Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

NI NINI kilichomchochea mkulima wa tumbaku abadili kazi yake na pia imani yake ya kidini aliyokuwa ameshikilia kwelikweli? Mwanamke aliyekuwa na zoea la kunywa pombe kupita kiasi alipataje nguvu za kubadili maisha yake? Soma mambo ambayo watu hawa wanasema.

“Ninafurahia Kuwa Sehemu ya Familia Hii Kubwa.”​—DINO ALI

MWAKA WA KUZALIWA: 1949

NCHI: AUSTRALIA

HISTORIA: MKULIMA WA TUMBAKU

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Mnamo 1939 wazazi wangu walihama Albania na kwenda Mareeba, mji mdogo ulio Queensland, Australia. Pia, watu wengi kutoka Bosnia, Italia, Serbia, Ugiriki, na nchi nyinginezo walihamia eneo hilo na walikuwa na imani, tamaduni, na desturi mbalimbali. Tumbaku ilikuzwa katika eneo hilo la Mareeba, na wazazi wangu walianza kukuza mmea huo.

Muda mfupi baadaye, dada yangu mkubwa alizaliwa na kufuatiwa na kaka zangu wawili, kisha mimi nikazaliwa. Kwa kusikitisha, Baba alikufa nilipokuwa na umri wa mwaka mmoja. Mama aliolewa tena na kupata wavulana wengine wanne. Sote tulilelewa katika shamba la tumbaku la baba yangu wa kambo.

Niliondoka nyumbani nilipokuwa tineja. Nikiwa na miaka 20 hivi, nilimwoa Saime katika msikiti uliokuwa katika eneo letu kwa sababu sote tulikuwa Waislamu. Watu wangu wote wa ukoo walikuwa Waislamu. Nilisoma Kurani na kitabu cha historia ya nabii Muhammad. Wakati huohuo, pia nilisoma Biblia ndogo. Kurani inataja manabii fulani ambao pia wanatajwa katika Biblia, na kusoma Biblia kulinisaidia kujua wakati walioishi.

Mashahidi wa Yehova walitutembelea nyumbani na mara kwa mara walituachia magazeti na vitabu, ambavyo mimi na Saime tulifurahia kusoma. Ninakumbuka tukiwa na mazungumzo mengi yenye kuchochea pamoja na Mashahidi kuhusu mambo mbalimbali ya kidini. Kila mara walipojibu maswali yangu walitumia Biblia badala ya kutoa maoni yao ya kibinafsi. Jambo hilo lilinigusa moyo sana.

Mashahidi walitaka kujifunza Biblia pamoja nami na hata walinikaribisha kwenye mikutano yao, lakini nyakati zote nilikataa. Wakati huo lengo langu kuu lilikuwa kupata shamba langu mwenyewe na kuwa na familia kubwa. Sikuwahi kumiliki shamba, lakini mwishowe nilikuja kuwa baba ya watoto watano ninaowapenda sana.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Miaka tisa baada ya kukutana na Mashahidi wa Yehova, bado nilikuwa Mwislamu. Hata hivyo, nilifurahia kupokea na kusoma machapisho yao yote. Kila Jumapili, mimi na Saime tulitenga wakati wa kusoma machapisho hayo. Tulihifadhi magazeti yote ambayo tulikuwa tumepokea kwa miaka hiyo yote. Magazeti hayo yalikuwa na habari muhimu zilizonisaidia sana wakati wengine walipoanza kujaribu imani yangu.

Kwa mfano, nilikutana na mhubiri fulani wa kanisa la kiinjilisti aliyejaribu kunilazimisha nimkubali Yesu kuwa Mwokozi wangu. Alikuwa amefaulu kumshawishi ndugu ya Saime na mmoja wa ndugu zangu wa kambo wamfuate. Muda mfupi baadaye, marafiki zangu kutoka dini tofauti-tofauti walianza kunishawishi nijiunge na vikundi vyao vya kidini. Baadhi yao walinipa machapisho yaliyowashutumu Mashahidi wa Yehova. Niliwaomba watu hao wanionyeshe katika Biblia msingi wa mafundisho yao, lakini wakashindwa.

Upinzani huo wote ulifanya niichunguze Biblia kwa undani na kufanya utafiti zaidi nikitumia machapisho niliyokuwa nimepewa na Mashahidi. Mwishowe, nilitambua kwamba nilipaswa kufanya uamuzi wa kuishi kupatana na mambo niliyokuwa nikijifunza.

