Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Usitegemee Uelewaji Wako Mwenyewe”

“Usitegemee Uelewaji Wako Mwenyewe”

“Usitegemee Uelewaji Wako Mwenyewe”

“Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.”—MET. 3:5.

1, 2. (a) Tunaweza kupatwa na hali gani? (b) Tunapaswa kumtegemea nani tunapopatwa na hali zenye kuhuzunisha, tunapofanya uamuzi fulani, au tunapopambana na kishawishi fulani, na kwa nini?

MWAJIRI wa Cynthia * tayari amefunga idara kadhaa katika kampuni yake na kuwafuta kazi wafanyakazi fulani. Cynthia anahisi kwamba yeye pia atafutwa kazi. Atafanya nini akipoteza kazi yake? Atalipaje gharama zake zote? Dada Mkristo anayeitwa Pamela anataka kwenda katika eneo ambalo lina uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme, lakini je, ahamie huko? Kijana mmoja anayeitwa Samuel ana hangaiko tofauti. Alianza kutazama ponografia akiwa na umri mdogo. Sasa akiwa na umri wa miaka 20 hivi, Samuel anakabili kishawishi kikubwa cha kurudia tena zoea hilo. Anaweza kushindaje kishawishi hicho?

2 Unamtegemea nani unapopatwa na hali zenye kuhuzunisha, unapofanya maamuzi muhimu, au unapopambana na vishawishi? Je, unajitegemea mwenyewe tu, au ‘unamtupia Yehova mzigo wako’? (Zab. 55:22) Biblia inasema hivi: “Macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.” (Zab. 34:15) Basi, ni jambo muhimu kama nini kwamba tumtegemee Yehova kwa moyo wetu wote wala tusitegemee uelewaji wetu wenyewe!—Met. 3:5.

3. (a) Kumtegemea Yehova kunatia ndani nini? (b) Kwa nini huenda watu wengine wakawa na mwelekeo wa kutegemea uelewaji wao wenyewe?

3 Kumtegemea Yehova kwa moyo wetu wote kunatia ndani kufanya mambo kupatana na njia zake, yaani, kupatana na mapenzi yake. Njia muhimu ya kufanya hivyo ni kuendelea kusali kwake na kuomba kutoka moyoni atuongoze. Hata hivyo, watu wengi wanafikiri kwamba ni vigumu kumtegemea kabisa Yehova. Kwa mfano, dada Mkristo anayeitwa Lynn anakiri hivi: “Imekuwa vigumu sana kwangu kujifunza kumtegemea Yehova kabisa.” Kwa nini? Lynn anasema: “Sina uhusiano mzuri pamoja na baba yangu, na mama yangu hakunijali kihisia au kimwili. Hivyo, nilijifunza haraka sana kujitegemea mwenyewe.” Malezi ya Lynn yalifanya iwe vigumu kwake kumwamini kabisa mtu yeyote yule. Uwezo wa kiakili na mafanikio maishani yanaweza pia kumfanya mtu ajitegemee. Huenda mzee akaanza kutegemea uzoefu wake mwenyewe ili kushughulikia mambo ya kutaniko bila kuomba kwanza mwongozo wa Mungu katika sala.

4. Tutazungumzia nini katika makala hii?

4 Yehova anatutazamia tujitahidi kwa unyoofu kuishi kulingana na sala zetu na kutenda kulingana na mapenzi yake. Hivyo basi, tunaweza kuonyeshaje usawaziko kati ya kumtupia Yehova mahangaiko yetu na kujitahidi kibinafsi kutatua matatizo magumu? Inapohusu kufanya maamuzi, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu nini? Kwa nini sala ni muhimu tunapojitahidi kupinga vishawishi? Tutazungumzia maswali hayo kwa kufikiria mifano ya Kimaandiko.

Tunapopatwa na Hali Zenye Kuhuzunisha

5, 6. Hezekia alitendaje alipotishwa na mfalme wa Ashuru?

5 Biblia inasema hivi kuhusu Mfalme Hezekia wa Yuda: “Akaendelea kushikamana na Yehova. Hakugeuka kando na kuacha kumfuata, bali aliendelea kuzishika amri zake ambazo Yehova alimwamuru Musa.” Ndiyo, “alimtegemea Yehova Mungu wa Israeli.” (2 Fal. 18:5, 6) Hezekia alifanya nini Mfalme Senakeribu wa Ashuru alipowatuma wawakilishi wake Yerusalemu pamoja na jeshi kubwa, kutia ndani Rabshake? Jeshi lenye nguvu la Ashuru lilikuwa tayari limeyazingira majiji kadhaa yenye ngome ya Yuda, na Senakeribu alikuwa sasa amekazia fikira Yerusalemu. Hezekia alienda katika nyumba ya Yehova na kuanza kusali hivi: “Ee Yehova Mungu wetu, tafadhali, utuokoe kutoka mkononi mwake, ili falme zote za dunia zijue kwamba wewe, Ee Yehova, ndiye Mungu peke yako.”—2 Fal. 19:14-19.

