Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Kwa Nini Mungu Alimwambia Abrahamu Amdhabihu Mwana Wake?

Kwa Nini Mungu Alimwambia Abrahamu Amdhabihu Mwana Wake?

▪ Kama ilivyorekodiwa katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo, Yehova Mungu alimwambia Abrahamu amdhabihu mwana wake Isaka. (Mwanzo 22:2) Wasomaji fulani wa Biblia wanaona kwamba ni vigumu kuelewa simulizi hilo. Profesa mmoja anayeitwa Carol anasema: “Niliposikia hadithi hiyo kwa mara ya kwanza nikiwa mtoto nilikasirika sana. Ni Mungu wa aina gani ambaye angemwambia mwanadamu afanye jambo baya kama hilo?” Ingawa hisia kama hizo zinaeleweka, ingefaa tukumbuke mambo fulani.

Kwanza fikiria jambo ambalo Yehova hakufanya. Hakumruhusu Abrahamu amdhabihu mwana wake, hata ingawa Abrahamu alikuwa tayari kufanya hivyo, wala Mungu hajawahi tena kumwambia mwanadamu afanye jambo kama hilo. Yehova anataka waabudu wake wote, kutia ndani watoto, waendelee kuishi—wafurahie maisha marefu yenye kuridhisha.

Pili, Biblia inaonyesha kwamba Yehova alikuwa na sababu ya pekee ya kumwambia Abrahamu amdhabihu Isaka. Mungu alijua kwamba karne nyingi baadaye, Angemruhusu Mwana wake, * Yesu, afe kwa ajili yetu. (Mathayo 20:28) Yehova alitaka tuelewe kwamba dhabihu hiyo ingemgharimu sana. Kwa kufanya hivyo pia, Yehova alitaka kuonyesha waziwazi jinsi ambavyo dhabihu hiyo ingetolewa wakati ujao. Kwa njia gani?

Fikiria maneno ambayo Yehova alimwambia Abrahamu: “Tafadhali, mchukue mwana wako, mwana wako wa pekee unayempenda sana, Isaka, . . . umtoe kama toleo la kuteketezwa.” (Mwanzo 22:2) Ona kwamba Yehova anamwita Isaka mwana “unayempenda sana.” Yehova alijua jinsi Isaka alivyokuwa mwenye thamani kwa Abrahamu. Mungu alijua pia jinsi alivyohisi kumhusu Mwana wake, Yesu. Yehova alimpenda Yesu sana hivi kwamba alizungumza mara mbili kutoka mbinguni, akimwita Yesu moja kwa moja “Mwanangu, mpendwa.”—Marko 1:11; 9:7.

Ona kwamba alipokuwa akizungumza na Abrahamu, Yehova alitumia neno “tafadhali.” Msomi mmoja wa Biblia anasema kwamba kwa kutumia neno hilo, “BWANA anaona uzito wa jambo ambalo anamwambia Abrahamu afanye.” Kama tunavyowazia, ombi hilo lingemhuzunisha sana Abrahamu; vivyo hivyo, tunaweza kuwazia uchungu mwingi ambao Yehova alihisi alipokuwa akimtazama Mwana wake akiteseka na kufa. Kwa kweli, huo ndio uchungu mwingi zaidi ambao Yehova amepata au atapata kuhisi.

Hivyo basi, ingawa huenda tusipendezwe na jambo ambalo Yehova alimwambia Abrahamu afanye, ni jambo la hekima kukumbuka kwamba Yehova hakumruhusu mzee huyo wa ukoo aliyekuwa mwaminifu amdhabihu mwana wake. Alimzuia Abrahamu asipatwe na pigo kubwa zaidi linaloweza kumpata mzazi; alimlinda Isaka kutokana na kifo. Ingawa hivyo, Yehova hakumkinga “Mwana wake mwenyewe bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote.” (Waroma 8:32) Kwa nini Yehova alijiruhusu apatwe na hali hiyo yenye kuumiza sana? Alifanya hivyo “ili tupate uzima.” (1 Yohana 4:9) Hicho ni kikumbusho kilichoje kuhusu upendo wa Mungu kutuelekea! Bila shaka, sisi pia tunachochewa kumpenda. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Biblia haifundishi kwamba Mungu alikuwa baba ya Yesu kupitia uhusiano wa kimwili na mwanamke. Badala yake, Yehova aliumba kiumbe wa roho ambaye baadaye alitumwa duniani na kuzaliwa na bikira Maria. Hivyo, kwa kufaa Mungu anaweza kuitwa Baba yake kwa kuwa yeye ndiye aliyemuumba Yesu.

^ fu. 8 Ili ujifunze mengi kuhusu kwa nini Yesu alipaswa kufa na jinsi tunavyoweza kuonyesha tunathamini jambo hilo, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?