Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kupata Furaha Katika Familia Iliyogawanyika

Unaweza Kupata Furaha Katika Familia Iliyogawanyika

Unaweza Kupata Furaha Katika Familia Iliyogawanyika

“Unajuaje kama utamwokoa [mwenzi] wako?”—1 KOR. 7:16.

JE, UNAWEZA KUPATA MAJIBU?

Watu ambao ni waamini wanaweza kufanya nini ili kusitawisha amani katika familia iliyogawanyika kidini?

Mkristo anaweza kuwasaidiaje washiriki wa familia yake wasio waamini ili wakubali ibada ya kweli?

Wengine wanaweza kuwasaidiaje waamini wenzao ambao wako katika familia iliyogawanyika kidini?

1. Kukubali ujumbe wa Ufalme kunaweza kuwa na matokeo gani katika familia?

PINDI moja Yesu alipowatuma mitume wake, alisema hivi: “Mnapoenda, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:1, 7) Habari hiyo njema ingewaletea amani na furaha wale ambao wangeikubali na kuithamini kikweli. Hata hivyo, Yesu aliwaonya mitume wake kwamba watu wengi wangeipinga kazi yao ya kuhubiri kuhusu Ufalme. (Mt. 10:16-23) Mtu anakabili upinzani wenye kuumiza zaidi wakati watu wa familia wanapokataa ujumbe wa Ufalme.—Soma Mathayo 10:34-36.

2. Kwa nini Wakristo wanaoishi katika familia zilizogawanyika kidini wanaweza kupata furaha?

2 Je, hilo linamaanisha kwamba wafuasi wa Kristo ambao wanaishi katika familia zilizogawanyika kidini hawawezi kupata furaha? Hapana! Ingawa nyakati fulani upinzani wa familia unaweza kuwa mkali, lakini haiwi hivyo nyakati zote. Pia, huenda upinzani wa familia usiendelee kwa muda mrefu. Inategemea hasa jinsi washiriki wa familia ambao ni waamini wanavyokabiliana na upinzani au ubaridi kuelekea kweli. Isitoshe, Yehova anawabariki wale ambao ni washikamanifu kwake, na kuwafanya wawe wenye shangwe licha ya hali ngumu. Wale ambao ni waamini wanaweza kuongeza shangwe yao (1) kwa kujitahidi kusitawisha amani nyumbani na (2) kwa kujaribu kwa unyoofu kuwasaidia washiriki wa familia ambao si waamini wakubali ibada ya kweli.

SITAWISHA AMANI NYUMBANI

3. Kwa nini Mkristo aliye katika familia iliyogawanyika kidini anapaswa kusitawisha amani?

3 Ili mbegu ya uadilifu izae matunda katika mazingira ya familia, ni muhimu kuwe na hali zenye amani nyumbani. (Soma Yakobo 3:18.) Hata ikiwa familia ya Mkristo bado haijaungana katika ibada safi, ni lazima ajitahidi kabisa kusitawisha amani nyumbani. Anaweza kufanya hivyo jinsi gani?

4. Wakristo wanaweza jinsi gani kudumisha amani yao ya akili?

4 Ni lazima Wakristo wadumishe amani yao ya akili. Ili tufanye hivyo, tunahitaji kusali kutoka moyoni na hivyo kupata “amani ya Mungu” isiyo na kifani. (Flp. 4:6, 7) Furaha na amani inatokana na kuendelea kupata ujuzi kumhusu Yehova na kutumia kanuni za Kimaandiko maishani. (Isa. 54:13) Ili tupate amani na furaha ni muhimu pia tushiriki katika mikutano ya kutaniko na kushiriki kwa bidii katika huduma ya shambani. Kwa ujumla, waamini ambao wanaishi katika familia zilizogawanyika kidini wanaweza kushiriki katika utendaji wa Kikristo kwa njia fulani. Kwa mfano, mfikirie Enza, * ambaye mume wake anampinga kijeuri. Anashiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi baada ya kufanya kazi zake za nyumbani. Enza anasema hivi: “Kila mara ninapojitahidi kuwahubiria wengine habari njema, Yehova ananibariki sana kwa kuniwezesha kupata matokeo mazuri.” Bila shaka, baraka kama hizo zinaleta amani, uradhi, na furaha.