Sikuwa nikijifunza Biblia na Shahidi yeyote; nilianza tu kuhudhuria mikutano yao. Mwanzoni, nilikuwa mwenye haya na wasiwasi, lakini nilipata marafiki wengi kwenye mikutano hiyo, na nilifurahia mambo niliyojifunza. Niliazimia kuwa Shahidi wa Yehova, na katika mwaka wa 1981, nilionyesha nimejiweka wakfu ili kumtumikia Mungu kwa kubatizwa.

Mke wangu hakupinga uamuzi wangu lakini wakati fulani alifikiri kwamba nilikuwa nikidanganywa. Lakini bado alikuwepo wakati nilipobatizwa. Niliendelea kumweleza kuhusu mambo mengi ya kweli niliyokuwa nikijifunza. Mwaka mmoja baada ya ubatizo wangu, tulipokuwa ndani ya gari tukirudi nyumbani baada ya likizo, Saime aliniambia kwamba anataka kuwa Shahidi. Nilishtuka sana hivi kwamba karibu nishindwe kulidhibiti gari barabarani! Alibatizwa mwaka wa 1982.

Halikuwa jambo rahisi kubadili maisha yetu. Nilikuwa nimeacha kazi ya kukuza tumbaku kwa sababu ilipingana na kanuni za Biblia. (2 Wakorintho 7:1; Yakobo 2:8) Muda fulani ulipita kabla hatujapata kazi ambayo ingetosheleza mahitaji yetu. Pia, kwa miaka mingi baadaye, watu fulani wa ukoo walikataa kututembelea. Tulijaribu kuwatendea kupatana na kanuni za Biblia kwa kuwaonyesha upendo. Mwishowe, walibadili maoni yao na sasa wanatutembelea.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Magumu mengi niliyopitia, kwa mfano kuacha kuwa na haya, kukabiliana na mahangaiko ya kifedha, au kukabiliana na upinzani kutoka kwa watu wa familia, yamenisaidia kuelewa jinsi Yehova Mungu alivyo na subira anaponisaidia kukabiliana na matatizo. Kwa mfano, sasa ninatumika nikiwa mzee wa kutaniko na mara nyingi lazima nifundishe nikiwa jukwaani. Bado jambo hilo ni gumu kwangu kwa sababu ninapatwa na kigugumizi ninapokuwa na wasiwasi. Lakini kwa kuendelea kusali na kupitia msaada wa Yehova, sasa ninafaulu kutimiza majukumu yangu.

Mimi na mke wangu tumekuwa na uhusiano wa karibu zaidi, na sasa tunafurahia sana ndoa yetu. Tulifanya makosa fulani tulipokuwa tukiwalea watoto wetu lakini tulijaribu tuwezavyo kukazia ndani yao kweli za Biblia tulizojifunza. (Kumbukumbu la Torati 6:6-9) Mwanangu wa kwanza sasa anatumika na mke wake wakiwa wamishonari.

Ninakumbuka jambo fulani lililotukia muda mfupi baada ya kuanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi tukiwa familia. Niliegesha gari na kuangalia ndani ya jumba na nikaona watu waliokuwa wamekusanyika ndani. Nikauliza familia yangu, “Mnaona nini?” Ndani ya jumba kulikuwa na watu wa jamii, malezi, na lugha mbalimbali—Waaborijini, Waalbania, Waaustralia, Wakroatia—na wote walikuwa wakichangamana kwa furaha. Ninafurahia kuwa sehemu ya familia hii kubwa ya ndugu na dada wa kiroho, ambayo inapatikana Australia na kotekote duniani.—1 Petro 5:9.

“Dada Yangu Hakuchoka Kunisaidia.”​—YELENA VLADIMIROVNA SYOMINA

MWAKA WA KUZALIWA: 1952

NCHI: URUSI

HISTORIA: ALIKUWA NA ZOEA LA KUNYWA POMBE KUPITA KIASI NA ALIJARIBU KUJIUA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa Krasnogorsk, jiji dogo, lenye amani lililo karibu na Moscow. Wazazi wangu walikuwa walimu wa shule. Nilikuwa mwanafunzi mwenye bidii na nilijifunza somo la muziki. Ilionekana kwamba ningekuwa na wakati ujao mzuri.

