Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Jinsi ya Kukesha Kutoka kwa Mitume wa Yesu

Jifunze Jinsi ya Kukesha Kutoka kwa Mitume wa Yesu

“Mwendelee kukesha pamoja nami.”​—MT. 26:38.

1-3. Mitume walishindwa jinsi gani kuendelea kukesha usiku wa mwisho wa maisha ya Yesu duniani, na ni nini kinachoonyesha kwamba walijifunza kutokana na kosa lao?

WAZIA tukio hili usiku wa mwisho wa maisha ya Yesu duniani. Yesu ameenda katika mojawapo ya mahali ambapo anapenda sana, bustani ya Gethsemane, upande wa mashariki wa Yerusalemu. Amewahi kwenda mara kadhaa mahali hapo pamoja na mitume wake waaminifu. Akiwa na mambo mengi mazito akilini na moyoni mwake, Yesu anahitaji kupata mahali ambapo atakuwa peke yake ili aweze kusali.​—Mt. 26:36; Yoh. 18:1, 2.

2 Mitume watatu, yaani, Petro, Yakobo, na Yohana, wanamsindikiza Yesu hadi ndani kabisa ya bustani hiyo. “Kaeni hapa na mwendelee kukesha pamoja nami,” anawaambia, na kisha anaondoka kwenda kusali. Anaporudi, anawakuta marafiki wake tayari wamelala. Kwa mara nyingine anawasihi kwa kuwaambia: “Endeleeni kukesha.” Hata hivyo, wanalala tena mara mbili zaidi! Baadaye usiku huohuo, mitume wote wanashindwa kubaki macho kiroho. Hata wanamwacha Yesu na kukimbia zao!​—Mt. 26:38, 41, 56.

3 Bila shaka, mitume walijuta kwa sababu ya kushindwa kuendelea kukesha. Wanaume hao waaminifu walijifunza haraka kutokana na makosa yao. Kitabu cha Biblia cha Matendo kinaonyesha kwamba baadaye walikuja kuwa mifano bora zaidi ya watu ambao waliendelea kukesha. Huenda mfano wao mzuri wa uaminifu uliwasaidia Wakristo wenzao kufanya vivyo hivyo. Sasa kuliko wakati mwingine wowote, huu ndio wakati wa kuendelea kukesha. (Mt. 24:42) Acheni basi tuzungumzie masomo matatu kuhusu kuendelea kukesha ambayo tunaweza kujifunza kutokana na kitabu cha Matendo.

WALIKUWA MACHO ILI KUONA WANGEELEKEZWA MAHALI GANI PA KUHUBIRI

4, 5. Roho takatifu ilimwongozaje Paulo na wasafiri wenzake?

4 Somo la kwanza ni kwamba mitume walikuwa macho ili kuona jinsi ambavyo wangeelekezwa mahali pa kuhubiri. Simulizi moja la Biblia linaonyesha jinsi Yesu alivyotumia roho takatifu aliyopewa na Yehova ili kumwongoza mtume Paulo na wasafiri wenzake katika safari isiyo ya kawaida. (Mdo. 2:33) Acheni tujiunge nao.​—Soma Matendo 16:6-10.

5 Paulo, Sila, na Timotheo walikuwa wametoka katika jiji la Listra lililo upande wa kusini mwa Galatia. Baada ya siku kadhaa, walifika kwenye barabara kuu ya Roma inayoelekea upande wa magharibi kwenda kwenye eneo lililo na watu wengi zaidi la wilaya ya Asia. Walitaka kusafiri kwenye barabara hiyo ili watembelee majiji ambayo maelfu ya watu walihitaji kusikia kuhusu Kristo. Lakini kitu fulani kiliwazuia wasiende huko. Mstari wa 6 unasema hivi: “Wakapitia Frigia na nchi ya Galatia, kwa sababu walikatazwa na roho takatifu wasiseme lile neno katika wilaya ya Asia.” Katika njia fulani isiyofunuliwa, roho takatifu iliwazuia wasafiri hao kutohubiri katika jimbo la Asia. Ni wazi kwamba Yesu, kupitia roho ya Mungu, alitaka kumwongoza Paulo na wenzake waelekee upande tofauti.

6, 7. (a) Kulitukia nini Paulo na wasafiri wengine walipokaribia Bithinia? (b) Ni uamuzi gani ambao wanafunzi walichukua, na matokeo yakawaje?