6 Hezekia alitenda kulingana na sala yake. Hata kabla ya kwenda katika hekalu ili kusali, aliwaagiza watu wasijibu dhihaka za Rabshake. Pia, Hezekia alituma wajumbe kwa nabii Isaya ili kutafuta shauri. (2 Fal. 18:36; 19:1, 2) Hezekia alichukua hatua zinazofaa. Katika pindi hiyo, hakujaribu kutafuta suluhisho ambalo lilipingana na mapenzi ya Yehova kwa kutafuta msaada kutoka Misri au kutoka mataifa jirani. Badala ya kutegemea uelewaji wake mwenyewe, Hezekia alimtegemea Yehova. Baada ya malaika wa Yehova kuwaua wanaume wa Senakeribu 185,000, Senakeribu “akaondoka” na kurudi Ninawi.—2 Fal. 19:35, 36.

7. Tunaweza kupata faraja gani kutokana na sala ya Hana na ya Yona?

7 Hana, mke wa Mlawi Elkana, aliyehuzunika sana kwa sababu ya kuwa tasa alimtegemea pia Yehova. (1 Sam. 1:9-11, 18) Nabii Yona aliokolewa kutoka tumbo la samaki mkubwa baada ya kusali hivi: “Katika taabu yangu nilimwita Yehova, naye akanijibu. Katika tumbo la Kaburi nilililia msaada. Ulisikia sauti yangu.” (Yona 2:1, 2, 10) Inafariji kama nini kujua kwamba hata hali yetu iwe mbaya kadiri gani, tunaweza kusali kwa Yehova na ‘kuomba kibali’ chake!—Soma Zaburi 55:1, 16.

8, 9. Hezekia, Hana, na Yona walihangaikia mambo gani katika sala zao, na tunajifunza nini kutokana na sala hizo?

8 Mifano ya Hezekia, Hana, na Yona inatufundisha pia somo muhimu kuhusu mambo tusiyopaswa kusahau tunaposali tukiwa chini ya mikazo. Wote watatu walihisi uchungu moyoni kwa sababu ya hali ngumu walizokuwa wakipitia. Hata hivyo, sala zao zinaonyesha kwamba hawakujihangaikia tu na kutafuta kitulizo kwa sababu ya matatizo yao. Mambo muhimu zaidi kwao yalikuwa kuliheshimu jina la Mungu, kumwabudu kwa njia inayokubalika, na kufanya mapenzi yake. Hezekia alihuzunika kwa sababu watu hawakuliheshimu jina la Yehova. Hana aliahidi kumtoa mwana ambaye alimpenda sana ili amtumikie Mungu kwenye maskani huko Shilo. Naye Yona alisema hivi: “Nilichoweka nadhiri, nitakitimiza.”—Yona 2:9.

9 Tunaposali ili tupate msaada kwa sababu ya hali fulani ngumu tunayopitia, ni jambo la hekima kuchunguza nia yetu. Je, tunasali tu ili tupate kitulizo kwa sababu ya matatizo yetu, au tunamkumbuka Yehova na kusudi lake katika sala zetu? Tunapoteseka, ni rahisi kuhangaikia sana hali yetu hivi kwamba mambo ya kiroho yanakuwa si muhimu kwetu. Tunaposali kwa Mungu ili atusaidie, tunapaswa kukaza akili yetu juu ya Yehova, kutakaswa kwa jina lake, na kutetewa kwa enzi yake kuu. Kufanya hivyo kunaweza kutusaidia kuendelea kuwa na mtazamo mzuri hata ikiwa hatupati suluhisho ambalo tulitazamia. Huenda Mungu akajibu sala zetu kwa kutupatia nguvu tunazohitaji ili kuvumilia hali yetu.—Soma Isaya 40:29; Wafilipi 4:13.

Tunapofanya Maamuzi

10, 11. Yehoshafati alifanya nini alipohitaji kufanya uamuzi mgumu?

10 Wewe unafanyaje maamuzi mazito maishani? Je, labda unaamua kwanza mambo ambayo unataka na kisha unasali ili Yehova abariki uamuzi ambao tayari umefanya? Fikiria yale ambayo Yehoshafati, mfalme wa Yuda alifanya wakati majeshi ya Wamoabu na Waamoni yalipoungana ili kupigana naye. Taifa la Yuda halingeweza kufaulu kupigana nao. Yehoshafati alifanya nini?

