Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ukuhani wa Kifalme Utakaowaletea Wanadamu Wote Baraka

Ukuhani wa Kifalme Utakaowaletea Wanadamu Wote Baraka

Ukuhani wa Kifalme Utakaowaletea Wanadamu Wote Baraka

“Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee.’”​—1 PET. 2:9.

UNAWEZA KUELEZA?

Ukuhani wa kifalme uliahidiwa kwa mara ya kwanza wakati gani?

Namna gani agano jipya linatokeza ukuhani wa kifalme?

Ukuhani wa kifalme utawaletea wanadamu baraka gani?

1. Kwa nini ‘mulo wa jioni wa Bwana’ unaitwa pia Ukumbusho, na una kusudi gani?

 MANGARIBI ya Nisani 14, mwaka wa 33, Yesu Kristo na mitume wake 12 waliazimisha Pasaka ya Wayahudi kwa mara ya mwisho. Baada ya Yuda Iskariote aliyemusaliti Yesu kuondoka, Yesu akaanzisha mwazimisho tofauti ulioitwa baadaye ‘mulo wa jioni wa Bwana.’ (1 Kor. 11:20) Yesu alisema mara mbili: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” Tukio hilo linaitwa pia Ukumbusho, yaani ukumbusho wa kifo cha Kristo. (1 Kor. 11:24, 25) Ili kutii amri hiyo, kila mwaka Mashahidi wa Yehova wanaazimisha Ukumbusho. Katika mwaka wa 2012, Nisani 14 kulingana na kalenda ya Wayahudi, itakuwa tarehe 5 mwezi wa 4 baada ya jua kutua.

2. Yesu alisema nini kuhusu mukate na divai aliyotumia?

2 Katika maandiko mawili, mwanafunzi Luka alionyesha kwa kifupi yale ambayo Yesu alifanya na kusema wakati wa tukio hilo: “Akachukua mukate, akashukuru, akaumega, akawapa, akisema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao utatolewa kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’ Pia, kikombe vivyo hivyo baada ya wao kula mulo wa jioni, akasema: ‘Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa musingi wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.’” (Luka 22:19, 20) Mitume walielewa maneno hayo namna gani?

3. Mitume walielewa maneno ya Yesu kuhusu mwili na damu yake kuwa yanamaanisha nini?

3 Mitume walikuwa Wayahudi, kwa hiyo walijua vizuri zabihu za wanyama ambazo makuhani walitolea Mungu kwenye hekalu huko Yerusalemu. Wayahudi walitoa zabihu hizo ili wakubaliwe na Mungu, na zabihu zingine nyingi zilitolewa ili kusamehewa zambi. (Law. 1:4; 22:17-29) Kwa hiyo, Yesu aliposema kwamba mwili wake ‘ungetolewa kwa ajili yao’ na kwamba damu yake ‘ingemwagwa kwa ajili yao,’ mitume walielewa kwamba Yesu atatoa uzima wake mukamilifu kama zabihu. Hiyo ilikuwa zabihu yenye bei kubwa sana kuliko zabihu za wanyama.

4. Yesu alimaanisha nini aliposema: ‘Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa musingi wa damu yangu’?

4 Tuseme nini kuhusu maneno haya ya Yesu: ‘Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa musingi wa damu yangu’? Mitume walijua unabii unaozungumuzia agano jipya kwenye andiko la Yeremia 31:31-33. (Soma.) Maneno hayo ya Yesu yalionyesha kwamba wakati huo, yeye alianzisha agano jipya hilo, ambalo lilichukua nafasi ya agano la Sheria ambalo Yehova alifanya pamoja na Israeli kupitia Musa. Je, maagano hayo mawili yalipatana?

5. Agano la Sheria liliwatolea Waisraeli pendeleo gani?

5 Ndiyo, maagano hayo mawili yalipatana. Alipoanzisha Agano la Sheria, Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: ‘Ikiwa mutaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mutakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, kwa sababu dunia nzima ni yangu. Na ninyi wenyewe mutakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.’ (Kut. 19:5, 6) Maneno hayo yalimaanisha nini kwa Waisraeli?

AHADI YA UKUHANI WA KIFALME

6. Agano la Sheria lilisaidia kutimiza ahadi gani?

6 Waisraeli walielewa neno “agano,” kwa kuwa Yehova alifanya maagano pamoja na mababu wao, Noa na Abrahamu. (Mwa. 6:18; 9:8-17; 15:18; 17:1-9) Katika agano alilofanya na Abrahamu, Yehova aliahidi hivi: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki.” (Mwa. 22:18) Agano la Sheria lilisaidia kutimiza ahadi hiyo. Kupitia agano hilo, Israeli ingekuwa ‘mali ya pekee [ya Yehova] kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu.’ Kwa kusudi gani? Ili ‘kuwa kwa Yehova ufalme wa makuhani.’

