Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufanya Wakati wa Kujifunza Uwe Wenye Kufurahisha na Kunufaisha

Kufanya Wakati wa Kujifunza Uwe Wenye Kufurahisha na Kunufaisha

Kufanya Wakati wa Kujifunza Uwe Wenye Kufurahisha na Kunufaisha

Tunaweza kufanya nini ili tufurahie zaidi kujifunza Biblia? Tunaweza jinsi gani kuufanya wakati wetu wa kujifunza uwe wenye manufaa? Acheni tufikirie kwa ufupi hatua tatu zinazoweza kutusaidia kunufaika kabisa tunapojifunza Biblia kibinafsi.

1 SALI: Jambo la kwanza la kufanya kabla ya kuanza kujifunza ni kusali. (Zab. 42:8) Kwa nini? Tunapaswa kuona funzo la Neno la Mungu kuwa sehemu ya ibada yetu. Hivyo, tunapaswa kumwomba Yehova atusaidie kufungua akili na mioyo yetu na kutupatia roho yake takatifu. (Luka 11:13) Barbara, ambaye ni mmishonari aliyetumikia kwa muda mrefu anasema hivi: “Siku zote mimi husali kabla ya kusoma au kujifunza Biblia. Baada ya kufanya hivyo, mimi huhisi kwamba Yehova yupo pamoja nami na kwamba anapendezwa na jambo ninalofanya.” Kusali kabla ya kuanza kujifunza kunatufungua akili na mioyo ili tupokee kwa ukamili chakula kingi cha kiroho kilicho mbele yetu.

2 TAFAKARI: Kwa sababu ya kukosa wakati, wengine husoma Neno la Mungu kijuu-juu tu. Hata hivyo, watu hao hukosa faida ambazo wangepata kutokana na kujifunza Biblia. Carlos, ambaye amekuwa akimtumikia Yehova kwa miaka zaidi ya 50, amekuja kutambua umuhimu wa kutenga wakati ili kutafakari na kufanya funzo lake liwe lenye manufaa hata zaidi. Anasema hivi: “Sasa mimi husoma kurasa chache sana za Biblia kwa wakati mmoja—karibu kurasa mbili kila siku. Hivyo, ninaweza kutumia wakati mwingi hata zaidi kutafakari yale ambayo nimesoma ili kujifunza masomo muhimu.” (Zab. 77:12) Tunapotenga wakati ili kutafakari, tunaboresha ujuzi na ufahamu wa mapenzi ya Mungu.​—Kol. 1:9-11.

3 TUMIA MAMBO UNAYOJIFUNZA: Tunapoona thamani ya jambo fulani tunalofanya, tunanufaika hata zaidi kutokana na jambo hilo. Hilo ni kweli kuhusiana na funzo la Biblia. Gabriel, ndugu aliye na zoea la kujifunza Biblia kwa kawaida anasema hivi: “Funzo linanisaidia kukabiliana na matatizo ya kila siku ya maisha na kunitayarisha ili niweze kuwasaidia wengine.” Anaongeza hivi: “Mimi hujaribu kutumia katika maisha yangu kila jambo ninalojifunza.” (Kum. 11:18; Yos. 1:8) Ndiyo, kuna ujuzi mwingi wa Mungu ambao tunaweza kujifunza na kuutumia maishani mwetu.​—Met. 2:1-5.

MUHTASARI: Tumependelewa kama nini kuchunguza kwa undani ujuzi ulioandaliwa na Yehova, Chanzo cha hekima yote! (Rom. 11:33) Hivyo basi, wakati mwingine kabla ya kuanza kujifunza anza kwa sala ili kumwomba Yehova afungue akili na moyo wako na pia akupatie roho yake takatifu. Kisha, nyakati fulani tua ili utafakari mambo unayojifunza. Pia, endelea kufikiria na kutumia katika maisha yako ya kila siku mambo ambayo umejifunza. Unapochukua hatua hizo muhimu, utaona kuwa funzo lako la Biblia ni lenye kufurahisha na lenye manufaa zaidi.