11 Biblia inasema hivi: “Yehoshafati akaogopa, akauelekeza uso wake kumtafuta Yehova.” Alitangaza kwamba watu wote wa Yuda wafunge na akawakusanya pamoja ili “kuuliza habari kutoka kwa Yehova.” Kisha akasimama katikati ya kutaniko la Yuda na Yerusalemu na kusali. Kwa sehemu, alisihi hivi: “Ee Mungu wetu, je, hutafanya hukumu juu yao? Kwa maana hakuna nguvu ndani yetu mbele ya umati huu mkubwa unaokuja juu yetu; nasi wenyewe hatujui tunalopaswa kufanya, lakini macho yetu yanakuelekea wewe.” Mungu wa kweli alisikia sala ya Yehoshafati na aliwaokoa kimuujiza. (2 Nya. 20:3-12, 17) Tunapofanya maamuzi, hasa yale ambayo yanaweza kuathiri hali yetu ya kiroho, je, hatupaswi kumtegemea Yehova badala ya kutegemea uelewaji wetu wenyewe?

12, 13. Mfalme Daudi alituwekea mfano gani kuhusiana na kufanya maamuzi?

12 Tunapaswa kufanya nini tunapokabiliana na hali ambazo huenda zinaonekana kuwa rahisi zaidi kusuluhisha—labda kwa sababu ya uzoefu wetu tunafikiria suluhisho haraka? Simulizi moja linalomhusu Mfalme Daudi linatusaidia kuelewa jambo hilo. Waamaleki walipovamia jiji la Siklagi, waliwachukua wake na watoto wa Daudi, pamoja na wake na watoto wa wanaume waliomuunga mkono. Daudi alimuuliza Yehova hivi: “Je, nikifuatilie kikundi hiki cha waporaji?” Yehova akajibu: “Nenda, uwafuatilie, kwa maana bila shaka utawafikia, nawe bila shaka utaleta ukombozi.” Daudi alitii, naye “akakomboa vyote ambavyo Waamaleki walikuwa wamechukua.”—1 Sam. 30:7-9, 18-20.

13 Wakati fulani baada ya Waamaleki kuvamia, Wafilisti walikuja kupigana na Israeli. Kwa mara nyingine tena Daudi alimuuliza Yehova naye akapewa jibu la wazi. Mungu alisema: “Panda uende, kwa maana bila shaka nitawatia Wafilisti mikononi mwako.” (2 Sam. 5:18, 19) Muda mfupi baadaye, Wafilisti walikuja tena kupigana na Daudi. Angefanya nini mara hii? Huenda Daudi angefikiri hivi: ‘Nimewahi kukabili hali kama hii mara mbili. Acha niende kupigana na maadui wa Mungu, kama nilivyofanya hapo awali.’ Au je, Daudi angetafuta mwongozo wa Yehova? Daudi hakutegemea uzoefu wake. Kwa mara nyingine tena alisali kwa Yehova. Alifurahi kama nini kwamba alifanya hivyo! Pindi hiyo maagizo aliyopewa yalikuwa tofauti. (2 Sam. 5:22, 23) Tunapokabili hali au tatizo ambalo tumewahi kupata, ni lazima tuwe waangalifu ili tusitegemee tu uzoefu wetu.—Soma Yeremia 10:23.

14. Ni somo gani tunaloweza kujifunza kutokana na jinsi Yoshua na wanaume wazee wa Israeli walivyoshughulika na Wagibeoni?

14 Kwa kuwa sisi sote si wakamilifu, kutia ndani wazee wenye uzoefu, tusisahau kamwe kuomba mwongozo wa Yehova tunapofanya maamuzi. Fikiria jinsi Yoshua, mrithi wa Musa, na wanaume wazee wa Israeli walivyofanya walipofikiwa na Wagibeoni werevu waliovalia kwa njia iliyofanya wasiweze kutambuliwa na kujifanya kwamba walitoka nchi ya mbali. Bila kumuuliza Yehova na kuomba mwongozo wake, Yoshua na wengine waliamua haraka kufanya amani na Wagibeoni, na kufanya agano pamoja nao. Hata ingawa Yehova alikubali mapatano hayo, alihakikisha kwamba kisa hicho cha kukosa kutafuta mwongozo wake kimeandikwa katika Biblia kwa faida yetu.—Yos. 9:3-6, 14, 15.