7. Maneno “ufalme wa makuhani” yalimaanisha nini?

7 Waisraeli walijua kwamba mutu hangepaswa kuwa mufalme na wakati uleule kuwa kuhani, lakini ni Melkizedeki tu ndiye Yehova alikubali awe mufalme na wakati huohuo awe kuhani. (Mwa. 14:18) Sasa kupitia Agano la Sheria Yehova alitolea taifa pendeleo la kuwa na “ufalme wa makuhani.” Kama maandiko yalivyoonyesha baadaye, hilo lilimaanisha kuwatolea pendeleo la kuwa na ukuhani wa kifalme, yaani wafalme ambao pia ni makuhani.​—1 Pet. 2:9.

8. Kuhani aliyechaguliwa na Mungu alikuwa na kazi gani?

8 Tunajua kwamba kazi ya mufalme ni kutawala. Lakini kazi ya kuhani ni nini? Waebrania 5:1 inaeleza: ‘Kila kuhani mukuu anayechukuliwa kutoka kati ya wanadamu huwekwa rasmi kwa ajili ya wanadamu juu ya mambo yanayohusiana na Mungu, ili atoe zawadi na zabihu kwa ajili ya zambi.’ Kwa hiyo, kuhani aliyechaguliwa na Yehova aliwakilisha watu wafanya zambi mbele ya Mungu kwa kutoa zabihu zilizoombwa ili zambi zao zisamehewe. Vilevile, kuhani aliwakilisha Yehova mbele ya watu, akiwafundisha sheria zake. (Law. 10:8-11; Mal. 2:7) Kwa njia hizo, kuhani aliyechaguliwa na Mungu alitumika ili kupatanisha watu pamoja na Mungu.

9. (a) Waisraeli walipaswa kutimiza takwa gani ili wawe “ufalme wa makuhani”? (b) Kwa nini Yehova alianzisha ukuhani katika Israeli? (c) Ni nini kilichozuia Israeli kuwa na “ufalme wa makuhani” katika agano la Sheria?

9 Kwa hiyo agano la Sheria lilitolea Waisraeli pendeleo la kuwa na ukuhani wa kifalme ambao ungeletea “vikundi vingine vyote vya watu” baraka. Hata hivyo ili kuwa na pendeleo hilo la pekee iliwaomba watimize takwa ambalo Mungu aliwatolea: ‘Ikiwa mutaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu.’ Je, Waisraeli wangeweza “kutii sauti ya Yehova kabisa”? Ndiyo, kwa kadiri fulani. Je, wangeweza kufanya hivyo kwa ukamilifu? Hapana. (Rom. 3:19, 20) Ni kwa sababu hiyo, Yehova alifanya kuwe makuhani katika Israeli ili kutoa zabihu za wanyama kwa ajili ya zambi ambazo Waisraeli wangefanya; makuhani hao hawakuwa wafalme. (Law. 4:1–6:7) Zambi hizo za Waisraeli zilitia ndani zambi za makuhani. (Ebr. 5:1-3; 8:3) Yehova alikubali zabihu hizo, lakini hazikumaliza kabisa zambi za mutu aliyezitoa. Ukuhani wa agano la Sheria haukuwa na uwezo wa kupatanisha kikamili hata Waisraeli waadilifu na Mungu. Mutume Paulo alisema hivi: ‘Haiwezekani damu ya ng’ombe na ya mbuzi kuondolea mbali zambi.’ (Ebr. 10:1-4) Kwa kuwa Waisraeli walivunja Sheria, wao walilaaniwa. (Gal. 3:10) Katika hali hiyo, hawangeweza kuwa makuhani na wafalme kwa ajili ya ulimwengu muzima.

10. Agano la Sheria lilikuwa na kusudi gani?

10 Je, ahadi ya Yehova kwamba Waisraeli wangetokeza “ufalme wa makuhani” haikuwa na maana yoyote? Sivyo. Ikiwa wangetii kwa moyo wote, wangepata nafasi hiyo, lakini si wakati walikuwa wangali bado chini ya Sheria. Kwa nini? (Soma Wagalatia 3:19-25.) Kwa wale waliojikaza kwa uaminifu kutii Sheria, Sheria hiyo iliwasaidia kuendeleza ibada safi. Iliwasaidia Wayahudi wajue kwamba wao ni wafanya zambi na kwamba walihitaji zabihu kubwa kuliko ile ambayo kuhani mukuu alitoa. Sheria ilikuwa mutunzaji ambaye aliwaongoza kwa Kristo, ao Masiya, majina ya cheo yanayomaanisha “Mutiwa-Mafuta.” Lakini, Masiya alipofika duniani, alianzisha agano jipya lililotabiriwa na nabii Yeremia. Wale waliokubali Kristo walialikwa wawe sehemu ya agano jipya na wakawa kabisa “ufalme wa makuhani.” Namna gani?

