Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukuhani wa Kifalme Utawanufaisha Wanadamu Wote

Ukuhani wa Kifalme Utawanufaisha Wanadamu Wote

“Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee.’”​—1 PET. 2:9.

1. Kwa nini “mlo wa jioni wa Bwana” unaitwa pia Ukumbusho, na una kusudi gani?

WAKATI wa jioni ya Nisani 14 mwaka wa 33 W.K., kwa mara ya mwisho, Yesu Kristo na mitume wake 12 waliadhimisha Pasaka ya Kiyahudi. Baada ya kumfukuza msaliti Yuda Iskariote, Yesu alianzisha maadhimisho tofauti, ambayo baadaye yalikuja kuitwa “mlo wa jioni wa Bwana.” (1 Kor. 11:20) Yesu alisema hivi mara mbili: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” Tukio hilo linajulikana pia kuwa Ukumbusho, yaani, ukumbusho wa kifo cha Kristo, ambao unakazia kifo chake. (1 Kor. 11:24, 25) Ili kutii amri hiyo, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hufanya Ukumbusho wa kifo hicho kila mwaka. Kulingana na kalenda ya Biblia, Nisani 14 mwaka wa 2012, itaanza baada ya jua kutua, Alhamisi, Aprili 5.

2. Yesu alisema mkate na divai vilifananisha nini?

2 Katika mistari miwili mwanafunzi Luka anazungumza kwa ufupi yale ambayo Yesu alifanya na kusema wakati wa tukio hilo: “Akachukua mkate, akashukuru, akaumega, akawapa, akisema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao utatolewa kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’ Pia, kikombe vivyo hivyo baada ya wao kula mlo wa jioni, akasema: ‘Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.’” (Luka 22:19, 20) Mitume waliyaelewaje maneno hayo?

3. Mitume walielewa nini kuhusu maana ya mkate na divai?

3 Wakiwa Wayahudi, mitume walielewa vizuri kuhusu dhabihu za wanyama ambazo makuhani walizitoa kwa Mungu hekaluni huko Yerusalemu. Dhabihu hizo zilitolewa ili kupata kibali cha Yehova, na nyingi zilitumiwa zikiwa mfano wa kufunikwa kwa dhambi. (Law. 1:4; 22:17-29) Hivyo, mitume walielewa jambo ambalo Yesu alimaanisha aliposema kuwa mwili na damu yake ‘ingetolewa na kumwagwa kwa ajili yao.’ Yesu alimaanisha kwamba angetoa uhai wake mwenyewe mkamilifu kuwa dhabihu. Ingekuwa dhabihu yenye thamani ya hali ya juu zaidi kuliko ile ya wanyama.

4. Yesu alimaanisha nini aliposema hivi: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu”?

4 Lakini vipi kuhusu maneno haya ya Yesu, “kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu”? Mitume waliujua unabii uliohusu agano jipya, uliorekodiwa katika Yeremia 31:31-33. (Soma.) Maneno hayo ya Yesu yalionyesha kwamba alikuwa akianzisha agano hilo jipya, ambalo lingechukua mahali pa agano la Sheria ambalo Yehova alikuwa amefanya na taifa la Israeli kupitia Musa. Je, maagano hayo mawili yalikuwa na uhusiano wowote?

5. Agano la Sheria liliwapa Waisraeli matarajio gani?

5 Naam, maagano hayo mawili yalikuwa na makusudi yaliyohusiana. Alipoanzisha agano la Sheria, Yehova aliliambia taifa la Israeli hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mtakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, kwa sababu dunia nzima ni yangu. Na ninyi wenyewe mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.” (Kut. 19:5, 6) Maneno hayo yalimaanisha nini kwa taifa la Israeli?

AHADI YA UKUHANI WA KIFALME

6. Agano la Sheria lilikuwa utimizo wa ahadi gani?

6 Waisraeli walielewa neno “agano,” kwa kuwa Yehova alikuwa amefanya mapatano rasmi pamoja na mababu zao Noa na Abrahamu. (Mwa. 6:18; 9:8-17; 15:18; 17:1-9) Yehova alipofanya agano pamoja na Abrahamu alimwahidi hivi: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki.” (Mwa. 22:18) Yehova alifanya agano la Sheria ili kutimiza ahadi hiyo. Kwa msingi wa agano hilo, taifa la Israeli lingekuwa ‘mali ya pekee ya Yehova kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu.’ Kwa kusudi gani? Ili taifa hilo ‘liwe ufalme wa makuhani kwa Yehova.’

