Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Biblia Inatabiri Kuhusu Wakati Ujao?

Je, Biblia Inatabiri Kuhusu Wakati Ujao?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Je, Biblia Inatabiri Kuhusu Wakati Ujao?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Je, unabii wa Biblia unataja mambo kihususa?

Mungu Mweza Yote pekee ndiye anayeweza kujua mambo hususa kuhusu wakati ujao. (Amosi 3:7) Kwa mfano, tangu zamani alitabiri kutokea kwa mtu fulani anayeitwa Masihi, au Kristo. Masihi angetoka katika uzao wa mwanamume mwaminifu, Abrahamu. Angekuwa mtawala ambaye angewawezesha wanadamu waaminifu kufurahia uhai mkamilifu bila magonjwa. (Mwanzo 22:18; Isaya 53:4, 5) Masihi Aliyeahidiwa angetokea Bethlehemu.—Soma Mika 5:2.

Yesu alithibitika kuwa Masihi. Zaidi ya miaka 700 mapema, Biblia ilikuwa imetabiri kwamba Masihi angezaliwa na bikira na angedharauliwa. Angetoa uhai wake kwa ajili ya dhambi za wengi, na angezikwa pamoja na matajiri. (Isaya 7:14; 53:3, 9, 12) Pia, zaidi ya miaka 500 mapema, Biblia ilikuwa imetabiri kwamba angeingia Yerusalemu akiwa juu ya mwana-punda na kwamba angesalitiwa kwa vipande 30 vya fedha. Mambo hayo yote yalitimia.—Soma Zekaria 9:9; 11:12.

2. Je, Mungu anatabiri tarehe hususa?

Zaidi ya miaka 500 mapema, Biblia ilikuwa imetabiri mwaka hususa ambao Yesu angetokea akiwa Masihi. Muda uliopita hadi wakati alipotokea ulipimwa kwa majuma ya mfano yaliyoitwa “majuma ya miaka.” Kwa hiyo, kila “juma” lilikuwa na urefu wa miaka 7. Hivyo basi, kungekuwa na majuma 7 ambayo yangejumlishwa na majuma mengine 62 na hivyo kuwa majuma 69 ya miaka. Hiyo ni sawa na miaka 483. Miaka hiyo ilianza kuhesabiwa wakati gani? Kulingana na Biblia, ilianza kuhesabiwa wakati mtumishi wa Mungu Nehemia alipofika Yerusalemu na kuanza tena kujenga jiji hilo. Historia ya Waajemi inaonyesha alianza kazi hiyo mwaka wa 455 K.W.K. (Nehemia 2:1-5) Yesu alibatizwa na kuwa Masihi miaka 483 baadaye, katika mwaka wa 29 W.K., mwaka hususa ambao alitarajiwa kutokea.—Soma Danieli 9:25.

3. Je, unabii wa Biblia unatimia leo?

Yesu alitabiri kuhusu matukio muhimu sana ambayo yangetokea wakati wetu. Unabii wake unataja habari njema za Ufalme wa Mungu, ambao utawaletea kitulizo wanadamu wote wanaompenda Mungu. Ufalme huo utaondoa kabisa mfumo huu mwovu uliopo.—Soma Mathayo 24:14, 21, 22.

Unabii mbalimbali wa Biblia unaeleza kwa undani kipidi hiki cha umalizio wa mfumo huu. Biblia inafunua kwamba tofauti na yale ambayo huenda yangetazamiwa kwa sababu ya maendeleo ya mwanadamu, watu wangekuwa wakiiharibu dunia. Matatizo yanayosababishwa na vita, ukosefu wa chakula, matetemeko ya ardhi, na magonjwa yenye kuenea haraka yangeongezeka. (Luka 21:11; Ufunuo 11:18) Watu wangeishi maisha mapotovu kiadili. Katika nyakati hizo ngumu, wafuasi wa Yesu wangehubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kwa mataifa yote.—Soma Mathayo 24:3, 7, 8; 2 Timotheo 3:1-5.

4. Wakati ujao wa mwanadamu utakuwaje?

Mungu Mweza Yote amewaandalia wanadamu waaminifu mambo mazuri. Yesu Kristo, yule Masihi, pamoja na wachaguliwa wake, wataitawala dunia kutoka mbinguni. Wanafanyiza serikali hiyo ya Kifalme ambayo itatawala kwa miaka elfu moja. Wafu watafufuliwa na kupata nafasi ya kuhukumiwa kama wanastahili kupata uzima wa milele au la. Zaidi ya hayo, Ufalme huo utaponya kila mtu atakayeishi wakati huo. Magonjwa yatakwisha na kifo hakitakuwapo tena.—Soma Ufunuo 5:10; 20:6, 12; 21:4, 5.

Ili upate habari zaidi ona ukurasa wa 23-25 na 197-201 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kinachoonyeshwa hapa.