AGANO JIPYA LINAZAA UKUHANI WA KIFALME

11. Namna gani Yesu alikuwa musingi wa ukuhani wa kifalme wa kweli?

11 Katika mwaka wa 29, Masiya alionekana, na Masiya huyo alikuwa ni Yesu wa Nazarethi. Wakati huo alikuwa na miaka 30 hivi, alijitoa yeye mwenyewe kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake, na alionyesha jambo hilo kwa kubatizwa katika maji. Yehova alimukubali kuwa ‘Mwana wake, mupendwa,’ akamutia mafuta, si mafuta halisi, lakini kwa roho takatifu. (Mt. 3:13-17; Mdo. 10:38) Kutiwa huko mafuta kulimufanya awe Kuhani Mukuu kwa ajili ya wanadamu wote wanaomwamini na kuwa Mufalme wao wakati ujao. (Ebr. 1:8, 9; 5:5, 6) Kwa hiyo, alikuwa musingi wa ukuhani wa kifalme wa kweli.

12. Zabihu ya Yesu iliwezesha nini?

12 Kwa kuwa Yesu alikuwa sasa Kuhani Mukuu, ni zabihu gani ambayo angetoa ambayo ingemaliza kabisa zambi tuliyoriti? Kama alivyosema alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake, yeye angetoa uzima wake mukamilifu kuwa zabihu hiyo. (Soma Waebrania 9:11, 12.) Tangu kubatizwa kwake katika mwaka wa 29, Yesu, akiwa Kuhani Mukuu, alivumilia majaribu na kuzoezwa mupaka kufa. (Ebr. 4:15; 5:7-10) Kisha kufufuliwa, alipanda mbinguni ili kumutolea Yehova bei ya zabihu yake. (Ebr. 9:24) Kuanzia hapo, Yesu angewaombea sasa kwa Yehova wale wanaoamini zabihu yake, na kuwasaidia wamutumikie Mungu wakiwa na tumaini la kuishi milele. (Ebr. 7:25) Zabihu yake ilisaidia pia kufanya agano jipya likubaliwe kisheria.​—Ebr. 8:6; 9:15.

13. Wale walioitwa ili kuwa sehemu ya agano jipya walikuwa na tumaini gani?

13 Wale walioitwa ili kuwa sehemu ya agano jipya walipaswa pia kutiwa mafuta na roho takatifu. (2 Kor. 1:21) Wayahudi waaminifu na baadaye Watu Wasio Wayahudi waliingizwa katika agano hilo. (Efe. 3:5, 6) Wale walioingizwa katika agano hilo jipya walikuwa na tumaini gani? Walikuwa na tumaini la kusamehewa kabisa zambi zao. Yehova aliahidi hivi: ‘Nitalisamehe kosa lao, na zambi yao sitaikumbuka tena.’ (Yer. 31:34) Kwa kuwa zambi zao zilikuwa zimesamehewa, wangestahili kuwa “ufalme wa makuhani.” Petro aliandika hivi kuhusu Wakristo watiwa​-mafuta: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mutangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:9) Hapa Petro anarudilia maneno ya Yehova kwa Israeli wakati aliwatolea Sheria na anayatumia kwa Wakristo katika agano jipya.​—Kut. 19:5, 6.

UKUHANI WA KIFALME UNAWALETEA WANADAMU WOTE BARAKA

14. Wale walio katika agano jipya wanatumikia wapi?

14 Wale walio katika agano jipya wanatumikia wapi? Duniani, mahali ambapo, wakiwa kikundi wanatumika kama makuhani, wanamwakilisha Yehova kwa watu kwa kufanya kazi ya ‘kutangaza kotekote sifa zake bora’ na kutoa chakula cha kiroho. (Mt. 24:45; 1 Pet. 2:4, 5) Wanapokufa na kufufuliwa, wanatumika pamoja na Kristo huko mbinguni wakiwa wafalme na makuhani. (Luka 22:29; 1 Pet. 1:3-5; Ufu. 1:6) Ili kuhakikisha jambo hilo, mutume Yohana aliona katika maono viumbe vingi vya kiroho karibu na kiti cha enzi cha Yehova huko mbinguni. Katika ‘wimbo mupya’ kwa ajili ya “Mwana Kondoo,” wanaimba hivi: ‘Kwa damu yako ukamununulia Mungu watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa, nawe ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’ (Ufu. 5:8-10) Baadaye Yohana anasema yale aliyoona tena kuhusu watawala hao: “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.” (Ufu. 20:6) Pamoja na Kristo, wanafanyiza ukuhani wa kifalme ili kuwaletea wanadamu wote baraka.

