Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Usitegemee Uelewaji Wako Mwenyewe”

“Usitegemee Uelewaji Wako Mwenyewe”

“Usitegemee Uelewaji Wako Mwenyewe”

‘Mutegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.’—MET. 3:5.

1, 2. (a) Tunaweza kupatwa na magumu gani katika maisha? (b) Tunapaswa kumutegemea nani, tunapokutana na hali ngumu, tunapochukua maamuzi ya maana, ao tunaposhindana na vishawishi, na kwa nini tumutegemee?

 BWANA wa kazi wa Sintia * amefukuza wafanyakazi fulani. Sasa Sintia anaogopa kwamba labda yeye pia atafukuzwa karibuni. Anajiuliza atafanya namna gani ikiwa anapoteza kazi yake. Atapata feza wapi za kulipia mambo mbalimbali? Dada mwengine anayeitwa Pamela anataka kuhamia katika eneo ambako kuna uhitaji wa wahubiri. Je, ni lazima kabisa ahamie huko? Ndugu anayeitwa Samweli, yeye ana tatizo tofauti. Alipokuwa bado kijana sana, alikuwa na tabia ya kutazama ponografia, yaani picha na habari za ngono. Sasa Samweli ana miaka zaidi ya 20 na anatamani sana kurudilia tabia hiyo. Namna gani anaweza kushindana na kishawishi hicho?

2 Unapokutana na hali ngumu, unapochukua maamuzi ya maana, ao unaposhindana na vishawishi, unamutegemea nani? Je, unajitegemea, ao ‘unamutupia Yehova muzigo wako’? (Zab. 55:22) Biblia inasema: ‘Macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba musaada.’ (Zab. 34:15) Basi ni jambo la maana kabisa tumutegemee Yehova kwa moyo wetu wote kuliko kutegemea uelewaji wetu wenyewe!—Met. 3:5.

3. (a) Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tunamutegemea Yehova? (b) Ni mambo gani yanayoweza kufanya wengine wategemee uelewaji wao?

3 Tunaonyesha kwamba tunamutegemea Yehova kwa moyo wote tunapofanya mambo anayotaka sisi tufanye, yaani kulingana na mapenzi yake. Ili tufanye mapenzi yake, ni lazima tumukaribie katika sala kwa moyo wote na kwa ukawaida ili kumwomba uongozi. Lakini, watu wengi wanafikiri kwamba ni vigumu kumutegemea Yehova kwa moyo wote. Tuchukue mufano wa dada Lynn. Yeye anasema hivi: “Imekuwa vigumu sana kwangu kumutegemea Yehova kwa moyo wote.” Kwa nini? Anasema, “Sina urafiki wowote na baba yangu, na mama yangu hakunionyesha upendo wala kuhangaikia mahitaji yangu ya kimwili. Kwa hiyo, nilianza kujitegemea mimi mwenyewe.” Kwa sababu ya maelezi hayo, ilikuwa vigumu kwa Lynn kumutegemea mutu yeyote kwa moyo wote. Watu wengine wanajitegemea kwa sababu ya uwezo wao ao kwa sababu ya mambo waliyotimiza katika maisha. Kwa mufano, muzee fulani wa kutaniko ambaye amekuwa muzee kwa siku nyingi anaweza kuanza kujitegemea mwenyewe. Namna gani? Anaweza kuanza kushugulikia mambo ya kutaniko bila kuomba Yehova uongozi katika sala.

4. Tutajifunza kuhusu nini katika habari hii?

4 Yehova anataka sisi tujikaze kuishi kulingana na yale tunayomwambia katika sala na kutenda kulingana na mapenzi yake. Basi, namna gani tunaweza kujua wakati wa kumutupia Yehova mahangaiko yetu na kujikaza sisi wenyewe kuyatatua? Tunapochukua maamuzi, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu nini? Kwa nini ni jambo la maana kusali tunapojikaza kushinda vishawishi? Mifano ya watu fulani wanaozungumuziwa katika Biblia itatusaidia kujibu maulizo hayo.

Tunapopambana na Magumu

5, 6. Hezekia alifanya nini wakati mufalme wa Asuria alipotisha kushambulia Yerusalemu?

