Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Nilitaka Kuwa Kama Binti ya Yeftha

Nilitaka Kuwa Kama Binti ya Yeftha

Nilitaka Kuwa Kama Binti ya Yeftha

Limesimuliwa na Joanna Soans

Nilipokuwa kijana, nilitamani sana kuwa kama binti ya Yeftha. Acheni nieleze mambo niliyokuwa nikiwazia na jinsi nilivyokuja kuwa kama yeye kwa kadiri fulani.

MNAMO mwaka wa 1956, nilihudhuria kwa mara ya kwanza kusanyiko la Mashahidi wa Yehova jijini Bombay (ambalo sasa ni Mumbai), nchini India. Kusanyiko hilo lilibadili maisha yangu. Niliguswa moyo sana na hotuba niliyosikia kumhusu binti ya Yeftha.

Kama vile ambavyo huenda umesoma katika Biblia, binti ya Yeftha alipokuwa kijana, aliamua kwamba hataolewa. Jambo hilo lilimwezesha baba yake atimize ahadi aliyokuwa ametoa. Kwa hiyo, alitumikia akiwa mseja katika nyumba ya Yehova, au hema la kukutania, kwa maisha yake yote.—Waamuzi 11:28-40.

Nilitamani sana kuwa kama yeye! Lakini nilikabili tatizo kubwa sana—kubaki mseja kulikuwa kinyume cha utamaduni wa Kihindi wakati huo.

Maelezo Kuhusu Familia Yetu

Nilikuwa mtoto wa tano kati ya watoto sita wa Benjamin na Marcelina Soans na tuliishi Udipi, jiji lililo magharibi mwa pwani ya India. Tunazungumza lugha ya Tulu ambayo inatumiwa na watu milioni mbili hivi. Hata hivyo, kama vile tu wakazi wengine wa Udipi, shuleni tulifundishwa kwa lugha ya Kannada.

Kwa muda mrefu, watu wanaoishi katika eneo hili wameamini kwamba ni muhimu sana kuolewa na kupata watoto. Nilipokuwa mtoto sikumbuki nikijifunza maneno kama vile “useja,” “upweke,” au “tamaa ya kurudi nyumbani” katika lugha ya Tulu. Ni kana kwamba watu hawakupatwa na hali hizo. Kwa mfano, katika familia yetu tuliishi pamoja na babu, nyanya, wajomba, shangazi, na binamu wengi sana.

Katika utamaduni wetu, watoto walionwa kuwa sehemu ya ukoo wa mama. Ukoo ulifuatwa kupitia upande wa mama na mabinti waligawiwa sehemu kubwa ya urithi. Katika jamii fulani za Tulu, msichana aliendelea kuishi na mama yake hata baada ya kuolewa, na mume wake angeenda kuishi naye.

Kwa kuwa washiriki wa familia yetu walikuwa wafuasi wa dini fulani ya Kikristo, tulifanya mambo fulani kwa njia tofauti. Kila jioni, babu yangu aliongoza familia katika ibada, akisali na kusoma Biblia kwa sauti kubwa katika lugha ya Tulu. Kila wakati alipofungua Biblia yake iliyoraruka-raruka ili atusomee, ni kana kwamba alikuwa akifungua sanduku lenye vitu vya thamani. Tulisisimuka kama nini! Andiko la Zaburi 23:1 lilinivutia sana: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.” Nilijiuliza, ‘Yehova ni nani, na kwa nini anaitwa mchungaji?’

Macho Yangu Yalifunguka

Kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi yaliyotokea baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, tulihamia Bombay, jiji lililokuwa umbali wa zaidi ya kilomita 900. Mwaka wa 1945, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea baba yangu na kumpa kijitabu kilichokuwa na ujumbe kutoka katika Biblia. Baba alikisoma kwa shauku na kukubali ujumbe uliokuwa ndani yake, kisha akaanza kuwaeleza watu wengine waliozungumza lugha ya Kannada ujumbe huo. Mwanzoni mwa miaka ya 1950, kikundi cha kujifunza kilikuwa kimeanzishwa na kuwa kutaniko la kwanza la lugha ya Kannada jijini Bombay.