15, 16. Ukuhani wa kifalme utawaletea wanadamu baraka gani?

15 Ni baraka gani wale 144,000 wataletea watu walio duniani? Ufunuo sura ya 21 inawaita jiji la mbinguni, Yerusalemu mupya, ‘muke wa Mwana-Kondoo.’ (Ufu. 21:9) Kwenye mustari wa 2 mupaka wa 4 inaelezwa hivi: “Nikaona pia lile jiji takatifu, Yerusalemu Jipya, likishuka kutoka mbinguni kwa Mungu na limetayarishwa kama bibi​-arusi aliyepambwa kwa ajili ya mume wake. Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’” Hizo ni baraka za ajabu kabisa! Kuondoa kifo kutamaanisha kumaliza mambo yote yanayoleta machozi, maombolezo, kilio, na maumivu. Kutamaanisha pia kwamba wanadamu waaminifu wanafikia ukamilifu, na kupatanishwa kabisa na Mungu.

16 Baraka zingine ambazo ukuhani wa kifalme utaleta zinaelezwa hivi katika Ufunuo 22:1, 2: ‘Naye akanionyesha muto wa maji ya uzima, mwangavu kama fuwele, ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu na cha Mwana​-Kondoo ukiteremuka kupitia katikati ya njia pana [ya Yerusalemu mupya]. Na upande huu wa muto na upande ule kulikuwa na miti ya uzima yenye kuzaa mazao kumi na mawili ya matunda, ikitoa matunda yake kila mwezi. Na majani ya miti ile yalikuwa ya kuponya mataifa.’ Kupitia mipango hiyo ya mufano, “mataifa,” ao wanadamu, wataponyeshwa kabisa na kutokamilika tulikoriti kutoka kwa Adamu. Kwa kweli, ‘mambo ya zamani yatakuwa yamepitilia mbali.’

UKUHANI WA KIFALME UNAMALIZA KAZI YAKE

17. Ukuhani wa kifalme utatimiza nini mwishowe?

17 Mwishoni mwa ile miaka 1,000 ya kazi, ukuhani wa kifalme utakuwa umesaidia wanadamu watiifu duniani kufikia ukamilifu. Kwa hiyo Kristo, Kuhani Mukuu na Mufalme, atamutolea Yehova familia ya kibinadamu yenye kukamilika. (Soma 1 Wakorintho 15:22-26.) Ndipo ukuhani wa kifalme utakuwa umetimiza kabisa kusudi lake.

18. Wale wafalme na makuhani pamoja na Kristo wakisha kutimiza kazi yao, Yehova atawatumia namna gani tena?

18 Kisha hapo namna gani Yehova atawatumia wale waliotawala kama wafalme na makuhani pamoja na Kristo? Kulingana na Ufunuo 22:5, “watatawala wakiwa wafalme milele na milele.” Watatawala nani? Biblia haisemi kitu. Kwa kuwa wataendelea kuwa na miili isiyokufa na kwa sababu ya uzoevu watakaopata katika kuwasaidia wanadamu wasiokamilika, wataendelea kuwa wafalme na kutumiwa na Yehova ili kutimiza makusudi yake milele.

19. Wale watakaohuzuria Ukumbusho watakumbushwa jambo gani?

19 Tutakapokutana ili kuazimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu, Siku ya Ine, tarehe 5 mwezi wa 4, 2012, tusisahau mafundisho haya ya Biblia. Mabaki ya watiwa-mafuta walio duniani leo, watakula mukate usiotiwa chachu na kunywa divai nyekundu, ili kuonyesha kwamba wako sehemu ya agano jipya. Mukate na divai, mifano ya zabihu ya Kristo, itawakumbusha pendeleo lao nzuri na madaraka yao katika kusudi la Mungu la milele. Acheni sisi wote tuhuzurie Ukumbusho tukiwa na shukrani kwa ajili ya mupango wa Yehova Mungu kuhusu ukuhani wa kifalme unaowaletea wanadamu wote baraka.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ukuhani wa kifalme utawaletea wanadamu baraka za milele