5 Kuhusu Hezekia Mufalme wa Yuda, Biblia inasema hivi: ‘Alimutegemea Yehova. Hakugeuka kando na kuacha kumufuata, bali aliendelea kuzishika amri zake ambazo Yehova alimwamuru Musa.’ Bila shaka, ‘alimutegemea Yehova Mungu wa Israeli.’ (2 Fal. 18:5, 6) Hezekia alifanya nini wakati Senakeribu Mufalme wa Asuria alimutuma Rabshake na wajumbe wengine Yerusalemu pamoja na jeshi kubwa? Wakati huo jeshi la Asuria lilikuwa limekwisha kukamata majiji fulani ya Yuda yenye kulindwa sana. Sasa Senakeribu alikusudia kuishambulia Yerusalemu. Basi mufalme Hezekia alienda kwenye nyumba ya Yehova na kuanza kusali hivi: ‘Ee Yehova Mungu wetu, tafazali, utuokoe kutoka mukononi mwake, ili falme zote za dunia zijue kwamba wewe, Ee Yehova, ndiye Mungu peke yako.’—2 Fal. 19:14-19.

6 Mufalme Hezekia aliomba Yehova amusaidie, lakini alitenda pia kulingana na sala yake. Kwa mufano, hata mbele apande kwenye hekalu ili kusali, aliwaambia watu wasimujibu Rabshake aliyekuwa akiwatukana. Pia, alituma watu fulani kwa nabii Isaya, ili kuomba mashauri. (2 Fal. 18:36; 19:1, 2) Hezekia alichukua hatua ambazo alistahili kuchukua. Wakati huo, yeye hakwenda kutafuta musaada huko Misri ao kutoka kwa mataifa jirani, kwa sababu alijua kwamba kufanya hivyo hakupatane na mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo, Hezekia alimutegemea Yehova kuliko kutegemea uelewaji wake mwenyewe. Malaika wa Yehova aliwaua wanaume wa Senakeribu 185,000, naye Senakeribu “akaondoka” na kurudi Ninawi.—2 Fal. 19:35, 36.

7. Sala ya Hana na pia sala ya Yona zinaweza kutufariji namna gani?

7 Mufano mwingine ni ule wa Hana, muke wa Mulawi Elkana. Mwanamuke huyo alimutegemea Yehova alipokuwa katika hali ngumu kwa kuwa hakuwa akizaa. (1 Sam. 1:9-11, 18) Pia, kuna mufano wa nabii Yona aliyemezwa na samaki mukuu na kisha akaokolewa. Alipokuwa katika tumbo la samaki alisali hivi: ‘Katika taabu yangu nilimwita Yehova, naye akanijibu. Katika tumbo la Kaburi nilililia musaada. Ulisikia sauti yangu.’ (Yona 2:1, 2, 10) Ni jambo lenye kufariji kabisa kujua kwamba hata tukiwa wenye kupambana na magumu ya namna gani, tunaweza kumulilia Yehova ‘kwa kufanya ombi la kupata kibali’!—Soma Zaburi 55:1, 16.

8, 9. Hezekia, Hana, na Yona walihangaikia nini katika sala zao, na tunajifunza nini kutokana na mifano hiyo?

8 Mifano ya Hezekia, Hana, na Yona inatufundisha pia tuelewe mambo ya maana tunayopaswa kuomba tunapopambana na magumu. Wote watatu waliteseka walipokuwa katika magumu. Hata hivyo, sala zao zinaonyesha kwamba hawakuhangaikia tu hali yao wala kumalizika tu kwa magumu yao. Mambo ya maana ambayo walihangaikia ilikuwa heshima ya jina la Mungu, ibada yake, na kufanya mapenzi yake. Hezekia aliumizwa moyoni kwa kuwa jina la Yehova lilivunjiwa heshima. Hana alimupenda mwana wake sana, lakini aliahidi kumutoa ili atumike kwenye maskani huko Shilo. Na Yona alisema: ‘Nilichoweka naziri, nitakitimiza.’—Yona 2:9.

9 Tunaposali ili Yehova atusaidie katika magumu yanayotusumbua, ni jambo la hekima kufikiri juu ya sababu zinazotuchochea kusali. Je, tunahangaikia tu kuona magumu yetu yakimalizika? Mateso tunayopata yanaweza kwa urahisi kutufanya tuhangaikie sana hali yetu hivi kwamba tunaanza kuregea na kupuuza mambo ya kiroho. Tunaposali ili Yehova atusaidie, acheni tumufikirie yeye, kutakaswa kwa jina lake, na kutetewa kwa utawala wake. Kufanya hivyo kutatusaidia tusivunjike moyo hata ikiwa hatupate jibu tulilotazamia. Mungu anaweza kujibu sala yetu kwa kutupatia tu nguvu tunayohitaji ili kuvumilia magumu yetu.—Soma Isaya 40:29; Wafilipi 4:13.

Tunapochukua Maamuzi

10, 11. Yehoshafati alifanya nini alipopambana na hali iliyomwomba achukue uamuzi muzito?