7. Maneno “ufalme wa makuhani” yalimaanisha nini?

7 Waisraeli waliwajua wafalme na makuhani, lakini Melkizedeki ndiye mwanamume pekee wa zamani aliyeruhusiwa na Yehova kutumikia akiwa mfalme na kuhani wakati uleule. (Mwa. 14:18) Sasa Yehova alilipa taifa la Israeli fursa ya kutokeza “ufalme wa makuhani.” Kama maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yalivyoonyesha baadaye, hilo lilimaanisha kwamba taifa hilo lingetokeza ufalme wa kikuhani, yaani, wafalme ambao wangekuwa pia makuhani.—1 Pet. 2:9.

8. Makuhani waliowekwa rasmi na Mungu walitoa huduma gani?

8 Bila shaka, mfalme hutawala. Hata hivyo, kuhani hufanya kazi gani? Andiko la Waebrania 5:1 linasema hivi: “Kila kuhani mkuu anayechukuliwa kutoka kati ya wanadamu huwekwa rasmi kwa ajili ya wanadamu juu ya mambo yanayohusiana na Mungu, ili atoe zawadi na dhabihu kwa ajili ya dhambi.” Hivyo, kuhani aliwekwa rasmi na Yehova ili kuwakilisha watu wenye dhambi mbele za Mungu kupitia matoleo yaliyoamriwa, akimsihi Yehova kwa niaba yao. Kwa upande mwingine, kuhani pia alimwakilisha Yehova mbele ya watu, akiwafundisha sheria za Mungu. (Law. 10:8-11; Mal. 2:7) Kwa njia hizo, kuhani aliyewekwa rasmi na Mungu alifanya kazi ya kuwapatanisha watu na Mungu.

9. (a) Waisraeli walipaswa kufanya nini ili kutimiza ahadi ya kuwa “ufalme wa makuhani”? (b) Kwa nini Yehova alianzisha ukuhani katika Israeli? (c) Ni nini kilichowazuia Waisraeli wasiwe “ufalme wa makuhani” chini ya agano la Sheria?

9 Hivyo, agano la Sheria liliwapa Waisraeli fursa ya kutokeza ukuhani wa kifalme ambao ungenufaisha “vikundi vingine vyote vya watu.” Hata hivyo, taraja hilo la pekee lilikuwa na sharti hili: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu.” Je, Waisraeli wangeweza ‘kuitii kabisa sauti ya Yehova’? Naam, walifanya hivyo kwa kadiri fulani. Je, wangeweza kufanya hivyo kwa ukamili? Hapana. (Rom. 3:19, 20) Kwa sababu hiyo, Yehova aliweka katika Israeli ukuhani, uliotenganishwa na utawala wa kifalme, ili ukuhani huo utoe dhabihu za wanyama kwa ajili ya dhambi ambazo bila shaka Waisraeli wangetenda. (Law. 4:1–6:7) Dhambi hizo zilitia ndani dhambi za makuhani wenyewe pia. (Ebr. 5:1-3; 8:3) Yehova alikubali dhabihu hizo, lakini hazikuweza kulipia kwa ukamili dhambi za wale waliotoa dhabihu hizo. Ukuhani chini ya agano la Sheria haukuweza hata kuwapatanisha kikamili Waisraeli wanyoofu na Mungu. Mtume Paulo alisema hivi: “Haiwezekani damu ya ng’ombe na ya mbuzi kuondolea mbali dhambi.” (Ebr. 10:1-4) Kwa sababu ya kuvunja Sheria hiyo, Waisraeli wakawa chini ya laana. (Gal. 3:10) Wakiwa katika hali hiyo hawangeweza kuutumikia ulimwengu wakiwa ukuhani wa kifalme.

10. Agano la Sheria lilitimiza nini?

10 Je, ahadi ya Yehova ya kwamba Waisraeli wangekuwa “ufalme wa makuhani” haikuwa na maana yoyote? Sivyo hata kidogo. Ikiwa kwa kweli wangejitahidi kutii, wangepata pendeleo hilo, hata hivyo, haingekuwa chini ya agano la Sheria. Kwa nini? (Soma Wagalatia 3:19-25.) Kwa wale waliojitahidi kuishika Sheria kwa uaminifu, Sheria hiyo ilisaidia kuilinda ibada safi. Iliwasaidia Wayahudi watambue makosa yao na kwamba walihitaji dhabihu ya hali ya juu zaidi kuliko ile ambayo kuhani wao mkuu aliweza kuitoa. Sheria ilikuwa mtunzaji ambaye angewaongoza Waisraeli kwa Kristo, au Masihi, jina la cheo linalomaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Hata hivyo, Masihi alipofika, alianzisha agano jipya lililotabiriwa na Yeremia. Wale waliomkubali Kristo walialikwa wawe sehemu ya agano jipya na hatimaye wangekuwa “ufalme wa makuhani.” Acheni tuone ni kwa jinsi gani.

