa miaka 10 au hata mapema zaidi. Mvulana anaweza kuanza kutokwa na shahawa usiku akiwa na umri wa miaka 11 au 12. Mabadiliko hayo ya mwili yanaweza kumtatiza sana mtoto ikiwa haelewi kinachoendelea. Watoto wanahitaji kuhakikishiwa mapema kwamba mabadiliko hayo ya mwili ni ya kawaida tu. Huo pia ndio wakati wa kuwasaidia waelewe thamani na umuhimu wa kufuata viwango vya Biblia kuhusu maadili—jambo ambalo hawaelezwi katika programu nyingi za kuwafundisha watoto kuhusu ngono.—Methali 6:27-35.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Wazazi wanaweza kupata habari zinazofaa kuhusu mambo hayo katika machapisho yafuatayo ya Mashahidi wa Yehova: Gazeti la Amkeni! la Mei 2006, kwenye makala “Kumweleza Binti Yako Kuhusu Hedhi,” ukurasa wa 10-13; kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, sura ya 6, “Kwa Nini Mwili Wangu Unabadilika?”; na gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2010, “Siri ya Furaha ya Familia—Zungumza na Watoto Wako Kuhusu Ngono,” ukurasa wa 12-14.