Baba na Mama walitufundisha sisi watoto kuwa wanafunzi na walimu wazuri wa Biblia. Kila siku walitafuta nafasi ya kusali na kujifunza pamoja nasi. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; 2 Timotheo 3:14-16) Siku moja nilipokuwa nikisoma Biblia, ni kana kwamba macho yangu yalifunguka. Nilijifunza kwamba Yehova anafananishwa na mchungaji kwa sababu anawaongoza, anawalisha, na kuwalinda waabudu wake.—Zaburi 23:1-6; 83:18.

Yehova Ameniongoza Maishani

Nilibatizwa muda mfupi tu baada ya kusanyiko ninalokumbuka sana lililofanywa Bombay mwaka wa 1956. Miezi sita baadaye nilifuata mfano wa ndugu yangu mkubwa Prabhakar na kuwa mweneza-injili wa wakati wote. Ingawa nilitamani sana kuwaeleza watu wengine kweli za Biblia, niliingiwa na woga sana nilipojaribu kuwahubiria. Nilishikwa na kigugumizi na sauti yangu ilitetemeka sana. ‘Ninaweza kufanya kazi hii tu kwa msaada wa Yehova!’ Nilijiambia maneno hayo huku nikilia.

Yehova alinisaidia kupitia wamishonari Homer na Ruth McKay kutoka nchi ya Kanada, waliokuwa wamehudhuria shule ya wamishonari ya Mashahidi wa Yehova huko New York, Marekani, mwaka wa 1947. Walinisaidia sana katika kazi nilipoanza kazi ya kuhubiri. Mara kwa mara, tulifanya mazoezi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba pamoja na Ruth. Alijua jinsi ya kunituliza nilipokuwa na wasiwasi. Alishika mikono yangu iliyokuwa ikitetemeka na kuniambia, “Usiwe na wasiwasi. Acha tujaribu nyumba inayofuata.” Sauti yake yenye uhakikisho ilinitia moyo sana.

Siku moja, nilipata habari kwamba Elizabeth Chakranarayan, dada mwenye umri mkubwa na mwalimu stadi wa Biblia, angekuwa mwenzi wangu katika kazi ya kuhubiri. Mwanzoni nilijiuliza: ‘Je, nitafaulu kuishi na huyo dada? Ana umri mkubwa zaidi kuliko wangu!’ Lakini nikatambua kwamba ndiye mtu hasa niliyehitaji katika kazi ya kuhubiri.

“Kwa Kweli Hatuko Peke Yetu”

Mgawo wetu wa kwanza ulikuwa katika jiji la kihistoria la Aurangabad, lililo karibu kilomita 400 upande wa kusini wa Bombay. Mara moja tukatambua kwamba sisi wawili tu ndio tuliokuwa Mashahidi katika jiji hilo lililo na watu milioni moja hivi. Zaidi ya hilo, nilihitaji kujifunza lugha ya Marathi iliyozungumzwa sana na watu wa jiji hilo.

Nyakati fulani nilijihisi mpweke na kulia kama mtoto asiye na mama. Lakini Elizabeth alinitia moyo kwa sauti nzuri kama ya mama. Aliniambia: “Ijapokuwa nyakati fulani tunaweza kuhisi ni kana kwamba tuko peke yetu, kwa kweli hatuko peke yetu. Ingawa uko mbali kutoka kwa rafiki zako na familia yako, kila wakati Yehova yuko pamoja nawe. Ukiwa rafiki yake, hutajihisi mpweke tena.” Bado ninathamini shauri lake.

Tulipokuwa na kiasi kidogo cha pesa za nauli, tulitembea kilomita 20 hivi kila siku katika eneo lenye vumbi na matope, joto na hata baridi. Katika majira ya joto, kiwango cha joto kingefikia digrii 40 Selsiasi. Katika majira ya mvua, sehemu nyingi za eneo hilo zilikuwa na matope kwa miezi kadhaa. Hata hivyo, mara nyingi tuliona kwamba ilikuwa rahisi zaidi kukabiliana na hali ya hewa kuliko kukabiliana na utamaduni wa watu wa eneo hilo.

Wanawake hawakuzungumza na wanaume hadharani labda iwe watu wao wa ukoo, na kwa kawaida wanawake hawakuwafundisha wanaume. Kwa hiyo, mara nyingi tulidhihakiwa na kutendewa vibaya. Miezi ya kwanza sita, mimi na Elizabeth tu ndio tuliohudhuria mikutano ya Biblia kila juma. Baada ya muda watu wengine waliopendezwa wakajiunga nasi. Kisha kikundi kidogo kilianzishwa. Hata wengine walijiunga nasi katika kazi ya kuhubiri.

