Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wote Wanaodai Kuwa Wakristo Ni Wakristo Kikweli?

Je, Wote Wanaodai Kuwa Wakristo Ni Wakristo Kikweli?

Je, Wote Wanaodai Kuwa Wakristo Ni Wakristo Kikweli?

JE, UNAJUA idadi ya Wakristo ulimwenguni? Kulingana na kitabu Atlas of Global Christianity, katika mwaka wa 2010 kulikuwa na Wakristo bilioni 2.3 hivi duniani kote. Lakini kitabu hichohicho kinasema pia kwamba Wakristo hao ni wafuasi wa madhehebu 41,000, kila moja ya madhehebu hayo ikiwa na mafundisho na sheria zake kuhusu mwenendo. Kwa sababu kuna dini nyingi hivyo zinazodai kuwa za Kikristo, tunaelewa ni kwa nini watu fulani wamechanganyikiwa na hata kuvunjwa moyo. Huenda wakajiuliza, ‘Je, wote wanaodai kuwa Wakristo ni Wakristo kikweli?’

Acheni tuchunguze jambo hilo kwa njia tofauti. Kwa kawaida, msafiri hutarajiwa kutambulisha uraia wake kwa ofisa wa uhamiaji aliye mpakani. Pia, anahitaji kuthibitisha yeye ni nani kwa kuonyesha kitu cha kumtambulisha, labda pasipoti. Vivyo hivyo, Mkristo wa kweli anahitaji kufanya mengi zaidi ya kudai tu kwamba anamwamini Kristo. Anahitaji pia kujitambulisha kwa njia nyinginezo. Njia gani hizo?

Neno “Mkristo” lilianza kutumiwa mara ya kwanza muda fulani baada ya mwaka wa 44 W.K. Luka, mwanahistoria aliyeishi nyakati za Biblia aliandika hivi: ‘Kule Antiokia ndiko ambako kwa mara ya kwanza wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.’ (Matendo 11:26) Ona kwamba wale walioitwa Wakristo walikuwa wanafunzi wa Kristo. Ni nini kinachothibitisha kwamba mtu ni mwanafunzi wa Yesu Kristo? Kamusi ya The New International Dictionary of New Testament Theology inaeleza hivi: “Kuwa mwanafunzi wa Yesu kunamaanisha kwamba mtu amejidhabihu kabisa bila masharti . . . kwa muda wote wa maisha yake.” Hivyo basi, Mkristo wa kweli ni yule anayefuata kikamili na bila masharti mafundisho na maagizo ya Yesu, yule Mwanzilishi wa Ukristo.

Je, inawezekana kuwapata watu kama hao miongoni mwa wengi wanaodai kuwa Wakristo leo? Yesu mwenyewe alisema ni nini ambacho kingewatambulisha wafuasi wake wa kweli? Tunakutia moyo uchunguze jinsi Biblia inavyojibu maswali hayo. Katika makala zinazofuata, tutachunguza mambo matano yaliyotajwa na Yesu ambayo yanawatambulisha wafuasi wake wa kweli. Tutachunguza jinsi Wakristo wa karne ya kwanza walivyotimiza mambo hayo. Na tutajitahidi kuona ni akina nani kati ya wengi wanaodai kuwa Wakristo ambao wanafanya hivyo leo.