Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Mimi, Yehova Mungu Wako, Ninaushika Mkono Wako wa Kuume”

“Mimi, Yehova Mungu Wako, Ninaushika Mkono Wako wa Kuume”

Mkaribie Mungu

“Mimi, Yehova Mungu Wako, Ninaushika Mkono Wako wa Kuume”

“SHIKA mkono wangu,” baba anamwambia mwana wake wanapotaka kuvuka barabara. Mkono wake mdogo ukiwa umeshikwa na babake, mtoto huyo anahisi akiwa salama bila kuogopa. Je, umewahi kutamani mtu akushike mkono na kukuongoza katika nyakati zenye hatari maishani? Ikiwa ndivyo, huenda ukafarijiwa na maneno yaliyoandikwa na Isaya.—Soma Isaya 41:10, 13.

Isaya alikuwa akizungumza na Waisraeli. Ingawa Mungu aliliona taifa la Israeli kuwa ‘mali yake ya pekee,’ taifa hilo lilikuwa limezungukwa na maadui. (Kutoka 19:5) Je, Waisraeli walihitaji kuogopa? Yehova alimtumia Isaya kutoa ujumbe wenye kufariji. Tunapochunguza maneno hayo, acheni tukumbuke kwamba yanawafaa pia waabudu wa Mungu leo.—Waroma 15:4.

“Usiogope,” Yehova anahimiza. (Mstari wa 10) Hayo si maneno yasiyo na msingi. Yehova anaeleza ni kwa nini watu wake hawapaswi kuogopa: “Kwa maana mimi nipo pamoja nawe.” Yeye si kama watu wanaotoa msaada wakiwa mbali, wakiahidi kufanya hivyo tu wakati kunapokuwa na uhitaji. Anataka watu wake wajue kwamba yuko pamoja nao—kana kwamba yuko kando yao—akiwa tayari kuwasaidia wakati wowote. Bila shaka, hilo ni jambo lenye kutia moyo sana.

Yehova anaendelea kuwafariji waabudu wake kwa kusema: “Usitazame huku na huku.” (Mstari wa 10) Neno la Kiebrania lililotumiwa hapa linaweza kurejelea watu “wanaotazama huku na huku ili kuona kama kuna chochote kinachoweza kuwadhuru.” Yehova anaeleza ni kwa nini watu wake hawapasi kutazama huku na huku kwa woga: “Kwa maana mimi ni Mungu wako.” Kwa kweli, hayo ni maneno yenye kufariji sana. Yehova ndiye “Aliye Juu Zaidi,” “Mweza-Yote.” (Zaburi 91:1) Mungu wao, Yehova, ana nguvu zote, kwa hiyo hawapaswi kuogopa.

Hivyo basi, waabudu wa Yehova wanaweza kutazamia nini kutoka kwake? Anaahidi hivi: “Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” (Mstari wa 10) Pia, anasema: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume.” (Mstari wa 13) Unafikiria nini unaposikia maneno hayo? Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza hivi: “Mistari hiyo miwili inapochunguzwa pamoja, inatokeza akilini picha iliyo wazi kabisa ya mtoto na mzazi wake.” Pia kinasema: “[Baba] hasimami tu ili kumlinda mtoto wake, bali amemshika na haruhusu chochote kiwatenganishe.” Hebu wazia—Yehova hataruhusu chochote kimtenganishe na watu wake, hata wakati ambapo wanakabili hali inayoonekana kuwa ngumu kabisa maishani mwao.—Waebrania 13:5, 6.

Leo, waabudu wa Yehova wanaweza kufarijiwa sana na maneno hayo ya Isaya. Katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” huenda wakati mwingine tukahisi tumelemewa na mahangaiko ya maisha. (2 Timotheo 3:1) Lakini hatupaswi kukabili hali hizo peke yetu. Yehova yuko tayari kunyoosha mkono wake na kutushika. Kama watoto wanaomwamini baba yao, sisi pia tunaweza kushika mkono wa Yehova wenye nguvu, tukiwa na uhakika kwamba atatuongoza katika njia inayofaa na kutusaidia tunapokuwa na uhitaji.—Zaburi 63:7, 8.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Januari:

Isaya 24-42