5. Kwa kawaida waamini ambao wako katika familia zilizogawanyika kidini wanakabili tatizo gani, na wanaweza kupata wapi msaada?

5 Tunahitaji kujitahidi sana kusitawisha uhusiano wenye amani na washiriki wa familia ambao si waamini. Huenda ikawa vigumu kufanya hivyo kwa sababu nyakati nyingine mambo ambayo wanataka tufanye labda yanapingana na kanuni za Biblia. Washiriki fulani wa familia ambao si waamini wanaweza kukasirika tunaposhikilia kwa uthabiti kanuni zinazofaa, lakini mwishowe msimamo huo unadumisha amani. Bila shaka, kushikilia sana maoni yetu wakati ambapo jambo halipingani na kanuni za Kimaandiko kunaweza kusababisha ugomvi usio wa lazima. (Soma Methali 16:7.) Unapokabili tatizo, ni muhimu kutafuta mashauri ya Kimaandiko kutoka katika machapisho ya jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara na kutoka kwa wazee.—Met. 11:14.

6, 7. (a) Kwa nini watu fulani wanawapinga washiriki wao wa familia ambao wanaanza kujifunza na Mashahidi wa Yehova? (b) Mwanafunzi wa Biblia au mwamini anapaswa kukabilianaje na upinzani wa familia?

6 Ili kusitawisha amani katika familia tunahitaji kumtegemea Yehova na kufahamu hisia za washiriki wa familia ambao si waamini. (Met. 16:20) Hata wanafunzi wapya wa Biblia wanaweza kuonyesha utambuzi katika jambo hilo. Waume au wake fulani ambao si waamini huenda wasiwakataze wenzi wao wa ndoa kujifunza Biblia. Huenda hata wakakiri kwamba kufanya hivyo kunaweza kuinufaisha familia. Lakini huenda wengine wakaonyesha uadui. Esther, ambaye sasa ni Shahidi, anakiri kwamba alitenda kwa “hasira” wakati mume wake alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Nilikuwa nikitupa vitabu vyake au kuviteketeza.” Howard, ambaye mwanzoni alimpinga mke wake alipoanza kujifunza Biblia, anasema hivi: “Waume wengi wanaogopa kwamba wake zao wanadanganywa ili wajiunge na dhehebu la kidini. Huenda mume asijue jinsi ya kukabiliana na hali hiyo inayoonekana kuwa hatari na hivyo anaweza kumpinga vikali.”

7 Mwanafunzi wa Biblia ambaye mwenzi wake wa ndoa anampinga anapaswa kusaidiwa kuona kwamba si lazima aache kujifunza Biblia. Kwa kawaida, ataweza kusuluhisha matatizo akiwa mwenye tabia-pole na kumheshimu mwenzi wake wa ndoa ambaye si mwamini. (1 Pet. 3:15) Howard anasema hivi: “Ninashukuru sana kwamba mke wangu alibaki mtulivu na hakutenda kwa hasira!” Mke wake anaeleza hivi: “Howard aliniambia kwa ukali niache kujifunza Biblia. Alisema kwamba nilikuwa nikipumbazwa akili. Badala ya kubishana naye, nilimwambia kwamba huenda anasema kweli, lakini pia nilimwambia kuwa kwa hakika sijaona wakinidanganya. Hivyo, nilimwomba asome kitabu nilichokuwa nikijifunza. Alikisoma na hakupinga mambo ambayo kilisema. Mambo hayo yalimgusa moyo sana.” Ni vizuri kukumbuka kwamba huenda wenzi wa ndoa ambao si waamini wakahisi upweke au wakafikiri kwamba ndoa yao iko hatarini wakati mwenzi wao anapoenda kushiriki katika utendaji wa Kikristo, lakini mwenzi ambaye ni mwamini akimhakikishia kwamba anampenda anaweza kusaidia sana kuondoa wasiwasi huo.

