Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kuwa na Furaha Katika Familia Inayogawanyika Kidini

Kuwa na Furaha Katika Familia Inayogawanyika Kidini

Kuwa na Furaha Katika Familia Inayogawanyika Kidini

“Unajuaje kama utamwokoa [bwana yako ao bibi yako]?”​—1 KOR. 7:16.

JE, UNAWEZA KUJIBU?

Wakristo wanaweza kufanya nini ili kuishi kwa amani pamoja na wengine katika familia inayogawanyika kidini?

Namna gani Mukristo anaweza kuwasaidia washiriki wengine wa familia wakubali kweli?

Wengine katika kutaniko wanaweza kufanya nini ili kusaidia Wakristo wenzao wanaoishi katika familia inayogawanyika kidini?

1. Mutu anapokubali ujumbe wa Ufalme, washiriki wengine wa familia wanaweza kumutendea namna gani?

 SIKU moja, Yesu alipowatuma mitume wake, aliwaambia: “Munapoenda, hubirini, mukisema, ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:1, 7) Habari njema hiyo ingewaletea amani na furaha wale walioikubali kweli kweli. Hata hivyo, Yesu aliwaambia mitume wake kwamba watu wengi wangepinga kazi yao ya kuhubiri Ufalme. (Mt. 10:16-23) Wakati washiriki fulani wa familia wanapinga ujumbe wa Ufalme jambo hilo linatokeza magumu sana.​—Soma Mathayo 10:34-36.

2. Kwa nini Wakristo wanaoishi katika familia zinazogawanyika kidini wanaweza pia kuwa wenye furaha?

2 Je, hilo linamaanisha kwamba Wakristo wanaoishi katika familia zinazogawanyika kidini hawawezi kuwa wenye furaha? Sivyo! Ijapokuwa wakati fulani upinzani wa familia unaweza kuwa mukali, si kila familia inayojiendesha hivyo. Pia upinzani katika familia unaweza kuwa wa muda fulani tu. Mengi yanategemea jinsi Mukristo atakavyojiendesha wakati washiriki wengine wa familia wanapomupinga ao hawaonyeshi kupendezwa na kweli. Zaidi ya hilo, Yehova anawabariki wale walio washikamanifu kwake, na anawafanya wawe wenye furaha, ijapokuwa wanapambana na hali ngumu. Mukristo anayepambana na upinzani anaweza kuongeza furaha yake (1) kwa kujikaza sana kuishi na wengine katika familia kwa amani na (2) kwa kuwasaidia kwa moyo wote washiriki wengine wa familia waikubali ile kweli.

UISHI NA WENGINE KATIKA FAMILIA KWA AMANI

3. Kwa nini Mukristo aliye katika familia inayogawanyika kidini anapaswa kujikaza kuishi pamoja na wengine kwa amani?

3 Ili ile mbegu ya uadilifu izae matunda katika familia yetu, amani ni ya lazima sana. (Soma Yakobo 3:18.) Hata ikiwa familia yote haijaungana katika ibada safi, yule aliye Mukristo anapaswa kujikaza ili kuishi pamoja na wengine katika familia kwa amani. Anaweza kufanya hivyo namna gani?

4. Namna gani Wakristo wanaweza kulinda amani yao ya moyoni?

4 Wakristo wanapaswa kulinda amani yao ya moyoni. Kwa hiyo, sala ya kutoka moyoni inaweza kutuletea “amani ya Mungu” isiyolinganishwa. (Flp. 4:6, 7) Tutakuwa wenye amani na furaha ikiwa tunajifunza kuhusu Yehova na kuishi kulingana na kanuni za Biblia tunazojifunza. (Isa. 54:13) Ni jambo la maana kushiriki mikutano ya kutaniko na kuhubiri kwa bidii ili tuwe wenye amani na furaha. Kwa kawaida, Wakristo wanaoishi katika familia zinazogawanyika kidini wanaweza kupata nafasi ya kushiriki katika utendaji mbalimbali wa Kikristo. Tuchukue mufano wa dada Enza. * Ingawa bwana yake ni mupinzani mukali, dada huyo anashiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi kisha kufanya kazi zake za nyumbani. Dada Enza anasema hivi: “Yehova ananibariki sana, kila wakati ninapojikaza kuwahubiria watu habari njema ninapata matokeo mazuri.” Bila shaka, baraka kama hizo zinamuletea Mukristo amani, kutosheka, na furaha.