6 Wasafiri hao wenye bidii walielekea wapi? Mstari wa 7 unaeleza hivi: “Tena, walipofika Misia wakafanya jitihada za kuingia Bithinia, lakini roho ya Yesu haikuwaruhusu.” Kwa kuwa hawakuruhusiwa kuhubiri katika Asia, Paulo na wenzake walielekea upande wa kaskazini, wakikusudia kuhubiri katika majiji ya Bithinia. Hata hivyo, walipokaribia Bithinia, kwa mara nyingine tena Yesu alitumia roho takatifu ili kuwazuia. Kufikia hapo ni lazima wanaume hao walianza kuchanganyikiwa. Walijua ni ujumbe gani wangehubiri na jinsi ya kuuhubiri, lakini hawakujua wangehubiri wapi. Tunaweza kusema hilo kwa njia hii: Walikuwa wamebisha mlango unaoelekea Asia, lakini mlango huo haukufunguliwa. Walibisha mlango unaoelekea Bithinia, kwa mara nyingine tena mlango huo haukufunguliwa. Je, waliacha kubisha mlango? Hapana, wahubiri hao wenye bidii hawakuacha!

7 Kufikia hapo, wanaume hao walifanya uamuzi ambao unaweza kuonwa kuwa usio wa kawaida. Mstari wa 8 unatuambia hivi: “Wakapita Misia na kushuka mpaka Troa.” Hivyo, wasafiri hao walielekea magharibi na wakatembea kilomita 563, huku wakipita jiji baada ya jiji hadi walipofika kwenye bandari ya Troa, ambayo kutoka hapo watu walisafiri kwenda Makedonia kwa meli. Wakiwa huko, kwa mara ya tatu, Paulo na wenzake walibisha mlango, lakini mara hii mlango ulifunguliwa wazi! Mstari wa 9 unatuambia mambo yaliyotukia baadaye: “Usiku maono yakamtokea Paulo: mwanamume fulani Mmakedonia alikuwa amesimama akimsihi na kusema: ‘Vuka uingie Makedonia utusaidie.’” Hatimaye, Paulo alijua ni wapi wangehubiri. Bila kukawia, wanaume hao walisafiri kwa meli kwenda Makedonia.

8, 9. Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi la safari ya Paulo?

8 Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi hilo? Ona kwamba ilikuwa baada tu ya Paulo kuanza safari yake ya kwenda Asia ndipo roho ya Mungu ilianza kumwongoza. Kisha, ilikuwa baada tu ya Paulo kukaribia Bithinia ndipo Yesu aliingilia kati. Na hatimaye, ilikuwa baada tu ya Paulo kufika Troa ndipo Yesu alimwongoza kwenda Makedonia. Akiwa Kichwa cha kutaniko, Yesu anaweza kushughulika nasi kwa njia hiyohiyo. (Kol. 1:18) Kwa mfano, huenda ukafikiria kutumikia ukiwa painia au kuhamia katika eneo ambalo lina uhitaji mkubwa zaidi. Lakini huenda ikawa kwamba baada tu ya kufanya jitihada ili kufikia mradi wako, ndipo Yesu, kupitia roho ya Mungu, atakuongoza. Kwa mfano: Dereva anaweza kuongoza gari lake ili kuelekea upande wa kushoto au upande wa kulia ikiwa tu gari hilo linasonga. Vivyo hivyo, Yesu anaweza kutuongoza kupanua huduma yetu ikiwa tu tunasonga mbele, yaani, ikiwa tunajitahidi kufikia mradi wetu.

9 Namna gani basi ikiwa jitihada zako hazizai matunda papo hapo? Je, unapaswa kuacha na kukata kauli kwamba huongozwi na roho ya Mungu? Kumbuka kwamba Paulo alipatwa na vipingamizi. Hata hivyo, aliendelea kutafuta na kubisha mlango hadi alipopata mlango ambao ulifunguka. Vivyo hivyo, ukiendelea kutafuta “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji,” huenda wewe pia ukathawabishwa.​—1 Kor. 16:9.