WASAIDIE WAKUBALI IBADA YA KWELI

8. Ni shauri gani ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo ambao wana wenzi wa ndoa ambao si waamini?

8 Mtume Paulo anawashauri Wakristo wasimwache mwenzi wao wa ndoa eti kwa sababu mwenzi huyo si mwamini. * (Soma 1 Wakorintho 7:12-16.) Kukumbuka kwamba mwenzi wa ndoa ambaye si mwamini anaweza kuwa Mkristo kunaweza kumsaidia mwenzi ambaye ni mwamini kudumisha furaha yake hata ingawa anaishi katika familia iliyogawanyika kidini. Hata hivyo, anapojaribu kuzungumza na mwenzi asiye mwamini ujumbe wa kweli, anapaswa kuzingatia tahadhari fulani, kama mambo yafuatayo yaliyoonwa yanavyoonyesha.

9. Unapowahubiria kweli ya Biblia washiriki wa familia ambao si waamini, unapaswa kuzingatia tahadhari gani?

9 Akitafakari kuhusu jinsi alivyotenda baada ya kujifunza kweli ya Biblia, Jason anasema hivi: “Nilitaka kumwambia kila mtu!” Mwanafunzi wa Biblia anapoona kwamba mambo ambayo amefundishwa kutoka katika Maandiko ni ya kweli, anaweza kufurahi sana hivi kwamba anazungumza kuhusu mambo hayo karibu kila wakati. Huenda akatarajia washiriki wa familia ambao si waamini wakubali ujumbe wa Ufalme papo hapo, lakini wanaweza kukataa habari njema. Msisimko ambao Jason alikuwa nao mwanzoni ulimwathirije mke wake? Mke wake anasema hivi: “Alinichosha sana kwa kunihubiria kila wakati.” Mwanamke fulani ambaye alikubali kweli miaka 18 baada ya mume wake kuikubali anasema hivi: “Kwanza, mimi nilihitaji kujifunza kweli hatua kwa hatua.” Ikiwa kwa sasa unajifunza Biblia na mwanafunzi ambaye mwenzi wake wa ndoa hapendi kushiriki katika ibada ya kweli, kwa nini msiwe na vipindi vya kawaida vya mazoezi ili kumsaidia mwanafunzi huyo kushughulikia mambo kwa busara? Musa alisema hivi: “Mafundisho yangu yatatiririka kama mvua, maneno yangu yatadondoka kama umande, kama mvua ya rasharasha juu ya majani.” (Kum. 32:2) Kwa kawaida, maneno machache ya kweli yanayosemwa kwa njia inayofaa na wakati unaofaa kama matone ya mvua yatakuwa na matokeo mazuri zaidi kuliko gharika ya maneno.

10-12. (a) Ni shauri gani ambalo mtume Petro aliwapa Wakristo wenye wenzi wa ndoa ambao si waamini? (b) Mwanafunzi mmoja wa Biblia alijifunza jinsi gani kufuata shauri la 1 Petro 3:1, 2?

10 Mtume Petro alitoa shauri lililoongozwa na roho ya Mungu kwa wake Wakristo walio katika familia zilizogawanyika kidini. Aliandika hivi: “Jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:1, 2) Mke anaweza kumshawishi mume wake ajiunge na ibada ya kweli kwa kujitiisha kwake na kumheshimu sana, hata ikiwa anamtendea kwa ukali. Vivyo hivyo, mume ambaye ni mwamini anapaswa kujiendesha kwa njia inayompendeza Mungu na kuwa kichwa cha familia mwenye upendo licha ya upinzani wowote ambao anaweza kupata kutoka kwa mke wake ambaye si mwamini.—1 Pet. 3:7-9.