5. Wakristo wanaoishi katika familia inayogawanyika kidini wanapata matatizo gani, na wanaweza kupata musaada wapi?

5 Inaomba kwa Mukristo kujikaza sana ili kuishi pamoja na washiriki wa familia yake kwa amani. Hata hivyo, huenda matatizo yakatokea kwa kuwa mambo wanayotaka sisi tufanye yanaweza wakati fulani kupingana na kanuni za Biblia. Kushikamana kwetu na kanuni za Biblia kunaweza kuwakasirisha washiriki wengine wa familia yetu, lakini kuendelea kushikamana na kanuni hizo kutaleta mwishowe amani katika familia. Kwa kweli, ni vizuri kushirikiana na familia yetu wakati hakuna kanuni yoyote ya Biblia inayovunjwa, tusipofanya hivyo, hilo linaweza kutokeza matatizo (Soma Methali 16:7.) Tunapopambana na matatizo, ni jambo la maana kutafuta mashauri ya Biblia katika vichapo vya mutumwa mwaminifu na mwenye busara na kutoka kwa wazee.​—Met. 11:14.

6, 7. (a) Kwa nini watu fulani wanawapinga washiriki wa familia wanaoanza kujifunza na Mashahidi wa Yehova? (b) Namna gani mwanafunzi wa Biblia ao Mukristo anayepingwa na washiriki wa familia anapaswa kujiendesha?

6 Ili kuishi kwa amani katika familia inaomba kumutegemea Yehova na kuwaelewa kabisa washiriki wengine wa familia wasio Wakristo. (Met. 16:20) Hata wale ambao wameanza kujifunza Biblia hivi karibuni wanaweza kujikaza kufanya hivyo. Wanaume fulani wasio Mashahidi wamekubali bibi zao wajifunze Biblia na kuna wanawake fulani wanaofanya hivyo kuhusu bwana zao. Wanaweza hata kusema kwamba hilo linaweza kuwa jambo nzuri kwa familia yao. Lakini, wengine wanaweza kuonyesha upinzani mukali. Ester, ambaye sasa ni Shahidi, anasema kwamba alikuwa akikasirika sana wakati bwana yake alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ester anasema hivi: “Nilikuwa nikitupa ao kuchoma vitabu vyake.” Ndugu Howard, ambaye mwanzoni alimupinga bibi yake alipoanza kujifunza Biblia, anasema hivi: “Wanaume wengi wanaogopa kwamba bibi zao wanadanganywa wanapoingia katika dini fulani. Labda mwanaume hajui jinsi ya kumukataza bibi yake aache kujifunza na kwa hiyo anaweza kuwa mupinzani wake.”

7 Tunapaswa kumusaidia mwanafunzi wa Biblia ambaye anapingwa na mwenzi wake wa ndoa ili aelewe kwamba hapaswi kuacha kujifunza Biblia kwa sababu ya upinzani. Mara nyingi anaweza kutatua tatizo hilo kwa kuwa na tabia pole na kwa kumuheshimu mwenzi wake wa ndoa aliye mupinzani. (1 Pet. 3:15) Ndugu Howard anasema hivi: “Ninashukuru sana kwa kuwa bibi yangu alibaki mwenye kutulia na hakunikasirikia!” Bibi yake anaeleza: “Howard aliniomba niache kujifunza Biblia. Alisema kwamba Mashahidi walikuwa wakinidanganya. Kuliko kubishana naye, nilimuambia kwamba anaweza kuwa na haki, lakini pia nilimuambia kwamba kwa kweli sioni namna gani wanaweza kunidanganya. Basi, nilimuomba asome kitabu nilichokuwa nikijifunza. Alikisoma na hakupinga mambo aliyosoma. Mambo hayo yalimugusa moyo sana.” Ni vizuri kukumbuka kwamba wenzi wa ndoa wasio Wakristo wanaweza kujisikia kuwa pekee yao ao kuwa na woga fulani wakati wenzi wao wa ndoa wanawaacha ili kwenda kwenye mikutano ao katika mahubiri. Kuzungumuza nao kwa upole na kwa upendo kunaweza kuwatuliza.

