Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

MSICHANA aliyepatwa na hali ngumu alipokuwa mtoto, alipataje kusudi la kweli maishani? Ni nini kilichomfanya mwasi wa kisiasa awe mhubiri wa habari njema mwenye kufanya amani? Soma masimulizi yafuatayo ili upate majibu.

“Nilitamani Sana Kuonyeshwa Upendo na Fadhili.”—INNA LEZHNINA

MWAKA WA KUZALIWA: 1981

NCHI: URUSI

HISTORIA: ALIPITIA HALI NGUMU ALIPOKUWA MTOTO

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa nikiwa kiziwi na pia wazazi wangu walikuwa viziwi. Nilifurahia miaka sita ya kwanza ya maisha yangu. Kisha wazazi wangu wakatalikiana. Ingawa bado nilikuwa mtoto, nilielewa maana ya kutalikiana na jambo hilo liliniumiza sana. Baada ya talaka hiyo, baba na kaka yangu waliendelea kuishi Troitsk, lakini mimi na mama yangu tukahamia Chelyabinsk. Baada ya muda, Mama aliolewa tena. Baba yangu wa kambo alikuwa mlevi, na mara kwa mara alitupiga—mimi na mama yangu.

Mnamo 1993, kaka yangu mpendwa alikufa maji. Aksidenti hiyo ilitushtua sana sote katika familia. Mama yangu alianza kunywa pombe kupita kiasi, naye akajiunga na baba yangu wa kambo kunitesa. Nilianza kutafuta maisha bora. Nilitamani sana kuonyeshwa upendo na fadhili. Nilianza kwenda katika makanisa tofauti-tofauti, nikitafuta faraja, lakini sikuipata.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipokuwa na umri wa miaka 13 mwanafunzi mwenzangu aliyekuwa Shahidi wa Yehova alinisimulia hadithi fulani za Biblia. Nilifurahia kujifunza kuhusu watu kama Noa na Ayubu, ambao walimtumikia Mungu ingawa walipatwa na hali ngumu. Muda si muda, nikaanza kujifunza Biblia na Mashahidi na kuhudhuria mikutano yao.

Kujifunza Biblia kulinisaidia kujua mafundisho mengi ya kweli na yenye kuvutia. Niliguswa moyo sana kujua kwamba Mungu ana jina. (Zaburi 83:18) Nilivutiwa kuona jinsi Biblia inavyotabiri kwa usahihi hali ambazo zingekuwapo katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Pia, nilisisimuka sana kujifunza kuhusu tumaini la ufufuo. Hebu wazia—nitamwona kaka yangu tena!—Yohana 5:28, 29.

Hata hivyo, si kila mtu aliyefurahia mambo hayo mapya niliyokuwa nikijifunza. Mama yangu na baba yangu wa kambo waliwachukia sana Mashahidi wa Yehova. Walijaribu kunilazimisha niache kujifunza Biblia. Lakini nilifurahia mambo niliyokuwa nikijifunza, hivyo nikaazimia kusonga mbele.

Haikuwa rahisi kukabiliana na upinzani kutoka kwa familia yangu. Pigo lingine lilitukia wakati ndugu yangu mdogo, ambaye nilikuwa nimeenda naye kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova, alipokufa maji pia. Hata hivyo, Mashahidi walinitia moyo sikuzote. Walinionyesha fadhili na upendo ambao nilikuwa nimetamani katika maisha yangu yote. Nilijua kwamba lazima hii iwe ndiyo dini ya kweli. Mnamo 1996, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Miaka sita iliyopita nilifunga ndoa na mwanamume mwenye sifa nzuri aitwaye Dmitry. Sote wawili tunatumika kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliyo St. Petersburg. Baada ya muda, mtazamo usiofaa wa wazazi wangu kuelekea imani yangu ulibadilika.

Ninashukuru kama nini kwa kumjua Yehova! Na nimepata kusudi la kweli maishani kwa kumtumikia.

“Nilikuwa na Maswali Mengi Yaliyonisumbua.”—RAUDEL RODRÍGUEZ RODRÍGUEZ

MWAKA WA KUZALIWA: 1959

NCHI: KUBA

HISTORIA: MWASI WA KISIASA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa Havana, nchini Kuba, na nililelewa katika mtaa wa watu maskini ambapo vita vya mitaani vilikuwa jambo la kawaida. Nilipoendelea kukua, nilianza kupenda mchezo wa judo na michezo mingine ya kupigana kwa kutumia mikono.

