Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu Ni Yehova”

“Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu Ni Yehova”

Mkaribie Mungu

“Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu Ni Yehova”

IKIWA ungechagua neno moja linaloeleza kumhusu Yehova Mungu, yaani, jinsi alivyo au utu wake, ungechagua neno gani? Katika karne ya nane K.W.K., nabii Isaya aliona maono na kusikia viumbe wa roho wakimtukuza Yehova kwa neno ambalo linaeleza sehemu kuu ya utu wake—utakatifu. Mambo ambayo Isaya aliona na kusikia yanapaswa kutufanya tumheshimu, tumwogope, na kumkaribia Yehova. Tunapozungumzia maneno yaliyo katika Isaya 6:1-3, jiwazie ukiwa mahali hapo.

Isaya anaona nini? “Nilimwona Yehova, akiwa ameketi juu ya kiti cha ufalme kilicho juu na kilichoinuliwa,” anasema Isaya. (Mstari wa 1) Kwa kweli, Isaya hamwoni Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Macho ya wanadamu hayawezi kuwaona viumbe wa roho. Biblia inasema hivi waziwazi: “Hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” (Yohana 1:18) Isaya anaona maono. * Lakini, maono hayo yanaonekana waziwazi—ni halisi sana hivi kwamba Isaya anajawa na woga na kutenda kana kwamba anamwona Yehova mwenyewe.

Kisha Isaya anaona maono ambayo huenda hakuna mwanadamu mwingine ambaye amewahi kuyaona. Anaandika: “Maserafi walikuwa wamesimama juu yake [Yehova]. Kila mmoja alikuwa na mabawa sita. Aliufunika uso wake kwa mawili, na kwa mawili aliifunika miguu yake, na kwa mawili aliruka huku na huku.” (Mstari wa 2) Maserafi ni viumbe wa roho wenye cheo cha juu. Isaya ndiye mwandikaji pekee wa Biblia anayewataja. Maserafi huwa tayari sikuzote kufanya lolote ambalo Mungu anawataka wafanye. Wanajifunika uso na miguu yao kuonyesha kwamba wanamheshimu Yehova sana na pia kuonyesha kwamba ni pendeleo kubwa kutumika mbele zake.

Isaya anajawa na woga na heshima si kwa sababu ya mambo anayoona tu, bali pia kwa sababu ya mambo anayosikia. Maserafi wanaunganisha sauti zao na kuimba pamoja. Isaya anaandika: “Huyu akamwita yule na kusema: ‘Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova wa majeshi.’” (Mstari wa 3) Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “mtakatifu” linamaanisha usafi na utakato. Neno hilo pia lina maana ya “kuwa huru na kutengwa kabisa na dhambi.” Katika wimbo huo ambao inaelekea kikundi kimoja cha maserafi kinaimba huku kingine kikiitikia, maserafi hao wanataja neno “mtakatifu” mara tatu, wakikazia kwamba Yehova ni mtakatifu kwa njia isiyo na kifani. (Ufunuo 4:8) Kwa hiyo, utakatifu ni sifa ya kipekee ya utu wa Mungu. Kwa kweli, Yehova ni safi kabisa na hana doa lolote la uovu.

Kujua kwamba Yehova ni mtakatifu kunapaswa kutuchochea kumkaribia hata zaidi. Kwa nini? Tofauti na watawala wa kibinadamu ambao wanaweza kuwa wafisadi na kutumia mamlaka vibaya, Yehova hana dhambi hata kidogo. Utakatifu wake unatuhakikishia kwamba sikuzote atakuwa Baba anayefaa, Mtawala mwadilifu, na Mwamuzi asiye na ubaguzi. Tuna kila sababu za kuwa na uhakika kwamba Mungu ambaye ni mtakatifu hatatuvunja moyo kamwe.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Desemba:

Isaya 1-23

[Maelezo ya Chini]

^ Buku la Insight on the Scriptures linaeleza: “Mtu alipopata maono kutoka kwa Mungu akiwa macho, inaonekana mambo aliyoona yalibaki katika akili yake. Baadaye, angekumbuka maono hayo na kuyaeleza au hata kuyaandika kwa maneno yake mwenyewe.”—Limechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 26]

Kujua kwamba Yehova ni mtakatifu kunapaswa kutuchochea kumkaribia hata zaidi