10 Namna gani unachukua maamuzi mazito katika maisha yako? Je, unaamua kwanza yale unapenda yafanyike na kisha unamwomba Yehova abariki maamuzi yako? Fikiria jambo ambalo Yehoshafati, mufalme wa Yuda alifanya wakati majeshi ya Wamoabu na Waamoni yalikuja kumupiganisha. Jeshi la Yuda halikuwa na uwezo. Yehoshafati alifanya nini?

11 Biblia inasema: ‘Yehoshafati akaogopa, akauelekeza uso wake kumutafuta Yehova.’ Basi aliamuru wakaaji wa Yuda wasile chakula kwa muda fulani na pia alikusanya watu pamoja ili “kuuliza habari kutoka kwa Yehova.” Kisha akasimama katika kutaniko la Yuda na la Yerusalemu na kuanza kusali. Alimulilia Yehova hivi: ‘Ee Mungu wetu, je, hutafanya hukumu juu yao? Kwa maana hakuna nguvu ndani yetu mbele ya umati huu mukubwa unaokuja juu yetu; nasi wenyewe hatujui tunalopaswa kufanya, lakini macho yetu yanakuelekea wewe.’ Mungu wa kweli alisikia sala ya Yehoshafati na akawaokoa kwa njia ya muujiza. (2 Nya. 20:3-12, 17) Tunapochukua maamuzi, hasa yale yanayogusa uhusiano wetu pamoja na Mungu, tunapaswa kumutegemea Yehova kuliko kutegemea uelewaji wetu wenyewe.

12, 13. Mufalme Daudi alituachia mufano gani kuhusiana na kufanya maamuzi?

12 Tunaweza kufanya nini tunapokutana na magumu fulani ambayo inaonekana kwamba sisi wenyewe tunaweza kutatua kwa wepesi?—labda tunafikiri kwamba tunaweza kutatua hali fulani kwa vyepesi kwa sababu tumekwisha kupambana na hali kama hiyo hapo zamani? Mufano wa Mufalme Daudi utatusaidia kujua nini tunaweza kufanya katika hali kama hizo. Wakati Waamaleki walishambulia jiji la Ziklagi, walichukua wake wa Daudi, watoto wake, na wa watu wake. Daudi akamuuliza Yehova: “Je, nikifuatilie kikundi hiki cha waporaji?” Yehova akamujibu: “Nenda, uwafuatilie, kwa maana bila shaka utawafikia, nawe bila shaka utaleta ukombozi.” Daudi akatii, na “akakomboa vyote ambavyo Waamaleki walikuwa wamechukua.”—1 Sam. 30:7-9, 18-20.

13 Muda fulani kisha kushambuliwa na Waamaleki, Wafilisti wakashambulia Israeli. Daudi akamuuliza tena Yehova naye akamujibu waziwazi na kusema: “Panda uende, kwa maana bila shaka nitawatia Wafilisti mikononi mwako.” (2 Sam. 5:18, 19) Muda kidogo baadaye, Wafilisti wakapanda ili kumushambulia tena Daudi. Mara hii huenda Daudi angefikiri hivi: ‘Ninajua kile nitafanya kwa kuwa nimekwisha kupambana na hali kama hii mara mbili. Acha nishambulie maadui hao wa Mungu, kama nilivyofanya hapo mbele.’ Je, Daudi alifanya hivyo ao alitafuta uongozi wa Yehova? Daudi hakutegemea uzoefu wake. Alimwendea tena Yehova katika sala. Maagizo ambayo Yehova alimupatia wakati huu yalikuwa tofauti. Bila shaka, Daudi alifurahi sana na kwa kuwa alifuata maagizo hayo mapya aliwashinda maadui. (2 Sam. 5:22, 23) Tunapopambana na hali ao tatizo fulani ambalo tulitatua hapo zamani, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusijitegemee ao kutegemea uzoefu wetu.—Soma Yeremia 10:23.

14. Tunaweza kujifunza nini kulingana na jinsi Yoshua na wazee wa Israeli walivyoshugulika na Wagibeoni?

14 Kwa kuwa hatukamilike, hata wazee wenye uzoefu, tusikose kumuomba Yehova uongozi tunapochukua maamuzi. Fikiria jinsi Yoshua aliyechukua nafasi ya Musa na wanaume wazee Waisraeli walikosa kumuomba Yehova uongozi wakati Wagibeoni wenye busara walidanganya kwa kujifanya kama watu waliotoka mbali. Bila kumuuliza Yehova, Yoshua na wengine walikubali kufanya amani na Wagibeoni hao, na wakafanya agano pamoja nao. Hata ikiwa Yehova mwishowe alikubali mapatano hayo, yeye aliandikisha habari hiyo katika Biblia ili tujue kwamba Yoshua na wazee wa Israeli walikosa kufuata uongozi wake.—Yos. 9:3-6, 14, 15.