Nilipoolewa, mimi na mume wangu tulihamia eneo ambalo watu walizoea kutumia maneno machafu, kulewa, na kuvuta sigara. Wakati huo sikutambua kwamba mazingira hayo yangeniathiri. Mwanzoni, nilihudhuria sherehe mbalimbali nikiwa na kusudi la kuimba tu au kucheza gitaa. Hata hivyo, nilipokuwa huko, watu walinialika nivute sigara na kunywa pombe pamoja nao. Muda mfupi baadaye nikawa na zoea la kunywa kupita kiasi.

Zoea hilo likaanza kuharibu maisha yangu. Muda fulani ulipita kabla hali hiyo kunilemea, lakini nilipolemewa kabisa na zoea hilo, hata sikuweza kula chochote. Nilitamani kufa, na hata nilijaribu kujiua. Ninashukuru kwamba sikufaulu kujiua.

Nilipokuwa nikikabiliana na hali hiyo, dada yangu alinitembelea mara kwa mara. Alikuwa amejifunza na kuwa Shahidi wa Yehova, na alijaribu kunieleza jinsi Biblia inavyoweza kunisaidia. Sikupendezwa na Biblia, kwa hiyo, mwanzoni nilimfukuza. Lakini dada yangu hakuchoka kunisaidia. Alinitendea kwa upendo na kunionyesha subira sana hivi kwamba mwishowe nikakubali kujifunza Biblia.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Baada ya kuanza kujifunza Biblia, niliazimia kabisa kuacha kunywa pombe. Karibu na wakati huo, jirani yangu mmoja aliyekuwa amelewa alinishambulia na kunipiga. Nilipelekwa hospitalini nikiwa mahututi. Mbavu zangu nne zilikuwa zimevunjika na jicho langu moja lilikuwa limeumizwa vibaya. Hata hivyo, kukaa hospitalini kulinisaidia kukabiliana na athari zinazotokana na kuacha pombe.

Wakati huo, nilisali kwa ukawaida. Nilifarijiwa sana na andiko la Maombolezo 3:55, 56, linalosema: “Nimeita jina lako, Ee Yehova, kutoka katika shimo la chini kabisa. Uisikilize sauti yangu. Usifiche sikio lako kwa ombi langu la kitulizo, kwa kilio changu cha kuomba msaada.”

Ninaamini kabisa kwamba Yehova alijibu sala zangu. Alinitia nguvu ili nisirudie hali yangu ya zamani. Kuna nyakati ambazo nilishawishiwa kuanza kunywa pombe tena. Ninafurahi kwamba sikulemewa na kishawishi hicho.

Nilipoendelea kujifunza Biblia, nilitambua kwamba nilihitaji kumuunga mkono mume wangu kutimiza jukumu lake akiwa kichwa cha familia. (1 Petro 3:1, 2) Haikuwa rahisi kwangu kufanya hivyo kwa sababu nilikuwa nimezoea kumwongoza. Nilisali kwa Yehova ili anisaidie. Sikubadilika kwa siku moja tu, lakini polepole nikawa mtu mzuri, na mke anayemuunga mkono zaidi mume wake.

Mume wangu mpendwa alipoona mabadiliko hayo, alishangaa sana. Kufikia wakati huo, hakupendezwa na Biblia. Lakini wakati nilipoamua kuacha kuvuta sigara, alisema hivi: “Ikiwa utaacha kuvuta sigara, basi nitaanza kujifunza Biblia!” Tuliacha kuvuta sigara wakati uleule.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Mume wangu alitimiza ahadi yake na akaanza kujifunza Biblia. Sasa tunasoma Biblia pamoja kila siku, kutafakari mambo tunayosoma, na kujitahidi kufuata mashauri yake katika maisha yetu.

Kwa kweli, maisha ya familia yetu yamekuwa bora sana, na vilevile mimi mwenyewe nimefaidika sana. Ninamshukuru Yehova kwa kunivuta kwake. (Yohana 6:44) Pia, ninamshukuru dada yangu ambaye hakuchoka kunisaidia. Kwa kweli, nimejionea mwenyewe jinsi Biblia inavyobadili maisha.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Nilitambua kwamba nilipaswa kufanya uamuzi

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Dada yangu alinitendea kwa upendo na kunionyesha subira sana hivi kwamba mwishowe nikakubali kujifunza Biblia