UWASAIDIE WAKUBALI KWELI

8. Ni shauri gani ambalo mutume Paulo alitolea Wakristo walio na wenzi wasioamini?

8 Mutume Paulo aliwashauri Wakristo kwamba bwana asimuache bibi yake ao bibi asimuache bwana yake kwa kuwa tu ni asiyeamini. * (Soma 1 Wakorintho 7:12-16.) Kukumbuka kwamba kuna uwezekano kwa mwenzi asiyeamini kuwa Mukristo, hilo linaweza kumusaidia mwenzi Mukristo kulinda furaha yake ijapokuwa familia yake ni yenye kugawanyika kidini. Kwa hiyo, Mukristo anapomuhubiria bibi yake ao bwana yake asiye Mukristo, anapaswa kuwa mwangalifu, kama hali zilizo hapa chini zinavyoonyesha.

9. Tunapohubiria washiriki wa familia kweli ya Biblia, kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu?

9 Anapokumbuka jinsi alivyojisikia alipoanza kujifunza kweli ya Biblia, Jason anasema: “Nilitaka kuelezea kila mutu yale niliyojifunza!” Wakati mwanafunzi wa Biblia anapendezwa sana na ukweli wa mambo anayojifunza katika Biblia, anaweza kuwa mwenye furaha sana hivi kwamba atataka azungumuzie watu mambo hayo karibu kila wakati. Anaweza kutazamia kwamba washiriki wa familia watakubali ujumbe wa Ufalme bila kusita, anasahau kwamba wanaweza kumupinga. Bidii ya mwanzo​-mwanzo ya Jason ilikuwa na matokeo gani juu ya bibi yake? Bibi yake anakumbuka: “Kila wakati alikuwa akinihubiria.” Mwanamuke mumoja ambaye alikubali kweli miaka 18 kisha bwana yake kukubali kweli, anasema: “Mimi, nilitaka kujifunza kweli pole pole.” Ikiwa unajifunza na mutu ambaye mwenzi wake hana nia ya kujifunza kweli, kwa nini usimuonyeshe mwanafunzi huyo jinsi anaweza kushugulikia mwenzi wake kwa busara? Musa mutumishi wa Mungu alisema hivi: “Mafundisho yangu yatatiririka kama mvua, maneno yangu yatadondoka kama umande, kama mvua ya rasharasha juu ya majani.” (Kum. 32:2) Maneno machache kuhusu ukweli yanayodondoka kama umande yanaweza kusaidia sana kuliko maneno mengi yaliyo kama maji ya mvua kali yanayomuangika.

10-12. (a) Ni shauri gani ambalo mutume Petro alitolea Wakristo waliokuwa na wenzi wa ndoa wasioamini? (b) Namna gani mwanafunzi mumoja wa Biblia alijifunza kutumia shauri lililo katika 1 Petro 3:1, 2?

10 Mutume Petro alitolea wanawake Wakristo wanaoishi katika familia zinazogawanyika kidini shauri lililoongozwa na roho ya Mungu. Aliandika: “Jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:1, 2) Mwanamuke anaweza kumuvuta bwana yake kwenye ibada ya kweli kwa kujitiisha na kumuheshimu sana, hata ikiwa ni mukali. Vivyo hivyo, mwanaume Mukristo anapaswa kujiendesha kama vile Mungu anavyopenda na kuwa baba anayependa washiriki wa nyumba yake hata ikiwa bibi yake anamupinga.​—1 Pet. 3:7-9.

