Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Namna Gani Nitaweza Kuhubiri?’

‘Namna Gani Nitaweza Kuhubiri?’

‘Namna Gani Nitaweza Kuhubiri?’

Ulimwenguni pote, tuna mifano mizuri sana ya ndugu na dada ambao wanahubiri kwa uaminifu ijapokuwa wana matatizo makubwa ya afya. Tuchukue mufano wa Dalia, anayeishi huko Vilnius, muji mukuu wa Lithuanie.

Dalia ni dada na ana miaka 30 hivi. Tangu kuzaliwa amesumbuliwa na matokeo ya ugonjwa wa ubongo wa kuvuya damu unaoitwa apoplexie. Ugonjwa huo umemuacha kilema na mwenye magumu ya kusema. Kwa hiyo, ni watu wa familia yake tu ndio wanaoelewa vizuri mambo anayosema. Dalia anaishi pamoja na mama yake Galina anayemuhangaikia. Ijapokuwa maisha ya Dalia yamejaa taabu na mahangaiko, yeye anaendelea kuwa na maoni yanayofaa kuelekea hali yake. Hilo linawezekana namna gani?

Galina anaeleza: “Katika mwaka wa 1999, binamu yangu mwanamuke, Apolonija alikuja kututembelea. Tulitambua kwamba Apolonija, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alielewa Biblia vizuri, na Dalia akaanza kumuuliza maulizo mengi. Bila kukawia, funzo la Biblia likaanzishwa na Dalia. Mara kwa mara, nilihuzuria kwenye funzo lao ili nimusaidie Apolonija aelewe maneno ya Dalia. Ingawa hali yake, nilitambua kwamba kila jambo ambalo Dalia alikuwa akijifunza lilimusaidia kabisa. Bila kukawia mimi pia nikaomba funzo la Biblia.”

Dalia alipoanza kuelewa mafundisho ya Biblia, jambo moja lilianza kumusumbua sana. Mwishowe, alimuuliza Apolonija hivi: “Namna gani kilema kama mimi anaweza kuhubiri?” (Mt. 28:19, 20) Kwa utulivu, Apolonija akamuhakikishia Dalia: “Usiogope. Yehova atakusaidia.” Bila shaka, Yehova alimusaidia.

Sasa, Dalia anahubiri namna gani? Yeye anatumia njia tofauti-tofauti. Dada wanamusaidia kuandika barua zenye ujumbe wa Biblia. Kwanza, Dalia anawatolea mawazo yake. Kisha wanayaandika katika barua. Dada Dalia anatuma pia ujumbe mbalimbali wa Biblia kupitia telefone yake. Na wakati hali ya hewa ni nzuri, washiriki wa kutaniko wanaenda pamoja naye kuhubiri watu katika mabustani na barabarani.

Dalia na mama yake waliendelea kufanya maendeleo ya kiroho hivi kwamba wote wawili walitoa maisha yao kwa Yehova na kubatizwa mwezi wa 11, 2004. Katika mwezi wa 9, 2008, kikundi cha luga ya Kipolishi (luga inayozungumuziwa Pologne) kiliundwa katika Vilnius. Kwa kuwa kikundi hicho kilihitaji wahubiri wa Ufalme wa zaidi, Dalia na mama yake walijiunga na kikundi hicho. Dalia anasema: “Miezi fulani nilikuwa na wasiwasi ikiwa sijatokea bado katika mahubiri. Lakini ilikuwa ikifanyika hivi, nikiisha tu kusali kwa Yehova kuhusu jambo hilo, papohapo mutu fulani alikuwa akifanya mupango ili kuhubiri pamoja nami.” Dada yetu mupendwa Dalia anajisikia namna gani kuhusu hali yake? Anasema: “Ugonjwa umelemaza mwili wangu, lakini haukulemaza akili yangu. Mimi ni mwenye furaha kwa kuwa ninaweza kuwaelezea wengine kumuhusu Yehova!”