KUKESHA KUHUSIANA NA SALA

10. Ni nini kinachoonyesha kwamba kukesha katika sala ni muhimu sana ili kuendelea kuwa macho kiroho?

10 Fikiria sasa somo la pili kuhusu kukesha ambalo tunaweza kujifunza kutokana na ndugu zetu Wakristo wa karne ya kwanza: Walikesha kuhusiana na sala. (1 Pet. 4:7) Kudumu katika sala ni muhimu ili kuendelea kukesha. Kumbuka kwamba katika bustani ya Gethsemane kabla tu ya kukamatwa kwake, Yesu aliwaambia mitume wake watatu hivi: “Endeleeni kukesha na kusali sikuzote.”​Mt. 26:41.

11, 12. Kwa nini na ni jinsi gani Herode aliwatendea vibaya Wakristo, kutia ndani Petro?

11 Petro, ambaye alikuwepo wakati huo, baadaye alijionea mwenyewe nguvu ya sala zenye bidii. (Soma Matendo 12:1-6.) Katika mistari ya kwanza ya sura ya 12 ya kitabu cha Matendo, tunajifunza kwamba ili apendwe na Wayahudi, Herode aliwatendea Wakristo vibaya. Inaelekea Herode alijua kwamba Yakobo alikuwa mtume aliyekuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yesu. Hivyo, Herode akamuua Yakobo “kwa upanga.” (Mstari wa 2) Kwa hiyo, kutaniko likapoteza mtume aliyependwa sana. Lilikuwa jaribu kama nini kwa akina ndugu!

12 Herode alifanya nini baadaye? Mstari wa 3 unaeleza hivi: “Alipoona kuwa jambo hilo limewapendeza Wayahudi, akamkamata Petro pia.” Lakini mapema kabla ya tukio hilo baadhi ya mitume kutia ndani Petro walikuwa wamefunguliwa kimuujiza kutoka gerezani. (Mdo. 5:17-20) Huenda Herode alijua vizuri hilo. Mwanasiasa huyo mjanja alitaka kuhakikisha kwamba Petro hatoroki. Hivyo, akamkabidhi Petro kwa “zamu nne za askari-jeshi wanne kila moja ili kumlinda, kwa kuwa alikusudia kumleta mbele ya watu baada ya pasaka.” (Mstari wa 4) Fikiria hilo! Herode alimfunga Petro minyororo katikati ya walinzi 2, huku walinzi 16 wakifanya kazi kwa zamu mchana na usiku ili kuhakikisha kwamba mtume huyo hatoroki. Herode alikusudia kumtoa Petro kwa watu baada ya Pasaka, ili hukumu ya kifo cha Petro iwe zawadi ya kuufurahisha umati. Katika hali hizo hatari, Wakristo wenzake wangefanya nini kwa ajili ya Petro?

13, 14. (a) Kutaniko lilifanya nini Petro alipofungwa gerezani? (b) Tunaweza kujifunza nini kuhusu sala kutokana na yale ambayo kutaniko lilifanya kwa ajili ya Petro?

13 Kutaniko lilijua jambo hususa la kufanya. Mstari wa 5 unasomeka hivi: “Kwa hiyo Petro alikuwa gerezani; lakini kutaniko lilikuwa likisali kwa Mungu kwa juhudi nyingi kwa ajili yake.” Naam, sala zao kwa ajili ya ndugu yao mpendwa zilikuwa dua za bidii za kutoka moyoni. Hivyo, kifo cha Yakobo hakikuwafadhaisha kabisa; wala kuwafanya wafikiri kwamba sala zao hazikuwa na maana yoyote. Badala yake, walijua kwamba sala za waabudu waaminifu ni zenye thamani kubwa machoni pa Yehova. Ikiwa sala hizo zinapatana na mapenzi yake, anazijibu. ​—Ebr. 13:18, 19; Yak. 5:16.

14 Tunaweza kujifunza nini kutokana na yale ambayo Wakristo walifanya kwa ajili ya Petro? Kuendelea kukesha kunatia ndani kusali si tu kwa ajili yetu wenyewe bali kwa ajili ya ndugu na dada zetu pia. (Efe. 6:18) Je, unawajua waamini wenzetu ambao wanapambana na majaribu? Huenda baadhi yao wanavumilia mateso, marufuku ya serikali, au misiba ya kiasili. Kwa nini usitoe sala za kutoka moyoni kwa ajili yao? Labda unawajua wengine ambao wanapambana na matatizo ambayo huenda waamini wenzao hawajui. Huenda wanakabiliana na vurugu za familia, kuvunjika moyo, au matatizo ya afya. Kwa nini usiwafikirie watu hususa ambao unaweza kuwataja kwa majina unapozungumza na Yehova, “Msikiaji wa sala”?​—Zab. 65:2.