AGANO JIPYA LATOKEZA UKUHANI WA KIFALME

11. Yesu alikuwa msingi wa ukuhani wa kifalme jinsi gani?

11 Yesu wa Nazareti alifika mwaka wa 29 W.K., akiwa Masihi. Akiwa na umri wa miaka 30 hivi, Yesu alijitoa mwenyewe ili afanye mapenzi ya pekee ya Yehova, akifanya hivyo kwa kubatizwa katika maji. Yehova alisema waziwazi hivi kumhusu Yesu: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa,” akamtia mafuta, si kwa mafuta halisi, bali kwa roho takatifu. (Mt. 3:13-17; Mdo. 10:38) Kutiwa mafuta huko kulimfanya Yesu awekwe rasmi kuwa Kuhani Mkuu wa jamii nzima ya kibinadamu inayomwamini akiwa Mfalme wao wa wakati ujao. (Ebr. 1:8, 9; 5:5, 6) Angekuwa msingi wa jamii ya kweli ya ukuhani wa kifalme.

12. Dhabihu ya Yesu ilifanya jambo gani liwezekane?

12 Akiwa Kuhani Mkuu, Yesu angetoa dhabihu gani ambayo ingefunika kabisa dhambi iliyorithiwa ya watu walioamini? Kama alivyoonyesha alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake, uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ulikuwa ndio dhabihu. (Soma Waebrania 9:11, 12.) Tangu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., Yesu akiwa Kuhani Mkuu aliruhusu ajaribiwe na kuzoezwa hadi wakati alipokufa. (Ebr. 4:15; 5:7-10) Baada ya kufufuliwa, alipaa kwenda mbinguni na kutoa thamani ya dhabihu yake kwa Yehova. (Ebr. 9:24) Baada ya hapo, Yesu angeweza kuwatetea mbele za Yehova wale wanaoweka imani katika dhabihu yake na kuwasaidia kumtumikia Mungu wakiwa na taraja la kuishi milele. (Ebr. 7:25) Pia, dhabihu yake ilitumiwa kulifanya agano jipya kuwa halali.​—Ebr. 8:6; 9:15.

13. Wale walioingizwa katika agano jipya walikuwa na matazamio gani?

13 Wale walioalikwa kuwa katika agano jipya walipaswa pia kutiwa mafuta na roho takatifu. (2 Kor. 1:21) Wayahudi waaminifu na baadaye Watu wa Mataifa walitiwa ndani ya agano hilo. (Efe. 3:5, 6) Wale walioingizwa katika agano jipya walikuwa na matazamio gani? Wangepata msamaha wa kweli kwa ajili ya makosa yao. Yehova alikuwa ameahidi hivi: “Nitalisamehe kosa lao, na dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yer. 31:34) Dhambi zao zikiwa zimeondolewa, wangeweza kustahili kuwa “ufalme wa makuhani.” Akizungumza na Wakristo watiwa-mafuta, Petro aliandika hivi: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mtangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:9) Katika andiko hilo Petro ananukuu maneno ambayo Yehova aliwaambia Waisraeli alipokuwa akilianzisha agano la Sheria na Petro anayatumia maneno hayo kuwahusu Wakristo katika agano jipya.​—Kut. 19:5, 6.

UKUHANI WA KIFALME UTAWANUFAISHA WANADAMU WOTE

14. Ukuhani wa kifalme utatumikia wapi?

14 Wale walio katika agano jipya watatumikia wakiwa wapi? Wakiwa kikundi, wangetumikia duniani wakiwa jamii ya kikuhani, wakimwakilisha Yehova kwa watu kwa ‘kutangaza kotekote sifa bora’ na kwa kuandaa chakula cha kiroho. (Mt. 24:45; 1 Pet. 2:4, 5) Baada ya kufa na kufufuliwa kwao, wanatumikia pamoja na Kristo huko mbinguni wakiwa wafalme na makuhani, wakitimiza kwa ukamili majukumu hayo yote mawili. (Luka 22:29; 1 Pet. 1:3-5; Ufu. 1:6) Akithibitisha hilo, mtume Yohana aliona idadi kubwa ya viumbe wa roho karibu na kiti cha ufalme cha Yehova huko mbinguni. Katika “wimbo mpya” unaoelekezwa kwa “Mwana-Kondoo,” viumbe hao wanaimba hivi: “Kwa damu yako ukamnunulia Mungu watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa, nawe ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufu. 5:8-10) Katika maono yanayofuata, Yohana anasema hivi kuhusu watawala hao: “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.” (Ufu. 20:6) Wakiwa pamoja na Kristo, wanafanyiza ukuhani wa kifalme ili kuwanufaisha wanadamu wote.