Tunapopambana ili Kupinga Vishawishi

15. Eleza kwa nini sala ni muhimu ili kushinda kishawishi.

15 Kwa kuwa “sheria ya dhambi” imo ndani ya viungo vyetu, tunahitaji kupambana vikali na mielekeo yetu ya dhambi. (Rom. 7:21-25) Tunaweza kushinda pambano hilo. Jinsi gani? Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba sala ni muhimu sana ili kushinda kishawishi. (Soma Luka 22:40.) Hata tamaa au mawazo mabaya yakiendelea baada ya kusali kwa Mungu, tunahitaji ‘kuendelea kumwomba Mungu’ ili atupatie hekima ya kuvumilia jaribu hilo. Tuna hakika kwamba yeye “huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu.” (Yak. 1:5) Yakobo pia aliandika hivi: “Je, kuna yeyote mgonjwa [kiroho] kati yenu? Na awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, nao wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamponya huyo asiyejisikia vizuri.”—Yak. 5:14, 15.

16, 17. Tunapotafuta msaada ili kushinda kishawishi, ni wakati gani unaofaa wa kusali?

16 Sala ni muhimu sana ili kushinda kishawishi, lakini ni lazima tutambue uhitaji wa kusali kwa wakati unaofaa. Fikiria kisa cha kijana mmoja mwanamume anayetajwa katika Methali 7:6-23. Wakati wa gizagiza, anatembea kwenye barabara ambayo anajua vizuri kwamba mwanamke fulani mwenye maadili mapotovu anaishi. Akipotoshwa na mwanamke huyo kwa ushawishi wake na kutongozwa kwa ulaini wa midomo yake, kijana huyo anamfuata mwanamke huyo kama ng’ombe-dume anayepelekwa machinjioni. Kwa nini kijana huyo alienda kwenye barabara hiyo? Kwa kuwa alikuwa “amepungukiwa moyoni,” yaani, hakuwa na uzoefu, inaelekea alikuwa akipambana na tamaa mbaya. (Met. 7:7) Sala ingemsaidia kijana huyo wakati gani hasa? Bila shaka, kusali wakati mwanamke huyo alipokuwa akizungumza naye kungemsaidia kushinda kishawishi hicho. Lakini wakati mzuri zaidi wa yeye kusali ungekuwa wakati alipopata kwanza wazo la kupita au kutembea kwenye barabara hiyo.

17 Leo, huenda mtu anajitahidi sana asitazame ponografia. Hata hivyo, vipi akiingia kwenye vituo vya Intaneti ambavyo anajua kwamba vina picha au video chafu? Je, kisa chake hakitakuwa kama tu cha mwanamume huyo kijana anayezungumziwa katika Methali sura ya 7? Ni hatari kama nini kuanza kutembea kwenye barabara hiyo! Ili kushinda kishawishi cha kutazama ponografia, mtu anahitaji kutafuta msaada wa Yehova kupitia sala kabla ya kuanza kutembea kwenye barabara ya Intaneti.

18, 19. (a) Kwa nini inaweza kuwa vigumu kushinda kishawishi, lakini unaweza jinsi gani kushinda pambano hilo? (b) Umeazimia kufanya nini?

18 Si jambo rahisi kushinda kishawishi au mazoea mabaya. Mtume Paulo aliandika hivi: “Mwili katika tamaa yake unapingana na roho, na roho inapingana na mwili.” Kwa hiyo, ‘mambo yale ambayo tunapenda kufanya hatuyafanyi.’ (Gal. 5:17) Ili kushinda pambano hilo, tunahitaji kusali kwa bidii tunapoanza tu kufikiria mawazo mabaya au vishawishi na kisha kutenda kulingana na sala zetu. “Hakuna jaribu ambalo limewapata ninyi ila lile lililo kawaida kwa watu,” na kwa msaada wa Yehova, tunaweza kubaki waaminifu kwake.—1 Kor. 10:13.

19 Iwe tunapambana na hali ngumu, tunafanya uamuzi mzito, au tunajitahidi kushinda kishawishi, Yehova ametupatia zawadi nzuri ajabu, yaani, uandalizi wenye thamani wa sala. Kupitia zawadi hiyo, tunaonyesha kwamba tunamtegemea. Tunapaswa pia kuendelea kumwomba Mungu atupatie roho yake takatifu, ambayo inatuongoza na kutuimarisha. (Luka 11:9-13) Na kwa vyovyote vile, acheni tumtegemee Yehova na tusitegemee uelewaji wetu wenyewe.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Majina yamebadilishwa.

Je, Unakumbuka?

• Ulijifunza nini kutokana na Hezekia, Hana, na Yona kuhusu kumtegemea Yehova?

• Mfano wa Daudi na wa Yoshua unakaziaje uhitaji wa kuwa waangalifu tunapofanya maamuzi?

• Ni wakati gani hasa tunapopaswa kusali ili kushinda vishawishi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ili kushinda kishawishi, ni wakati gani unaofaa zaidi wa kusali?