15, 16. (a) Eleza jinsi malaika wa Yehova alivyomwokoa Petro kutoka gerezani. (Ona picha hapa chini.) (b) Kwa nini inatia moyo kuona jinsi Yehova alivyomwokoa Petro?

15 Lakini mambo yalimwendeaje Petro? Usiku wake wa mwisho gerezani alipokuwa amelala katikati ya walinzi wawili, Petro alijionea matukio yenye kustaajabisha. (Soma Matendo 12: 7-11.) Wazia mambo yaliyotukia: Kwa ghafula, nuru iling’aa katika gereza. Malaika akasimama pale, bila walinzi kumwona, na upesi akamwamsha Petro. Minyororo ambayo Petro alikuwa amefungwa ikaanguka! Kisha, malaika akamwongoza Petro nje ya gereza, mbele ya walinzi waliokuwa wamesimama nje, na walipokuwa wakipita lango kubwa la chuma, lango hilo “likafunguka lenyewe mbele yao.” Mara tu walipokuwa nje ya gereza, malaika akatoweka. Petro alikuwa huru!

16 Je, hilo haliimarishi imani yetu kuona kwamba Yehova anatumia nguvu zake ili kuwaokoa watumishi wake? Bila shaka, leo hatumtazamii Yehova atuokoe kimuujiza. Hata hivyo, tuna imani kabisa kwamba anatumia nguvu zake kwa faida ya watu wake leo. (2 Nya. 16:9) Kupitia roho yake takatifu yenye nguvu sana, anaweza kutuimarisha ili tuvumilie jaribu lolote lile. (2 Kor. 4:7; 2 Pet. 2:9) Na hivi karibuni Yehova atampa Mwana wake mamlaka ya kuwafufua mamilioni ya watu ambao sasa ni kama wafungwa wa kifo. (Yoh. 5:28, 29) Imani yetu katika ahadi za Mungu inaweza kutupatia ujasiri mkubwa tunapokabiliana na majaribu leo.

KUTOA USHAHIDI KAMILI LICHA YA VIPINGAMIZI

17. Paulo aliwekaje mfano wa pekee katika kuhubiri kwa bidii na kwa uharaka?

17 Hapa tuna somo la tatu kuhusu kukesha ambalo tunaweza kujifunza kutoka kwa mitume. Hawakuruhusu majaribu yawazuie kuhubiri. Ili kuendelea kukesha, ni lazima tuwe wenye bidii na wenye hisi ya uharaka katika kazi yetu ya kuhubiri. Kuhusu hilo, mtume Paulo alikuwa mfano bora sana. Alijitahidi kwa bidii, akasafiri sana na kuanzisha makutaniko mengi. Alistahimili hali nyingi ngumu, hata hivyo hakupoteza kamwe bidii yake au hisi yake ya uharaka.2​2 Kor. 11:23-29.

18. Paulo alifanya nini ili kuendelea kutoa ushahidi alipokuwa kifungoni huko Roma?

18 Tunasoma mara ya mwisho kumhusu Paulo katika kitabu cha Matendo sura ya 28. Paulo alifika Roma ili kujibu mashtaka mbele ya mtawala Nero. Alikuwa amezuiliwa kifungoni, labda akiwa amefungiliwa mnyororo kwa mlinzi wake. Hata hivyo, hakuna mnyororo ambao ungemnyamazisha mtume huyo mwenye bidii! Paulo aliendelea kutafuta njia mbalimbali za kutoa ushahidi. (Soma Matendo 28:17, 23, 24.) Baada ya siku tatu, Paulo aliwaita wanaume wazee Wayahudi ili kuwatolea ushahidi. Kisha, katika siku hususa ambayo Wayahudi walichagua, alitoa ushahidi mkubwa zaidi. Mstari wa 23 unasema hivi: “Basi [Wayahudi wa mahali hapo] wakapanga siku fulani ya kuwa pamoja naye, nao wakaja kwake wakiwa hesabu kubwa zaidi katika makao yake. Naye akawaeleza jambo hilo kwa kutoa ushahidi kamili kuhusiana na ufalme wa Mungu na kwa kutumia ushawishi kwao kuhusu Yesu kutoka katika sheria ya Musa na pia Manabii, tangu asubuhi mpaka jioni.”