15, 16. Ukuhani wa kifalme utailetea jamii ya kibinadamu manufaa gani?

15 Wale 144,000 watawanufaisha wanadamu duniani jinsi gani? Kitabu cha Ufunuo sura ya 21 kinawataja watiwa-mafuta hao kuwa jiji la mbinguni, Yerusalemu Jipya, linaloitwa “mke wa Mwana-Kondoo.” (Ufu. 21:9) Mstari 2 hadi wa 4 unasema hivi: “Nikaona pia lile jiji takatifu, Yerusalemu Jipya, likishuka kutoka mbinguni kwa Mungu na limetayarishwa kama bibi-arusi aliyepambwa kwa ajili ya mume wake. Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’” Hizo ni baraka za ajabu kama nini! Kuondolewa kwa kifo kutakomesha kisababishi kikuu cha machozi, maombolezo, kilio, na maumivu. Hilo litamaanisha kwamba wanadamu waaminifu watafanywa kuwa wakamilifu na watapatanishwa kwa ukamili na Mungu.

16 Likieleza zaidi kuhusu baraka ambazo ukuhani wa kifalme utaleta, andiko la Ufunuo 22:1, 2 linasema hivi: “Akanionyesha mto wa maji ya uzima, mwangavu kama fuwele, ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo ukiteremka kupitia katikati ya njia pana [ya Yerusalemu Jipya]. Na upande huu wa mto na upande ule kulikuwa na miti ya uzima yenye kuzaa mazao kumi na mawili ya matunda, ikitoa matunda yake kila mwezi. Na majani ya miti ile yalikuwa ya kuponya mataifa.” Kukiwa na maandalizi hayo ya ufananisho, “mataifa,” au vikundi vya jamii za watu, wataponywa kwa ukamili kutokana na kutokamilika walikorithi kutoka kwa Adamu. Kwa kweli, ‘mambo ya zamani yatakuwa yamepitilia mbali.’

UKUHANI WA KIFALME WAKAMILISHA KAZI YAKE

17. Hatimaye ukuhani wa kifalme utatimiza nini?

17 Kufikia mwishoni mwa miaka 1,000 ya kazi yenye manufaa, jamii ya ukuhani wa kifalme itakuwa imewainua raia wake hapa duniani kufikia hali ya ukamilifu. Kisha, akiwa Kuhani Mkuu na Mfalme, Kristo atamkabidhi Yehova jamii ya kibinadamu iliyo kamilifu. (Soma 1 Wakorintho 15:22-26.) Ukuhani wa kifalme utakuwa umetimiza kwa ukamili kusudi lake.

18. Baada ya ukuhani wa kifalme kutimiza kazi yake, Yehova atawatumia jinsi gani wale watakaotawala pamoja na Kristo?

18 Baada ya hiyo miaka 1,000, Yehova atawatumiaje wale waliopewa pendeleo kubwa la kutawala pamoja na Kristo? Kulingana na Ufunuo 22:5, “watatawala wakiwa wafalme milele na milele.” Watatawala juu ya nani? Biblia haisemi lolote. Lakini aina ya uhai walionao na uzoefu wa kuwasaidia watu wasio wakamilifu duniani utawasaidia kuendelea kuwa na daraka muhimu katika kutimizwa kwa makusudi ya Yehova milele.

19. Wale watakaohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu watakumbushwa nini?

19 Tutakapokusanyika kwa ajili ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu Alhamisi, Aprili 5, 2012, mafundisho haya ya Biblia yatakuwa bado akilini mwetu. Wakristo watiwa-mafuta wachache ambao bado wapo hapa duniani watakula mkate usiotiwa chachu na kunywa divai nyekundu, kuonyesha kwamba wao ni sehemu ya agano jipya. Mifano hiyo ya dhabihu ya Kristo itawakumbusha mapendeleo na majukumu makubwa waliyo nayo katika makusudi ya milele ya Mungu. Acheni sisi sote tuhudhurie Ukumbusho tukiwa na uthamini mkubwa kwa uandalizi huo wa ukuhani wa kifalme ambao Yehova Mungu alifanya ili kuwanufaisha wanadamu wote.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ukuhani wa kifalme utailetea jamii ya kibinadamu faida za milele