11 Mifano mingi leo inaonyesha umuhimu wa kufuata shauri la Petro. Fikiria mfano wa Selma. Alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, mume wake, Steve, hakufurahia. Mume wake anakiri hivi: “Nilikasirika, nikawa na wivu, nikamnyima uhuru nikiogopa kwamba ataniacha.” Selma anasema hivi: “Hata kabla sijapata kweli, haikuwa rahisi kuishi na Steve. Alikuwa na hasira kali. Nilipoanza kujifunza Biblia, hasira yake iliongezeka.” Ni nini kilichosaidia?

12 Selma anakumbuka somo ambalo alijifunza kutoka kwa Shahidi aliyemfundisha Biblia. Selma anasema, “Siku moja, sikutaka kujifunza Biblia. Usiku uliotangulia, Steve alinipiga nilipojaribu kumthibitishia jambo fulani, na nilihuzunika na kujisikitikia. Baada ya kumwambia dada huyo jambo lililotukia na jinsi nilivyohisi, aliniomba nisome andiko la 1 Wakorintho 13:4-7. Nilipokuwa nikilisoma, nilianza kusema, ‘Steve hanitendei kamwe jambo lolote kati ya mambo haya yanayoonyesha upendo.’ Lakini dada huyo akanisaidia kufikiri kwa njia tofauti kwa kuniuliza, ‘Ni mambo mangapi kati ya mambo haya yanayoonyesha upendo ambayo wewe unamtendea mume wako?’ Nilimjibu hivi: ‘Hakuna, kwa kuwa ni vigumu sana kuishi naye.’ Dada huyo akasema hivi kwa upole, ‘Selma, ni nani anayejaribu kuwa Mkristo kati yenu? Ni wewe au ni Steve?’ Nilipotambua kwamba nilihitaji kubadili njia yangu ya kufikiri, nilisali kwa Yehova ili anisaidie kumtendea Steve kwa njia ya upendo zaidi. Pole kwa pole, mambo yakaanza kubadilika.” Baada ya miaka 17, Steve alikubali kweli.

JINSI WENGINE WANAVYOWEZA KUSAIDIA

13, 14. Wengine katika kutaniko wanaweza kuwasaidiaje wale wanaoishi katika familia iliyogawanyika kidini?

13 Kama matone ya mvua yanayoanguka taratibu na kulowesha udongo na kuifanya mimea ikue, ndivyo mtu mmoja-mmoja katika kutaniko anavyochangia furaha ya Wakristo walio katika familia zilizogawanyika kidini. Elvina anayeishi Brazili anasema hivi: “Upendo wa ndugu na dada zangu ndio ulionisaidia kusimama imara katika kweli.”

14 Wengine katika kutaniko wanapoonyesha fadhili na upendezi wa kibinafsi wanaweza kuugusa sana moyo wa mshiriki wa familia ambaye si mwamini. Mume fulani nchini Nigeria ambaye alikubali kweli miaka 13 baada ya mke wake kuukubali anasema hivi: “Nilipokuwa nikisafiri na Shahidi mmoja, gari lake liliharibika. Aliwatafuta Mashahidi wengine katika kijiji cha karibu, nao wakatupatia mahali pa kulala usiku huo. Walitutunza kana kwamba tulifahamiana tangu utotoni. Mara moja, niliona upendo wa Kikristo ambao mke wangu alikuwa akizungumzia sikuzote.” Huko Uingereza, mke ambaye alikubali kweli miaka 18 baada ya mume wake anakumbuka hivi: “Mashahidi walitualika sote wawili kwa ajili ya chakula. Sikuzote walinifanya nihisi nimekaribishwa.” * Mume mwingine katika nchi hiyo ambaye mwishowe alikuja kuwa Shahidi anasema: “Akina ndugu na dada walikuwa wakitutembelea, au walitualika katika nyumba zao, na niligundua kwamba wanajali. Hilo lilionekana wazi hasa nilipokuwa nimelazwa hospitalini, wengi wao walikuja kunitembelea.” Je, unaweza kutafuta njia za kupendezwa vivyo hivyo na familia za wale ambao wako peke yao katika kweli?