“Endelea Kuboresha Ustadi Wako”

Baada ya miaka miwili na nusu hivi tukapata mgawo mpya, jijini Bombay. Elizabeth aliendelea na kazi ya kuhubiri, nami nikaombwa nimsaidie baba yangu ambaye alikuwa akitafsiri peke yake machapisho ya Biblia katika lugha ya Kannada. Alifurahia sana msaada wangu kwa sababu alikuwa na majukumu mengi kutanikoni.

Mwaka wa 1966, wazazi wangu waliamua kurudi Udipi, eneo tulilokuwa tukiishi zamani. Kabla ya kuondoka Bombay, Baba aliniambia: “Endelea kuboresha ustadi wako, binti yangu. Tafsiri kwa maneno rahisi na yanayoeleweka. Epuka kujiamini sana, na uendelee kuwa mnyenyekevu. Mtegemee Yehova.” Hayo ndiyo mashauri ya mwisho aliyonipa kwa sababu alikufa muda mfupi baada ya kurudi Udipi. Nimejitahidi kufuata mashauri yake mpaka leo ninapoendelea kufanya kazi ya kutafsiri.

“Hutaki Kuolewa na Kuishi Maisha ya Kawaida?”

Katika utamaduni wa Kihindi, wazazi huwapangia binti na wana wao kuolewa, watoto hao wakiwa bado na umri mdogo sana, na kuwatia moyo wapate watoto. Hivyo, mara nyingi niliulizwa “Hutaki kuolewa na kuishi maisha ya kawaida? Ni nani atakayekutunza utakapozeeka? Je, hutakuwa mpweke?”

Nyakati nyingine maneno hayo yalinilemea sana kihisia. Ingawa sikuonyesha hisia zangu hadharani, nilimweleza Yehova yote yaliyokuwa moyoni mwangu. Nilitiwa moyo kujua kwamba hakuona nimepungukiwa kwa sababu nilikuwa mseja. Ili niendelee kumtumikia Yehova bila kukengeushwa, nilimfikiria binti ya Yeftha na pia Yesu—wote walibaki waseja na walijishughulisha sana na kufanya mapenzi ya Mungu.—Yohana 4:34.

Zawadi Kutoka kwa Yehova

Mimi na Elizabeth, tuliendelea kuwa marafiki kwa miaka 50 hivi. Alikufa mwaka wa 2005, akiwa na umri wa miaka 98. Ingawa hakuweza kusoma Biblia katika miaka yake ya uzeeni kwa sababu ya matatizo ya macho, Elizabeth alitumia muda wake mwingi kila siku akisali kwa Mungu. Nyakati nyingine nilifikiri alikuwa akizungumzia andiko fulani pamoja na mtu aliyekuwa amemtembelea chumbani, kumbe alikuwa akizungumza na Yehova. Yehova alikuwa halisi kwake, na aliishi kana kwamba alikuwa akimwona. Nimejifunza kwamba hiyo ndiyo siri ya kufaulu kuendelea kumtumikia Mungu, kama vile binti ya Yeftha alivyofanya. Ninamshukuru sana Yehova kwa kunipa dada mkomavu na mwenye umri mkubwa ili anizoeze na kunitia moyo nilipokuwa kijana na nilipokabili hali ngumu.—Mhubiri 4:9, 10.

Nimepata baraka nyingi kwa kumtumikia Yehova kama vile tu binti ya Yeftha alivyofanya! Kuendelea kuwa mseja na kufuata mashauri ya Biblia kumeniwezesha kuishi maisha yenye kusudi, yenye kuridhisha, huku nikiendelea “kumhudumia Bwana daima bila kukengeushwa fikira.”—1 Wakorintho 7:35.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Baba yangu akitoa hotuba ya watu wote huko Bombay miaka ya 1950

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nikiwa na Elizabeth muda mfupi kabla ya kifo chake

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikitangaza kuhusu hotuba ya Biblia jijini Bombay mwaka wa 1960

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na wafanyakazi wenzangu katika ofisi ya kutafsiri