11 Mifano mingi ya siku zetu inaonyesha faida ya kutumia shauri hilo la Petro. Tufikirie mufano wa dada Selma. Alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, bwana yake Steve, hakufurahi. Steve anasema, “Nilikuwa mwenye kukasirika, mwivu, mwenye kushikilia, na mwenye wasiwasi.” Dada Selma anakumbuka: “Hata mbele nijue kweli, nilipaswa kuwa mwangalifu kuhusu kila neno nililosema na kila jambo nililofanya. Alikuwa akikasirika bure na kwepesi. Wakati nilianza kujifunza Biblia, tabia hiyo ikawa mbaya hata zaidi.” Ni nini kilichomusaidia dada Selma?

12 Dada Selma anakumbuka jambo fulani alilojifunza kutoka kwa dada aliyejifunza naye. Anasema: “Siku moja sikupenda kujifunza Biblia. Kwa sababu siku iliyotangulia, Steve alinipiga nilipojaribu kutetea jambo fulani, kwa hiyo sikuwa mwenye furaha na nilikuwa mwenye kuhuzunika sana. Nilipomujulisha dada huyo mambo yaliyonipata na jinsi nilivyojisikia, aliniomba nisome andiko la 1 Wakorintho 13:4-7. Niliposoma andiko hilo, nikaanza kufikiri hivi, ‘Steve hajanifanyia hata jambo moja kati ya mambo haya yenye kuonyesha upendo.’ Lakini dada huyo akafikiri nami kwa kuniuliza, ‘Ni matendo mangapi ya upendo yanayozungumuziwa katika andiko hilo ambayo unamutendea bwana yako?’ Nikamujibu, ‘Hakuna hata moja, kwa kuwa ni vigumu kuishi naye.’ Kwa upole, dada akaniambia, ‘Selma, kati yako na Steve, ni nani anayetaka kuwa Mukristo?’ Nilipotambua kwamba ilinifaa kubadili mawazo yangu, nilisali kwa Yehova ili anisaidie nimwonyeshe Steve upendo zaidi. Polepole, mambo yakaanza kubadilika.” Kisha miaka 17, Steve akakubali ukweli.

JINSI WENGINE WANAVYOWEZA KUSAIDIA

13, 14. Namna gani wengine katika kutaniko wanaweza kuwasaidia wale wanaoishi katika familia inayogawanyika kidini?

13 Kama matone ya mvua yanavyolowanisha udongo na kusaidia mimea kukomaa, watu wengi katika kutaniko wanategemeza Wakristo wanaoishi katika familia zinazogawanyika kidini ili wawe wenye furaha. Dada Elvina, anayeishi huko Brazili anasema: “Upendo wa ndugu na dada zangu ulinisaidia ili kusimama imara katika kweli.”

14 Ndugu na dada katika kutaniko wanapoonyesha wema na kupendezwa na mushiriki wa familia asiye Mukristo, hilo linaweza kugusa moyo wake. Mwanaume mumoja huko Nigeria ambaye alikubali ukweli miaka 13 kisha bibi yake, anasema hivi: “Nilipokuwa nikisafiri na Shahidi mumoja, motokari yake ikakufa. Alitafuta Mashahidi wenzake katika kijiji kilichokuwa karibu, nao wakatupangisha usiku huo. Walituhangaikia kama kwamba tulijuana nao tangu utoto. Mara moja, nikaona upendo wa Kikristo ambao bibi yangu alikuwa akinielezea.” Huko Uingereza, mwanamuke mumoja aliyekubali kweli miaka 18 kisha bwana yake, anakumbuka: “Mashahidi walitualika sisi wawili ili kula chakula. Siku zote walinikaribisha vizuri.” * Mwanaume mwingine katika inchi hiyo ambaye mwishowe akaja kuwa Shahidi, anasema hivi: “Ndugu na dada walitutembelea, ao walitualika kwao, na niliona kwamba walikuwa watu wazuri. Hilo lilionekana wazi hasa wakati nilipokuwa katika hospitali, wengi walikuja kuniona.” Je, unaweza kufanya jambo fulani ili kuonyesha pia kwamba unapendezwa na washiriki wa familia ya ndugu ao dada wasio Mashahidi?