19, 20. (a) Kwa nini Paulo alipata matokeo mazuri katika kutoa ushahidi? (b) Paulo alifanya nini licha ya kwamba si kila mtu aliyekubali habari njema?

19 Kwa nini Paulo alipata matokeo mazuri katika kutoa ushahidi? Ona kwamba mstari wa 23 unakazia sababu kadhaa hususa. (1) Alifundisha kuhusu Ufalme wa Mungu na kuhusu Yesu Kristo. (2) Alijaribu kuvuta uangalifu wa wasikilizaji wake “kwa kutumia ushawishi.” (3) Alijadiliana nao kutokana na Maandiko. (4) Alionyesha mtazamo wa kujidhabihu, kwa kuwatolea ushahidi “tangu asubuhi mpaka jioni.” Paulo alitoa ushahidi wenye nguvu, lakini si kila mtu aliyekubali. Mstari wa 24 unasema hivi: “Wengine wakaanza kuamini mambo yaliyosemwa; wengine hawakuamini.” Kukatokea kutoelewana, na watu wakaondoka.

20 Je, Paulo alivunjika moyo kwa kuwa si kila mtu aliyekubali habari njema? Hapana! Andiko la Matendo 28:30 na 31 linatuambia hivi: “Akakaa miaka miwili kamili katika nyumba yake mwenyewe ya kukodiwa, naye akawa akiwakaribisha kwa fadhili wale wote walioingia ndani kwake, akiwahubiria ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu Bwana Yesu Kristo kwa uhuru wa kusema ulio mkubwa zaidi, bila kizuizi.” Kitabu cha Matendo kilichoongozwa na roho ya Mungu, kinafikia mwisho wake kwa maneno hayo yenye kutia moyo.

21. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Paulo alipokuwa katika kifungo cha nyumbani?

21 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Paulo? Alipokuwa mfungwa katika nyumba yake, Paulo hakuwa na uhuru wa kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, alidumisha mtazamo mzuri, huku akiwahubiria wote waliokuja kumwona. Vivyo hivyo leo, watu wengi wa Mungu wanadumisha shangwe yao na wanaendelea kuhubiri licha ya kufungwa isivyo haki kwa sababu ya imani yao. Baadhi ya ndugu na dada zetu wapendwa hawawezi kutoka nyumbani kwao, labda hata wanaishi katika makao ya kuwatunzia wazee kwa sababu ya uzee au ugonjwa. Kwa kadiri ya uwezo wao, wanawahubiria madaktari na wafanyakazi, watu wanaowatembelea, na wengineo. Tamaa yao ya moyoni ni kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu. Tunathamini kama nini mfano wao mzuri!

22. (a) Ni uandalizi gani unaotusaidia kufaidika kutokana na kitabu cha Biblia cha Matendo? (Ona sanduku lililo juu.) (b) Ni nini azimio lako unapongojea mwisho wa mfumo huu wa kale wa mambo?

22 Ni wazi kwamba kuna mengi ya kujifunza kuhusu kukesha kutoka kwa mitume na Wakristo wengine wa karne ya kwanza kama inavyoonyeshwa katika kitabu cha Biblia cha Matendo. Tunapongojea mwisho wa mfumo huu wa kale wa mambo, acheni tuazimie kuwaiga Wakristo wa karne ya kwanza kwa kutoa ushahidi kwa ujasiri na kwa bidii. Leo, tuna pendeleo kubwa zaidi kama nini la kushiriki katika kazi ya “kutoa ushahidi kamili” kuhusu Ufalme wa Mungu!​—Mdo. 28:23.

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

“MAONI YANGU KUHUSU KITABU CHA MATENDO YAMEBADILIKA KABISA”

Baada ya kusoma kitabu “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu, mwangalizi mmoja anayesafiri alifunua hisia zake kwa kusema maneno yafuatayo: “Maoni yangu kuhusu kitabu cha Matendo yamebadilika kabisa.” Alisoma mara nyingi simulizi la kitabu cha Matendo, lakini sasa kwa kuwa amesoma kitabu hicho kipya, anahisi kwamba angeweza kufaidika hata zaidi kwa kusoma kitabu cha Matendo.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Malaika alimwongoza Petro kupitia lango kubwa la chuma