Tunaposhindana na Vishawishi

15. Eleza kwa nini ni jambo la maana kusali ili kushinda vishawishi.

15 Kwa kuwa tuna ‘sheria ya zambi’ katika miili yetu, ni lazima tupiganishe mielekeo yenye zambi. (Rom. 7:21-25) Tunaweza kushinda vita hiyo. Namna gani? Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba kusali ni jambo la maana sana ili kushinda vishawishi. (Soma Luka 22:40.) Hata ikiwa kisha kusali bado tamaa ao mawazo mabaya yanaendelea, ni vizuri ‘tuendelee kumwomba Mungu’ hekima ili kushindana na majaribu hayo. Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu ‘anawapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu.’ (Yak. 1:5) Yakobo pia aliandika: ‘Je, kuna yeyote mugonjwa kati yenu? Na awaite wazee wa kutaniko, nao wasali juu yake, wakimupakaa mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamuponya huyo asiyejisikia vizuri.’—Yak. 5:14, 15.

16, 17. Tunatafuta musaada ili kushinda kishawishi, ni wakati gani hasa inafaa kusali?

16 Bila sala hatuwezi kushinda vishawishi. Lakini ni lazima tukumbuke kusali wakati unaofaa. Fikiria mufano wa kijana anayezungumuziwa kwenye Methali 7:6-23. Wakati wa gizagiza, anapitia barabara, mahali panapojulikana vema kwamba mwanamuke kahaba anaishi hapo. Kahaba huyo akamudanganya kwa ushawishi wake mwingi na akamutongoza kwa maneno matamu ya mudomo wake, akamufuata, kama ngombe-dume anayeenda machinjoni. Kwa nini kijana huyo alienda huko? Kwa kuwa alikuwa “amepungukiwa moyoni,” yaani, hakuwa na uzoefu, labda alikuwa akipigana na tamaa mbaya. (Met. 7:7) Ili kupata musaada angepaswa kusali wakati gani hasa? Bila shaka, angepaswa kusali ili kushinda majaribu wakati wowote yalipotokea. Lakini wakati ambao ungefaa zaidi kwake kusali, ni wakati wazo la kupitia barabara hiyo lilipomufikia kwa mara ya kwanza.

17 Leo, mutu anaweza kujikaza ili kuepuka kutazama ponografia. Lakini, itakuwa namna gani ikiwa anafungua Internet mahali ambako anajua vizuri kwamba kuna picha ao video za kuamusha tamaa za ngono? Bila shaka, hali yake itakuwa kama ya yule kijana anayezungumuziwa katika Methali sura ya 7, sivyo? Hiyo ni barabara yenye hatari kabisa! Ili kushinda kishawishi cha kutazama ponografia, ni lazima kutafuta musaada wa Yehova katika sala mbele ya kufungua Internet mahali panapoonyesha mambo ya ponografia.

18, 19. (a) Kwa nini si vyepesi kushinda vishawishi, hata hivyo tunaweza kuvishinda namna gani? (b) Azimio lako ni nini?

18 Si rahisi kushinda kishawishi ao kuacha tabia mbaya. Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Mwili katika tamaa yake unapingana na roho, na roho inapingana na mwili. Kwa hiyo, mambo yale ambayo tunapenda kufanya hatuyafanyi.’ (Gal. 5:17) Kwa hiyo, lazima tusali kwa bidii wakati mawazo mabaya ao majaribu yanakuja katika akili na hivyo kutenda kulingana na sala zetu. Biblia inasema hivi: “Hakuna jaribu ambalo limewapata ninyi ila lile lililo kawaida kwa watu.” lakini kwa musaada wa Yehova, tunaweza kubaki waaminifu kwake.—1 Kor. 10:13.

19 Iwe tunapambana na magumu, ao tunataka kuchukua maamuzi mazito, ao tunashindana na vishawishi, Yehova ametutolea zawadi nzuri ya sala. Tunapotumia zawadi hiyo, tunaonyesha kwamba tunamutegemea yeye. Tunapaswa pia kuendelea kumwomba Mungu roho takatifu, ili ituongoze na kututia nguvu. (Luka 11:9-13) Basi, na tujikaze kila siku kumutegemea Yehova kuliko kutegemea uelewevu wetu wenyewe.

[Maelezo ya chini]

^ Majina yamebadilishwa.

Je, Unakumbuka?

• Ulijifunza nini kutokana na mufano wa Hezekia, Hana, na Yona kuhusu kumutegemea Yehova?

• Namna gani mifano ya Daudi na Yoshua inakazia uhitaji wa kuwa waangalifu tunapochukua maamuzi?

• Kuhusiana na vishawishi, ni wakati gani inafaa kabisa kusali?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ni wakati gani inafaa kusali ili kushinda vishawishi?