15, 16. Ni nini kinachoweza kumusaidia Mukristo aendelee kuwa na furaha hata ikiwa washiriki wengine wa familia wanaendelea kupinga kweli?

15 Kwa kweli, si wenzi wote wa ndoa, watoto, wazazi ao watu wengine wa jamaa watakaoikubali ile kweli, hata ikiwa unaendelea kuwa na mwenendo safi na kuwatolea ushahidi kwa busara kwa miaka mingi. Wengine wataendelea kuwa wasiopendezwa ao wapingaji wakali. (Mt. 10:35-37) Hata hivyo, wakati Wakristo wanaonyesha sifa nzuri zinazoombwa na Mungu, hilo linaweza kuwa na matokeo mazuri. Mwanaume mumoja aliyefikia kukubali ukweli anasema: “Mwenzi aliye Mukristo anapoanza kuonyesha sifa hizo nzuri, haujui namna zinagusa moyo na akili ya mwenzi wake asiyeamini. Kwa hiyo, usimuchoke mwenzi wako asiye Mukristo.”

16 Inawezekana Mukristo awe mwenye furaha hata ikiwa mushiriki wa familia habadiliki. Muda wa miaka 21, dada mumoja alijaribu kumusaidia bwana yake akubali ujumbe wa Ufalme lakini haikuwezekana, na dada huyo anasema: “Ninalinda furaha yangu kwa kujikaza kumufurahisha Yehova, kwa kuendelea kuwa mwaminifu kwake, na kwa kufanya mambo yanayosaidia hali yangu ya kiroho iwe nguvu. Mambo kama vile, funzo la pekee, mikutano, mahubiri, na kuwasaidia wengine katika kutaniko, yamenisaidia niwe na uhusiano muzuri na Yehova na kulinda moyo wangu.”​—Met. 4:23.

USICHOKE!

17, 18. Namna gani Mukristo anaweza kuendelea kuwa na tumaini hata ikiwa anaishi katika familia inayogawanyika kidini?

17 Ikiwa wewe ni Mukristo mwaminifu na unaishi katika familia inayogawanyika kidini, usichoke. Kumbuka kwamba “Yehova hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.” (1 Sam. 12:22) Atakuwa pamoja nawe ikiwa wewe pia unashikamana naye. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 15:2.) Kwa hiyo ‘pata furaha tele katika Yehova. Mukabizi Yehova njia yako, na kumutegemea.’ (Zab. 37:4, 5) ‘Dumu katika sala,’ na uwe na imani kwamba Baba yetu wa mbinguni anaweza kukusaidia ili uvumilie majaribu ya kila namna.​—Rom. 12:12.

18 Umusihi Yehova akupatie roho yake takatifu ili ikusaidie kuendelea kuishi pamoja na washiriki wengine wa familia kwa amani. (Ebr. 12:14) Ndiyo, inawezekana kuishi pamoja na washiriki wa familia wasio Wakristo kwa amani, na hivyo kugusa mioyo yao mwishowe. ‘Unapofanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu,’ utakuwa mwenye furaha na amani moyoni. (1 Kor. 10:31) Unapojikaza kufanya hivyo, inafurahisha kabisa kujua kwamba ndugu na dada katika kutaniko watakutegemeza kwa upendo!

[Maelezo ya chini]

^ Majina yamebadilishwa.

^ Shauri la Paulo halipinge kanuni ya kutengana na mwenzi wa ndoa wakati hali haziruhusu kuendelea kuishi pamoja. Huo ni uamuzi muzito na wa pekee. Ona kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” ukurasa wa 220-221.

^ Maandiko hayakatazi kukula pamoja na watu wasio Wakristo.​—1 Kor. 10:27.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Chagua wakati unaofaa ili kumuelezea mwenzi wako asiye Mukristo mambo unayoamini

[Picha katika ukurasa wa 29]

Onyesha kwamba unahangaikia mwenzi wa ndoa asiye Mukristo