Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Abrahamu—Mwanamume Mwenye Upendo

Abrahamu—Mwanamume Mwenye Upendo

Abrahamu​—Mwanamume Mwenye Upendo

Abrahamu amelemewa na huzuni. Sara, mke wake mpendwa, amekufa. Mwanamume huyu mzee anafikiria mambo mengi sana anapomzika. Huzuni inapoongezeka moyoni, Abrahamu analia. (Mwanzo 23:1, 2) Machozi hayo si ishara ya udhaifu ambao anapaswa kuuonea aibu, bali yanathibitisha mojawapo ya sifa nzuri zaidi za Abrahamu—upendo wake.

UPENDO NI NINI? Upendo ni hisia nyororo au hisia za ndani sana kumwelekea mtu fulani. Mtu mwenye upendo huonyesha kwa matendo hisia zake kuelekea wale anaowapenda, hata kama atahitaji kujidhabihu ili kufanya hivyo.

ABRAHAMU ALIONYESHAJE UPENDO? Abrahamu alionyesha kwamba aliipenda familia yake. Hapana shaka kwamba Abrahamu alikuwa mtu mwenye shughuli nyingi. Hata hivyo, hakupuuza mahitaji ya kihisia na ya kiroho ya familia yake. Hata Yehova mwenyewe alitambua kwamba, Abrahamu aliongoza familia yake katika ibada akiwa kichwa cha familia. (Mwanzo 18:19) Isitoshe, Yehova alitaja waziwazi upendo wa Abrahamu. Akizungumza na Abrahamu, Yehova alimtaja Isaka kuwa ‘mwana ambaye Abrahamu anampenda sana.’—Mwanzo 22:2.

Pia, tunaweza kutambua upendo wa Abrahamu kupitia jinsi alivyotenda wakati Sara, mke wake mpendwa, alipokufa. Abrahamu alimlilia mke wake. Ingawa alikuwa mwanamume hodari na mwenye nguvu, hakuogopa kuonyesha huzuni yake. Abrahamu alikuwa mwanamume mwenye nguvu lakini mpole.

Abrahamu alidhihirisha kwamba alimpenda Mungu wake. Alionyesha upendo huo katika maisha yake yote. Jinsi gani? Huenda jambo hilo likatukumbusha maneno ya Biblia kwenye 1 Yohana 5:3: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.” Kupatana na maneno hayo, Abrahamu aliweka mfano mzuri sana wa kumpenda Mungu.

Yehova alipomwagiza Abrahamu afanye jambo fulani, nyakati zote alitii bila kusita. (Mwanzo 12:4; 17:22, 23; 21:12-14; 22:1-3) Abrahamu hakuzingatia kama amri aliyopewa ilikuwa rahisi au ngumu kutii, wala kama alijua kwa nini Yehova alimwambia aifuate. Mambo hayo hayakuwa muhimu kwake. Ikiwa Mungu wake alitaka afanye jambo fulani, alikuwa tayari kulifanya. Abrahamu aliiona kila amri kuwa nafasi ya kuonyesha upendo wake kwa Yehova.

TUNAJIFUNZA NINI? Tunaweza kumwiga Abrahamu kwa kuwaonyesha wengine upendo mwororo, hasa watu wa familia yetu. Hatungependa kamwe mahangaiko ya maisha yatulemee kiasi cha kutopata wakati wa kuwa pamoja na wapendwa wetu.

Pia, tunapaswa kusitawisha upendo kwa Yehova katika mioyo yetu. Upendo huo unaweza kuwa kichocheo chenye nguvu katika maisha yetu. Kwa mfano, unaweza kutuchochea kubadili mitazamo, usemi, na mwenendo wetu ili kumpendeza Mungu.—1 Petro 1:14-16.

Kwa kweli, si rahisi sikuzote kutii amri za Yehova. Lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yule aliyemsaidia Abrahamu—Yule aliyemwita “rafiki yangu”—atatutegemeza pia. (Isaya 41:8) Biblia, Neno lake, inaahidi hivi: “Atawafanya ninyi kuwa imara, atawafanya ninyi kuwa wenye nguvu.” (1 Petro 5:10) Ni ahadi yenye kuchangamsha kama nini kutoka kwa Rafiki huyo mwaminifu wa Abrahamu!

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Je, Ni Udhaifu kwa Mwanamume Kulia?

Wengi wangejibu ndiyo. Labda wangeshangaa kujua kwamba Abrahamu ni mmoja kati ya wanaume kadhaa waaminifu na hodari ambao Biblia inasema walilia nyakati za taabu. Wengine wanatia ndani Yosefu, Daudi, mtume Petro, wazee wa kutaniko la Efeso, na hata Yesu. (Mwanzo 50:1; 2 Samweli 18:33; Luka 22:61, 62; Yohana 11:35; Matendo 20:36-38) Bila shaka, Biblia haifundishi kwamba ni udhaifu kwa mwanamume kulia.