15, 16. Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu ambaye ni mwamini kudumisha furaha wakati washiriki wengine wa familia yake wanapoendelea kuwa wasioamini?

15 Bila shaka, si wenzi wote wasioamini, watoto, wazazi, au watu wengine wote wa ukoo wanaokubali kweli, hata baada ya yule ambaye ni mwamini kutoa ushahidi kwa busara na kujiendesha kwa uaminifu kwa miaka mingi. Wengine wao wanaendelea kuipinga kweli au kutopendezwa nayo. (Mt. 10:35-37) Hata hivyo, Wakristo wanapoonyesha sifa zinazompendeza Mungu, matokeo yanaweza kuwa mazuri sana. Mume mmoja ambaye zamani hakuwa mwamini alisema hivi: “Mwenzi wa ndoa ambaye ni mwamini anapoanza kuonyesha sifa hizo nzuri, hujui zitagusa jinsi gani akili na moyo wa mwenzi asiye mwamini. Basi usikate tamaa kamwe unaposhughulika na mwenzi wako asiye mwamini.”

16 Hata ikiwa mshiriki wa familia si mwamini, yule mwamini bado anaweza kuwa mwenye furaha. Ingawa dada mmoja amejitahidi kwa miaka 21 kumhubiria mume wake, hata hivyo, mume huyo hajakubali ujumbe wa Ufalme. Dada huyo anasema hivi: “Ninadumisha shangwe yangu kwa kujitahidi kumpendeza Yehova, kwa kuendelea kuwa mshikamanifu kwake, na kujitahidi kuimarisha hali yangu ya kiroho. Kujishughulisha sana na utendaji wa kiroho kama vile kujifunza kibinafsi, kuhudhuria mikutano, huduma ya shambani, na kuwasaidia wengine katika kutaniko, kumenisaidia kumkaribia Yehova zaidi na kumeulinda moyo wangu.”—Met. 4:23.

USIKATE TAMAA!

17, 18. Mkristo anaweza jinsi gani kuwa na tumaini hata katika familia iliyogawanyika kidini?

17 Ikiwa wewe ni Mkristo mwaminifu na unaishi katika familia iliyogawanyika kidini, usikate tamaa. Kumbuka kwamba “Yehova hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.” (1 Sam. 12:22) Atakuwa pamoja nawe maadamu unaendelea kushikamana naye. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 15:2.) Kwa hiyo, ‘pata furaha tele katika Yehova.’ Naam, ‘mkabidhi Yehova njia yako, na kumtegemea.’ (Zab. 37:4, 5) ‘Dumu katika sala,’ na uwe na imani kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anaweza kukusaidia kuvumilia matatizo ya kila aina.—Rom. 12:12.

18 Mwombe Yehova kwa bidii ili akupe roho yake takatifu ili ikusaidie kudumisha amani nyumbani. (Ebr. 12:14) Naam, inawezekana kusitawisha hali zenye amani ambazo huenda mwishowe zitawagusa moyo washiriki wa familia ambao si waamini. Utapata furaha na amani ya moyo na akili ‘unapofanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’ (1 Kor. 10:31) Unapofanya jitihada hizo, inatia moyo kama nini kujua kwamba unaungwa mkono kwa upendo na ndugu na dada zako katika kutaniko la Kikristo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 8 Shauri la Paulo halimaanishi kwamba wenzi wa ndoa hawawezi kutengana kisheria hali zinapokuwa mbaya zaidi katika ndoa. Huo ni uamuzi mzito wa kibinafsi. Ona kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” ukurasa wa 220-221.

^ fu. 14 Maandiko hayakatazi kula na watu ambao si waamini.—1 Kor. 10:27.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Chagua wakati unaofaa wa kueleza imani yako

[Picha katika ukurasa wa 29]

Onyesha kwamba unawajali wenzi wa ndoa wasio waamini