Nilikuwa mwanafunzi mwerevu, na wazazi wangu walinitia moyo nijiunge na chuo kikuu. Nilipokuwa huko, nilianza kuhisi kwamba mfumo wa kisiasa wa nchi yetu ulihitaji kubadilishwa. Hivyo, nikaamua kuwa mwasi. Mimi na mwanafunzi mwenzangu tulimvamia ofisa wa polisi, tukitaka kumnyang’anya bunduki yake. Ofisa huyo alipata majeraha mabaya kichwani. Tulitiwa gerezani na kuhukumiwa kifo kwa kupigwa risasi na kikundi cha askari. Nilikuwa na umri wa miaka 20 tu, na kifo kilikuwa kikinikodolea macho!

Nilipokuwa peke yangu kwenye chumba changu gerezani, nilifanya mazoezi ya jinsi nitakavyojiendesha mbele ya askari hao. Sikutaka kuonekana mwoga. Wakati huohuo, nilisumbuliwa na maswali mengi. Nilijiuliza: ‘Kwa nini kuna ukosefu mwingi wa haki duniani? Je, uhai ndio uu huu tu?’

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mwishowe, hukumu yetu ya kifo ilibadilishwa na kuwa kifungo cha miaka 30 gerezani. Wakati huo ndipo nilipokutana na Mashahidi wa Yehova ambao walikuwa wamefungwa kwa sababu ya imani yao. Nilivutiwa sana na jinsi Mashahidi hao walivyokuwa wajasiri lakini wenye kufanya amani. Ingawa walikuwa wamefungwa kimakosa, hawakuwa na hasira wala uchungu.

Mashahidi hao walinifundisha kwamba Mungu ana kusudi kwa ajili ya wanadamu. Walinionyesha katika Biblia kwamba Mungu atabadili dunia iwe paradiso na hakutakuwa na uhalifu wala ukosefu wa haki. Walinifundisha kwamba dunia itajaa watu wazuri, ambao wataishi milele chini ya hali kamilifu.—Zaburi 37:29.

Nilifurahia mambo niliyojifunza kutoka kwa Mashahidi, lakini nilifikiri ingekuwa vigumu kwangu kujiendesha kama wao. Nilifikiri ingekuwa vigumu kwangu kutounga mkono upande wowote wa kisiasa au kugeuza shavu lile lingine ninapopigwa. Hivyo nikaamua kujisomea Biblia. Nilipomaliza, nilitambua kwamba Mashahidi wa Yehova tu ndio wanaojiendesha kama Wakristo wa mapema.

Kwa kujifunza Biblia, nilitambua nilihitaji kufanya mabadiliko makubwa maishani mwangu. Kwa mfano, nilihitaji kubadili usemi wangu, kwa sababu nilipenda kutumia maneno machafu. Pia nilihitaji kuacha kuvuta sigara na kutounga mkono upande wowote wa kisiasa. Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo, lakini kwa msaada wa Yehova nilifaulu.

Jambo lililokuwa gumu zaidi ni kudhibiti hasira yangu. Bado ninasali niweze kujidhibiti ninapokuwa na hasira. Nimesaidiwa sana na maandiko kama vile Methali 16:32 linalosema: “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu, naye anayezuia roho yake ni bora kuliko mtu anayeteka jiji.”

Mnamo 1991, nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilibatizwa ndani ya tangi la maji nikiwa gerezani. Mwaka uliofuata, mimi na wafungwa wengine tuliachiliwa na kupelekwa nchini Hispania kwa sababu tulikuwa na watu wa ukoo huko. Nilipofika Hispania, mara moja nilihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Mashahidi hao walinikaribisha kana kwamba nilikuwa nimeshirikiana nao kwa miaka mingi, na wakanisaidia kuanza maisha upya nchini Hispania.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Sasa ninafurahi kumtumikia Mungu pamoja na mke wangu na binti zetu wawili. Nina pendeleo la kutumia muda wangu mwingi kuwasaidia watu wengine wajifunze Biblia. Nyakati fulani ninafikiria wakati nilipokuwa karibu kufa, na ninathamini sana jinsi ambavyo nimenufaika kufikia sasa. Mbali na kuwa hai leo, nina tumaini pia. Ninatazamia kwa hamu Paradiso iliyoahidiwa—wakati ambapo haki itakuwapo na “kifo hakitakuwapo tena.”—Ufunuo 21:3, 4.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

“Niliguswa moyo sana kujua kwamba Mungu ana jina”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mimi na mume wangu tunafurahia kujifunza machapisho ya Biblia ya lugha ya ishara pamoja na viziwi